- Malasen Hamida, mwanamke Muislamu kutoka jamii ya Wanubi katika mtaa wa Kibera jijini Nairobi, anatarajiakupata kiti katika Bunge la Kenya huku akiendeleza harakati zake za kutetea mazingira.
- Hamida alianzisha shirika laMazingira Women Initiative, lililojikita katika masuala ya usimamizi wa taka, kilimo cha kisasa, haki za kumiliki ardhi na uongozi wa wanawake.
- Alizungumza na Mongabay kuhusu historia ya jamii yake, ambayo ililetwa Afrika Mashariki kama askari katika kikosi chaKing’s African Rifles na kupewa eneo la hekta 1,698, eneo ambalo sasa limebaki na hekta 116 pekee.
- Anasema kuwaukweli kwamba Mazingira inaongozwa na wanawake ni mkakati wa kimakusudi: “Iwapo suala la mazingira litakuwa kipaumbele kwa mwanamke, atahakikisha linafanikiwa kwa sababu anajua halimnufaishi yeye pekee. Ni kwa ajili ya ustawi wa muda mrefu wa familia nzima.”
Malasen Hamida, mwanamke Muislamu kutoka jamii ya Wanubi katika mtaa wa Kibera, jijini Nairobi, ni mwanasiasa mtarajiwa na mwanaharakati wa mazingira mwenye uzoefu wa zaidi ya miaka 25 katika utetezi. Kibera, jina ambalo katika lugha ya Kinubi linamaanisha “ardhi ya misitu”, ndilo eneo kubwa zaidi la makazi yasiyo rasmi nchini Kenya; lililoko kwenye ardhi ambayo serikali ya ukoloni ya Uingereza iliitengea jamii ya Wanubi baada ya mababu zao kutumikia kama askari kwenye jeshi la King’s African Rifles. Awali, eneo hilo lilikuwa na ukubwa wa hekta 1,698 (ekari 4,197). Leo, kutokana na ukuaji wa miji, kufukuzwa kwa nguvu, uporaji wa ardhi na miradi mbalimbali ya serikali iliyotekelezwa kwa nyakati tofauti, ni hekta 116 (ekari 288) pekee zilizosalia mikononi mwa Wanubi, bila wao kuwahi kulipwa fidia yoyote.
Kupitia Mazingira Women Initiative, Hamida ametumia zaidi ya miaka 25 kujihusisha na masuala ya usimamizi wa taka, kilimo kinachotumia teknolojia za kisasa, haki za kumiliki ardhi, na uongozi wa wanawake. Pia amewahi kugombea ubunge mara tatu katika eneo bunge la Kibera na ana mpango wa kugombea tena mwaka wa 2027.
Hamida alizungumza na Mongabay mchana wa Jumamosi ya baridi, wakati alipokuwa akiondoka kwenye msikiti mkubwa zaidi katika eneo bunge la Kibera. Ofisi zake zilikuwa karibu, mwendo mfupi tu kutoka hapo. Tulipokuwa tukielekea huko, watu kadhaa walimsimamisha ili kumsalimia. Aliwajibu kila mmoja kwa kusema “Assalaamu aleikum,” akasimama kidogo ili kupiga nao gumzo, na akamshika msichana mdogo usoni kwa upole. Aliniongoza kupitia lango la mabati hadi kwenye eneo tulivu lenye nyumba zenye kuta za udongo na paa za mabati. Eneo hilo lilikuwa safi sana; hakukuwa na maji yaliyotuama wala takataka zilizoonekana, hali iliyo tofauti na mazingira ya kawaida katika mtaa wa Kibera. Tulikaa kwenye ukumbi wa nyumba yake.

Mahojiano haya yamehaririwa ili kuyafupisha na kuongeza uwazi.
Mongabay: Nirudishe nyuma kwenye ule wakati ulipoamua kuanzisha shirika la Mazingira Women Initiative. Ni yapi yaliyokuwa yakiendelea mtaani Kibera yaliyokufanya ufikiri: “Hili lazima liwepo, na lazima nilianzishe”?
