- Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Katavi imefuta hukumu ya kifungo cha miaka 20 jela dhidi ya Elvis Kalonga baada ya kubaini dosari na mkanganyiko katika ushahidi wa upande wa mashtaka kuhusu nyara za Serikali alizodaiwa kumiliki.
- Mahakama ilibaini tofauti kati ya nyara zilizoandikwa kwenye hati ya ukamataji, zilizothaminiwa na zile zilizoorodheshwa kwenye fomu ya uteketezaji wa vielelezo, hali iliyotia shaka mlolongo wa utunzaji wa ushahidi na kuifanya kesi ya mashtaka kutothibitishwa pasipo shaka.
- Hata hivyo, Mahakama ilidumisha hatia ya Kalonga kwa kuingia Hifadhi ya Taifa ya Katavi bila kibali na kubeba silaha, na kumuachia adhabu ya faini ya TSh500,000 kwa kila kosa au kifungo cha miezi 12 iwapo atashindwa kulipa
DAR ES SALAAM, Tanzania – Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Katavi imemuondolea adhabu ya kifungo cha miaka 20 jela Elvis Kalonga aliyetiwa hatiani kwa kukutwa na nyara za Serikali kwa sababu ya dosari na mkanganyiko uliobainika katika ushahidi wa upande wa mashtaka.
Jaji Mfawidhi, Godfrey Isaya ilitoa hukumu Juni 16,2026 baada ya kusikiliza rufani iliyowasilishwa na Kalonga dhidi ya Jamhuri akipinga kutiwa hatiani pamoja na adhabu aliyopewa
Awali, Mahakama ya Wilaya ya Mlele ilimhukumu Kalonga kifungo cha miaka 20 jela kwa makosa manne ya kumiliki nyara za Serikali kinyume cha sheria, pamoja na kosa la kuingia hifadhi ya taifa bila kibali na kubeba silaha ndani ya hifadhi.
Ilidaiwa kwamba Novemba 8, 2025, askari wa Hifadhi ya Taifa ya Katavi walimkamata Kalonga katika eneo la Kasandalala ndani ya hifadhi hiyo akiwa hana kibali na akiwa na silaha mbalimbali zikiwemo panga, shoka, vipande vya nondo, goroli na unga wa baruti.
Pia alidaiwa kukutwa na nyama na viungo vya wanyamapori vinavyokadiriwa kuwa na thamani ya TSh17,800,000.
Sehemu ya ushahidi wa Jamhuri
Upande wa mashtaka ulidai kuwa mshtakiwa alikamatwa ndani ya Hifadhi ya Taifa ya Katavi akiwa na nyara za Serikali na vifaa vinavyohusishwa na uwindaji haramu.
Kwa mujibu wa ushahidi uliotolewa mahakamani, Novemba 8, 2025 askari wanyamapori Joel Kabuga ambaye alikuwa shahidi wa pili (PW2), Christian Ruyemamu (PW3) na Rahimu Hamadi Yusuf (PW4) wakiwa doria eneo la Kasandalala ndani ya Hifadhi ya Taifa ya Katavi waliona moshi ukitoka porini.
Mashahidi hao kwa nyakati tofauti wakidai kuwa walipofuatilia chanzo cha moshi huo walikuta watu watatu, ambapo wawili walitoroka na mmoja, ambaye ni mrufani, akakamatwa.
Mashahidi hao walidai kuwa baada ya kumhoji, mrufani hakuwa na kibali chochote cha kumruhusu kuwepo ndani ya hifadhi hiyo.
Ilidaiwa kuwa upekuzi ulipofanywa kwa mrufani alibainika kuwa na vifaa mbalimbali ikiwemo shoka, panga, magoroli 13, vipande tisa vya nondo na chupa moja yenye unga wa baruti.
Pia alikutwa akiwa na nyara za serikali zinazodhaniwa kuwa za wanyamapori, zikiwemo miguu minne, mikia minne, masikio mawili, kichwa kimoja na vipande 18 vya nyama, bila kuwa na kibali cha kuvimiliki.
