- Kulinda bahari si kazi ya BMU pekee, bali ni wajibu wa kila mwananchi.
- Kuanzishwa kwa BMU 11 kumechangia kupungua kwa uvuvi haramu.
- Sasa samaki, pweza wameongezeka na viumbe wengine wameanza kuzaliana tena.
- Mafanikio ya kurejesha uhai wa bahari yametokana na ushirikiano wa wadau.
Miaka minne iliyopita, ikolojia ya bahari katika kijiji cha Namakongoro kilichopo katika Kata ya Limaliyao, Wilaya ya Kilwa, Mkoa wa Lindi, kwenye ukanda wa kusini wa Bahari ya Hindi, ikiwamo matumbawe, nyasi bahari na mikoko iliharibika vibaya kutokana na kukithiri kwa matukio ya uvuvi haramu hasa wa kutumia vilipuzi kama baruti.
Hali hiyo ilisababisha uharibifu mkubwa wa makazi ya viumbe baharini, hivyo kupunguza idadi ya samaki, pweza na viumbe wengine wanaotegemea mazingira hayo kuishi na kuzaliana. Baadhi ya viumbe walihamia kwenye maeneo yenye kina kirefu, jambo lililovuruga mfumo wa ikolojia wa bahari na kupunguza bioanuwai.
Hata hivyo, tangu mwaka 2021 hali ilianza kubadilika kufuatia juhudi za pamoja za jamii, Serikali, Kitengo cha Usimamizi Shirikishi wa Ufukwe (BMU) na taasisi ya Sea Sense, inayojihusisha na uhifadhi wa mazingira ya bahari na ukanda wa pwani, kuanzisha mikakati ya uhifadhi wa bahari.

Juhudi hizo zimeleta mabadiliko makubwa ikiwa ni pamoja na kusaidia kurejesha matumbawe, kuongeza wingi wa samaki waliokuwa wamepungua pamoja na kupungua kwa kiwango kikubwa kwa uvuvi haramu.
Kurejesha uhai wa bahari
Mafanikio ya kurejesha uhai wa bahari Namakongoro yametokana na ushirikiano wa karibu kati ya wanakijiji, Kitengo cha Usimamizi Shirikishi wa Ufukwe (BMU), Sea Sense na Serikali.
Baada ya kubaini kuwa chanzo kikuu cha uharibifu huo kilikuwa ni uvuvi haramu, taasisi ya Sea Sense iliingia katika kijiji cha Namakongoro. Mratibu wa Mradi wa Sea Sense, Bernard Kaitira, anasema ili kuweka mifumo mizuri ya uongozi, walianzisha Kitengo cha Usimamizi Shirikishi wa Ufukwe (BMU).
Kaitira anasema baada ya BMU kuanzishwa waliwapatia viongozi mafunzo kuhusu umuhimu wa kuhifadhi matumbawe, mikoko na nyasi bahari pamoja na mbinu endelevu za usimamizi wa bahari.
Anasema hatua iliyofuata ilikuwa kuhakikisha wavuvi wote wanasajiliwa na kupata leseni ili watambulike na iwe rahisi kuwachukulia hatua wale wanaokiuka sheria.
“Tuligundua wavuvi wengi walikuwa hawafuati sheria za uvuvi endelevu kutokana na uelewa mdogo. Lakini pia hawakuwa wanawajibishwa kisheria, hivyo tukaanza kwa kuwasajili na kuwapa leseni pamoja na elimu ya uhifadhi,” anasema.
Mbali na hilo, Sea Sense iliwawezesha kutengeneza mpango wa usimamizi wa BMU wa miaka mitano, kuwapatia vifaa vya doria ikiwamo boti, mafuta na tochi pamoja na kuwasaidia kuanzisha vikundi vya kuweka na kukopa ili kuwapa wananchi vyanzo mbadala vya kipato.
