- Maandamano dhidi ya mpango wa serikali wa kujenga kiwanda cha nguvu za nyuklia karibu na Bondo, Kaunti ya Siaya, yaligeuka vurugu, huku mtu mmoja akijeruhiwa kwa risasi na watu 17 kukamatwa baada ya mkutano wa mashauriano ya umma.
- Wanajamii wamechangisha fedha ili kuwasaidia watuhumiwa kulipia dhamana, huku 15 kati ya 17 tayari wakiachiwa huru, licha ya dhamana kufikia KSh180,000 kwa baadhi yao.
- Waliokamatwa wanachunguzwa kwa tuhuma za shambulio na makosa chini ya Sheria ya Kuzuia Ugaidi ya Kenya, hatua ambayo wakili wao anasema inalenga kuwatisha na kuwanyamazisha wanaopinga mradi huo.
- Ripoti ya tathmini ya kimkakati ya mazingira ya mwaka 2023 ilipendekeza kuepukwa kwa eneo la Ziwa Victoria kwa mradi wa nyuklia, ikitaja hatari ya shughuli za volkeno zinazoweza kuathiri usalama wa kiwanda, wakati mamilioni ya watu wanategemea ziwa hilo kwa riziki, chakula na maji.
Maandamano yaliyozuka wakati wa mkutano wa umma kuhusu mpango wa kujenga kiwanda cha nguvu za nyuklia nchini Kenya yalimalizika kwa mtu kupigwa risasi na watu 17 kukamatwa.
Serikali ya Kenya inakusudia kujenga kiwanda cha nguvu za nyuklia chenye uwezo wa megawati 2,000 karibu na mji wa Bondo katika Kaunti ya Siaya, kando ya Ziwa Victoria. Mnamo Julai 24, 2026, maafisa wakiwemo wawakilishi wa Nuclear Power and Energy Agency (NuPEA) walikuwa wakiendesha mkutano wa mashauriano ya umma mjini Bondo ndipo msukosuko ulipoanza.
Dickens Ochieng’, wakili na mwanaharakati wa kijamii aliyehudhuria mkutano huo, aliiambia Mongabay kwa simu kuwa wamiliki wa ardhi walioalikwa kwenye mkutano huo wakisema “Wadagi,” neno la Kidholuo linalomaanisha “tunakataa,“ kuonyesha upinzani wao dhidi ya mradi wa nyuklia. “Kisha afisa mmoja wa polisi aliyekuwa akilinda mashirika ya serikali alitumia silaha yake na kumjeruhi mtu mmoja kwa risasi, na mkutano ukageuka msukosuko papo hapo,” alisema Ochieng’.
Katika siku zilizofuata, watu 17 walikamatwa na kufungwa. Hati rasmi iliyopitiwa na Mongabay inaonyesha kwamba watuhumiwa hao wanachunguzwa kwa tuhuma za shambulio na makosa chini ya Sheria ya Kuzuia Ugaidi ya Kenya (Prevention of Terrorism Act).
Ochieng’, ambaye amechukua jukumu la kuwatetea kisheria, alisema “kuna ukandamizaji mkubwa unaofanywa na serikali dhidi ya wanaopinga mradi huu.”
“Kama wakili, ninaendelea kuiambia jamii kwamba lazima wasimame imara, kwa sababu tuhuma za ugaidi hazina uhusiano wowote na tukio lililotokea,” alisema. “Zinakusudiwa kuwatisha na kuwanyamazisha, si kuhakikisha haki inatendeka.”
Hadi sasa, watuhumiwa 15 kati ya 17 wameachiwa huru baada ya wanajamii kukusanya pesa kupitia michango ya umma ili kulipia dhamana zao, zilizowekwa kati ya KSh15,000 na KSh180,000 ($116 hadi $1,391). “Katika jamii hii, watu wengi ni wavuvi na wafanyabiashara wadogo,” Ochieng’ alieleza. “Kulingana na takwimu, wengi wao wanaishi kwa chini ya dola moja kwa siku. Muungano wa watetezi wa haki uliweza kulipia dhamana za baadhi yao, lakini kwa wengine, hali ni ngumu.”
Mongabay iliwasiliana na kamanda wa polisi wa Bondo na NuPEA kutafuta maoni yao, lakini hakuna aliyejibu kufikia wakati wa kuchapishwa kwa makala hii.
Mwezi Mei, jamii zilifanya maandamano dhidi ya mpango huo, huku ombi la mtandaoni linaloitaka serikali kusimamisha mradi likiendelea kusambazwa.
Ripoti ya Strategic Environmental Assessment iliyochapishwa mwaka 2023 kwa ajili ya mpango wa nguvu za nyuklia nchini Kenya ilionyesha kwamba eneo la Ziwa Victoria linapaswa kuepukwa kwa sababu liko katika hatari ya shughuli za volkeno, jambo ambalo, kwa mujibu wa ripoti hiyo, “linaweza kuathiri usalama” wa kiwanda cha nguvu za nyuklia.
Ziwa Victoria ndilo ziwa kubwa zaidi la maji baridi barani Afrika. Linashirikiwa na Kenya, Uganda na Tanzania, na mamilioni ya watu katika nchi hizo tatu wanategemea ziwa hilo kwa riziki, usalama wa chakula na maji ya kunywa.
Picha ya bango: Mashua za uvuvi katika Luanda Kotieno, eneo la Bondo, Kaunti ya Siaya, ambapo serikali ya Kenya inapanga kujenga kiwanda cha nguvu za nyuklia. Picha na Victor Ochieng’ kupitia Flickr (CC BY-SA 2.0).
Habari hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza hapa kwa lugha ya Kiingereza mnamo tarehe 04/08/2026.
Taarifa hii imehaririwa kuondoa madai kwamba polisi walitumia vitoa machozi dhidi ya waandamanaji. Baadaye, Mongabay ilibaini kuwa aliyetoa taarifa hiyo alikosea.