- Katikajamii za wavuvi kando ya pwani ya Afrika, wanawake mara nyingi ndio uti wa mgongo wa uchumi majumbani mwao. Wanasindika na kuuza samaki, wanasaidia familia zao, wanagharamia mahitaji ya nyumbani, na kulipa karo za shule, huku wakikabiliwa na changamoto kubwa za kiuchumi na kijamii.
- Hoteli, bandari na maendeleo mengine yanabadilisha ufuo mwingi barani Afrika. Ingawa yanaweza kuleta ajira na uwekezaji, baadhi ya wanawake wanaofanya kazi kwenye uvuvi wanasema pia wanasukumwa mbali na bandari za wavuvi za kitamaduni na maeneo ambayo wamekuwa wakiyategemeakwa vizazi vingi.
- Katika mkutano wa hivi karibuni wa mashirika ya baharini nchini Kenya, mwanamke mmoja alisimama mbele ya hadhira kuelezea hali halisi inayowakabili wanawake wavuvi, wafanyabiashara wa samaki na wengine wanaofanya kazi katika mnyororo wa thamani wa uvuvi.
- Lovin Kobusingye wa Uganda anajua hali halisi hizo vizuri. Baada ya kushinda vikwazo vingi binafsi ili kuwa mjasiriamali aliyefanikiwa, sasa anatetea kwa niaba ya mamilioni ya wanawake wanaofanya kazi katika mnyororo wa thamani wa uvuvi wa Afrika, wengi wao wakiwa wanawake ambao michango yao katika uvuvi bado haionekani na haithaminiwi sana.
Akizungumza kwenye mkutano wa vikundi vya uhifadhi wa bahari na wataalamu wa maendeleo huko Watamu, Kenya, Lovin Kobusingye alikuwa na ujumbe mfupi: Wanawake wanaovua, wanaosindika na wanaouza samaki bado hawako kwenye mazungumzo kuhusu uchumi wa bahari unaokua barani Afrika.
Kwa Kobusingye, changamoto zinazowakabili wanawake katika uvuvi ni sehemu ya maisha yake ya kila siku. “Uhalisia wangu kila siku ni kwamba naamka na mtu mwenye bidii ya kazi akichukua sehemu yangu ya kutua, akichukua eneo langu la uvuvi,” aliiambia hadhira, akielezea jinsi maendeleo ya utalii na uwekezaji mwingine wa pwani yanavyoendelea kushindana na jamii za uvuvi wa jadi kwa ajili ya kupata ufikiaji wa bahari.
Kobusingye alisema wanawake wengi wanakabiliwa na hatari katika sekta ya uvuvi, mazingira duni ya kazi na shinikizo linaloongezeka kutoka kwa maendeleo yanayozidi kusukuma shughuli za uvuvi pembezoni. Katika baadhi ya jamii, haki za kitamaduni zinapuuzwa na serikali; huku kuongezeka kwa kina cha bahari, mmomonyoko wa udongo na kupungua kwa samaki wanaovuliwa kukifanya maisha ambayo tayari ni magumu kuwa magumu zaidi, aliwaambia waliohudhuria mkutano ulioandaliwa na Ocean Resilience Climate Alliance (ORCA).
Licha ya changamoto hizi, Kobusingye alisema wanawake wanasalia kuwa muhimu katika kuendeleza uvuvi na uchumi wa pwani. Husindika samaki, huuza vyakula vya baharini na kusaidia familia zao, ikiwa ni pamoja na kulipa ada za shule, kutokana na mapato wanayopata. Hata hivyo, licha ya jukumu lao katika sekta hiyo, wanawake wengi bado hawana usemi mkubwa katika jinsi uvuvi unavyosimamiwa.

“Usipoonekana, unapokea bajeti zisizoonekana. Usipoonekana, unapokea uwekezaji usioonekana. Na usipoonekana, pia utapokea sera zisizoonekana,” alisema, akizihimiza serikali na wafadhili kuhakikisha wanawake wana nafasi mezani wakati maamuzi kuhusu mustakabali wa uvuvi yanapofanywa.
Lakini hadithi ya Kobusingye mwenyewe ni ngumu zaidi. Wakati Kobusingye alipoingia katika sekta ya uvuvi ya Uganda, ilikuwa ni lazima, si kwa ubunifu. Alikuwa mama mchanga mwenye shahada ya sayansi ya chakula, akiwa mjamzito na akiwa na chaguo chache maishani baada ya mumewe kuondoka. Kile kilichoanza kama mapambano ya kuwasaidia watoto wake kilikua na kuwa biashara ya usindikaji wa samaki ambayo sasa inaajiri watu wengi na inasaidia wengi zaidi kwa njia isiyo ya moja kwa moja. Leo, anaongoza Mtandao wa Wasindikaji na Wafanyabiashara wa Samaki Wanawake wa Kiafrika (AWFISHNET), ambao unawaleta pamoja wanawake wanaohusika katika uvuvi na ufugaji wa samaki katika nchi 44 za Afrika.