Kwa mujibu wa Kaitira, hadi sasa Sea Sense imesaidia kuanzishwa BMU 11 katika Halmashauri ya Kilwa, zikiwamo BMU ya Namakongoro, hatua iliyochangia kwa kiasi kikubwa kupungua kwa uvuvi haramu.
Kurejesha matumbawe
Kwa kushirikiana na Sea Sense, Kitengo cha Usimamizi Shirikishi wa Ufukwe (BMU), Serikali ya kijiji na maafisa wa uvuvi, mwaka 2021, wavuvi walianzisha mpango wa kurejesha matumbawe katika maeneo yaliyokuwa yameharibika vibaya.
“Tulikuwa tunapanda matumbawe asubuhi wakati bahari imetulia ili kurahisisha upandaji na kuongeza nafasi ya matumbawe kushika kwenye miamba. Kila mvuvi alipewa jukumu la kufuatilia maendeleo ya matumbawe hadi yalipokuwa,” anasema Eliasa Mohamed, mvuvi katika kijiji cha Namakongoro.

Mvuvi mwingine, Athumani Hamisi anasema kwa miaka minne tangu wapande matumbawe hali imebadilika, maeneo yaliyokuwa wazi sasa yamejaa matumbawe na samaki wamepata makazi.
“Zamani ulikuwa ukifika kwenye maeneo haya unaona miamba iliyokufa na hakukuwa na samaki wengi. Sasa samaki wameanza kurejea, pweza wameongezeka na tunaona viumbe wengine wakianza kuzaliana tena,” anasema.
Katibu wa BMU ya Namakongoro, Khatibu Mohamed, anasema matumbawe yaliyopandwa mwaka 2021 sasa yamefikia urefu wa takribani sentimita 30, huku baadhi yake yakianza kutoa matawi.
“Kwa sasa samaki wameanza kurejea na kuzaliana kwenye matumbawe tuliyopanda. Hilo linatupa matumaini kuwa bahari yetu inaanza kurejea katika hali yake ya zamani,” anasema.
Chanzo cha uvuvi haramu
Uvuvi haramu uliokuwa umekithiri kiasi cha kuhatarisha ikolojia ya bahari katika kijiji cha Namakongoro, ulichangiwa na mambo mbalimbali, kubwa likiwa kukosekana kwa usimamizi thabiti na shirikishi wa bahari katika eneo husika, hali iliyotoa uhuru kwa wavuvi kufanya watakavyo kwa sababu hakukuwa na wa kuwaongoza.
Ripoti ya Shirika la Ushirikiano Mpya wa Maendeleo ya Afrika (NEPAD, 2016) kuhusu Namna ya Kudhibiti Uvuvi Haramu Afrika inathibitisha kuwa kukithiri kwa matukio ya uvuvi haramu kunachangiwa kwa kiasi kikubwa na usimamizi hafifu na usio endelevu wa bahari. Inasema kukosa usimamizi kunawafanya wavuvi kutofuata sheria na kanuni zilizowekwa.
Ripoti hiyo pia inaeleza kuwa kutoshirikishwa kwa wavuvi na wanakijiji husika wakati wa kufanya maamuzi ya usimamizi wa bahari kunachangia kutokuaminiana na kupunguza uhalali wa kanuni za uvuvi katika jamii husika.
Prof Yunus Daud Mgaya, Mtaalamu wa Biolojia ya Bahari katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, anasema kuwa mahali popote pasipokuwa na usimamizi thabiti, uharibifu lazima utokee na kwamba hali hiyo ipo hata katika bahari.
Anasema wavuvi wanapokosa usimamizi na mipango endelevu ya uvuvi kama vile programu za kufunga mwamba na elimu ya uhifadhi, wanashawishika kuvunja sheria kama vile kutumia mabomu au baruti kupata samaki wengi, hasa katika kipindi hiki ambapo kuna uhaba wa samaki unaotokana na athari za mabadiliko ya tabianchi.
