- Wanawake wa Maasai Mara wanatumia pilipili, rosemary na mimea mingine ya manukato kupunguza uvamizi wa tembo huku wakiongeza kipato chao.
- Takwimu za Mara Elephant Project zinaonyesha migogoro kati ya binadamu na tembo imeongezeka katika mfumo wa ikolojia wa Greater Mara, ikisababisha hasara kubwa kwa wakulima.
- Utafiti wa MEP na wataalamu unaonyesha harufu kali ya pilipili na mimea mingine inaweza kuwazuia tembo kuingia mashambani bila kuwadhuru.
- Mbinu hii ya kilimo mseto inalenga kulinda mazao, kuimarisha usalama wa chakula na kuwezesha watu na tembo kuishi pamoja kwa amani.
Nyimbo za jadi za Kimaasai zinasikika taratibu katika Enkutoto, eneo la Maasai Mara, ambalo kwa miaka mingi limeishi katika kivuli cha migogoro mikali kati ya binadamu na tembo.
Chini ya jua kali la mchana, wanawake wameinama mashambani. Mikono yao inasonga kwa ustadi ikipalilia mistari mirefu ya pilipili, rosemary, mti wa chai, na lavender.
Mabadiliko makubwa ya mandhari yameshuhudiwa hapa. Badala ya mashamba mapana ya mahindi pekee kama ilivyokuwa zamani, ardhi sasa imepambwa na rangi ya kijivu, kijani kibichi na zambarau, ya mimea hii ya manukato. Wanawake hapa wana matumaini mapya, si tu ya kulinda maisha yao, bali ya kuendeleza kilimo chenye tija ya kiuchumi.
Miongoni mwa wanawake hao ni Nelly Musana kutoka Enkutoto, na mwanachama wa kikundi cha kina mama cha Oloisesiai Self Help Group. Karibu yake yupo Mama Arami Musekenya, mama wa watoto sita, mfugaji na mkulima mzaliwa wa Maasai Mara ambaye maisha yake yote ameshuhudia migogoro kati ya binadamu na wanyamapori.
Kwa miaka mingi, wanawake hawa waliishi kwa hofu kubwa. Hofu hiyo haikuja mchana; ilikuja usiku, hasa wakati mahindi yalipoanza kuzaa na kukomaa. “Tembo walikuwa wakija bila hodi,” anasema Musekenya, huku akitazama shamba lililojaa rosemary. “Kitu kibaya si kuona tembo; ni kuamka asubuhi ukute hakuna kitu kabisa.”
Kiwango cha uharibifu unaofanywa na wanyama hawa wakubwa ni jambo la kutia wasiwasi mkubwa na linaloacha familia katika umaskini wa ghafla. Musekenya anasimulia kuwa kuna nyakati ambapo kundi la tembo watano tu linaweza kuingia shambani na ndani ya usiku mmoja tu, wanamaliza kabisa ekari tano za mahindi.
Uharibifu huo wa kasi ya ajabu unamaanisha kuwa jasho la miezi minne linatoweka ndani ya saa chache. “Unaamka asubuhi unakuta shamba lote limechezewa na kusawazishwa chini. Unaanza kujiuliza watoto watakula nini, na ada ya shule itatoka wapi? Unaumia sana moyoni,” anasema Arami.
Hali hii imekuwa ikiongezeka katika mfumo mzima wa ikolojia wa Greater Mara. Takwimu za Mara Elephant Project (MEP) zinaonyesha kuwa matukio ya uharibifu wa mazao unaosababishwa na tembo yaliongezeka kwa asilimia 268 kati ya mwaka 2016 na 2019, huku matukio yakiongezeka kutoka 45 hadi 121. Kwa ujumla, matukio yote ya migogoro kati ya binadamu na tembo yaliongezeka kutoka 84 hadi 181 katika kipindi hicho.
