- Mnamo Juni 16, Taasisi ya Uhifadhi wa Bahari ilitambua maeneo sita yaliyohifadhiwa baharini, matatu nchini Madagaska na moja kila moja nchini Senegal, Chile na Kanada, kama hifadhi za buluu.
- Tuzo hizo, zilizotangazwa katika kongamano la Our Ocean huko Mombasa, Kenya, zinatambua maeneo yaliyohifadhiwa baharini yaani (MPAs) ambayo usimamizi wao ni wa ” kudumu, usawa na ufanisi” katika kulinda viumbe vya baharini.
- Chini ya Mfumo wa kimataifa wa Bioanuwai wa Kunming-Montreal, nchi zilikubali kulinda 30% ya ardhi, maji safi na maeneo ya baharini ifikapo mwaka wa 2030, lakini wataalam wanasema kwamba ulinzi sharti uwe na maana, si tu wa ishara.
- Mojawapo ya sifa za kawaida za wanaotunukiwa ni kuwa na mifumo ya usimamizi inayowashirikisha watu wa kiasili na jamii za wenyeji.
MOMBASA, Kenya — Katika kongamano la “Our Ocean” mjini Mombasa, Kenya, ujumbe ulisisitizwa katika vikao vyote: Maeneo yaliyohifadhiwa ya baharini (MPAs) ni muhimu katika kulinda bahari.
Tuzo za Blue Park, zilizoanzishwa na Taasisi ya Uhifadhi wa Bahari yenye makao yake makuu nchini Marekani, zinaangazia maeneo yaliyohifadhiwa yanayokidhi viwango vinavyohitajika. Mwaka huu, sita zilitambuliwa<: Eneo Lililolindwa la Bahari la Banc-des-Américains nchini Kanada; Eneo Lililolindwa la Rapa Nui nchini Chile; eneo la turathi ya Jamii asili ya Kawawana nchini Senegali; na Hifadhi ya Kitaifa ya Nosy Hara, Mbuga ya Kitaifa ya Sahamalaza – Îles Radama, na Hifadhi ya Kitaifa ya Nosy Tanihely (pia huandikwa Tanikely) ya Madagaska.
Kongamano hilo lililofanyika mjini Mombasa kuanzia Juni 16-18 lilishuhudia zaidi ya wajumbe 6,000 kutoka serikali mbalimbali, mashirika yasiyo ya faida, sekta ya kibinafsi na taasisi nyingine wakikusanyika kuzungumzia uhifadhi wa bahari.

Chini ya Mfumo wa Kimataifa wa Bioanuwai wa Kunming-Montreal uliopitishwa na washiriki wa Mkataba wa Umoja wa Mataifa wa Anuwai wa Kibiolojia mwaka wa 2022, mataifa yalikubaliana kulinda 30% ya ardhi, maji safi na maeneo ya baharini duniani ifikapo 2030, katika kile kinachofahamika kuwa lengo la 30 kwa 30.
“Kundi hili la hifadhi za buluu ni ukumbusho wa nguvu wa kile ambacho lengo la 30 kwa 30 linahitaji,” Lance Morgan, rais wa Taasisi ya Uhifadhi wa Bahari, alisema katika tangazo la tuzo huko Mombasa mnamo Juni 16. “Maeneo haya sita yaliyohifadhiwa baharini, yanayolinda mifumo mbalimbali ya ikolojia ya baharini chini ya mbinu tofauti za utawala, yanaonyesha kuwa ulinzi mzuri wa baharini unaweza kufikiwa katika tamaduni, mazingira ya kijiografia na mifumo tofauti ya kisiasa.”
Sehemu hizo sita zinawakilisha mifumo mbalimbali ya utawala na zinatofautiana sana kwa ukubwa, kuanzia zaidi ya kilomita za mraba 700,000 (kama maili za mraba 270,000) kwa upande wa Rapa Nui, chini ya kilomita za mraba 5 (1.9 mi2) kwa Nosy Tanihely.