Malasen Hamida: Nililelewa mtaani Kibera wakati ilipokuwa kijiji kizuri, chenye kijani kibichi na utulivu. Nakumbuka nyumba nyingi na miti mingi ya matunda kama parachichi, maembe, mikomamanga, mapera na mingine mingi. Kwa kuwa jamii yetu ilijishughulisha na ufugaji, pia tulijishughulisha na kilimo. Tulistawisha hata mimea yetu wenyewe ya viungo, kama vile giligilani (dhania).
Baada ya muda, ukuaji wa miji ulibadilisha kila kitu. Kadri matumizi ya ardhi yalivyobadilika kutoka ya kilimo hadi ya maendeleo ya makazi, changamoto za mazingira zilijitokeza. Usimamizi duni wa taka ndio uliokamilisha uharibifu wa uzuri wa Kibera. Mazingira ndiyo mchango wangu katika kujenga upya kile tulichokijua hapo awali kuwa Kibera. Nilianza kwa kuwahamasisha wanawake kusafisha mitaa na mifumo ya mifereji ya maji. Baadaye, tulianzisha kilimo kinachotumia teknolojia za kisasa, ikiwemo kilimo kisichotumia udongo (hydroponics), bustani wima na mbinu za kubadilisha taka kuwa rasilimali ambazo sasa zinasaidia bustani za jikoni. Leo, wanawake wanaweza kulima chakula cha kutosha kulisha familia zao na kuuza ziada. Kushuhudia mabadiliko hayo kumekuwa na manufaa makubwa.
Mongabay: Wewe ni Mnubi, kutoka katika jamii ambayo imekuwa ikiishi Kibera kwa vizazi vingi lakini mara chache imekuwa ikipewa kipaumbele katika mazungumzo kuihusu. Historia hiyo inachangiaje mtazamo wako kuhusu mgogoro wa kimazingira unaoendelea kukuzunguka?
Malasen Hamida: Mababu zetu waliletwa Afrika Mashariki wakiwa wanajeshi wa kikosi cha King’s African Rifles kutoka maeneo ambayo leo ni kusini mwa Misri na kaskazini mwa Sudan, ili kusaidia operesheni za kijeshi za Uingereza wakati wa Vita vya Kwanza na vya Pili vya dunia. Baada ya kumaliza huduma yao, walihamishiwa hapa kuishi. Tulikuwapo Kibera kabla ya Nairobi kuwa jiji ilivyo leo. Mwaka wa 1917, eneo letu lilipimwa na tukatengewa ekari 4,197. Kutokana na uporaji wa ardhi na kufukuzwa kwa nguvu, eneo letu limepungua hadi kufikia ekari 288, bila watu wetu kulipwa fidia yoyote.
Kutoka katika jamii ya wachache kumeathiri sana mtazamo wangu kuhusu masuala haya. Kwa miaka mingi baada ya uhuru, kulikuwa na dhana kwamba jamii ya Wanubi hawakuwa sehemu kamili ya Kenya. Hiyo ndiyo sababu wengi wetu tulijihusisha na harakati za utetezi, ili kuikumbusha nchi kuwa uwepo wetu hapa ni sehemu ya historia yake. Nikifikiria kuhusu majanga ya kimazingira huko Kibera, siwezi kuyatenganisha na masuala ya dhuluma za ardhi, kuhama makazi na kunyang’anywa mali. Kupungua kwa eneo la ardhi na ukuaji usio na mpangilio wa makazi vimebadilisha mazingira yenyewe pamoja na uhusiano wa watu na mahali wanapoita nyumbani.

Mongabay: Baada ya mlipuko wa bomu jijini Nairobi mwaka wa 1998, mambo yaliwabadilikia jamii ya Wanubi huko Kibera. Kipi kilibadilika hasa, na historia hiyo inahusianaje na mapambano ya kimazingira na ya ardhi ambayo umekuwa ukielezea?
Malasen Hamida: Kabla ya mwaka wa 1998, sisi tulikuwa tayari jamii inayopigania utambulizi. Baada ya mlipuko huo, tuligeuka kuwa jamii inayotiliwa shaka. Kwa sababu sisi ni Waislamu, kwa sababu majina yetu yanafanana na ya Waarabu au Wasomali, na kwa sababu lugha yetu ina mdundo wa Kiarabu (lugha ya Kinubi ni lugha iliyotokana na Kiarabu cha Sudan), serikali ilianza kutuchukulia kama suala la kiusalama badala ya watu wenye historia na makazi. Mimi nilipata kitambulisho changu kabla ya hayo yote kutokea; wenzangu hawakuwa na bahati hiyo.
