DAR ES SALAAM, Tanzania – Katika moja ya eneo la uzalishaji wa lava wa nzi chuma (Black Soldier Fly Larvae) Jijini Dar es Salaam, yanaonekana matenga yaliyopangwa kwa safu, maelfu ya lava wenye rangi ya kijivu wakijongea juu ya mabaki ya chakula yaliyooza.
Ingawa wadudu hawa wanaonekana kama funza wa kawaida, lava wa nzi chuma wameanza kuchukuliwa kama sehemu ya suluhisho la tatizo linalozidi kukua la udhibiti wa taka oza katika maeneo ya miji mikubwa kama Dar es Salaam.
Kadri miji inavyoendelea kupanuka, ndivyo changamoto ya usimamizi wa taka inavyozidi kuwa kubwa.
Dar es Salaam, jiji kubwa zaidi nchini Tanzania na moja ya miji inayokua kwa kasi zaidi Afrika Mashariki, ni mfano halisi wa changamoto hiyo, ambapo kwa mujibu wa ripoti ya Dar es Salaam Urban Resilience Programme (DURP) ya mwaka 2024, jiji hilo huzalisha takribani tani 5,300 za taka ngumu kila siku.

Asilimia 72 ya taka hizo, sawa na takribani tani 3,800 huishia katika madampo au maeneo yasiyo rasmi ya kutupia taka. Matokeo yake imekuwa kuongezeka kwa harufu mbaya, kuzaliana kwa wadudu, kuziba kwa mifereji ya maji na uzalishaji wa gesi chafu zinazochangia mabadiliko ya tabianchi.
Lakini wakati mamlaka za mijini zikihangaika kutafuta njia za kukabiliana na tatizo hilo, teknolojia inayotumia lava wa nzi chuma inaanza kuonyesha uwezekano wa kubadili taka oza kuwa rasilimali.
Kutoka taka za kikaboni hadi rasilimali
Lava wa nzi chuma ni wadudu wanaojulikana kwa uwezo wao wa kula na kuvunja mabaki ya chakula yanayooza kwa kasi kubwa.
Wataalamu wa mazingira wanaeleza kuwa wadudu hao hubadilisha taka za kikaboni (ambazo huwa na athari nyingi hasi kwenye mazingira) kuwa biomasi yenye protini na mafuta, huku mabaki yakitumika kama mbolea ya asili.
Kiwanda cha Mboji cha Mabwepande kilichopo Manispaa ya Kinondoni jijini Dar es salaam, ni mfano halisi unaoonyesha mchakato wa kubadilisha taka oza hizo kuwa chakula cha mifugo na mbolea.

Jimson Mkenda, Mhandisi wa kiwanda hicho anasema taka zinazotoka kwenye masoko mbalimbali likiwemo soko la Tegeta na baadhi ya viwanda.
“Baadhi ya taka tunazipeleka kwenye mashine ya kusaga, tukishazisaga, tunaziweka kwenye mabeseni makubwa kwa ajili ya kwenda kuwalisha wale funza wadogo…Wakikua, asilimia 90 tutawakausha kwa ajili ya kuwauza kama protini mbadala, na asilimia 10, tunawabakisha kwa ajili ya kuendeleza mchakato,” Mkenda aliiambia Mongabay katika mahojiano maalum.
Kwa mujibu wa Jimson, kiwanda hicho kilichoanza kufanya kazi tangu mwaka 2021, kina uwezo wa kupokea hadi tani 50 za taka kwa siku. Hii inamaanisha kuwa kila siku, taka nyingi ambazo kama zingeachwa, zingetapakaa na kuleta uharibifu kwa mazingira, zinarejezwa na kupata matumizi mengine.
“Hili linasaidia kwanza taka zisizagae katika mazingira yetu na kuleta athari. Lakini kikubwa zaidi inapunguza hewa ukaa kwa sababu taka oza hutoa methani ambayo inaharibu mazingira,” anasema Jimson.
Mohamed Mussa, mtaalamu wa mazingira na mashine za urejeleshaji wa taka, anaelezea zaidi uwezo wa lava wa nzi chuma wa kurejesha thamani ya mabaki ya chakula.
“Gramu moja ya lava nzi chuma inaweza ikala karibu kilo kumi za taka oza ndani ya siku 14. Kwa maana nyingine kilo moja ya lava wa nzi chuma inaweza kuchakata tani kumi za taka kwa siku 14 tu,” anafafanua Mohamed.
Manufaa kwa mazingira
Faida ya kwanza ya teknolojia hii ni kwamba inasaidia kupunguza taka oza ambazo ni hatari kutokana na uwezo wake wa kuzalisha gesi ya methani, hewa chafu ambayo huchangia kwa kiasi kikubwa ongezeko la joto duniani.