Nosy Tanihely ni sehemu ndogo ya kisiwa katika visiwa vya Nosy Be karibu na pwani ya kaskazini-magharibi ya Madagaska. Kilicho cha kipekee kuhusu hifadhi hiyo ndogo ni kwamba inajifadhili kikamilifu, Landisoa Randimbison, mkurugenzi wa mbuga hiyo, aliiambia Mongabay. Mapato yake yanatokana na ada za watalii, na ndilo eneo pekee lililohifadhiwa nchini Madagaska lililofikia kiwango hicho cha kujitegemea kifedha, alisema.

Sehemu ya Nosy Tanihely haina makazi ya kudumu au makao ya watalii. Usimamizi wake unashirikiwa kati ya Mbuga za Kitaifa za Madagaska (MNP), wakala wa umma unaohusika na maeneo mengi ya hifadhi ya Madagaska, na chama ambacho kinawakilisha washikadau katika kisiwa kikubwa zaidi cha visiwa hivyo, Nosy Be. Hawa ni pamoja na wavuvi na waendeshaji utalii ambao shughuli zao zinaweza kuathiri mfumo ikolojia wa bahari karibu na Nosy Tanihely.
Maeneo yaliyohifadhiwa baharini ya Banc-des-Américains yaasimamiwa kwa pamoja na serikali ya shirikisho ya Kanada, serikali ya mkoa wa Québec, na Mi’kmaq First Nations, ambao ardhi na bahari za mababu zao zinajumuishwa katika eneo hilo.
Jamii hizi zilihusika katika kuanzishwa kwa eneo hilo lililohifadhiwa baharini mnamo mwaka 2019, na zinaendelea kushiriki katika usimamizi unaoendelea wa eneo hilo.
Kwa upande mwingine, kuanzishwa kwa eneo lililolindwa baharini la Rapa Nui kumekuwa na utata zaidi. Eneo hilo kubwa lililohifadhiwa baharini linajumuishaeneo lote la kiuchumi la Rapa Nui (pia linajulikana kama Kisiwa cha Pasaka) na visiwa vya Motu Motiro Hiva, ambavyo ni maeneo ya Chile kusini mwa Bahari ya Pasifiki. Leo, eneo hilo lililohifadhiwa baharini linasimamiwa na jamii asili za wenyeji wa visiwa hivyo na serikali ya Chile. Mongabay imeripoti kuhusu matatizo ya usimamizi wa hifadhi hiyo kabla ya makundi ya Wenyeji kushiriki kama wasimamizi.
Hisia hizi za umiliki na fahari miongoni mwa wajumbe wa Rapa Nui zilionekana wazi katika sherehe ya tuzo. “Eneo hilo si la kulinda spishi tu, mfumo ikolojia au mchakato wa ikolojia. Pia linalinda utamaduni wetu na jinsi tunavyoishi na bahari,” Ludovic Burns Tuki, mratibu mtendaji wa Baraza la Bahari la Rapa Nui, alisema alipopokea tuzo hiyo.

Kawawana ilioko nchini Senegal pia iko chini ya uangalizi wa jamii za karibu. Inalinda mazingira ya pwani na ya mto, ikijumuisha misitu ya mikoko, njia za mawimbi na maeneo ya matope, kando ya Mto Casamance. Ilianzishwa mnamo mwaka 2008 kupitia mpango unaoongozwa na jamii na kikundi cha wavuvi katika manispaa ya vijijini ya Mangagoulack. Serikali iliitambua mwaka wa 2010 kama ICCA (Maeneo Yanayohifadhiwa na Kuhifadhiwa na Watu wa Kiasili na Jamii), ambayo inaunganisha mifumo ya utawala wa kimila na desturi za jadi katika usimamizi.
Eneo jingine ambalo usimamizi shirikishi ni muhimu ni Mbuga ya Kitaifa ya Nosy Hara ya Madagaska, ambayo inahifadhi mojawapo ya maeneo makubwa ya visiwa vya kuzalishia kasa wa baharini, kulingana na Taasisi ya Uhifadhi wa Baharini. Likienea katika zaidi ya kilomita za mraba 1,000, eneo lililohifadhiwa baharini linajumuisha eneo kuu lisilo na uvuvi la kilomita za mraba 310.