Baada ya mkutano huko Watamu, Mongabay ilikaa na Kobusingye kujadili vikwazo vya kibinafsi vilivyomsukuma kuingia katika biashara, jinsi jaribio la soseji ya samaki lilivyosaidia kuanzisha kampuni yake, na kwa nini sasa anatumia muda wake mwingi kutetea wanawake wanaofanya kazi katika uvuvi kote barani.
Mongabay: Safari yako katika sekta ya uvuvi ilianza na mgogoro wa kibinafsi. Ni kipi kilitokea?
Lovin Kobusingye: Nilijiunga na sekta ya uvuvi [kama mjasiriamali] mwaka wa 2012 jijini Kampala [Uganda]. Wakati huo, nilikuwa nimesoma sayansi na teknolojia ya chakula, lakini sikuwa na kazi. Nilikuwa mdogo, nilikuwa na watoto, na nilikuwa na mimba ya binti yangu wakati mume wangu alipoondoka.
Hali ya aina hiyo inaweza kukuvunja moyo. Nilikuwa dhaifu. Lakini pia nilijua nilikuwa na watoto wa kulisha. Hujadiliani kuhusu chakula, au ada ya shule, au huduma ya afya wakati watoto wanahusika. Kwa hivyo, niliamua kwamba ilinilazimu kutafuta kitu cha kufanya. Kilichonivutia kwenye uvuvi ni kwamba ulikuwa mojawapo ya sekta chache ambapo ungeweza kuanza bila kuhitaji wasifu binafsi yaani CV, mitandao ya kitaaluma au cheo kikubwa. Sikuitupa shahada yangu. Badala yake, nilifikiria jinsi ya kuitumia tofauti.

Mongabay: Tueleze zaidi kuhusu kilichokupa nguvu ya kuendelea katika nyakati hizo ngumu uliposhuhudia mumeo akiondoka, huku ukiwa tegemeo la familia lakini hukuwa na kazi.
Lovin Kobusingye: Ilikuwa uchungu sana. Sitaki kujifanya kuwa nilikuwa na nguvu wakati wote; nililia na kuyahisi maumivu hayo kwa kina. Hata hivyo, nilijua pia kuwa hakuna mtu angenijengea upya maisha yangu. Baba yangu alikuwa chachu kubwa ya msukumo kwangu. Ingawa hakuwa na elimu rasmi ya juu, alikuwa mfanyabiashara.
Alifanya biashara katika nchi mbalimbali, zikiwemo Kongo na Kenya, na kupitia kazi hiyo, aliweza kutusomesha. Mimi ndiye niliyekuwa mtu wa kwanza kuhitimu masomo ya juu katika familia yetu. Hivyo, nilishuhudia tangu nyumbani jinsi biashara inavyoweza kubadilisha maisha. Pia, sikutaka watoto wangu wakue wakiniona kama mtu aliyeshindwa na kukata tamaa. Badala ya kuzama katika hali hiyo ngumu, nilijikita zaidi kwenye kazi. Kazi ndiyo iliyonipa nguvu ya kusonga mbele.
Mongabay: Vipi hilo lilisaidia kujenga biashara?
Lovin Kobusingye: Awali, nilianza kama mfanyabiashara wa samaki na msindikaji, lakini haikuwa rahisi. Kuuza samaki kwa njia ya kawaida hakukuwa kunanifaa. Kwa hivyo, nilianza kufikiria kama mwanasayansi wa chakula: ningetengeneza kipi kipya, cha bei nafuu na chenye lishe? Hivi ndivyo nilivyoanza kutengeneza soseji za samaki. Nilitaka bidhaa ambayo ingevutia udadisi, lakini pia kujibu wasiwasi wa kiafya kuhusu vyakula vilivyosindikwa. Ilinichukua kama miezi minane ya majaribio ili kuipata sawa.
Kisha nikapata fursa isiyotarajiwa. Nilikuwa nimealikwa kwenye warsha ya uvuvi, na niliwauliza waandaalizi kama ningeweza kutoa kilo 10 za soseji kwa washiriki kujaribu. Walikubali, kwa uangalifu. Mpishi alizionja kwanza, akazipenda, na siku iliyofuata nilipewa dakika chache kuelezea bidhaa kabla ya mapumziko ya chai. Hiyo ndiyo ilikuwa hatua ya mabadiliko. Waandishi wa habari walikuwa chumbani. Siku iliyofuata, bidhaa hiyo ilikuwa kwenye magazeti na kwenye televisheni. Kilichoanza kama kuonjesha bidhaa kidogo kikageuka kuwa uzinduzi wa biashara yangu.
Mongabay: Biashara iliendeleaje kutoka hapo?
Lovin Kobusingye: Mnamo mwaka wa 2013, nilikuwa nimeanza peke yangu. Nilisajili kampuni, nikaanza kuuza, na kukua hatua kwa hatua. Leo, kampuni inaajiri takriban Waganda 38 moja kwa moja. Tuna kiwanda chetu cha kusindika samaki, na tunasafirisha nje. Biashara hiyo pia imeunda fursa nyingi zisizo za moja kwa moja. Kupitia usambazaji na uuzaji wa samaki wa kuchoma kando ya barabara, mamia ya watu wengine hupata mapato kutokana na bidhaa hizo. Kwa hivyo, kwangu mimi, ujasiriamali si kuhusu mafanikio ya mtu mmoja tu. Unaweza kuwapatia wengine wengi fursa za kujipatia riziki. Hilo ni muhimu kwangu, kwa sababu najua maana ya kutokuwa na kitu imara cha kutegemea.