Faida nyingine ya teknolojia hiyo inayotumia wadudu ni kwamba mchakato wake mzima unafanywa kwa namna ambayo ni rafiki kwa mazingira.
“Wakichakata hicho chakula, hakuna chochote kinachotupwa. Hao wadudu wakishakuzwa, tunapata viini lishe kupitia miili yao, pia tunapata mbolea ya asili ambayo inatumika mashambani bila kuleta athari kwa mazingira lakini pia teknolojia hiyo inasaidia kupunguza hewa ukaa katika mazingira,’’ anasema Mohamed.
Uwezo wa lava wa nzi chuma katika kuchakata taka oza umeendelea kuvutia watafiti na wataalamu wa mazingira duniani. Utafiti wa Ankit Kumar, Anshika Singh na Dkt Kanchan Kumari kutoka taasisi ya CSIR-National Environmental Engineering Research Institute (CSIR-NEERI), uliochapishwa mwaka 2025 katika jarida la Waste and Biomass Valorization ulibainisha kuwa lava wa nzi chuma wanaweza kupunguza kati ya asilimia 65 hadi 80 ya taka oza huku wakizigeuza kuwa biomasi yenye thamani.

Ingawa teknolojia ya lava wa nzi chuma bado haijasambaa kwa kiwango kikubwa nchini Tanzania, juhudi za kuiendeleza zinaanza kuonekana. Januari 28, 2026 Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kilizindua mradi wa teknolojia hii, kubadilisha taka oza kuwa chakula cha mifugo chenye virutubisho pamoja na mbolea.
Chuo hicho kilibainisha kuwa mradi huo unalenga kuboresha usimamizi wa taka, kupunguza uchafuzi wa mazingira, kuunda ajira za kijani na kuongeza thamani ya taka ambazo zingetupwa.
“Mabadiliko makubwa yanayotarajiwa ni pamoja na madampo yetu kutojaa taka oza. Pia utoaji wa hewa ukaa utapungua kwa kiasi kikubwa, watu wengi watafahamu kuwa taka ni mali na wataaanza kuzigombania, hali itakayosaidia kuzagaa kwa taka kupungua,’’ anasema Mohamed.
Wazalishaji wadogo wavutiwa
Mbali na miradi mikubwa, teknolojia ya lava wa nzi chuma imeanza kuvutia wazalishaji wadogo wanaoiona kama njia ya kutatua changamoto mbili kwa wakati mmoja; uchafuzi wa mazingira unaotokana na taka oza na gharama za chakula cha mifugo.
Dango Muhina ni mmoja wao. Yeye na mwenzake Mohamed Musa, katika mradi wao mdogo uliopo Msewe kata ya Ubungo jijini Dar es Salaam, hukusanya taka oza kutoka majumbani, masokoni na maeneo mengine na kuzitumia kama chakula cha lava wa nzi chuma.
“Taka ambazo zimeoza na nyingine kuanza kuleta harufu kutoka majumbania na sehemu nyingine, tunazikusanya pamoja, kuzihifadhi na kuzitumia kuwalisha hao wadudu. Wanajipatia chakula na mazingira yanakuwa salama,” alisema Dango alipohojiwa na Mongabay.
Dango anasema tangu alipoanza mradi huo miezi minne iliyopita, ameshuhudia lava wa nzi chuma wakisaidia kupunguza taka oza huku wakizalisha rasilimali nyingine zenye manufaa.
Anasema awali lengo lake lilikuwa kupata chakula cha kuku, lakini baadaye aligundua kuwa teknolojia hiyo inaweza kuwa na mchango mkubwa zaidi katika kuhifadhi mazingira.
Kwa sasa hukusanya takribani kilo 30 za taka kwa siku, kiwango ambacho anaamini kitaongezeka kadri shughuli zinavyokua.
“Kwa sasa hivi ni kitu ambacho watu wengi sana wanakishangaa. Mwanzoni watu walikuwa wanashtuka lakini kadri siku zinavyosogea, watu wameanza kuelewa na mitazamo yao imeanza kubadilika,” anasema Dango.
Bidhaa zinazotokana na lava wa nzi chuma zimeanza kuvutia pia wafugaji katika maeneo mbalimbali ya Dar es Salaam kutokana na kuwa chanzo mbadala cha protini kwa kuku, samaki na mifugo mingine, pamoja na kuzalisha mbolea ya asili.
Benedict Mbwiga wa Mbezi anasema kuwa matumizi ya lava wa nzi chuma yamekuwa sehemu ya mkakati wake wa kupunguza gharama za uzalishaji.