Katika ukanda wa matumizi endelevu, wavuvi wanaendelea na shughuli za kitamaduni na za kujikimu. Shirika linaloungwa mkono na serikali la MNP husimamia mbuga hiyo, pamoja na wakaazi, ambao ni sehemu ya kamati ya pamoja ya usimamizi. Jamii pia inahusika katika doria, ufuatiliaji wa ikolojia na kazi ya kujenga ufahamu.
Sahamalaza-Iles Radama, iliyoanzishwa mwaka 2007, ni eneo jingine lililohifadhiwa baharini linalosimamiwa na shirika linaloungwa mkono na serikali la MNP pamoja na jamii za wakazi. Linahifadhi aina zote za mikoko inayojulikana ya Madagaska, mamia ya samaki na spishi za matumbawe, na wanyama wakubwa wa baharini, akiwemo papa nyangumi (Rhincodon typus) na nguva (Dugong dugon).
Hifadhi ya bahari ni sehemu ya hifadhi kubwa ya viumbe hai ambayo eneo la nchi kavu lina spishi nane za komba. Muungano wa Ulaya wa Utafiti na Uhifadhi wa Komba (AEECL) uliunga mkono uundaji wa mbuga hiyo na inaendelea kuandaa shughuli za uhifadhi wa kijamii na kujenga uhamasishaji katika eneo hilo. Hifadhi hii inafadhiliwa, kwa sehemu, na FAPBM (Wakfu wa Maeneo Yaliyohifadhiwa na Bioanuwai ya Madagaska), mfuko wa wakfu binafsi unaopata mapato kutokana na uwekezaji wa fedha za wakfu zilizowekezwa katika masoko ya kimataifa ili kufadhili uhifadhi.
“Ufadhili unasalia kuwa changamoto kubwa. Kuainisha maeneo yaliyohifadhiwa ni hatua ya kwanza tu. Usimamizi mzuri unahitaji uwekezaji wa muda mrefu katika taasisi, sayansi, ufuatiliaji, utekelezaji na ushirikishwaji wa jamii,” Fatou Ndoye, katibu mtendaji wa Mkataba wa Abidjan katika Mpango wa Mazingira wa Umoja wa Mataifa, alisema katika sherehe ya tuzo. Mkataba huo wa kikanda unasimamia rasilimali za baharini na pwani kutoka Mauritania hadi pwani ya Atlantiki ya Afrika Kusini.
Tuzo za Blue Park zilizinduliwa mwaka wa 2017, wakati huo ziliitwa Tuzo za Global Ocean Refuge, na hutolewa kila mwaka. Leo, kuna maeneo yaliyohifadhiwa ya baharini 40 yenye muhuri wa Blue Park, unaofunika jumla ya kilomita za mraba milioni 4.2 (milioni 1.6 mi2) za mali ya baharini katika nchi 30 na maeneo ya Wenyeji asili.

Tuzo hiyo inatambua maeneo yaliyohifadhiwa baharini ambayo usimamizi wao ni “wa kudumu, usawa na ufanisi” katika kulinda viumbe vya baharini.
Lakini kutambuliwa si tukio la mara moja. Mbuga zinazokaguliwa na kubainika kuwa zimeendelea kudumisha viwango vya Blue Park katika miaka inayofuata pia hutuzwa chini ya mfumo. Kwa mfano, mwaka huu hifadhi nyingine mbili barani Afrika, Aldabra Atoll Special Reserve huko Ushelisheli na Kisite-Mpunguti Marine Park and Reserve nchini Kenya, zilitambuliwa kwa kudumisha kiwango chao cha ulinzi.
Ulinzi wa kudumu ni hitaji la wakati huu, wataalamu katika mikutano midogo katika mkutano wa Bahari Yetu walisisitiza.
“Mafanikio hayatapimwa kutokana na idadi ya kilomita za mraba zilizowekwa kwenye ramani,” Ndoye alisema. “Badala yake, mafanikio yatapimwa kutokana na iwapo maeneo haya yanasimamiwa ipasavyo, kama yanafadhiliwa vya kutosha, kama yana uhusiano wa kiikolojia, na kama yanatoa manufaa yanayoonekana kwa viumbe hai na jamii za pwani.”
Picha ya bango: Nosy Tanihely. Picha kwa hisani ya Tanihely National Park Association.
Habari hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza hapa kwa lugha ya Kiingereza mnamo tarehe 24/06/2026.