Mongabay: Uliwezaje kuhamia kutoka kuendesha kampuni hadi kuongoza mtandao unaohusisha bara zima?
Lovin Kobusingye: Changamoto nilizopambana nazo kama mfanyabiashara, upatikanaji wa fedha, upatikanaji wa vifaa vya usindikaji, na kujaribu kukua hadi katika masoko ya kikanda na kimataifa, zilinifanya nigundue kwamba wanawake wengi walikuwa wakikabiliwa na vikwazo sawa. Kwa hivyo, nilianza kwa kujipanga nchini Uganda. Mnamo 2016, nilisaidia kuanzisha Shirika la Kitaifa la Wanawake la Samaki la Uganda, na nikawa rais wake. Wazo lilikuwa rahisi: Peke yangu, ni vigumu sana; kwa pamoja, mna nafasi nzuri zaidi.
Baadaye, kwa sababu tawi la Uganda lilikuwa likifanya vizuri, wanawake kutoka kote barani walinitia moyo kuchukua jukumu kubwa zaidi. Wakati wa mkutano mkuu mnamo 2025 huko Senegal, nilichaguliwa kuongoza AWFISHNET kwa miaka mitano iliyofuata. Nilienda huko kama mwakilishi wa taifa na kuondoka na jukumu la bara.
Mongabay: Je, ni changamoto zipi kuu bado zinawakabili wanawake katika sekta ya uvuvi?
Lovin Kobusingye: Suala moja kubwa ni ufahamu wa sera na sheria. Wafanyabiashara wengi wanawake hawaelewi sheria zinazosimamia biashara ya mpakani, kodi au leseni. Kwa sababu hawajui haki zao, ni rahisi kuwadhulumu. Kwa mfano, ikiwa mtu anasafirisha bidhaa ndani ya kizingiti fulani kinachoruhusiwa, anaweza asidaiwe kodi kisheria. Lakini ikiwa hawajui hilo, bado wanaweza kutozwa pesa ambazo hawapaswi kulipa. Wanawake wengi wanafanya kazi kwa ajili ya kujikimu. Wanaomba wapite mpakani, hawajadiliani wakiwa na maarifa ya kutosha.
Pia kuna vikwazo vya kitamaduni, hususan kwenye baadhi ya jamii za pwani ambapo wanawake wanakabiliwa na ubaguzi katika upatikanaji wa rasilimali, uhamaji, au kufanya maamuzi. Na bila shaka, kuna suala pana la fedha. Wanawake wengi wanatumia akiba yao wenyewe, au kuuza mali, kuanzisha biashara.
Mongabay: Mabadiliko ya tabianchi yanaathirije wanawake wanaofanya kazi nao?
Lovin Kobusingye: Wanawake huhisi mabadiliko ya hali ya hewa kwa njia za vitendo sana. Mafuriko huharibu nyumba, masoko na maeneo ya usindikaji wa samaki. Samaki wanaendelea kuwa vigumu kupatikana katika baadhi ya maeneo, na watu wanaweza kutumia siku nzima majini lakini wanarudi wakiwa na samaki kidogo au hata bila samaki wa kuuza. Kwa familia ambazo tayari zinaishi katika mazingira ya kujikimu, hilo linaweza kuwaangamiza sana.

Mongabay: Mustakabali unaonekanaje kwako kwa sasa?
Lovin Kobusingye: Kwa upande wa biashara, ninatanua. Ninajenga ghala kubwa karibu na bandari ya Kampala ili kusaidia ukuaji wa biashara. Pia ninawekeza katika ufugaji wa samaki; vizimba vya samaki ziwani, mabwawa ya kutotolea vifaranga na mabwawa ya kulelea samaki kwa sababu nataka kuchangia katika uzalishaji, si usindikaji na biashara tu.
Binafsi, nashukuru. Siko kule nilipokuwa mwaka wa 2013. Lakini pia najisikia kuwajibika. Kuna wanawake wengi katika hali niliyokuwa nayo hapo awali; wanawake wanaojaribu kujenga upya baada ya kupitia misukosuko, wanawake wenye watoto, wanawake wenye mawazo lakini hawana mtaji. Iwapo kisa changu kina maana yoyote, natumai inaonyesha kwamba ustahimilivu ni muhimu. Wanawake hawapaswi kulazimika kutegemea nguvu za kibinafsi pekee ili kufanikiwa.
Picha ya bango: Kulingana na Lovin Kobusingye, wanawake wanaovua, kuchakata na kuuza samaki bado hawajajumuishwa ipasavyo katika mijadala kuhusu uchumi wa bluu wa Afrika unaokua. Picha kwa hisani ya Environmental Justice Foundation.
Habari hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza hapa kwa lugha ya Kiingereza mnamo tarehe 26/06/2026.