Ili kupata kitambulisho cha taifa, cheti cha kuzaliwa, pasipoti, na nyaraka ambazo kila Mkenya ana haki ya kuwa nazo, watu wa jamii yangu walilazimika kupitia mchakato mkali wa uhakiki. Walipaswa kuthibitisha uhalali wa uwepo wao. Walipaswa kuthibitisha kuwa wao ni raia wa Kenya. Hebu fikiria kutakiwa kuthibitisha kuwa wewe ni raia wa nchi ambayo babu yako alisaidia kuijenga, kwenye ardhi ambayo familia yako imekuwa ikiishi kwa zaidi ya karne moja, na katika jiji ambalo ulikulia ukiwa hapo. Hilo ndilo tulilolazimika kufanya.
Na ndiyo maana mapambano ya uhifadhi wa mazingira na mapambano ya haki za uraia si mambo mawili tofauti. Iwapo huwezi kupata nyaraka rasmi, huwezi kumiliki ardhi kisheria, huwezi kupiga kura, na huwezi kuhesabiwa. Unakuwa mtu asiyeonekana machoni pa serikali, isipokuwa pale serikali inapokuona kama tishio. Hivyo, ninapozungumzia mgogoro wa mazingira wa Kibera, ninazungumzia pia jamii ambayo imefanywa isiweze kuonekana kwa makusudi na kwa utaratibu maalum. Kusafisha mitaa, kuzalisha chakula, na kuwahamasisha wanawake, hizi pia ni njia tunazotumia kusisitiza uwepo wetu na kuhakikisha tunaonekana.
Mongabay: Kwa nini ulichagua kimakusudi kuanzisha mradi unaoongozwa na wanawake? Ni kipi kilikufanya uone kuwa wanawake ndio walipaswa kuongoza mpango huu?
Malasen Hamida: Wanawake ndio wahusika wakuu katika usimamizi wa taka. Katika uzalishaji wa chakula, wanashughulika na malighafi pamoja na taka zinazotokana nazo. Wakiwa wasimamizi wa makazi, takwimu zinaonyesha kuwa wanawake ndio kundi kubwa zaidi la wamiliki na wasimamizi wa mashamba madogo nchini Kenya na mara nyingi ndio wanaosimamia usimamizi wa taka katika makazi yao.
Kuwalenga wanawake ilikuwa hatua ya kimkakati kwa sababu ni njia ya kuingia katika masuala ya udhibiti wa taka, uzalishaji wa chakula, na uwezeshaji wa kiuchumi. Iwapo suala la kimazingira litapewa kipaumbele kwa mwanamke, atahakikisha linafanikiwa kwa sababu anajua kuwa si kwa ajili yake pekee, bali ni kwa ajili ya ustawi wa muda mrefu wa familia nzima. Ikilinganishwa na wanaume, ambao huona udhibiti wa taka kama kazi ya muda mfupi hadi pale watakapopata kazi nyingine, kwa wanawake hii ni ahadi endelevu na hapo ndipo tunapopata fursa yetu kuu ya kufanikisha malengo.

Mongabay: Ni hali gani wanawake wa Kibera hukumbana nazo kuhusiana na mazingira, mafuriko, na taka, ambazo wanaume wanaoishi katika makazi hayo hayo hawakumbani nazo kwa namna hiyo hiyo?
Malasen Hamida: Wanawake hubeba mzigo mkubwa kwa sababu kwa kawaida wanawajibika kusimamia makazi yao. Mifumo mibovu ya mifereji ya maji iliyojaa taka husababisha mafuriko makubwa ndani ya nyumba. Wanawake huwa wa kwanza kushughulikia maji yanayoingia ndani ya nyumba, kupunguza athari za haraka, na kuhakikisha watoto wako salama.
