- Msitu wa Mrima wenye akiba kubwa ya madini unavutia wawekezaji tena, huku ukizua mvutano kati ya uchimbaji wa madini na uhifadhi wa mazingira.
- Wakaazi wanahofia kurejea kwa athari za tafiti za awali za madini na wanataka uwazi, ushirikishwaji na ulinzi wa maeneo matakatifu.
- Wataalamu wanasema teknolojia imepunguza athari za tafiti za madini, lakini shughuli za mara kwa mara bado zinaweza kutatiza ikolojia na maisha ya jamii.
- Wadau wanasisitiza umuhimu wa ushirikishwaji wa jamii, fidia ya haki na ulinzi wa bioanuwai ili kuepusha migogoro wakati wa uchimbaji wa madini.
Kwa miaka mingi, Nassir Abdallah Bege amekuwa akitembea katika njia za Msitu wa Mrima, katika Kaunti ya Kwale, akiangalia ukuaji wa miti na juhudi za jamii za eneo hilo katika kuulinda.
Akiwa mwenyekiti wa Muungano wa Msitu wa Kijamii wa Mrima (Mrima Community Forest Association), amekuwa nguzo muhimu katika uhifadhi wa Mrima, ulio takriban kilomita 65 kusini-magharibi mwa Mombasa. Anakumbuka mashimo yaliyoachwa baada ya baadhi ya sehemu za msitu kukatwa wakati kampuni zilipokuwa zikifanya tafiti za kutafuta madini. Zaidi ya mwongo mmoja baadaye, anasema, mashimo hayo yanaendelea kujiziba yenyewe.
Ukitembea msituni, si rahisi kuona mashimo hayo madogo kwani yamefinikwa, baada ya mimea ya asili kuota tena kwa zaidi ya muongo mmoja.

Neno ‘Mrima’ linatoka katika jamii ya Wadigo, kumaanisha mlima. Msitu huu wa Mrima una rutuba kubwa na bioanuwai ya kipekee. Kadri unavyozidi kupanda mlimani, msitu huwa mnene zaidi na mwanga hupungua. Eneo hili liko kimya, isipokuwa sauti za wanyama, wadudu na miti ambayo mara kwa mara inatikisika kutokana na upepo unaovuma.
Kwa mujibu wa Key Biodiversity Areas (KBA), eneo la Mrima lenye umuhimu wa bioanuwai lina ukubwa wa takriban kilomita za mraba 3.76 (sawa na takriban hekta 376), ambapo asilimia 95.77 ya eneo hilo iko chini ya hadhi mbalimbali za ulinzi wa kisheria.
Utafiti na uharibifu wa misitu
Kutokea miaka ya 1950, wataalamu wa jiolojia na makampuni ya madini wamekuwa wakifanya tafiti katika eneo la Mrima kutathmini uwepo wa madini ya niobium na madini adimu mengine.
Stakabadhi za rekodi za kesi ya kampuni ya Cortec zinaonyesha kuwa utafiti wa awali ulifanywa na taasisi za Serikali za jiolojia kabla ya kampuni kama Anglo American katika miaka ya 1950 na Pechiney Saint-Gobain mwishoni mwa miaka ya 1960 kufanya tathmini zaidi za eneo hilo.
Matokeo yake ni kwamba baadhi ya sehemu za msitu zilikatwa na mashimo kuchimbwa kwa ajili ya uchunguzi bila kujulikana iwapo uchimbaji rasmi utafuata.

Aidha, hakuna tathmini rasmi iliyofanywa katika msitu huo kuonyesha athari hizo. Hata hivyo, tafiti za awali katika sehemu nyingine duniani zinaonyesha kuwa hatua hizo huacha maeneo kama hayo na makovu ya ikolojia, huku wasiwasi ukizuka tena miongoni mwa wakaazi, ambao pia hulalamikia ukosefu wa uwazi na athari kwa mazingira.
Msitu wa Mrima ni eneo lenye makadirio ya akiba ya madini yenye thamani ya KSh8.1 trilioni (zaidi ya $62 bilioni). Ingawa uchimbaji mkubwa wa madini bado haujaanza rasmi, Serikali imeingia katika hatua ya kuendeleza mradi kibiashara ili hatimaye kutumia hazina hii ya madini ambayo haijatumika.
