- Takriban watu milioni 15 walipatahuduma za upishi safi katika eneo la Kusini mwa Jangwa la Sahara barani Afrika mwaka wa 2025, na eneo hilo linatarajiwa kushuhudia upanuzi wake wa haraka zaidi kuwahi kutokea katika upatikanaji wa huduma za upishi safi mwaka 2026.
- Hata hivyo, watu bilioni moja wanaendelea kupika wakitumia nishati zinazochafua mazingira kama vile kuni, mkaa na mafuta ya taa, huku ukuaji wa idadi ya watu ukizidi maendeleo.
- Kati ya dola bilioni 2.2 zilizoahidiwa kuendeleza upatikanaji wa upishi safi barani Afrika katika Mkutano wa 2024 kuhusu Upishi Safi Afrika, dola milioni 740 zimetolewa katika nchi 30, kulingana na ripoti ya Shirika la Nishati la Kimataifa.
- Ripoti hiyo inakadiria kwamba Afrika inaweza kufikia upatikanaji wa huduma hizi kwa wote ifikapo mwaka wa 2040 iwapo italingana na viwango vya haraka zaidi vya kihistoria vya maendeleo, vinavyoungwa mkono na uwekezaji endelevu na sera imara, ila mgogoro unaoendelea wa Mashariki ya Kati umeshuhudia ongezeko la bei za gesi ya kupikia.
Eneo la kusini mwa Jangwa la Sahara liko njiani kurekodi upanuzi wake wa haraka zaidi kuwahi kutokea wa kila mwaka katika upatikanaji wa huduma za upishi safi mwaka wa 2026, kulingana na ripoti mpya ya Shirika la Nishati la Kimataifa. Lakini ukuaji wa idadi ya watu unaendelea kuzidi kasi ya maendeleo hayo, na kuwaacha zaidi ya watu bilioni moja bila huduma za upishi safi.
Kanda hiyo ni nyumbani kwa idadi kubwa zaidi ya watu duniani ambayo bado inategemea kuni, mkaa na mafuta ya taa kwa ajili ya kupikia kila siku, kulingana na shirika la IEA. Shirika la Afya Duniani (WHO) linasema uchafuzi wa hewa wa makazi, ambao mwingi wake huzalishwa na nishati hizi za kupikia zinazochafua mazingira, unahusishwa na vifo vya mapema takriban milioni 2.9 kila mwaka, huku wanawake na watoto wakibeba mzigo mkubwa zaidi.
“Upishi Safi Afrika 2026: Ripoti ya Maendeleo” inakadiria kuwa karibu watu milioni 15 walipata fursa ya kutumia upishi safi katika eneo la Kusini mwa Jangwa la Sahara mwaka wa 2025, karibu 35% zaidi ya wastani wa faida ya kila mwaka iliyorekodiwa kwa miaka mitano iliyopita. Ikiwa itathibitishwa, hii itakuwa ongezeko kubwa zaidi la kila mwaka kuwahi kurekodiwa. Côte d’Ivoire, Kenya na Nigeria zilipata faida kubwa zaidi.
Makadirio hayo yametokana na mfumo wa hisabati unaounganisha takwimu za uingizaji wa majiko (vifaa vya kupikia vinavyochanganya jiko la kawaida na oveni) na gesi ya petroli iliyoshinikizwa (LPG), uwekezaji katika miundombinu, nishati na teknolojia zinazohitajika kwa ajili ya upikaji safi, pamoja na ufuatiliaji wa sera.
Badala ya kutegemea tafiti za makazi, ambazo ndizo kipimo cha kuaminika zaidi cha upatikanaji wa huduma za upikaji safi lakini huchukua miaka mingi kukamilika, mfumo huo hutumia vyanzo hivyo kukadiria maendeleo ya upatikanaji wa huduma hizo. Hivyo, IEA ilisema kwamba takwimu za mwaka 2025 zinafaa kuchukuliwa kama za mapema hadi pale zitakapothibitishwa na tafiti za makazi zitakazofanyika baadaye.
Hata hivyo, Fatih Birol, Mkurugenzi Mtendaji wa shirika la IEA, amesema makadirio hayo ya hivi karibuni ni hatua muhimu ya mabadiliko kwa bara la Afrika.
“Kasi ya kusambaza huduma za upishi safi katika eneo la Kusini mwa Jangwa la Sahara barani Afrika sasa ni mara tatu ya kiwango kilichorekodiwa mwaka 2010,” ripoti hiyo ilisema. Katika mkutano wa ngazi ya juu uliofanyika Julai 9 ili kutathmini maendeleo tangu kufanyika kwa Mkutano wa Kilele wa Upikaji Safi barani Afrika wa mwaka 2024, Birol alielezea maendeleo hayo kama “habari njema sana.”