Pia kuna mzigo maalum wa kiafya. Uchafuzi wa mazingira husababisha kuenea kwa magonjwa, na wanawake mara nyingi huwa wasimamizi wakuu wa afya ya nyumba zao na huduma za kinga. Iwapo mazingira yamechafuliwa, hawawezi kuwalinda watoto wao kutokana na magonjwa yanayotokana na uchafuzi huo. Mvua inaponyesha, naona vijito vyembamba vikibadilika kuwa mafuriko makubwa yanayobomoa nyumba na kuchukua maisha. Kupitia Mazingira, tunapanga usafi wa dharura ili kuzibua mifereji ya maji ili maji yaweze kupungua, na tunahimiza uvunaji wa maji ya mvua kwa mashamba yetu ya kisasa [mifumo inayotumia nafasi vizuri ambayo hutumia bustani zilizo wima, teknolojia ya kuchakata maji na ubadilishaji wa taka kuwa mboji ili kukuza chakula ambapo kilimo cha kawaida hakiwezi], kwa sababu ingawa wengi wanaona mvua kama janga, baadhi yetu tunaofanya kilimo cha mijini tunafahamu pia ni rasilimali.
Mongabay: Kilimo cha bustani majumbani na udhibiti wa taka mara nyingi hupuuzwa na kuonekana kama masuala madogo au ya ngazi ya makazi tu. Una maoni gani kuhusu ukubwa na umuhimu wa kazi hii, hasa ikizingatiwa kuwa mijadala mikubwa kuhusu sera za mabadiliko ya tabianchi mara chache sana huhusisha jamii kama vile za Kibera?
Malasen Hamida: Watu wanaweza kuiita hii kuwa ndogo, lakini kwetu sisi, huu ndiyo msingi. Tunabadilisha taka za chakula kuwa samadi na taka za makaratasi kuwa briketi za mkaa [kwa matumizi ya nyumbani na kuuzwa], jambo ambalo linatuzuia kukata miti na kuunda ajira za kijani kwa vijana na wanawake. Kwa sababu ardhi yetu imebanwa na kuchukuliwa kutoka kwetu, tunatetea kilimo kinachotumia teknolojia za kisasa ili kuhakikisha usalama wa chakula kwa familia ambazo hazina mahali pa kulima. Tumeshirikiana hata na Umoja wa Ulaya na muungano wa We World kujenga nyumba ya kitalu (greenhouse) katika moja ya shule zetu ili watoto waweze kujifunza ujuzi huu moja kwa moja.
Hii pia ni huduma ya afya ya msingi. Kudumisha mazingira safi na yaliyotunzwa vyema ni huduma ya kinga kwa sababu huzuia magonjwa kabla hayajaanza. Hata hivyo, jiji la Nairobi limetengwa kutoka kwa fedha za kupunguza makali kama FLoCCA [Ufadhili wa Hatua za Hali ya Hewa Zinazoongozwa na Wakazi], mara nyingi kwa sababu watunga sera hawaoni hali halisi ya msingi wa mapambano yetu. Mazungumzo ya hali ya hewa duniani yanazingatia zaidi misitu na ardhi za vijijini pekee, huku tukipuuza jinsi taka ngumu za mijini zinavyoweza kugeuzwa kuwa hifadhi ya kaboni inayowanufaisha maskini wa mijini. Uwezo ni mkubwa. Uelewa haupo kabisa.

Mongabay: Umewania nafasi ya kisiasa mara tatu. Watu wengi wangeachana na jambo hilo baada ya kushindwa mara moja. Ni kipi kinachokupa msukumo uendelee kujitosa katika uchaguzi?
Malasen Hamida: Kukata tamaa si chaguo. Huenda nikahisi kutaka kukata tamaa, lakini ninapotoka nje, nakutana na mtu anayeuliza, ‘Mama Mazingira, tufanye nini kuhusu hili?’ Kukata tamaa kungemaanisha kuwatelekeza watu wangu, kuacha ndoto zangu na kuzinyamazisha sauti zinazopata nguvu kupitia mimi.