Haya yanajiri wakati Wakala wa Kimataifa wa Nishati (International Energy Agency-IEA) umetangaza kuongezeka kwa uhitaji wa madini muhimu kama vile niobium, inayotumika katika utengenezaji wa vifaa vya kielektroniki na nishati mbadala. Wawekezaji wapya wameanza kujitokeza, Mrima ikiwa kitovu cha mvutano kati ya maslahi ya kiuchumi na uhifadhi wa mazingira.
Harry Kimtai, Katibu Mkuu wa Idara ya Madini katika Wizara ya Madini, Uchumi wa Buluu na Masuala ya Bahari, amethibitisha kuwa eneo hilo sasa limeanza kuvutia wawekezaji wengi huku Serikali ikiwa tayari imekamilisha awamu ya kwanza ya mchakato wa zabuni kwa mwekezaji atakayepewa haki za kuchimba madini eneo hilo.
Anasema kinyume na kampuni zilizofanya tafiti hapo awali, safari hii wanatumia mbinu ambayo itaiwezesha Serikali kuchagua mwekezaji anayezingatia maslahi ya wananchi.
“Siku za nyuma haikuwa lazima mwekezaji atangazwe kupitia zabuni. Hata hivyo, wakati huu tunataka kila kitu kiende kulingana na sheria,” alisema Kimtai.
Mwaka 2012, kampuni ya Cortec Mining Kenya ilifanya shughuli za utafiti ambazo wakaazi wanasema ziliacha baadhi ya maeneo yakiwa yameharibika. Wakaazi walilalamika kuwa wanyama kama mbega, aina ya tumbili wa pwani, walitoka msituni na kuharibu mimea yao, haswa mahindi na mboga. Ni jambo ambalo pia lilitatiza baadhi ya shughuli za utamaduni na sehemu takatifu ya jamii hiyo.
“Kuna mzuka mmoja mkubwa ambao unaitwa kigongoni. Halafu kuna mizuka mingine ambayo inazunguka huo mlima. Kuna Maetwe. Kuna Rong’o. Kuna Kaya Bege. Kuna Kaya Mzemani, na kuna Kaya Mwalimu,” Abdallah Bege aliiambia Mongabay.
Na sasa, zabuni mpya ya Machi 2026 inazua hofu ya kurejelea kwa makovu hayo. “Kuna wasiwasi miongoni mwa wakazi, hasa ukiangalia kwamba ni msitu ambao umekuwa ukitunzwa kwa muda mrefu,” anasema Abdallah Bege.
Anasema tayari wameiandikia Serikali barua kuhusu suala hilo ili wapate kufahamu hatma ya uhifadhi hata kabla ya zabuni kutolewa.
>“Iwapo uchimbaji wa madini utaanza, vijiji 12 vinavyozunguka Mrima, vikiwemo Mrima TM, Mwachanogo, Tsuni, Mwabovo, Bumbuni, Ziwani, Mwangwei, Mwabogolani, Kikobe, Mamba, Mkuduru A, na Mkuduru B, na wanakijiji takriban 10,000 wataathirika na mradi huo,” anaongezea Bege.Mrima upo katika eneo la Dzombo, na kulingana na tafiti za awali, kijiji hicho kina idadi ya watu 186 kwa kila kilomita mraba.
Kaya ndani ya Msitu wa Mrima
Mohammed Omari Juma Dari, msimamizi wa Kaya Mrima, anasema Kaya hiyo iko chini ya usimamizi wa Makumbusho ya Kitaifa. Anataja sehemu saba ndani yake, ikiwemo, Kaya Halima, Ngoni, Dziweni, Bege, Dindiri kauka, Rong’o na Mahetu.

Kaya ni sehemu takatifu yenye historia ya kufanya matambiko na kuomba kwa mujibu wa mila za jadi, endapo kutakuwa na hitaji katika jamii. Kaya hiyo ilitumika kama sehemu maalum ya ibada, ambapo palipotokea magonjwa, vita au tatizo lolote la kijamii, jamii ilizungumza na miungu ili kuondoa dhiki hizo. Pia kuna miti adimu inayotumika katika matambiko.
