- Salvinia inaathiri ikolojia ya ziwa, ubora wa maji na viumbe hai.
- Shughuli za binadamu karibu na ziwa ni chanzo cha magugu hayo kuenea kwa kasi.
- Wenyeviti wa Vitongoji wanatakiwa kusimamia sheria zilizopo.
- Lazima kuwe na mfumo wa kushirikisha jamii katika maamuzi ya masuala ya mazingira.
Victoria, ziwa kubwa zaidi Barani Afrika linalopatikana Kaskazini Magharibi mwa Tanzania, ambalo kwa muda mrefu limekuwa likisifika kwa kuwa kitovu cha bioanuwai ya maji baridi na makazi bora ya viumbe wa majini, huenda likapoteza sifa hizo iwapo uvamizi wa magugumaji aina ya Salvinia, hautadhibitiwa haraka.
Wataalam wanabainisha kuwa iwapo magugumaji hayo yataendelea kuenea katika ziwa hilo, mazingira ya majini, ikolojia pamoja na shughuli za kiuchumi kwa mamilioni ya wakazi wa Afrika Mashariki, vinaweza kuathirika. Hata hivyo Serikali ilinukuliwa ikisema kuwa magugu hayo yamedhibitiwa kikamilifu. Licha ya Tanzania, Ziwa hilo linapakana katika nchi za Kenya na Uganda. Kwa upande wa Tanzania, linazungukwa na mikoa ya Mwanza, Mara, Kagera, Simiyu na Geita.
Chanzo cha magugumaji vamizi
Kwa mujibu wa hifadhidata ya mimea duniani, Salvinia ni mimea vamizi hatari zaidi ya majini yenye uwezo wa kuzaliana na kukua haraka sana hadi kutengeneza jamvi zito juu ya maji. Salvinia ina aina kuu za Salvinia molesta – Spishi vamizi inayojulikana kwa kutengeneza magugu mengi kwenye maziwa na mito, Salvinia minima – Spishi ndogo inayotumika pia kwenye mapambo ya majini na Salvinia natans – Spishi ya asili inayoelea kwenye maji matulivu.
Jarome Kayombo, Meneja wa Kanda ya Ziwa wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) alinukuliwa na vyombo vya habari akisema kuwa wavuvi katika maeneo ya Buyagu (Sengerema), Chole, Nyahiti na Mbarika (Misungwi) walianza kuona magugumaji aina ya Salvinia katika Ziwa Victoria mwezi Agosti 2024.

Jenny Mroso, Mratibu wa Mazingira kutoka Bodi ya Bonde la Ziwa Victoria anasema magugu hayo yalianzia nchi jirani kabla ya kuonekana Ziwa Victoria. Hata hivyo hakuna taarifa za uhakika zinazoonyesha yalifikaje kwenye ziwa hilo.
Mroso anasema: “Haya magugumaji aina ya Salvinia hapa Afrika Mashariki wengi walikuwa wanayaita Kariba weeds, kwa sababu yalianzia ziwa Kariba siku za nyuma. Kwa wenzetu wa Uganda yalianzia ziwa Kyoga tangu mwaka 2011. Ukiangalia, ziwa Kyoga halina mwingiliano wowote na ziwa Victoria… bado haijajulikana yaliingiaje ziwa Victoria. Uchunguzi bado unaendelea kujua chanzo chake”.
David Muhasika, Afisa Mazingira kutoka Baraza la Uhifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) Kanda ya Mwanza, anasema: “Haya magugu yanakua kwa kasi. Kitaalamu inaonekana yanakua karibu mara mbili hadi tatu kwa muda wa siku nane. Lakini pia yana tabia ya kutanda na kufunika eneo kubwa. Hadi sasa hofu kubwa ni jinsi yanavyozaliana”.
Samwel Masumbuko, mvuvi katika eneo la Kigongo Ferry katika Wilaya ya Misungwi, anasema kuwa magugumaji haya yanakua kwa kasi sana ikilinganishwa na magugu mengine kama lutende.