Karibu watu bilioni 2.1 ulimwenguni kote, takriban robo ya idadi ya watu duniani, bado wanapika juu ya moto ulio wazi au kwenye majiko yasiyofaa yanayochoma mafuta ya taa, mimea (kuni, samadi, taka za mazao) au mkaa, na hivyo kusababisha uchafuzi hatari wa hewa majumbani, kulingana na WHO. Mbinu hizi za kitamaduni za kupikia hufukisha takriban tani bilioni 1.2 za kaboni dioksidi sawa kila mwaka, ikiwa ni pamoja na uzalishaji unaohusishwa na uharibifu wa misitu. Kiasi hicho ni sawa na uzalishaji wa anga za kimataifa na usafirishaji wa meli pamoja, kulingana na IEA.
Asia Kusini, Asia ya Kusini-mashariki na Uchina, zilizojumuishwa kwa upana na IEA kama “Asia inayoendelea,” kihistoria zilikuwa na idadi kubwa zaidi ya watu duniani bila upatikanaji wa huduma za upishi safi. Hata hivyo, tangu mwaka wa 2010, watu bilioni 1.7 katika eneo hilo wamepata huduma za upishi safi, kwa kiasi kikubwa kutokana na programu za serikali nchini China, India na Indonesia, kulingana na ripoti ya IEA.
Afrika inaweza kufikia upatikanaji wa huduma hizi kwa wote ifikapo mwaka 2040 iwapo italingana na viwango vya haraka zaidi vya kihistoria vya maendeleo, vinavyoungwa mkono na uwekezaji endelevu na sera madhubuti, shirika hilo linakadiria. Akizungumza katika mkutano wa IEA, Rais wa Kenya William Ruto alisema kwamba kufikia upatikanaji wa upishi safi kwa wote, ambapo ni 32% tu ya wakazi wanatumia upishi safi na takriban watu milioni 38 wanakosa huduma za upishi safi, kutahitaji takriban dola bilioni 1.

“Tatizo la ufadhili linaendelea kuwa changamoto kote barani Afrika,” alisema. “Kuziba pengo la upatikanaji wa huduma za upishi safi barani kutahitaji uwekezaji kwa kiwango kikubwa; huku ufadhili wa kila mwaka ukisalia chini sana ya kile kinachohitajika.”
Katika Mkutano wa kwanza wa Upishi Safi Afrika, uliofanyika jijini Paris mnamo mwaka wa 2024, serikali, washirika wa maendeleo na mashirika binafsi yaliahidi dola bilioni 2.2 katika ufadhili mchanganyiko kwa ajili ya kupikia safi barani Afrika. Kufikia Juni 2026, takriban dola milioni 740 za kiasi hiki zilikuwa zimetolewa kwa miradi katika nchi 30 za Afrika, ripoti ya IEA inasema, huku 84% ikitoka kwa sekta binafsi na 16% kutoka kwa serikali.
Kenya ilichukua sehemu kubwa zaidi ya ufadhili (19%), ikifuatiwa na Uganda, Tanzania na Afrika Kusini kwa 7% kila moja.
Takriban theluthi mbili ya dola milioni 740 zilitumika kwa vifaa kama vile majiko ya kupikia na mitungi ya gesi ya LPG, huku sehemu iliyobaki ikigawanywa kati ya usaidizi wa kiufundi na maendeleo ya soko (14%), uwekezaji katika biashara za kupikia safi (13%), na miundombinu ya usambazaji wa mafuta, kama vile kuhifadhi na kuweka gesi ya LPG kwenye chupa (7%).
Kwa upande wa mafuta, karibu nusu ya ufadhili wote (49%) ulitumika kwa gesi ya LPG, dhidi ya 17% kwa majiko yaliyoboreshwa ya nishati ya mimea, 8% kila moja kwa ajili ya kupikia kwa umeme na biogesi, na 26% kwa ajili ya suluhisho za kupikia zinazotumia mafuta mbalimbali au usaidizi mtambuka kwa suluhisho tofauti za kupikia safi kama vile programu za bei nafuu.
LPG inachukuliwa kuwa mafuta safi ya kupikia chini ya miongozo ya WHO kwa sababu huwaka kwa usafi zaidi kuliko kuni, mkaa na mafuta ya taa, na kutoa viwango vya chini sana vya uchafuzi wa hewa hatari. Lakini pia ni mafuta ya visukuku, ikimaanisha kuwa si chaguo endelevu kwa muda mrefu kuliko kupikia kwa umeme na njia zingine mbadala zinazoweza kutumika tena.
Kwenye mkutano huo wa ngazi ya juu, Birol alisema kuwa shirika la IEA limefanikiwa kupata ahadi za ufadhili wa ziada wa dola milioni 900 tangu mkutano wa kilele wa Paris na kubaini kuwepo kwa sera mpya 120 zinazohusu upikaji safi kote barani Afrika.
Licha ya mafanikio hayo, shirika la IEA linaonya kuwa ongezeko la idadi ya watu linaendelea kufuta sehemu kubwa ya maendeleo yaliyopatikana.
