- Teknolojia mpya ya kilimo cha mwani, hususan mfumo wa Double Made Loop (DML), imeongeza mavuno, kupunguza matumizi ya vigingi na kuwasaidia wakulima wa pwani ya Kwale kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.
- Wakulima wa mwani, wengi wao wanawake, wanasema mapato yatokanayo na zao hilo yameboresha maisha yao kwa kuwasaidia kusomesha watoto, kuongeza thamani ya bidhaa na kupanua masoko.
- Mbinu za kisasa za kukausha mwani na kuongeza thamani, pamoja na matumizi ya mitandao ya kijamii kama TikTok, zinawasaidia wakulima kufikia wanunuzi wengi zaidi na kuongeza kipato.
- Watafiti wa Taasisi ya Utafiti wa Bahari na Uvuvi Kenya (KMFRI)wanasema maendeleo ya sekta ya mwani yanategemea matumizi ya sayansi, teknolojia na mbegu zinazostahimili mabadiliko ya tabianchi ili kuhakikisha uzalishaji endelevu na faida za kiuchumi.
KWALE, Kenya – Kadri changamoto za soko zinavyoongezeka ndivyo wakulima wa mwani wanavyochangamkia mbinu mpya za uzalishaji na uuzaji wa mmea huo wa baharini.
Wakisaidiwa na utafiti, ubunifu na teknolojia, wakulima wa mwani katika vijiji vya Kibuyuni, Kijiweni, Mtimbwani na Changai, katika ukanda wa pwani wa Shimoni-Vanga, Kaunti ya Kwale, wameanza kuona matunda ya mbinu tofauti-tofauti wanazotumia baharini na hata katika kutafuta soko.
Marinda Masudi, mwenye umri wa miaka 40, ni miongoni mwa wakulima waliojitosa katika ukulima wa mwani kama njia moja ya kukidhi mahitaji ya familia yake. Ilimchukua muda kuamua kujiingiza katika kilimo hicho, lakini biashara yake ya mahamri ilipoanza kudorora, hakuwa na la ziada.

“Baada ya kujisajili na Kitengo cha Kusimamia Fukwe (BMU) cha Kibuyuni, nilionyeshwa sehemu ya kuanza kulima mwani, na baada ya takriban miezi miwili nilianza kuvuna mwani, kuukausha na kuuuza. Mapato niliyopata nilimsaidia mume wangu kuwasomesha watoto. Mara ya kwanza nilipovuna na kuuza mwani kutoka kwa bloki mbili, nilipata kima cha KSh30,000 ($230),” alisema Marinda.
Kama ilivyokuwa na wakulima wengine, alipoanza ukulima, walikuwa wakitumia mbinu ile ambayo imetumika tangu jadi, ambayo hufanyika katika maeneo karibu na ufuo wa bahari.
“Mkulima alihitajika kuingia msituni na kukata vigingi vingi vya kufungia kamba na kuweka mbegu. Kwa shamba moja la vipande sita, mtu alihitaji vigingi 300 kufanikisha ukulima wa mwani,” Marinda alieleza.
Mbinu ya jadi ilijulikana kama sikio moja au mfungo mmoja, yaani kufunga mbegu moja moja kwenye kamba.
Kwa mujibu wa kitabu “Sea Level Rise and Ocean Health in the Context of Climate Change” kilichochapishwa na IntechOpen mwaka 2024, na pia kama wanavyosema wakulima, ukulima wa mwani karibu na ufuo uko katika hatari kubwa kutoka kwa kuongezeka kwa joto la bahari. Hii inasababisha maambukizi ya ugonjwa wa ice-ice, ambao huathiri sana mazao.
Kupitia ujuzi na mafunzo, wakulima sasa wameanza kutumia mbinu wanayoita “masikio mawili”, ambayo pia wameipa jina la “kamatia chini”, ama “Double Made Loop (DML)”.
Kupitia mfumo huu, mavuno ya mwani huongezeka mara mbili na pia unatumia vigingi vichache kuliko ile ya mwanzo.