“Zamani kulikuwa na kitu kinaitwa ngambi, ambacho ungekivunja ungepigwa faini,” amesema Dari.
Akipeana historia, Dari anasema baadhi ya tafiti za uchimbaji madini zilifanyika tangu akiwa kijana. “Mara ya kwanza nilisikia shughuli za utafiti zikianza mwaka 1958, halafu kukafanywa tena 1968,” anasema.
Msitu wa Mrima ulitangazwa rasmi kuwa hifadhi ya misitu mnamo mwaka 1961 chini ya Idara ya Misitu wakati huo, ambayo ndiyo iliyokuwa na jukumu la kusimamia misitu nchini. Katika miaka ya 1980, eneo hilo lilipewa hadhi ya Strict Nature Reserve kutokana na umuhimu wake wa kiikolojia. Kwa sasa, usimamizi wa msitu huo uko chini ya Shirika la Huduma ya Misitu Kenya (KFS), kwa mujibu wa Sheria ya uhifadhi na usimamizi wa misitu ya mwaka 2016.
Nchini Kenya, shughuli zote za madini na utafiti wake hufanyika chini ya Sheria ya madini ya mwaka 2016, ambapo kampuni husika zinatakiwa kupata leseni na pia kufanya tathmini ya athari za mazingira. Sheria hizi zimewekwa ili kulinda misitu na pia kuweka uwazi katika masuala ya madini.
Kampuni ya Cortec ilipokonywa leseni baadaye kwa madai kuwa ripoti ya pili ya tathmini ya mwaka 2013 haikupitishwa na mamlaka ya mazingira nchini Kenya, NEMA. Hata hivyo, ripoti hiyo pia haikuwahi kuwekwa hadharani.
Profesa Saeed Mwaguni, mwanasayansi wa mazingira, anasema shughuli za utafiti zilizofanyika mwaka 2012 zilithibitisha uwepo wa madini ya niobium bila kuathiri bioanuwai kwa kiwango kikubwa, kwa kuwa shughuli hizo zilitumia teknolojia ya kisasa.
“Mashimo yalichimbwa, kisha kifaa maalumu kikawekwa na kikaonyesha jinsi madini yalivyo chini ya ardhi,” alielezea. Ni jambo ambalo pia Kimtai aliunga mkono.
Anabainisha pia kuwa eneo hilo lina mionzi ya asili ya atomiki, lakini si kwa kiwango cha kuhatarisha maisha ya binadamu au viumbe. Hata hivyo, anasema, utafiti wa mara kwa mara unaweza kutatiza ikolojia na kuathiri maisha ya wakaazi, hivyo kuna haja ya uwazi na ushirikishwaji wa jamii.
Japo hakuna utafiti wa moja kwa moja uliofanyika eneo la Mrima, tafiti za kisayansi zilizofanyika kwingineko zinaonyesha kuwa licha ya athari za uchunguzi wa madini kuwa ndogo, shughuli za utafiti wa mara kwa mara hutatiza ikolojia. Tafiti nyingine zinaonyesha kuwa kuhusishwa kwa jamii katika masuala ya uhifadhi ni muhimu katika kufanikiwa kwa shughuli hiyo.
Aidha, mara nyingi wakaazi wamesema licha ya Serikali kusema inashirikiana nao, masuala muhimu hujadiliwa katika ngazi za kitaifa, vijijini wakisalia tu kusikia ilhali wao ndio huathirika zaidi.
George Kimau, kijana kutoka eneo la Mrima, aliiambia Mongabay kuwa amefunzwa umuhimu wa kuhifadhi msitu huo tangu utotoni. “Nina hisia na matarajio mseto kwa Mrima; kwanza vile nimesikia kuhusu mambo ya madini,” anasema.
Anakubali mambo yote mawili. Hata hivyo, hakujawa na hamasisho la kutosha kuhusu utafiti, uchimbaji na hatma yao kama wakaazi wa eneo hilo.
Kimau anategemea sheria ya madini kuwalinda wakati wa utafiti na hata uchimbaji rasmi wa madini utakapoanza.