“Ingawa kumekuwa na hatua muhimu ya mabadiliko, huku tukishuhudia kasi ikiongezeka katika upatikanaji wa njia safi za kupikia, bado tuko mbali na lengo tunalotaka kufikia,” alisema Birol, huku akiongeza kuwa familia nne kati ya tano barani Afrika bado zinategemea njia za zamani za kupikia.
Kwa mujibu wa ripoti ya IEA, idadi ya watu wasio na uwezo wa kupata huduma za upikaji safi katika eneo la Kusini mwa Jangwa la Sahara barani Afrika iliongezeka kwa takriban watu milioni 14 mwaka 2024. Ndani ya eneo hilo, ukanda wa Kusini mwa Afrika pekee ndio uliorekodi kupungua kwa idadi ya watu wasio na huduma hizo, huku Ukanda wa Afrika ya Kati ukishuhudia ongezeko kubwa zaidi.

“Karibu watu bilioni 2 duniani kote bado hawana upatikanaji wa suluhisho za upishi safi, nusu yao wakiwa Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara,” Damilola Ogunbiyi, Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Nishati Endelevu kwa Wote (SEforALL) linaloungwa mkono na Umoja wa Mataifa, aliambia Mongabay kupitia barua pepe.
Alisema kupanua upatikanaji wa umeme na kupikia safi kunapaswa kwenda sambamba badala ya kuchukuliwa kama malengo tofauti ya sera.
“Kwa kuunganisha kupikia kwa umeme katika juhudi za kitaifa za umeme na kutumia shule kama kitovu cha kuhamasisha matumizi ya upishi safi, nchi zinaweza kuharakisha utumiaji wa kupikia safi katika jamii nzima huku zikiongeza faida za kijamii, kiuchumi na hali ya hewa za kupanua upatikanaji wa umeme,” alisema.
Caroline Sawe, mtafiti wa nishati katika Taasisi ya Mazingira ya Stockholm katika Chuo Kikuu cha York, Uingereza, alisema ripoti hiyo ilionyesha kasi ya kutia moyo, lakini utekelezaji lazima uharakishwe ili kuendana na idadi ya watu inayokua kwa kasi barani Afrika.
“Upatikanaji wa nishati una jukumu kubwa katika kuwezesha kaya, na faida za kuhamia vyanzo vya nishati safi ni kubwa, hasa kwa mtazamo wa afya na uchumi,” alisema katika barua pepe kwa Mongabay.
Kwa kuzingatia kwamba takriban theluthi moja ya ufadhili ulioahidiwa kwa ajili ya kupikia safi barani Afrika umetolewa, Sawe alisema wafadhili wanaweza kuongeza zaidi usaidizi kwa ajili ya mpito kuelekea nishati safi ya kupikia ili kupunguza mzigo wa kiafya na kiuchumi unaohusiana na kupikia kwa kutumia biomasi.
Shirika la IEA lilisema mgogoro wa Mashariki ya Kati, hasa kufungwa kwa Mlango-Bahari wa Hormuz, umeweka hatari ya usalama wa usambazaji wa mafuta kwa mpito wa kupikia safi barani Afrika. Ingawa eneo hilo lina uwezekano mdogo wa kupata gesi ya LPG kutoka Ghuba ya Uajemi, usumbufu huo umesababisha kupanda kwa bei na uhaba mkubwa katika nchi kadhaa.
Licha ya kuwa mzalishaji wa tatu kwa ukubwa wa gesi barani Afrika, Nigeria, kwa mfano, bado inaagiza baadhi ya gesi yake ya kupikia. Wakati mgogoro wa Mlango wa Hormuz ulipotokea, bei zilipanda kote nchini, na kusukuma familia nyingi kurudi kwenye mkaa na kuni.
Uzoefu huo ulisukuma shirika la IEA kuanza kujenga mpango maalum wa usalama wa gesi ya LPG, unaozingatia uhifadhi, minyororo ya usambazaji, na uratibu wa sekta na serikali, Birol alisema.
“Hili ni muhimu sana kwa sababu tunahitaji kujenga uwezo wa kuhifadhi, kufanya kazi na sekta ya umma na binafsi, na kushirikisha nchi zilizoendelea kiuchumi pamoja na nchi za Afrika zinazotumia LPG kwa kiwango kikubwa,” alisema.
Shirika hilo limeanza mashauriano na wazalishaji na wauzaji wakuu wa gesi ya LPG, huku mpango huo ukitarajiwa kuendelea zaidi katika mkutano wa tasnia baadaye mwaka huu, aliongeza.
Picha ya juu: Wanawake na vijana wajasiriamali nchini Kenya wakipata mafunzo kuhusu mbinu za upishi safi. Picha kwa hisani ya UNDP Kenya kupitia Flickr (CC BY-NC 4.0).
Habari hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza hapa kwa lugha ya Kiingereza mnamo tarehe 20/07/2026.