“Mbinu hii inataka maji mengi katika bahari. Unanyosha kamba kwenye vigingi kama 12 pekee badala ya 300, na kuufanya mwani kuning’inia kwenye maji na si kwa mchanga kama ilivyokuwa hapo awali. Mazao yake ni mara mbili zaidi kuliko yale ya mbinu ya zamani ya ukulima wa mwani inayofanyika karibu na ufuo wa bahari.
“Aina hii ya ukuzaji wa mwani ilianza kule Pemba, Tanzania kabla ya kuanza kutumika na wakulima wa Kenya mwaka 2024. Tulipatiwa mafunzo ya kutumia mbinu hii ya upandaji na mpaka sasa ndiyo hiyo ninayotumia katika shamba langu ambalo kwa sasa nimelazimika kuhamisha shamba langu kwenye eneo lenye maji mengi zaidi,” anasema Marinda.
Mfumo wa upandaji DML ni wa ubunifu na hutumia mbegu kwa umahiri. Unabadilisha taswira ya uzalishaji wa mwani wa wakulima wadogo-wadogo katika Afrika Mashariki, hususan Kenya na Tanzania.
Marinda, ambaye sasa anachanganya ukulima na kuongeza thamani ya mwani, anasema ule mfumo wa jadi ambao unafanyika karibu na ufuoni, wakulima hufunga mbegu kwenye kamba ndefu kwa kutumia kamba za plastiki. “Mbinu hii huchukua muda, kazi nyingi na mara nyingine kamba huachia au kuvunjika kutokana na mawimbi,” anasema.
Kilimo katika maji ya kina kirefu hupunguza kazi ngumu za kutembea kwenye maji ya kina kifupi na kuongeza mavuno kwa kuhamishia mwani kwenye maji yenye baridi zaidi.
Tima Mohamed, kutoka katika kijiji cha Kibuyuni, ni miongoni mwa wakulima wa mwani. Alianza safari yake kama kibarua wa shamba la dada yake. Baada ya kuvuna awamu ya kwanza, Tima alilipwa KSh20,000 ($155), pesa ambazo hakuwa ametarajia. Hapo ndipo akapata msukumo wa kuanzisha shamba lake dogo, akiwa na mumewe, kwa kutumia mbinu mpya ya ukulima wa mwani ya DML. Mavuno yao ya kwanza yaliwapatia KSh40,000 ($310).

Mwani ni mmea wa aina ya kipekee. Licha ya kutotambulika kwa sababu ya ulimaji wake baharini, mmea huo unaibuka kuwa nguzo muhimu katika uchumi wa samawati. Ukulima wa mwani ni chanzo muhimu cha mapato, hususan kwa wanawake. Zaidi ya asilimia 70 ya wakulima wa mwani ni wanawake, na wameifanya sekta ya ukulima wa mwani kuwa nguzo muhimu sana katika kuwawezesha wanawake kiuchumi ndani ya uchumi wa samawati.
Kuongezeka kwa mahitaji
Kadri mahitaji ya chakula na bidhaa zinazotokana na bahari yanavyoongezeka duniani, ndivyo umuhimu wa kutumia rasilimali za pwani kwa njia endelevu unavyozidi kuongezeka.
Ili kufikia mahitaji haya, shughuli za kilimo na ufugaji baharini zimeongezeka na moja ya maeneo yanayoibuka kama suluhisho ni ulimaji wa mwani kwa chakula na pia kama viungo katika chakula.
Hivi sasa wakazi wa Kibuyuni na vijiji vingine jirani, maeneo yaliyosheheni ukulima wa mwani, wanafurahia hali yao ya maisha inayozidi kuimarika kutokana na biashara hiyo.
Mwajumbe Mohamed, 25, pia amejitosa katika ukulima wa mwani kwa kutumia teknolojia ya kisasa licha ya kwamba baadhi ya wenzake wa rika lake wanaona anapoteza wakati wake kwa kazi ambayo inafanywa na wanawake wazee.

“Kilichonipa msukumo kupanda mwani ni kwamba ajira ilikuwa imekosekana baada ya kukaa nyumbani kwa miaka miwili tangu nimalize masomo yangu… badala ya kukaa nyumbani, niliamua kujiunga na akina mama katika upandaji wa mwani. Baadhi ya wenzangu wa rika moja wa kiume na kike waliniuliza kwa nini nijishughulishe na upandaji wa mwani ilhali nimeenda shule na kuhitimu,” alisema Mwajumbe.