Prof. Yunus anataja kitu kingine kilichochangia uharibifu wa bahari ni uvuvi wa kutumia mabomu au baruti. Anasema kutokana na ongezeko la joto la bahari linalozidi nyuzijoto 30, matumbawe yanaathirika, mengi hupoteza rangi yake na kuwa dhaifu kiasi cha kuyafanya yashindwe kuhimili kishindo cha milipuko inayotokana na uvuvi wa kutumia mabomu au baruti.
“Hali hiyo inaathiri sana viumbe bahari hasa wale wanaopendelea kukaa kwenye miamba hiyo wakifuata chakula pamoja na sehemu za kutaga mayai ambao hulazimika kuhama na kuelekea sehemu tulivu,” anasema Prof Yunus.
Ili kusimamia na kubuni mipango ya uvuvi endelevu ya uhifadhi bahari, Prof Yunus anashauri serikali na wadau wa maendeleo ya bahari kuzisaidia jamii za wavuvi kuwa na Kitengo cha Usimamizi Shirikishi wa Ufukwe (BMU) kama Sheria ya Uvuvi Namba 22 ya mwaka 2003 inavyoelekeza.
“Katika kipindi hiki ambacho ongezeko la joto linasababisha samaki kukimbilia katika kina kirefu cha maji, matukio ya uvuvi haramu yasipodhibitiwa yataongezeka, hivyo ushauri wangu ni kuwe na ulinzi shirikishi na mipango ya uvuvi endelevu,” anasema.
Udhibiti wa uvuvi haramu
Katibu wa BMU ya Namakongoro, Khatibu Mohamed anasema walipoingia madarakani jambo la kwanza walilolishughulikia lilikuwa uvuvi haramu kwani ulikuwa kero kubwa iliyochangia samaki kupotea. Anasema wakati huo ilikuwa vigumu kwa mvuvi kupata hata kilo 5 kwa siku lakini sasa hivi mvuvi anaweza kuvua hadi kilo 30 kwa siku.
“Miaka mitatu iliyopita, sauti za milipuko ya mabomu usiku zilikuwa jambo la kawaida masikioni mwetu. Tulipoingia madarakani, tuliikomesha hali hiyo. Wavuvi haramu waliokuwa wanakamatwa walikuwa wakipewa adhabu kama vile onyo, faini na hata kifungo. Kwa kufanya hivyo tuliweza kudhibiti matukio ya uvuvi haramu kutoka matukio 10 kwa mwezi mpaka sasa ambapo hakuna tukio kabisa,” anasema.

Anasema hatua nyingine ambayo imesaidia kupunguza uharibifu kwenye bahari ni kuanzisha programu ya kufunga mwamba. Chini ya mpango huo shughuli za uvuvi eneo moja husitiswa kwa miezi mitatu ili kurejesha ikolojia ya bahari ikiwamo matumbawe, mikoko na nyasi bahari ambazo zilikuwa zimepotea kutokana na kushamiri kwa uvuvi wa mabomu.
“Katika mwalo wa Namakongoro tuna miamba miwili mikubwa ambayo tunaifunga kwa kupokezana, wakati mmoja umefungwa, mwingine tunauacha wazi ili wavuvi wavue wajipatie kipato, na baadaye tunaufungua na kufunga mwingine,” anasema.
Nini kifanyike ili uharibifu usijirudie
Kwa mujibu wa Khatibu, ili kuhakikisha uharibifu uliokuwepo awali haujirudii, wameweka mfumo wa ulinzi wa kudumu unaojumuisha doria za mara kwa mara baharini, hutoa elimu ya uhifadhi kwa wavuvi, husajili na kuwapatia leseni wavuvi wote pamoja na kuzuia uvuvi katika miamba kwa kupokezana ili kuyapa matumbawe na samaki muda wa kujirejesha.