“Hayahitaji udongo kwenye ukuaji wake. Pia yanaenea kwa kasi sana. Kuna wakati yanapelekwa na upepo na kusogezwa mbali zaidi. Hilo linayafanya yasambae sehemu nyingi kwa haraka na kuleta changamoto kubwa, hasa kwa wavuvi,” anasema Samweli.
Kuenea kwa Salvinia
Muhasika anasema kuongezeka kwa magugumaji vamizi aina ya Salvinia katika Ziwa Victoria kumechangiwa kwa kiasi kikubwa na shughuli za kibinadamu zinazofanyika katika maeneo yanayozunguka ziwa hilo.
“Shughuli za kibinadamu ikiwemo watu kulima kandokando ya ziwa, husababisha mmomonyoko wa udongo kuelekea kwenye ziwa. Matokeo yake, udongo na mbolea vyote huishia ziwani na kurutubisha magugu hayo,” anasema Muhasika.
Kwa mujibu wa Muhasika, sababu nyingine ya kuongezeka kwa magugu hayo ni taka kutoka kwenye makazi ya watu na viwandani ambazo husababisha ziwa kuwa na rutuba, hali inayochochea kuota kwa magugumaji mapya.
“Mtu akilima kandokando ya ziwa umbali unaopungua mita 60, mvua zinaponyesha, husomba mbolea yote kutoka kwenye mashamba hadi ziwani. Maji yakiingia ziwani yakiwa na virutubisho, huyafanya haya magugu yamee kwa kasi na kunawiri,” anasema Muhasika.

Hoja hii inaungwa mkono na Laurent Kitogo, mtaalamu wa Mazingira kutoka EMEDO, shirika la linalofanya kazi ya kuboresha maisha ya jamii kupitia usimamizi endelevu wa mazingira na matumizi ya rasilimali asilia. Naye anahusisha kuenea kwa mimea vamizi aina ya Salvinia katika Ziwa Victoria na uchafuzi wa mazingira unaoingia ziwani kutoka vyanzo mbalimbali.
Jamii zote za magugumaji zinasababishwa na uchafuzi mkubwa kwenye ziwa, japokuwa hatujajua ni uchafuzi wa aina gani kati ya ule unaotokana na kutodhibiti taka ngumu au taka zinazoelekea ziwani, anasema Kitogo.
“Ili mimea ikue haraka katika maji inahitaji mambo makuu mawili; naitrojeni na fosforasi (nitrojeni ni kirutubisho kinachochochea ukuaji wa mimea na mwani wakati fosforasi ni huchochochea ukuaji wa mimea ya majini). Virutubisho hivi huingia kwa wingi kwenye ziwa kupitia mbolea za mashambani, maji taka, kinyesi cha mifugo na taka za viwandani. Ndiyo maana tunasema shughuli za binadamu zinazowezesha taka hizo kufika ziwani, ndiyo sababu kubwa ya mimea hii kuendelea kuenea ziwani,” anasema Kitogo.
Jenny Mroso, Mratibu wa Mazingira kutoka Bodi ya Bonde la Ziwa Victoria ambaye kitaaluma ni mhandisi, anasema kuwepo kwa magugu hayo ziwani inamaanisha kuwa ziwani kuna mazingira ambayo yanawezesha ukuaji na uzalishaji wa magugumaji hayo.
Athari za magugumaji
Magugumaji ya Salvinia kama ilivyo kwa jamii zingine za magugumaji, yanaendelea kuleta athari kubwa kwa mazingira ya majini, ikolojia pamoja na shughuli za kiuchumi kwa mamilioni ya wakazi wa Afrika Mashariki wanaotegemea ziwa hilo, hasa wale wa mikoa ya Mwanza, Mara, Kagera, Simiyu na Geita.