Safari yangu ya kisiasa ilianza moja kwa moja kutokana na harakati za kutetea maslahi ya jamii. Wakati nikitoa elimu ya uraia kuhusu Katiba ya mwaka 2010, nilishuhudia Eneo Bunge la Lang‘ata lililogawanywa na kuwa maeneo ya Langata na Kibera, na nikaona fursa ya kuiwakilisha jamii ya Wanubi; hii ni kwa sababu katika Katiba hiyo mpya [iliyozinduliwa mwaka 2010], jamii yangu haikutambuliwa chini ya mfumo wa hatua maalum za kuwapa nafasi makundi yaliyotengwa (hatua chanya). Baraza la Wazee limekuwa likiniunga mkono kila mara; katika kila mwaka wa uchaguzi, hufanya mchakato wa kuchuja wagombea wote, na nimefanikiwa kupita katika mchakato huo kila wakati. Changamoto kubwa imekuwa idadi na usambazaji wa watu. Jamii ya Wanubi ni wachache ndani ya Kibera, jambo linalofanya iwe vigumu kuhamasisha wapiga kura. Hata hivyo, kupitia kampeni tatu, nimeweza kujenga uelewa na kuonekana katika masuala ya haki ya kimazingira, na hatua kwa hatua jambo hili linazidi kupata msukumo.
Ninaamini jambo halijakamilika hadi litakapokamilika.
Mongabay: Kama utashinda mwaka wa 2027, ni kipi kipaumbele cha kwanza kuhusu mazingira?
Malasen Hamida: Kipaumbele changu kingekuwa ni kutekeleza Sheria ya Usimamizi Endelevu wa Taka ya mwaka 2022 katika ngazi ya mashinani, kwa kuweka mifumo iliyo wazi na inayotekelezeka katika ngazi ya jamii. Pia, nataka kuchunguza namna jamii za mijini zinavyoweza kunufaika na masoko ya kaboni na kugeuza taka ngumu kuwa rasilimali ya kiuchumi. Masoko ya kaboni hayapaswi kunufaisha misitu ya vijijini pekee; jamii kama yetu, ambazo zimetengwa katika upatikanaji wa fedha za kushughulikia mabadiliko ya tabianchi, zinapaswa kujumuishwa waziwazi katika mazungumzo yajayo kuhusu ufadhili wa hatua za kukabiliana na changamoto hiyo.
Mongabay: Ungependa wasomaji walio nje ya Kenya na nje ya makazi yasiyo rasmi wafahamu nini kuhusu wanawake wanaofanya kazi hii ya uhifadhi kimyakimya, bila ruzuku, bila majukwaa, na bila kutambuliwa?
Malasen Hamida: Wanawake hawa si tu washiriki katika mpango fulani. Wao ndio nguzo kuu za jamii yetu. Katika baadhi ya maeneo yenye msongamano mkubwa zaidi duniani, wao hubuni mbinu mpya, kama vile bustani za wima na kilimo kisichotumia udongo ili kuhakikisha watoto wao wanapata chakula wakati ambapo hakuna tena ardhi ya kutosha kwa ajili ya kilimo. Wanachukulia taka kama rasilimali. Wanatengeneza ajira rafiki kwa mazingira na biashara zenye tija kutokana na vitu ambavyo wengine huviita takataka. Lakini bado hawashirikishwi katika mijadala ya kimataifa kuhusu soko la kaboni na ufadhili wa masuala ya tabianchi.
Baada ya miaka kumi kuanzia sasa, nataka wanawake wa Mazingira waseme kuwa mpango huu uliwapa uhuru wa kiuchumi na heshima inayotokana na kujitegemea. Nataka waseme kuwa uliwapa uwezo wa uongozi, sauti, na ujasiri wa kuwasilisha hoja kuhusu uhifadhi wa mazingira katika majukwaa yoyote. Na nataka waseme kuwa walishiriki kikamilifu katika kurejesha hadhi ya Kibera, ili kizazi kijacho kirithi makazi yaliyojaa kijani na yanayofaa zaidi kwa maisha kuliko yale tuliyokabidhiwa sisi.
Huenda dunia ikawa haitilii maanani juhudi zao. Lakini kazi wanazofanya zinatengeza mustakabali wa haki ya kimazingira.
Picha ya bango: Kupitia Mazingira Women Initiative, Malasen Hamida ametumia miaka mingi akijishughulisha na masuala ya usimamizi wa taka, kilimo kinachotumia teknolojia za kisasa, haki za ardhi na uongozi wa wanawake. Picha kwa hisani ya Malasen Hamida.
Habari hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza hapa kwa lugha ya Kiingereza mnamo tarehe 14/07/2026.