Kulingana na Mpango wa Kitaifa wa Utekelezaji wa Uhifadhi wa Tembo nchini Kenya, matukio 25,422 ya migogoro kati ya binadamu na tembo yalirekodiwa kati ya mwaka 2008 na 2020. Hii ni sawa na wastani wa karibu matukio 2,000 kila mwaka. Katika kipindi hicho hicho, tembo waliwaua watu 297 na kuwajeruhi wengine 269.
Utafiti uliofanyika katika eneo la Trans–Mara ulibaini kuwa matukio ya uvamizi wa mashamba na tembo yaliongezeka kutoka wastani wa matukio 263 kwa mwaka kati ya 1999 na 2000 hadi 392 kwa mwaka kati ya 2014 na 2015, sawa na ongezeko la asilimia 49.

Jamii zinazopakana na mfumo wa ikolojia wa Maasai Mara zimekuwa zikiishi kwa muda mrefu katikati ya neema na changamoto ya kuwa karibu na wanyamapori.
Kwa upande mmoja, eneo hili ni miongoni mwa maeneo maarufu duniani kwa utalii, likivutia maelfu ya wageni wanaokuja kushuhudia maajabu ya asili, hasa mvuko wa nyumbu wanaotoka Serengeti kuingia Maasai Mara kupitia mto mkubwa Mara.
Lakini kwa upande mwingine, ni nyumbani kwa jamii za kiasili zinazoshiriki vyanzo vya maji, njia za kimila za uhamaji na ardhi na wanyama hawa wakubwa.
Mgongano huu wa kila usiku huanza pale chakula kinapokutana na njaa, na kuna sababu maalum ya kisayansi na kibaolojia inayowafanya tembo kuvutiwa na mashamba ya mahindi kuliko nyasi za mbugani.
Abigail Simaloi, Meneja wa Uhusiano kati ya Binadamu na Wanyamapori wa MEP, anafafanua tabia hii ya ulaji wa tembo.
“Tukitazama lishe ya tembo kwa mujibu wa wataalamu wa biolojia, mahindi yana kiwango kikubwa sana cha kuwapa nishati kutokana na sukari, na yana virutubisho vingi ukilinganisha na nyasi za kawaida za porini. Tembo ni wanyama wakubwa wanaohitaji nishati nyingi kila siku ili kuendesha miili yao,” aliiambia Mongabay.
Simaloi anasisitiza kuwa jinsi binadamu anavyosikia ladha tamu na kuvutiwa na chakula chenye nishati, ndivyo tembo anavyosikia na kutambua utamu huo. “Ni suala la utamu na chanzo cha haraka cha nishati,” anafafanua Simaloi.
Musana anaeleza: “Tembo wananusa kutoka mbali sana. Wanajua wakati mahindi yanaanza kutoa maziwa na kuwa matamu. Wanajua yako tayari kabla hata sisi wenyewe hatujaingia shambani kuvuna”.
Kutokana na kivutio hiki cha ladha, familia zililazimika kukesha usiku kucha zikitwanga mabati, kupiga kelele, na kuwasha moto wa asili nyanjani. Hata hivyo, mbinu hizi za kizamani hazikuweza kuzuia nguvu na njaa ya tembo.
Ili kutafuta suluhisho la kudumu zaidi, shirika la MEP lilianza kufanya majaribio ya kutambua kama mazao fulani yanaweza kusaidia kupunguza uvamizi wa tembo bila kuathiri maisha ya wakulima.
Simaloi anaeleza kuwa mwaka 2021, shirika hilo liliweka shamba la majaribio la ekari tano huko Trans-Mara, ambapo lilipanda zaidi ya aina 50 za mazao na kufuatilia tabia za wanyamapori.
“Tulitaka kuona ni mazao gani yanaliwa na ni yapi hayaguswi. Tulipanda mazao ya chakula kama mahindi, maharagwe, viazi, viazi vitamu, pamoja na mitishamba, na mazao maalum ya kuzalisha mafuta muhimu (essential oils). Baada ya utafiti huo tulielewa ni mimea gani inaweza kusaidia jamii,” anasema Simaloi.
