- Mbuzi mwitu wa Walia (Walia ibex), anayepatikana kaskazini mwa Ethiopia pekee, ameorodheshwa tena kuwa katika hatari kubwa ya kutoweka (Critically Endangered) baada ya tathmini za IUCN kubaini idadi yake imeporomoka hadi chini ya kiwango muhimu cha uhifadhi.
- Utafiti unaonyesha idadi ya Walia ibex imepungua kutoka wanyama 865 mwaka 2015 hadi 306 mwezi Mei 2024, huku idadi ya wanyama waliokomaa wenye uwezo wa kuzaliana ikishuka chini ya 250, hali inayokidhi vigezo vya IUCN vya hatari kubwa ya kutoweka.
- Watafiti wanahusisha kupungua kwa spishi hiyo na ujangili, uvamizi wa shughuli za binadamu kwenye makazi yake, athari za janga la COVID-19 na vita vya Ethiopia vya 2021–2022, huku visa vya ujangili vikiendelea kuripotiwa hata mwaka 2025.
Mbuzi mwitu wa Walia, spishi adimu ya mbuzi anayepatikana kaskazini mwa Ethiopia pekee, kwa mara nyingine ametambuliwa kama mnyama aliye katika hatari kubwa ya kutoweka(Critically Endangered) baada ya tathmini za hivi karibuni kuonyesha idadi yake imeendelea kupungua na kushuka chini ya kiwango muhimu kinachotumiwa na wataalamu wa uhifadhi.
Mnyama huyo maarufu hupatikana zaidi kwenye miamba mirefu na maeneo magumu kufikika ya Hifadhi ya Taifa ya Milima ya Simien. Awali alikuwa ameorodheshwa katika kundi la wanyama walio hatarini (Vulnerable) kwenye Orodha Nyekundu ya Muungano wa Kimataifa wa Uhifadhi wa Mazingira (IUCN).
Hali ya uhifadhi wa Walia ibex (Capra walie) imekuwa ikibadilika kwa miaka. Mwaka 1986, iliorodheshwa kuwa katika hatari ya kutoweka (Endangered), kisha ikawekwa katika kundi la walio katika hatari kubwa ya kutoweka (Critically Endangered) mwaka 1996, kabla ya kurejeshwa tena katika kundi la walio katika hatari ya kutoweka (Endangered) mwaka 2008.
Kati ya mwaka 2009 na 2012, tafiti zilionyesha idadi ya Walia ibex iliongezeka kutoka wanyama 680 hadi 850. Kutokana na mwenendo huo, watafiti walikadiria kuwa ifikapo mwaka 2020, idadi hiyo ingefikia wanyama 975. Kwa msingi huo, walihitimisha kuwa hali ya spishi hiyo ilikuwa imeimarika na kuishusha hadi kundi la walio hatarini (Vulnerable).
Hata hivyo, tathmini ya mwaka 2020 ilibaini kuwa mwaka 2019 idadi ya Walia ibex ilifikia 619 pekee, lakini ilihitimisha kuwa rekodi hiyo ya mwaka mmoja haikubadilisha mwenendo wa jumla wa ongezeko la idadi yao.
“Kwa uelewa tulionao sasa, hitimisho hilo halikuwa sahihi,” alisema Paul Scholte, mshauri mwandamizi wa Mamlaka ya Uhifadhi wa Wanyamapori ya Ethiopia na kiongozi wa tathmini ya IUCN kuhusu Walia ibex, katika mahojiano na Mongabay yaliyofanyika kwa njia ya barua pepe.
Utafiti uliochapishwa mwaka jana na Scholte pamoja na wenzake unaonyesha kuwa idadi ya Walia ibex imepungua kutoka wanyama 865 mwaka 2015 hadi 306 mwezi Mei 2024.
Kilichoibua wasiwasi zaidi ni kwamba mwaka 2023 na 2024 idadi ya wanyama waliokuwa wamekomaa na wenye uwezo wa kuzaliana ilikuwa chini ya 250. Kiwango hicho kinaangukia kwenye kigezo cha IUCN cha kuitambua spishi kuwa katika hatari kubwa ya kutoweka (Critically Endangered), alisema Scholte.
Aidha, sensa nyingine iliyofanyika Novemba 2024, ambayo haikujumuishwa kwenye utafiti wa mwaka 2025, ilihesabu Walia ibex 289 pekee, kati yao 228 wakiwa waliokomaa na wenye uwezo wa kuzaliana. Hesabu nyingine ya Desemba 2025 ilibaini kuwa walikuwa wamebaki 271 tu. “Kwa maneno mengine, ndani ya mwaka mmoja tulipoteza wanyama wengine 18,” alisema.
Katika utafiti wao, Scholte na wenzake pia waliwahoji karibu watu 200, wakiwemo watumishi wa hifadhi, viongozi wa serikali za mitaa na wakazi wa vijiji jirani, ili kubaini sababu za kupungua kwa idadi ya Walia ibex. Waliohojiwa walitaja ujangili kuwa tishio kubwa zaidi kwa mnyama huyo. Ujangili huo unadhaniwa kufanywa ili kupata nyama ya pori kwa matumizi ya kitoweo na tiba za jadi. Sababu nyingine zilizotajwa ni uvamizi wa shughuli za binadamu katika makazi ya wanyama na uharibifu wa makazi yao.
Hali hiyo ilizidishwa na athari za janga la COVID-19 pamoja na vita vya 2021–2022 kati ya Serikali ya Ethiopia na Tigray People’s Liberation Front (TPLF).
Kwa mujibu wa washiriki wa utafiti, machafuko yaliyotokana na vita yalitoa mwanya kwa ongezeko la ujangili, huku janga la COVID-19 “likisababisha kupungua kwa watalii, kushuka kwa mapato ya uhifadhi na kusitishwa kwa doria pamoja na shughuli za uhamasishaji,” watafiti hao walisema katika chapisho.
Scholte alisema ujangili bado unaendelea kuwa tishio kubwa. “Mnamo Aprili 2025, wawindaji haramu wanne walikamatwa wakiwa na mabaki ya Walia ibex wawili, jambo linaloonyesha kuwa shinikizo dhidi ya spishi hiyo bado linaendelea wakati eneo hilo la Ethiopia likikabiliwa na changamoto za muda mrefu za kiusalama,” alisema.

Picha ya bango ikimuonyesha mbuzi mwitu dume wa Walia (Walia ibex) nchini Ethiopia. Picha kwa hisani ya Paul Scholte.
Habari hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza hapa kwa lugha ya Kiingereza mnamo tarehe 09/07/2026.