- Upande wa mashtaka ulishindwa kuthibitisha mashitaka bila kuacha mashaka.
- Mshitakiwa adai hakusikilizwa ipasavyo na alilazimishwa kusaini maelezo.
- Jaji asema kulikuwa na kasoro zilizogusa uhalali wa mwenendo wa shauri.
- Kulikuwa na mapungufu makubwa katika mlolongo wa utunzaji wa vielelezo.
Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Musoma, imemwachia huru Marwa Nyamhanga aliyetiwa hatiani kwa kukutwa na nyara za Serikali, kuingia na kumiliki silaha ndani ya Hifadhi ya Taifa ya Serengeti baada ya kubaini dosari zilizojitokeza katika ushahidi wa upande wa mashtaka.
Mahakama hiyo Julai 20,2026 mbele ya Jaji Kamazima Kafanabo ilitengua hukumu ya Mahakama ya Wilaya ya Serengeti iliyokuwa imemhukumu Marwa kifungo cha miaka 20 jela kwa makosa hayo baada ya kukubali rufaa yake na hoja za Jamhuri za kuunga mkono rufani hiyo huku wakibainisha kuwa hawakuweza kuthibisha mashtaka bila kuacha shaka.
Mahakama ya Wilaya Serengeti
Mahakama ya Wilaya ilimtia hatiani kwa makosa matatu ambayo ni; kuingia hifadhini bila kibali, kumiliki panga ndani ya hifadhi bila kibali pamoja na kumiliki sehemu ya mguu wa nyumbu ambao haukuwa umechunwa ikiwa ni nyara ya Serikali yenye thamani ya Sh 1,586,000 (Dola za Marekani 603).

Upande wa mashtaka ulidai mahakamani kuwa Desemba 7, 2025, askari wa hifadhi walimkamata mshtakiwa katika eneo la Korongo la Nyamburi ndani ya Hifadhi ya Serengeti akiwa na panga na sehemu hiyo ya nyumbu.
Utetezi Mahakamani
Alipojitetea, Marwa Nyamhanga alidai kuwa Desemba 6, 2025 alikuwa akitoka kwenye sherehe ya harusi akiwa amelewa, ndipo askari wa hifadhi walipomkamata akiwa njiani.
Alidai kuwa askari hao walimshikilia katika kituo chao usiku kucha na asubuhi yake walimbambia panga pamoja na mguu wa nyuma wa nyumbu kabla ya kumpeleka Kituo cha Polisi Mugumu kwa hatua za kisheria.
Baada ya kusikiliza mashahidi wanne na kupokea vielelezo vitano, Mahakama ya Wilaya ilimtia hatiani kwa makosa yote matatu na kumhukumu kifungo cha mwaka mmoja kwa kosa la kwanza na la pili, pamoja na kifungo cha miaka 20 kwa kosa la tatu, adhabu ambazo zilielekezwa kutumikiwa kwa pamoja.
Marwa hakukubaliana na hukumu hiyo na aliwasilisha rufani Mahakamani Kuu akidai kuwa hakupatiwa haki ya kusikilizwa ipasavyo, ushahidi ulipokelewa kimakosa, alilazimishwa kusaini cheti cha ukamataji bila maelezo, na kwamba mashtaka hayakuthibitishwa pasipo shaka.
Jamhuri yaunga mkono Rufani
Katika usikilizwaji wa rufaa, upande wa Jamhuri kupitia Wakili wa Serikali, Beatrice Mgumba, uliiomba Mahakama Kuu ikubali rufaa hiyo.
Wakili Beatrice aliunga mkono rufaa akieleza kuwa upande wa mashtaka ulishindwa kuthibitisha kuwa panga na sehemu ya nyumbu vilivyodaiwa kukutwa kwa mshtakiwa ndio vilevile vilivyowasilishwa mahakamani kama vielelezo.
Alifafanua kuwa shahidi wa kwanza (PW1) alisema alimkamata mshtakiwa akiwa na panga na nyama iliyodhaniwa kuwa ni nyara za serikali, kisha akavipeleka Kituo cha Polisi Mugumu kwa kumbukumbu namba MUG/IR/3668/2025.
Hata hivyo, ushahidi wake ulitofautiana na maelezo yaliyopo kwenye cheti cha ukamataji (Exhibit P1), ambacho kilieleza kuwa panga lililokamatwa lilikuwa na mpini mweusi wenye alama “KN”.
Wakili Beatrice alidai PW1 hakueleza jinsi alivyorudishiwa panga hilo kutoka kituo cha polisi hadi kulipeleka mahakamani kama kielelezo.
Pia, Wakili Beatrice alidai kuwa mpelelezi wa kesi (PW4) alisema alichukua vielelezo kutoka kwa mhifadhi wa vielelezo, lakini hakueleza ni vielelezo gani hasa alivyovikuta stoo wala hakuthibitisha kuwa vilikuwa na namba ileile ya kumbukumbu iliyotajwa na PW1.
“Kuhusu sehemu ya nyumbu, PW4 hakufanikiwa kuonyesha uhusiano kati ya sehemu ya mnyama iliyodaiwa kukamatwa eneo la tukio na ile iliyowasilishwa kwa hakimu kwa ajili ya amri ya kuteketezwa,” alidai Wakili Beatrice.
Kwa kutegemea maamuzi ya Mahakama ya Rufani katika kesi za Paulo Maduka na Wenzake dhidi ya Jamhuri na Abas Kondo Gede dhidi ya Jamhuri, Wakili wa Serikali alisisitiza kuwa upande wa mashtaka ulishindwa kuthibitisha mlolongo wa uhifadhi wa vielelezo, hivyo hakukuwa na ushahidi wa kutosha kwamba vielelezo vilivyowasilishwa mahakamani ndivyo vilivyokamatwa kutoka kwa mshtakiwa.
Uamuzi wa Mahakama Kuu
Mahakama Kuu ilikubaliana na hoja za rufani na kubaini kuwa kulikuwa na kasoro zilizogusa uhalali wa mwenendo wa shauri, hivyo ikabatilisha hukumu ya Mahakama ya Wilaya na kuondoa adhabu zote alizopewa Marwa Nyamhanga.

Jaji Kafanabo alisema mahakama ilibaini kuwa upande wa mashtaka ulishindwa kuthibitisha kesi bila kuacha shaka.
“Ushahidi wa GPS uliotumika kuonyesha eneo la kukamatwa haukuthibitishwa ipasavyo kisheria, hivyo haukuweza kuthibitisha kuwa mshtakiwa alikamatwa ndani ya mipaka ya Hifadhi ya Taifa ya Serengeti.
“Mahakama pia ilibaini kuwepo kwa mapungufu makubwa katika mlolongo wa utunzaji wa vielelezo, upande wa mashtaka haukuonyesha kwa ushahidi jinsi panga na sehemu ya mguu wa nyumbu vilivyohifadhiwa na kuhamishwa kutoka vilipokamatwa hadi vilipowasilishwa mahakamani,”alisema Jaji Kafanabo.
Kutokana na kasoro hizo, Mahakama Kuu ilitengua hukumu zote za kutiwa hatiani na adhabu zilizokuwa zimetolewa na kuamuru Marwa Nyamhanga aachiliwe huru mara moja isipokuwa kama anashikiliwa kwa sababu nyingine halali.
Picha ya bango: Wanyama aina ya nyumbu wakirejea katika makazi yao ya Hifadhi ya Taifa ya Serengeti wakitokea katika nchi ya jirani ya Kenya, hususan kwenye mbuga ya Masai Mara. Picha kwa hisasi Blogu ya Michuzi.