Kwake, changamoto kubwa katika ukulima wa mwani ni nguvu kazi, hasa wakati wa kubeba na kugonga vigingi pamoja na kufanya kazi katika maji ya kina kirefu. Mara nyingi hulazimika kuwalipa wanaume kufanya baadhi ya kazi hizo.
Halima Nasoro, mkulima mwingine wa mwani anayetumia teknolojia ya kisasa, aliiambia Mongabay kuwa hapo zamani ukulima wa mwani ulikuwa wa wanawake pekee. “Nakumbuka wanaume walikuwa wakitusuta na kusema kwamba tunafanywa watumwa kwa kujishughulisha na mwani ambao bei yake ilikuwa duni sana,” anaeleza.
Lakini hivi sasa ameshuhudia mfano hai kupitia kwa wazazi wake. “Mama mzazi alianza ukulima wa mwani na ikafika mahali akamwambia baba aende kumsaidia kazi. Pindi alipopeleka mazao kwa soko na kupima, alikuwa anamgawia pesa mume wake. Hapo ndipo baba akang’amua kwamba kuna pesa katika zao hilo na ikamfanya na yeye kuanza kulima mwani katika sehemu yake tofauti. Hivi sasa wote ni wakulima hodari wa mwani,” aliongeza Halima.

Ingawa asilimia kubwa ya wakulima wa mwani ni wanawake, baadhi ya wanaume wamechukua nafasi hiyo, kwani wengine walisema ni bora kuwa na njia mbadala ya kupata kipato mbali na uvuvi.
Mmoja wa wanaume waliobobea katika upandaji wa mwani ni Abdalla Suleiman, ambaye kwa sasa ndiye mwenyekiti wa kikundi cha wakuza mwani Kijiweni. Alianza mwaka 2016 akitumia mbinu ya kupanda mwani kwa kutumia vijiti vingi kufunga mwani kwa kamba na kuweka mbegu.
Mabadiliko katika ukulima wa mwani
“Ukulima wa mwani umebadilika licha ya kuwa kumekuwa na mbinu tofauti-tofauti za upandaji. Mfumo huu wa kamatia chini unamaanisha kwamba mwani unazaa mara mbili zaidi.
“Katika ukulima huu, wakulima wamefundishwa mbinu bora za kusimamia mwani – Best Management Practices (BMP). Ni njia sahihi za kisasa za upandaji wa mwani, kutumia mbegu sahihi zinazokua vizuri, hazina magonjwa na huongeza uzalishaji maradufu,” alisema Abdalla.
Ufanisi wa ukulima wa mwani, alisema Abdalla, unaambatana na kufuatilia shamba. Yaani angalau kila baada ya majuma mawili, mkulima anafaa kwenda kuangalia hali ya shamba na kusafisha, na kuhakikisha kamba hazijafunguka.
Amiri Juma, mwenyekiti wa chama cha ushirika cha wakuzaji mwani Kibuyuni, anasema miongoni mwa mabadiliko ambayo yamefanya kilimo hicho kuchukua mwelekeo mpya ni teknolojia inayotumika, hususan katika kukausha mwani na kuongeza thamani.
“Katika kukabiliana na changamoto ya kukausha mwani na kutimiza viwango vinavyohitajika kukidhi matakwa ya soko la Kenya na hata la kimataifa, wakulima wa mwani sasa wanatumia mbinu ya kukausha kwa kutumia miale ya jua (solar dryer) ambayo ina uwezo wa kukausha mwani kwa muda mchache ikilinganishwa na mabanda ya kawaida ya kukaushia mwani.

“Mashine hiyo ililetwa pamoja na kiwanda mahsusi kwa kutengeneza bidhaa kutoka kwa mwani kupitia serikali kuu kwa gharama ya KSh10,000,000 ($77,200). Kifaa hicho cha kukaushia kwa kutumia miale ya jua kina uwezo wa kukausha kilo 400 kwa siku mbili ikilinganishwa na mabanda yanayochukua siku nne au tano. Kiwanda hicho pia kina sehemu ya kukausha mwani kwa kutumia umeme,” anasema Amiri.