Timu hiyo ilibaini kuwa rosemary, pilipili, mti wa chai, lavender na Eucalyptus citriodora zilikuwa miongoni mwa mimea yenye kiwango cha chini kabisa cha kushambuliwa na tembo na wanyamapori wengine.
Matokeo hayo ndiyo yaliyozaa mpango wa Outgrower, ambao ulianza rasmi mwaka 2025. Simaloi anasema ulianza na wakulima 37, lakini sasa umekua na kufikia wakulima 147 wanaofanya kazi kupitia vikundi 10 katika maeneo yanayopakana na mfumo wa ikolojia wa Maasai Mara.
Kwa mujibu wa MEP, shirika hilo limesaidia kudhibiti matukio zaidi ya 1,598 ya migogoro kati ya binadamu na tembo tangu kuanzishwa kwake kupitia mbinu mbalimbali za uhifadhi na ushirikiano na jamii.
Huku shirika la MEP likitafuta mbinu za kisayansi zilizofanyiwa utafiti wa kina, swali kubwa ambalo wanasayansi wanajiuliza ni: Je, ni vipi tunaweza kuthibitisha kwa takwimu na ushahidi thabiti kuwa pilipili na rosemary zinafukuza tembo?
Simaloi anafafanua ushahidi wa nyanjani uliopatikana wakati wa kipindi cha majaribio.
“Ushahidi mkuu tulioingiza kwenye data zetu ni ule wa nyayo. Wakati wa majaribio ya kwanza, tulizungushia mimea hii ya manukato kandokando ya mashamba ambayo ndani yake kulikuwa na mahindi matamu yaliyokomaa. Kupitia mifumo yetu ya ufuatiliaji, tuliona makundi ya tembo yakikaribia yale mashamba usiku,” anasema.
“Ushahidi ulikuwa wazi asubuhi: tulikuta nyayo zao zikiwa zimepita humo humo kandokando ya mashamba ya pilipili na rosemary, lakini hazikuingia ndani. Tembo walifika, wakanusa ile harufu kali, ikawafukuza na wakageuka na kuondoka bila kugusa hata jani moja la mahindi yaliyokuwa ndani,” anaongeza.
Baada ya kuona data hizi na ushahidi uliokusanywa nyanjani, MEP iliona kuna nafasi kubwa na salama ya kupanua mradi huu hadi kwa wakulima wengine. Utafiti wa kisayansi unaunga mkono kikamilifu ushahidi wa nyayo uliokusanywa na MEP.
Dkt Geoffrey Chege, mtaalamu wa ikolojia ya wanyamapori na mamalia wakubwa kutoka shirika la WWF-Kenya, anayeshughulikia uhifadhi na migogoro kati ya binadamu na wanyamapori, anafafanua nguvu ya kibaolojia iliyopo kwenye mbinu hii.
“Tembo wana mfumo nyeti na mkubwa sana wa harufu (olfactory system) kuliko mnyama yeyote yule wa ardhini. Wana jeni nyingi za kunusa kuliko hata mbwa wa uwindaji. Ndani ya pilipili kuna kemikali inayojulikana kama ‘capsaicin’.
“Tembo anaponusa kemikali hii, inachochea mwasho mkali sana kwenye utando wa mfumo wake wa kupumua na macho. Si kwamba pilipili inamdhuru kwa sumu, bali inamletea usumbufu mkubwa kisaikolojia kiasi kwamba hawezi kuthubutu kusogea karibu au kuvuka ule ukuta wa harufu,” anafafanua Chege.
Hata hivyo, Chege anatoa angalizo la kitaalamu kuwa mbinu hii ina mipaka yake ya kimazingira.
“Kuna changamoto ya kimazingira. Mvua kubwa hupunguza ufanisi wa kemikali ya capsaicin kwenye vizuizi vya pilipili, na jua kali la savana huharibu nguvu ya mafuta ya manukato. Hivyo wakulima wanatakiwa kuifanyia matengenezo ya mara kwa mara. Pia, baada ya muda mrefu, baadhi ya tembo wanaweza kuzoea tabia (habituation) na kutafuta mbinu ya kuikwepa. Ndiyo maana lazima itumike kama sehemu ya mkakati mpana,” Chege anaeleza.