“Lengo ni kupunguza gharama za uzalishaji, kwa sababu kwenye ufugaji, mifugo inahitaji vyakula vya aina tatu, protini, wanga na madini. Kutokana na gharama za vyakula vya aina hiyo, inabidi tujiongeze kwa kutumia lava wa nzi chuma,” amesema Benedict.
Msimamo wa Serikali
Mamlaka zimeanza kuingiza teknolojia ya lava wa nzi chuma kwenye mipango ya muda mrefu ya usimamizi wa taka katika maeneo ya miji.
Afisa Usafishaji na Mazingira wa Manispaa ya Kinondoni, Shedrack Maxmillian ameeleza kuwa manispaa imeanza kujenga mifumo ya kutumia taka oza kupitia miradi ya taka sifuri.
“Tunajenga taratibu mifumo ya kutumia taka oza, kwa maana ya miradi ya ‘Zero Waste’ kikiwemo kiwanda chetu cha Mabwepande. Pia kuna kiwanda binafsi kinachoitwa Chanzi kilichopo kata ya Wazo na tunaendelea kujenga vingine maeneo ya Mbweni,” Shedrack aliiambia Mongabay.
Mbali na hilo, manispaa imepanga kupeleka miradi hiyo katika shule na vikundi vya kijamii ili kuongeza ushiriki wa wananchi. Anasema hadi sasa wako kwenye maandalizi ya kujenga miradi ya taka sifuri kwenye shule nne, miradi ambayo itajihusisha na teknolojia ya lava wa nzi chuma.

“Vikundi vya vijana na wanawake jijini Dar es salaam vimeendelea kuhamasishwa kuingia katika uzalishaji wa lava wa nzi chuma kama njia ya kujiongezea kipato na kusaidia usimamizi wa taka oza na kutunza mazingira,” anasema.
Changamoto
Licha ya mafanikio yaliyoanza kuonekana, wadau wa sekta ya mazingira wanaamini bado kuna haja ya kuongeza elimu kwa umma, kuimarisha mifumo ya ukusanyaji wa taka na kuweka mazingira yatakayochochea uwekezaji zaidi katika teknolojia hiyo.
“Pamoja na fursa zake, bado kuna changamoto kadhaa zinazozuia matumizi yake kwa kiwango kikubwa. Uelewa mdogo kuhusu teknolojia hii miongoni mwa wananchi, wawekezaji na watunga sera,’’ anasema Wilyhard Shishikaye, Meneja wa Zero Waste Project.
Anataja changamoto nyingine kuwa ni ukosefu wa mifumo bora ya kutenganisha taka kwenye chanzo, jambo linalopunguza ubora wa taka zinazofaa.
Mafanikio zaidi
Wadau wa mazingira wanaamini kuwa mafanikio ya teknolojia ya lava wa nzi chuma hayatategemea uwezo wa wadudu hao pekee, bali pia hatua zitakazochukuliwa na serikali, sekta binafsi na jamii katika kuifanya kuwa sehemu ya mfumo rasmi wa usimamizi wa taka.
“Kuandaa sera na kanuni zinazotambua na kuhamasisha matumizi ya lava wa nzi chuma na kutoa motisha za kifedha na kikodi kwa wawekezaji wa teknolojia za uchumi mzunguko, vinaweza kusaidia kuharakisha matumizi ya lava wa nzi chuma na uwekezaji katika viwanda vya kuchakata taka oza na kuzigeuza kuwa bidhaa zenye thamani ya kiuchumi,’’ anasema Wilyhard.
Mbali na utoaji wa elimu kwa umma, Wilyhard amehimiza ushirikiano kati ya kampuni binafsi na halmashauri katika ukusanyaji na uchakataji wa taka, akisema kuwa hilo linaweza kusaidia kuongeza kiwango cha taka zinazorejelezwa badala ya kuishia kwenye madampo.
Kwa sasa, katika baadhi ya maeneo ya jiji la Dar es Salaam, mabaki ya matunda, mboga na vyakula vilivyooza ambayo zamani yangeishia dampo yanaanza kupata matumizi mapya kwa kugeuzwa kuwa protini kwa ajili ya mifugo, mbolea kwa ajili ya kilimo na sehemu ya suluhisho ya changamoto ya taka oza.
Lakini swali linalobaki ni kama teknolojia hiyo itaweza kupanuliwa kutoka miradi michache iliyopo na kuwa sehemu ya mfumo mpana wa usimamizi wa taka katika maeneo ya miji nchini Tanzania.
Picha ya Bango: Mmoja wa wafanyakazi wa Manispaa ya Kinondoni akipakia taka oza pamoja na matunda ambayo yanatarajiwa kupelekwa katika Kiwanda cha Mabwepande. Picha kwa hisani ya Kiwanda cha Mabwepande.