Changamoto sasa ni kupata wanunuzi wa moja kwa moja, wa kununua mwani mbichi kama malighafi. “Lakini bei wanayotoa ni duni sana, hivyo basi kupitia kiwanda chetu tunatengeza bidhaa na kuuza, na kwa mwezi mmoja mapato hufikia takriban KSh1,000,000 ($7,722). Kutokana na mapato haya huwa tunachukua kama KSh400,000 – 500,000 ($3,089 – 3,861) kununua mwani kutoka kwa wakulima na kuwalipa moja kwa moja,” alisema Amiri.
Anafafanua kuwa wakulima wengi, kwa sababu wameanza kulima mwani kwa wingi katika maji mengi, sasa wanatumia mbegu aina ya Cottonii, ambayo watafiti wanasema ina thamani mara tatu ya ile mbegu inayojulikana kama Spinosum (Eucheuma denticulatum).
Kulingana na Tathmini ya Kimkakati ya Mazingira ya Ukulima wa Viumbe vya Baharini nchini Kenya, Spinosum, iliyokaushwa, huuzwa kwa takriban KSh25–30 kwa kilo, huku Cottonii ikiuzwa kwa KSh50-60 kwa kilo, ambayo ni karibu mara mbili. Ripoti hiyo inapendekeza kuendelea kwa utafiti kuhusu Cottonii kutokana na thamani yake kubwa zaidi ya kiuchumi.
Dkt David Mirera, mwanasayansi mtafiti kutoka Taasisi ya Utafiti wa Bahari na Uvuvi Kenya (KMFRI), anaeleza: “Ukulima wa mwani unaweza kuwa biashara yenye faida kubwa, lakini ukuaji wake lazima uongozwe na sayansi na teknolojia ya kisasa ili kuhakikisha uendelevu wa mazingira na manufaa ya kiuchumi.”
Mafanikio ya uzalishaji na mbegu
Alibainisha kuwa mafanikio ya uzalishaji yanategemea mbegu bora na kuongeza kuwa mbegu zilizopo zimeathiriwa na mabadiliko ya tabianchi, hivyo kuna haja ya kuendeleza mbegu imara inayokuwa haraka na kustahimili athari za tabianchi.
“Mabadiliko ya tabianchi yameleta changamoto mpya, ikiwemo kuongezeka kwa joto la bahari, na magonjwa kama ice-ice syndrome, yanayoweza kuharibu mashamba yote ya mwani. Ili kukabiliana na hali hii, KMFRI inachukua hatua mbalimbali, zikiwemo kuendeleza mbegu zinazostahimili mabadiliko ya tabianchi na kujenga vitalu vya mwani katika kina kirefu kupitia mradi wa Kenya Marine Fisheries and Socio-Economic Development (Kemfsed),” alisema Mirera.

“Kwa ujumla, juhudi hizi zinaweka msingi wa sekta imara ya mwani nchini Kenya, sekta inayoweza kuchangia katika uchumi wa samawati, kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, na kuboresha maisha ya jamii za pwani,” alisema Mirera.
Kwa Fatuma Madonga kutoka Kijiweni, ukulima wa mwani umemfundisha mambo mengi ambayo hapo awali alikuwa akiyachukulia kama mzaha.
Mfano mzuri anaoongelea ni matumizi ya mitandao ya kijamii kama mbinu moja ya kutafutia soko kwa bidhaa zao.
“Hivi sasa tunatumia mtandao hususan TikTok kutangaza bidhaa zetu na tumekuwa tukipata wateja kutoka Nairobi, wakinunua bidhaa zetu, hasa sabuni na shampoo,” alisema Fatuma.
Picha ya bango: Mbinu nyingine ya upandaji mwani kwa kutumia fito za mianzi na kamba kama kitanda kinachoolea, Kijiweni, Shimoni, Kaunti ya Kwale. Picha na Anthony Kimani.
Mbinu za uchakachuaji wa mwani zaongeza juhudi za kuimarisha soko nchini