Anasema Mrima inapozungumziwa, madini ndiyo hutajwa zaidi, huku wakaazi wakikosa kuhusishwa. Kwake, kuwepo na uelimishaji na uwazi kwa wakaazi ndio njia itakayowafanya waelewe zaidi umuhimu wa shughuli za utafiti wa mara kwa mara na hata uchimbaji madini.
Aidha Kimtai anasema kuna kamati inayohusisha washikadau mbalimbali kutoka taasisi za Serikali, ikiwemo KFS, Makumbusho ya Kitaifa ya Kenya (National Museums of Kenya) na wengineo. Alisema kuwa jamii itahusishwa moja kwa moja punde baada ya Serikali kutambua mwekezaji atakayekuwa ameshinda zabuni ya uchimbaji madini.

“Ndiyo tunaanza katika mchakato wa kutambua mwekezaji. Kutokana na maombi yaliyotumwa, tutawakagua kabla ya kuamua. Tukipata mtu rasmi tutahusisha jamii,” aliongeza.
Kupatikana kwa madini Kwale
Aidha, hii haitakuwa mara ya kwanza kwa kaunti ya Kwale kupata madini ambayo yamevutia wawekezaji wa kimataifa. Kampuni ya Base Titanium, ambayo ilikamilisha kuchimba madini eneo hilo mnamo mwaka 2024, ilianza kuhusisha jamii mapema.
Kulingana na aliyekuwa meneja wa uhusiano wa kijamii wa kampuni hiyo Christine Mwaka, hata kabla ya kuanza zoezi lolote, walianza kuihusisha jamii. Alisema kuwa mahusiano hayo ya mapema yalipunguza pakubwa migogoro kati yao na jamii.
“Tulianza kuketi na jamii na kuwauliza masuala yanayowahusu kwanza hata kabla ya kuanza utafiti. Hili lilisaidia sana,” aliongeza.
Anasema kuwa mazungumzo hayo ya mara kwa mara yaliwasaidia kubaini umuhimu wa kaya. Hata walipoendelea kuchimba, walihakikisha kaya na mizimu haikuguswa kama heshima kwa jamii hiyo.
Alisema japo mikwaruzano ilikuwepo, mikutano ya mara kwa mara na jamii ilisaidia kuelewa mawazo yao. Hata hivyo, kuna nyakati ambapo viongozi wa jamii walikosa kufikisha ujumbe, jambo ambalo anasema wangelifanya, kwani wakati mwingine viongozi hukosa kueleza jambo lile kwa fasaha kama ambavyo kampuni ingefanya.
Pia, kuhusisha uongozi wa kaunti kungekuwa nguzo muhimu. Mara nyingi viongozi kama gavana walipata ripoti, lakini ingekuwa vyema zaidi kama wangekuwa wakipewa taarifa kwa kina kuhusu masuala yanayohusu jamii moja kwa moja.
Hata hivyo, kwa sasa hakuna kampuni yoyote inayofanya utafiti. Pia si rahisi kubaini vishimo vidogo vilivyopo ni asilia au labda vilichimbwa hapo awali, kwani upana wake ni kama sahani ya chakula.
Blessington Maghanga, afisa mkuu wa kuhifadhi misitu nchini, anayehusika na masuala ya leseni, anasema baadhi ya spishi adimu za mimea inayopatikana katika Mrima ni kama vile Mgurure (combretum schumannii) na mfunda (cynometra webberi). Miti mingine ni mvule (Milicia excelsa), mrunza (Nesogordonia holtzii), mkwakwata (Drypetes usambarica var. mrimae) miongoni mwa mimea mingine adimu.
Wanyama ni mbega, ambaye ni aina ya tumbili anayepatikana katika maeneo machache ya Pwani kusini.
Anaongeza kuwa utafiti wa madini umefanyika katika baadhi ya sehemu za eneo hilo na kuathiri mazingira kutokana na kukatwa kwa miti na viumbe kutafuta makazi mbadala.
Anasisitiza kuwa yote yalifanyika ndani ya sheria, wahusika wakipata vibali rasmi. Pia utafiti walioufanya kama shirika ulionyesha baadhi ya sehemu zina mashimo madogo. “Lakini athari haikuwa kubwa,” amesema. Aidha hakuna ukarabati uliofanyika rasmi kwani athari zilikuwa ndogo na hata hazionekani.