Muhasika anasema mimea hiyo huharibu ikolojia ya ziwa kwa kufunika uso wa maji na kuzuia mwanga wa jua kupenya, hali inayopunguza ukuaji wa mimea ya majini na kiwango cha oksijeni ndani ya maji.
“Magugumaji yakitanda juu ya maji, viumbe hai walioko majini wanashindwa kupumua kwa sababu wanakosa hewa ya oksijeni na kupelekea vifo,” anasema Kitogo.
Licha ya vifo, Kitogo anasema kutanda kwa magugu juu ya maji, huharibu makazi ya viumbe wa majini, kupunguza bioanuwai na kuvuruga mnyororo wa chakula, hali inayoathiri maisha ya viumbe wa majini.
Kwa mujibu wa Kitogo, athari hizi husababisha kupungua kwa samaki na viumbe wengine wa majini, kuvuruga makazi na maeneo ya kuzaliana, pamoja na kupunguza bioanuwai ya ziwa.

Aidha, huathiri ubora wa maji, huzuia usafiri na shughuli za uvuvi, na kuhatarisha uendelevu wa mfumo mzima wa ikolojia wa Ziwa Victoria.
Juvenali Matagili, Mkurugenzi wa Shirikisho la Vyama vya Wavuvi (FUO), anataja madhara mengine ya magugumaji haya kuwa ni pamoja na kuzuia mzunguko wa maji, kusababisha kuoza kwa viumbe ndani ya maji, kuongeza methane na gesi nyingine zinazochangia mabadiliko ya tabianchi, kusababisha maji kuwa na harufu mbaya pamoja na kupunguza ubora wake.
Muhasika anasema tathmini bado inaendelea kufanyika ili kubaini iwapo magugumaji hayo yana athari zozote za moja kwa moja kwa afya ya maji ya ziwa.
Hata hivyo, Mroso anazungumzia hilo akisema: “Ubora wa maji unaweza kupungua kwa sababu yale magugumaji yanazaliana mara tatu hadi mara nne kwa kipindi cha wiki moja tu. Yanapofikia hatua ya kuoza yakiwa ndani ya maji, ubora wa maji hupungua”.
Athari kwa shughuli za kiuchumi
Kuenea kwa magugumaji hayo pia kumeathiri kwa kiasi kikubwa shughuli za kiuchumi kwa jamii zinazozunguka ziwa hilo.
“Magugumaji yanapokuwa hapa mwaloni yanazuia wavuvi kwenda kwenye shughuli zao kwa sababu hawawezi kupita kwa kutumia mtumbwi wa kasia wala wa mashine kwa sababu yanaziba nafasi kabisa. Katika mazingira haya shughuli za uvuvi hukwama kwa sababu mtumbwi hauwezi kupita,” anasema Frank Musa, mvuvi kutoka katika kijiji Mwasonge wilayani Misungwi.
Anasema magugu hayo pia yana athari kwa vifaa vya uvuvi. “Magugu yakiwa kule katikati ya ziwa, mitego tuliyoweka huyanasa na kwenda nayo umbali mrefu kwa sababu yanakuwa yanasukumwa na upepo. Kwa ujumla, magugu haya yanafilisi wavuvi kwa sababu wanapoteza nyavu zao na mitaji yao,” anafafanua.
Musa anabainisha kuwa magugumaji hayo huathiri pia ufugaji wa samaki ambapo yakinasa kwenye vizimba, huharibu nyavu za wavuvi.
Kwa upande wake, Zabron Chananja, mvuvi kutoka kijiji cha Mwasonge ambaye ana uzoefu wa miaka 10, anasema magugumaji mapya aina ya Salvinia huathiri moja kwa moja shughuli za uvuvi katika maeneo yanayofunikwa na mimea hiyo.
Muhasika anasema magugumaji hayo yanaathiri pia shughuli za usafiri katika Ziwa Victoria. Anasema: “Mwanzoni kabla ya kujengwa daraja, yalileta changamoto kubwa kwenye usafirishaji hasa kwa wavuvi ambao wanatakiwa kusafiri kutoka sehemu moja kwenda sehemu nyingine”.
