- Kenya inachunguza vifo vya tembo 15 vilivyotokea katika mfumo wa ikolojia wa Amboseli kati ya Juni 24 na Julai 24, huku uchunguzi wa awali ukionyesha huenda walikula vitu vyenye sumu.
- Matokeo ya uchunguzi wa maabara yanatofautiana, ambapo Chuo Kikuu cha Nairobi kilibaini mabaki ya kemikali zinazoshukiwa kuwa na sumu, lakini Maabara ya Serikali haikupata sumu zilizokuwa zikitafutwa, na uchunguzi zaidi unaendelea.
- Tembo walioathirika walionyesha dalili za kupooza, wengi wao wakiwa majike wakubwa na watoto wao, huku viongozi wa Kajiado wakitaka ripoti ya haraka kubaini chanzo cha vifo hivyo.
- Mashirika ya uhifadhi yameelezea wasiwasi mkubwa, yakionya kuwa vifo vya tembo wengi kwa wakati mmoja vinaweza kuhatarisha mfumo wa ikolojia na kusisitiza umuhimu wa kuimarisha ufuatiliaji wa afya ya wanyamapori na uwezo wa kukabiliana na dharura.
KAJIADO, Kenya – Kenya inachunguza vifo vya tembo 15 vilivyotokea katika mfumo wa ikolojia wa Amboseli kati ya Juni 24 na Julai 24, 2026.
Huduma ya Wanyamapori Kenya (KWS) imeiambia Mongabay kuwa uchunguzi wa awali wa maabara kuhusu vifo hivyo katika maeneo ya hifadhi ya Kimana na ranchi ya Kuku, unaonyesha huenda tembo hao walikula vitu vyenye sumu.
Sampuli zilizochunguzwa katika Maabara ya Serikali, Chuo Kikuu cha Nairobi, pamoja na maabara nyingine zinazobobea katika uchunguzi wa sumu kwenye tishu na viungo, zimetoa matokeo yanayotofautiana. Uchunguzi wa Chuo Kikuu cha Nairobi uligundua uwepo wa mabaki ya kemikali zinazoshukiwa kuwa na sumu katika sampuli zilizochukuliwa kutoka kwa baadhi ya tembo walioathirika.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Mkurugenzi wa Mawasiliano wa KWS, Duncan Wanyama, tembo 10 walionyesha dalili zinazofanana, ikiwemo kupooza sehemu za mwili, hali iliyowafanya washindwe kusimama kabla ya kufa ndani ya siku moja hadi mbili. Mizoga ya tembo watano wengine ilikuwa imeharibika sana au kuliwa na wanyama wala mizoga, hivyo haikuwa rahisi kubaini chanzo cha vifo vyao. Walioathirika zaidi walikuwa tembo jike wakubwa na watoto wao, huku tembo dume aliyeripotiwa kufa akiwa mmoja tu.
Hata hivyo, vipimo vya Maabara ya Serikali havikuonyesha uwepo wa sumu zilizokuwa zikitafutwa, na KWS imesema “uchunguzi zaidi wa kina bado unaendelea”.
Jinsi vifo hivyo viligunduliwa
Wanyama aliiambia Mongabay kuwa baadhi ya vifo hivyo viligunduliwa baada ya vifaa vya kufuatilia mienendo ya baadhi ya tembo kuonyesha kuwa walikuwa hawasogei. Alisema uchunguzi wa sababu nyingine zinazoweza kusababisha vifo hivyo unaendelea ili kubaini kama tembo hao walikufa kutokana na chanzo kimoja cha sumu au la.
Alisisitiza kuwa hadi sasa hakuna ushahidi unaoonyesha kuwa tukio hilo linaweza kuhatarisha afya ya binadamu. “Dalili zilizoonekana zilijitokeza kwa tembo walioathirika pekee, na hakuna dalili kwamba linaweza kuwaathiri binadamu,” alisema.
Wakati huohuo, viongozi wa eneo hilo wametaka uchunguzi ukamilike haraka. Gavana wa Kaunti ya Kajiado, Joseph ole Lenku, alisema wananchi wanahitaji ripoti itakayobainisha chanzo halisi cha vifo hivyo. “Hatujawahi kushuhudia tukio kama hili. Tunataka ripoti itakayoeleza wazi kilichoua tembo wetu,” alisema katika mkutano wa hadhara.
Vifo vya tembo hao vimetokea wakati kuna mvutano wa kisheria kati ya Serikali ya Kenya na Serikali ya Kaunti ya Kajiado kuhusu usimamizi wa Hifadhi ya Taifa ya Amboseli. Serikali ya Kaunti ya Kajiado hivi karibuni iliishutumu KWS kwa kushindwa kuwasilisha asilimia 50 ya mapato ya hifadhi kwa mwaka 2025 kama ilivyokubaliwa wakati usimamizi wa hifadhi hiyo ulipokabidhiwa kwa Serikali ya Kaunti ya Kajiado kwa makubaliano yaliyolenga kuimarisha ushiriki wa jamii ya Wamasai.
Wakati huohuo, Shirika la Kimataifa la Ustawi wa Wanyama (IFAW) limetaka kuwepo kwa uwekezaji zaidi katika ufuatiliaji wa afya ya wanyamapori, uwezo wa kukabiliana haraka na matukio ya dharura, utafiti wa kisayansi na ushirikiano kati ya serikali, mashirika ya uhifadhi, watafiti na jamii.
Namna wanyamapori walivyo hatarini
“Tukio hilo linatia wasiwasi mkubwa na linaonyesha jinsi wanyamapori walivyo katika hatari kutokana na vitisho vinavyojitokeza bila kutarajiwa. Kila tembo ana mchango muhimu katika kudumisha afya ya mfumo wa ikolojia, na kupoteza idadi kubwa ya tembo kwa wakati mmoja, kunaathiri uimara wa mazingira yote,” Mkurugenzi wa IFAW nchini Kenya, Ben Wandago, aliiambia Mongabay.
Mkurugenzi Mtendaji wa Big Life Foundation, shirika la uhifadhi linalofanya kazi katika maeneo yanayomilikiwa na jamii ya Wamasai yanayozunguka Hifadhi ya Taifa ya Amboseli, Benson Leyian, aliiambia Mongabay kuwa juhudi za uhifadhi zinazoshirikisha jamii kwa miongo kadhaa zimeifanya Amboseli kuwa moja ya maeneo salama zaidi kwa tembo barani Afrika, huku kukiwa na mafanikio makubwa ya kutokomeza ujangili.
“Isipokuwa vifo vya tembo vinavyotokea wakati wa ukame mkali, eneo hilo halijashuhudia vifo vya tembo kwa kiwango hiki, jambo ambalo linaibua wasiwasi mkubwa,” alisema.
KWS imesema imeimarisha ulinzi na ufuatiliaji katika mfumo mzima wa ikolojia wa Amboseli na inaendelea kufuatilia kwa karibu idadi ya tembo. Aidha, hakuna kifo kingine cha tembo kilichoripotiwa katika wiki iliyopita.
Picha ya Bango: Kundi la tembo katika Hifadhi ya Taifa ya Amboseli, Kenya. Picha kwa hisani ya KWS.