Maghanga alisema kuwa teknolojia inayotumika tangu mwaka 2016 imeonyesha mafanikio makubwa kwa ushirikiano na maafisa wa misitu, kwani kupitia setilaiti inaweza kutuma picha za moja kwa moja endapo uharibifu wa aina yoyote unafanyika msituni.
Aidha, Titus Mitau, ambaye ni Mkurugenzi wa Shirika la Huduma ya Wanyamapori (KWS) katika Kaunti ya Kwale, amesema kuwa hakuna visa vyovyote vya migogoro kati ya wanyamapori na binadamu, kwani wanyama waliopo katika msitu huo ni wale wadogo kama mbega, ambao hawatii wakaazi hasara.

Mnamo Machi 2026, Wizara ya Madini ilitangaza zabuni kwa wawekezaji wanaotaka kufanya shughuli za utafiti na uchimbaji wa madini katika eneo la Mrima. Kimtai alisema shughuli ya kukagua wawekezaji na zabuni inaendelea na watahakikisha sheria zote zinazingatiwa ili wapate mwekezaji mzuri, ambaye ataweza kuchakata madini hayo ili kubaini thamani yake kabla ya kuyasafirisha nje.
Licha ya hayo, wakaazi wanasema kurejelewa mara kwa mara kwa shughuli hizo hutatiza maisha yao. Kwa mkaazi Domitilla Mweni Kamitu, msitu huo unawapa riziki, kwani wameweza kuwa na mizinga ya kufuga nyuki katika kikundi chao cha kina mama. Yeye binafsi ana mizinga mitano humo.
Pia anajishughulisha na kukuza miche ya miti kutoka msitu huo, ambayo baadhi yake ni adimu. Ana miche takriban 15,000. Anasema wakati shughuli za utafiti wa mwaka 2012 zilipokuwa zikifanyika, hawakuweza kwenda katika sehemu hizo, hivyo basi wakatatizika.
Mahmoud Barroh, naibu mshirikishi wa shirika la kijamii la Kwale Mining Alliance, anasema mara nyingi katika masuala ya maamuzi, wakaazi hubaki gizani bila kuhusishwa. Anasema shughuli za utafiti za mara kwa mara huwaathiri kisaikolojia.
Mojawapo ya masuala nyeti ni fidia. Kwa mfano, baadhi ya wakaazi waliohamishwa na kampuni ya Base Titanium kutoka Nguluku Maumba, wanasema hawakupata fidia inayostahili. Baadhi yao walihamia hadi eneo hilo la Mrima.

Kuhamishwa mara kadhaa
Alloys Musyoka ni mmoja wa wakaazi hao, na anasema endapo atahamishwa kwa mara nyingine, angeomba kuwe na uwazi kuhusu fidia na pia juhudi zao za kuhifadhi misitu. “Kuhamishwa mara ya pili kutoka sehemu ambayo nimelijua kama nyumbani tena kutakuwa pigo kwangu,” alisema.
Wakaazi wanasema kumbukumbu za mashimo na makovu yaliyosalia ni ishara ya athari ambazo hazijarekebishwa. Wanauliza iwapo Serikali na wawekezaji wapya watahakikisha ardhi itarejeshwa katika hali yake kabla ya uchimbaji rasmi kuanza.
Wasiwasi wao si tu kuhusu yaliyopita, bali pia kuhusu mustakabali wa msitu na maisha yao endapo zabuni mpya za utafiti zitatolewa tena, au uchimbaji wa madini kuanza.
“Ili kuepuka sintofahamu, ni sharti wadau wote washirikiane kwa uwazi, wakiwemo Serikali, wawekezaji, wataalamu na jamii. Bila ushirikishwaji wa jamii na marekebisho ya athari zilizopo, Mrima huenda ukabaki na makovu ya kihistoria badala ya kuwa mfano wa uwiano kati ya madini, maendeleo na uhifadhi,” alisema Barroh.
Picha ya bango: George Kimau akionyesha eneo la Mrima ambapo ndani ya ardhi hiyo kuna madini ya niobium. Picha na Asha Bekidusa, Mongabay.