Athari nyingine ya magugu hayo ni kupungua kwa samaki. Akifafanua kuhusu hilo, Kitogo anasema: “Samaki aina ya sato, mazalia yao ni pembeni ya maji, sasa uwepo wa hii mimea, unaharibu maeneo yao ya mazalia. Hata samaki aina ya sangara ambao wanaishi kwenye kina kirefu, uwepo kwa magugu haya unawaathiri”.
Matagili pia anaeleza athari za magugu hayo kwa wavuvi. Anasema: “Wavuvi hushindwa kufika katika maeneo ya uvuvi kutokana na magugumaji kuzuia njia. Hali hii husababisha nyavu na injini za boti kuharibika kutokana na kujazana kwa magugumaji,” anasema.

Anasema kutokana na changamoto hiyo, matumizi ya mafuta yanaongezeka pamoja na muda wa kufanya kazi, jambo linaloongeza gharama za shughuli za uvuvi. “Magugumaji haya pia huchangia kuongezeka kwa mazalia ya mbu na wadudu wengine wanaosababisha magonjwa,” anasema.
Udhibiti wa magugumaji
Hatua mbalimbali zimekuwa zikichukuliwa kudhibiti magugumaji hayo zikiwemo zile za kitaalam na za kawaida.
Juma Shilunga, Mwenyekiti wa Kitengo cha Usimamizi wa Ufukwe aliiambia Mongabay kuwa wavuvi katika mwalo wa kijiji cha Mwasonge wamekuwa wakiyatoa magugumaji hayo pale yanapozidi kwa kutumia nyavu ambapo huyavuta na kuyatupwa nje.
NEMC, kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais – Mazingira hutumia mbinu za kibailojia kudhibiti magugu hayo.
Muhasika aliiambia Mongabay kuwa NEMC, kwa kushirikiana ya Ofisi ya Rais Mazingira, ilituma wataalam nchini Uganda kwenda kujifunza mbinu za kukabiliana na magugu hayo kwa sababu Uganda walishakutana na hili tatizo na kulipatia ufumbuzi.
“Tulikwenda Uganda, tukachukua wadudu wanaoitwa Mbawakavu, ambao ni jamii ndogo inayokula mimea ya Salvinia. Baada ya mafunzo wataalam walipandikiza wadudu hao kwenye vizimba vyetu katika maeneo ya Mwanza na Kibaha ambao baadaye waliachiwa kwenye ziwa kwa ajili ya kula magugumaji. Bado tunaangalia kama kweli wadudu hawa wanafanya kazi kwa kiwango kinachotakiwa,” alisema Muhasika.
Katika zoezi hilo, NEMC inashirikiana na watu kutoka Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori Tanzania (TAWIRI), Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi Tanzania (TAFIRI) pamoja na Mamlaka ya Afya ya Mimea na Viuatilifu Tanzania, (TPHPA).
Mbali na matumizi ya wadudu, serikali pia imeanza mchakato wa kupata vifaa vya kusafisha magugumaji moja kwa moja kutoka ziwani kwa kuagiza mashine maalum za kusafisha ziwa pale yanapoibuka.
“Kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais Mazingira tumeagiza mashine kwa ajili ya kufanya usafi kwenye ziwa. Kwa sasa mashine hizo zipo kwenye utaratibu wa kununuliwa na zikipatikana zitatumika kwa ajili ya kutoa magugumaji nje ya ziwa,” anasema.
Mbali na juhudi hizo, Mroso, anasema wao wamefanya mambo kadhaa kuzuia magugumaji katika Ziwa Victoria. Baadhi ya shughuli walizofanya ni pamoja na kutoa elimu katika mikoa saba ambayo bodi hiyo inafanya kazi.