Mbinu hii inayotekelezwa katika Kaunti ya Trans-Mara inatokana na matokeo ya tafiti zilizofanikiwa katika maeneo mengine ya ukanda, nje ya Kenya. Katika mahojiano yake, Chege anatoa mifano ya kisayansi kutoka nchi jirani, ambapo mbinu hizi zimeimarisha uwezekano wa watu na tembo kuishi pamoja kwa amani.
“Tumeona mifano ya mafanikio makubwa katika maeneo ya Trans-Volta nchini Ghana, na kwa karibu zaidi katika Bonde la Zambezi nchini Zimbabwe, na maeneo ya ikolojia ya Serengeti nchini Tanzania.
Huko Zimbabwe, kwa mfano, programu za matumizi ya kamba zilizopakwa mafuta ya pilipili (chilli-strings) na makaa ya pilipili yanayochomwa usiku (chilli-briquettes) zimechangia kupungua kwa kiasi kikubwa kwa uvamizi wa mashamba ikilinganishwa na hali ilivyokuwa kabla ya miradi hiyo.
Data hizi za kikanda zinathibitisha kuwa mradi wa Trans-Mara unafuata nyayo za kisayansi zilizojaribiwa na kufanikiwa kimataifa,” anasema Chege.

Mabadiliko ya tabianchi na athari zisizotabirika za hali ya hewa ndizo zinazochochea ubunifu huu wa kuweka mazao mengi tofauti katika shamba moja (biodiverse inter-cropping), jambo ambalo halikuwepo kabisa zamani katika utamaduni wa kilimo wa jamii hizi. Ukame wa muda mrefu na kupungua kwa maeneo ya malisho vimesababisha wanyamapori kusogea karibu zaidi na makazi ya watu kutafuta rasilimali na maji.
Chege anafafanua mabadiliko haya ya kimkakati: “Mbinu hii inaweza kusambazwa kwa sababu inaleta mfumo wa kilimo mseto. Zamani, wakulima walitegemea zao moja tu la mahindi, ambalo likishambuliwa na tembo au ukame, familia hubaki njaa. Kuweka mazao mbadala kama pilipili na rosemary, yasiyopendwa na tembo kandokando ya mahindi kunatengeneza kinga thabiti huku kukipunguza hatari ya kiuchumi na usalama wa chakula kwa mkulima”.
Mimea hii pia imefungua milango mipya ya kipato kwa wanawake wa Maasai Mara kutokana na thamani yake kubwa katika matumizi ya kawaida ya kibinadamu ya kila siku.
Simaloi anabainisha kuwa mradi huu unalenga kubadilisha kabisa maisha ya kiuchumi ya kaya hizi: “Mimea kama rosemary, lavender, na mti wa chai ina soko kubwa sana la kimataifa na la ndani kwa matumizi ya kibinadamu. Mafuta yake yanayokamuliwa yanatumika kutengeneza vipodozi, sabuni za dawa, dawa za kuzuia wadudu, na matibabu kwa kutumia harufu (aromatherapy).
“Rosemary yenyewe pia ni kiungo maarufu sana. Hii ina maana kuwa wanawake hawa hawajengi tu ukuta wa ulinzi, bali wanatengeneza biashara endelevu inayowaletea pesa taslimu,” anasema Simaloi.
Musana anasema: “Hata tembo wakija sasa hivi, hunusa tu na kwenda zao. Na sasa, badala ya kupoteza kila kitu na kubaki mikono mitupu, tunapata amani na kipato chetu wenyewe cha kusomesha watoto wetu. Sasa tunalala usingizi mnono.”
Simaloi anahitimisha: “Wanyama na watu wanapaswa kuendelea kuishi pamoja katika mfumo huu wa Mara. Hatuwezi kuwahamisha tembo, na hatuwezi kuwahamisha watu. Suluhisho pekee ni kupata mbinu za kiubunifu zinazomwezesha kila mmoja kuwepo bila kumdhuru mwingine.”