Utetezi wa mshtakiwa
Kwa upande wake, mrufani alikana kutenda kosa hilo akidai kuwa siku ya tukio alikuwa akipita tu katika eneo la Mto Kavungu ndani ya Hifadhi ya Taifa ya Katavi alipokamatwa na askari wanyamapori.
Alisisitiza kwamba hakuwa na umiliki wa silaha wala nyara za Serikali zilizodaiwa kupatikana eneo hilo. Kwa mujibu wa utetezi wake, vitu hivyo havikuwa mali yake na hakuwa navyo.
Sababu za rufani
Katika rufani yake, mrufani alipinga hukumu ya Mahakama ya Wilaya kwa kuwasilisha hoja nne.
Hoja ya kwanza alidai Mahakama ya Wilaya ilikosea kisheria kumtia hatiani na kumhukumu wakati upande wa mashtaka haukuthibitisha mashtaka dhidi yake pasipo kuacha shaka yoyote inayostahili.
Alidai pia kuwa Mahakama ilikosea kutegemea hati ya ukamataji wa vielelezo (Kielelezo namba 2) bila kuwepo shahidi huru aliyeshuhudia upekuzi na ukamataji wa vitu vilivyodaiwa kupatikana kwa mrufani.
Mrufani aliendelea kudai kuwa Mahakama ilikosea kutathmini ushahidi wa utetezi, kwa kushindwa kuuzingatia ipasavyo kabla ya kufikia uamuzi wa kumtia hatiani.
Pia alidai Mahakama ilihamisha mzigo wa kuthibitisha kesi kwa mrufani, badala ya kuutwika upande wa mashtaka ambao kisheria una wajibu wa kuthibitisha mashitaka dhidi ya mshtakiwa.
Kutokana na hoja hizo mrufani aliomba Mahakama Kuu ibatilishe hukumu na adhabu zilizotolewa na mahakama ya chini.
Katika usikilizwaji wa kesi hiyo, mrufani alijiwakilisha mwenyewe wakati upande wa Jamhuri uliwakilishwa na Wakili wa Serikali, Kizito Kitandala.
Uamuzi wa Jaji Isaya
Baada ya kusikiliza rufani Jaji Isaya alibaini kuwa kulikuwa na tofauti kubwa kati ya nyara zilizoelezwa katika hati ya ukamataji, zile zilizofikishwa kwa mthamini na zile zilizoorodheshwa kwenye fomu ya uteketezaji wa vielelezo.
Alisema hati ya ukamataji ilionyesha kukamatwa kwa vipande 18 vya nyama pekee, wakati cheti cha uthamini kilijumuisha pia miguu, masikio, mikia na vichwa vya wanyama ambavyo havikuonekana kwenye hati ya ukamataji.
Jaji Isaya alisema ukinzani huo ulizua mashaka kuhusu mlolongo wa utunzaji wa vielelezo na kuifanya Mahakama ishindwe kuamini kuwa nyara zilizothaminiwa ndizo zilizokamatwa kwa mshtakiwa.
Mahakama ilibaini kuwa taratibu za kisheria za kuharibu vielelezo vinavyoharibika haraka hazikufuatwa ipasavyo, hivyo kuondoa fomu ya uteketezaji wa vielelezo kwenye kumbukumbu za kesi.
Kutokana na dosari hizo, Mahakama ilifuta hukumu na adhabu ya miaka minne jela kwa makosa manne ya kumiliki nyara za Serikali.
Hata hivyo Mahakama ilijiridhisha kuwa ushahidi ulithibitisha pasipo shaka kuwa Kalonga alikamatwa ndani ya Hifadhi ya Taifa ya Katavi bila kibali na akiwa na silaha, hivyo ikadumisha hukumu na adhabu ya faini ya TSh500,000 kwa kila kosa au kifungo cha miezi 12 gerezani endapo atashindwa kulipa.
Picha ya bango: Meno ya tembo yakiwa yaliyohifadhiwa kama kielelezo kwenye kesi za jinai. Picha na Maktaba.