Anasema pia wanatoa elimu juu ya umuhimu wa kulinda bahari kwa wanakijiji na kuwapa jukumu la kutoa taarifa juu ya vitendo vinavyoathiri bahari, huku BMU ikifanya ukaguzi wa mara kwa mara wa maeneo yaliyopandwa matumbawe ili kuhakikisha yanakua salama.
“Tumejifunza kwamba kulinda bahari si kazi ya BMU pekee, bali ni wajibu wa kila mwananchi. Ndiyo maana tumetoa elimu kwa wanakijiji wote na tumewapa jukumu la kulinda rasilimali za bahari. Kwa ushirikiano huu tunaamini bahari yetu itaendelea kuimarika na kunufaisha vizazi vya sasa na vijavyo,” anasema.
Uwezeshaji kiuchumi
Ili kuwafanya wavuvi wasitegemee uvuvi peke yake na kushawishika kujihusisha na shughuli zinazoweza kuleta uharibifu wa bahari, BMU hiyo ilitumia sehemu ya fedha walizopewa na Sea Sense kuanzisha kikundi cha kuweka na kukopa pesa, ili kuwawezesha wavuvi kuanzisha shughuli nyingine za kuongeza kipato.
Athumani Hamisi, anasema kipindi cha miezi mitatu ya kufunga mwamba anajishughulisha na kilimo cha ufuta na korosho ili kujiongezea kipato, mashamba aliyoyaanzisha baada ya kupata mkopo wa halmashauri kupitia udhamini wa BMU na serikali ya kijiji.
Awali ilikuwa ngumu kwa wavuvi kuikubali mipango ya BMU ya uvuvi endelevu wakidhani kuwa inapoteza muda, lakini baada ya kupata mafunzo waliona mwanga.
Changamoto
Pamoja na mafanikio ya uhifadhi wa bahari, wavuvi wanasema uhaba wa vifaa vya doria pamoja na ufinyu wa fedha za mikopo vinapunguza kasi ya uhifadhi.
Mvuvi Imani Bakari anasema kuwa uhaba wa boti za doria na tochi unasababisha kushindwa kuwakamata wavuvi haramu. Anasema boti iliyopo ni moja na kwamba siku inapopata hitilafu, hushindwa kufanya kazi.
“Kwa kuwa wavuvi wasio waaminifu tunao hapa kijijini, hii boti ikiharibika wanajua na wanakwenda kuvua kwa mabomu wakijua hamuwezi kuwafikia, tunaiomba serikali na wadau wa bahari watuongeze boti nyingine ili kuongeza ufanisi,” anasema
Kauli ya serikali
Ofisa Uvuvi wa Kata ya Limaliyao, Michael Moshi, anasema wanashirikiana na BMU kuandaa mikakati ya kudhibiti uvuvi haramu pamoja na kuendelea kuwasajili na kuwapa leseni wavuvi ili iwe rahisi kuwadhibiti.
Anasema wavuvi wengi katika eneo hilo walikuwa hawafahamu kama kutumia mabomu, baruti au nyavu za waya katika uvuvi ni kinyume cha sheria na kwamba baada ya kupewa elimu wengi wao wameacha.
Akizungumza katika maadhimisho ya siku ya Mazingira Duniani, Juni 5, mwaka huu, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Hamad Yusuph Masauni alisisitiza jamii kushiriki kikamilifu kuhifadhi bahari ili kupunguza athari za mabadiliko ya tabia nchi.
Alisema Serikali imezindua Programu ya Mapinduzi ya Usimamizi wa Mazingira kuelekea Dira ya 2050 ambayo inaangazia mikakati endelevu ya uhifadhi wa bahari ili kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.
Picha ya Bango: Wavuvi wa Namakongoro wakifurahia ongezeko la mavuno ya samaki aina ya pweza baada ya miaka minne ya uhifadhi bahari. Picha kwq hisani ya SeaSense.