“Sheria ya mazingira na Sheria ya Maji zote zinakataza shughuli za binadamu ndani ya mita 60 kwenda ziwani. Sisi kama bonde la ziwa Victoria tumekuwa tukitoa elimu kuhusu sheria hii. Lakini pia tumeanza kuweka mipaka ya mita 60. Pia tumeainisha mialo 184 ambapo kati ya hiyo tumeweka alama kwenye mialo 23,” anasema.
Anafafanua kuwa kazi hiyo wanaifanya katika eneo la Bonde la Ziwa Victoria lenye mikoa ya Mwanza, Mara, Kagera, Geita Simiyu, Shinyanga Tabora, na Arusha.
Changamoto
Kitogo anaona kukosekana kwa utekelezaji wa sheria zilizowekwa kwa ajili ya kudhibiti uchafuzi wa mazingira kama changamoto kubwa inayorudisha nyuma juhudi za kupambana na magugu hayo.
“Matumizi ya viatilifu kandokando ya ziwa una madhara. Sheria ya mazingira ipo, sheria ya viatilifu ipo. Kwa mujibu wa sheria, hawa Wenyeviti wa Kitongoji wanatakiwa pia kusimamia sheria. Tunahitaji usimamizi mzuri wa sheria,” anasema Kitogo.
Kwa upande wa Matagili, changamoto nyingine ni uelewa mdogo miongoni mwa jamii za pembeni mwa Ziwa Victoria kuhusu ulinzi wa ziwa.

“Changamoto nyingine ni kukosekana kwa usimamizi mzuri wa taka katika maeneo ya makazi na makambi ya wavuvi, pamoja na kukosekana kwa mfumo madhubuti wa ushirikishwaji wa jamii katika maamuzi ya masuala ya mazingira. Mara nyingi maamuzi hufanyika kutoka juu kwenda chini bila kuzingatia uzoefu wa watu wanaoishi ziwani kila siku,” anasema Matagili.
Nini kifanyike
Ili kuthibiti ombwe hili, Matangili anashauri kuwe na ushirikiano baina ya serikali pamoja na wadau wa mazingira katika kuhakikisha kunakuwa na usimamizi wa sheria, elimu inatolewa na pia jamii zinazoishi kandokando ya ziwa Victoria zinashirikishwa katika mipango yote.
Hatua muhimu zinazopaswa kuchukuliwa ni pamoja na kutolewa kwa elimu ya mazingira kwa jamii za wavuvi kwa lugha rahisi na endelevu, serikali kuongeza uwekezaji katika usimamizi wa taka na maji taka pamoja na kudhibiti matumizi holela ya mbolea na viuatilifu kandokando ya ziwa.
Hatua nyingine ni kupanda miti ya asili inayolinda kingo za ziwa na mazalia ya samaki pamoja na kuongeza tafiti za kisayansi kuhusu athari za mimea vamizi na mabadiliko ya tabianchi.
Kwa mujibu wa Matangili, jambo lingine linalotakiwa kufanyika ni kuweka utaratibu utakaohakikisha kunakuwa na uwajibikaji wa hali ya juu wa mamlaka zinazosimamia fukwe za ziwa yaani Beach Management Unit BMU pamoja na viwanda vinavyozalisha taka zinazochafua ziwa.
Kuimarisha BMU kwa mafunzo ya mazingira na ikolojia ya ziwa, kuongeza uwajibikaji wa viwanda na taasisi zinazochafua mazingira, pamoja na kujenga sera zinazowashirikisha moja kwa moja wavuvi na jamii za ziwani ni hatua nyingine zinazoweza kusaidia juhudi za kupambana na kuenea kwa magugumaji haya.
Picha ya bango: Magugumaji ya Salvinia yakiwa yamefunika maji katika mwalo wa Kijiji cha Mwasonge katika Wilaya ya Misungwi. Mwalo huu licha ya kutumiwa na wavuvi, magugumaji yanaendelea kukua kwa kasi. Picha na Yohani Gwangway.