- Jamii za pwani kutoka Kenya hadi Micronesia zinaonyesha jinsi elimu asili imekuwa msingi wa kulinda bahari, mikoko na rasilimali za uvuvi kwa vizazi vingi.
- Wataalamu wanasema kuchanganya elimu asili na teknolojia za kisasa, kama satelaiti na urejeshaji wa matumbawe, kunaweza kuimarisha uhifadhi wa bahari duniani.
- Bahari hufunika asilimia 71 ya uso wa dunia na kufyonza takriban asilimia 90 ya joto la ziada linalosababishwa na mabadiliko ya tabianchi, zikifanya uhifadhi wake kuwa muhimu kwa binadamu na sayari.
- Kongamano la Our Ocean nchini Kenya liliweka msisitizo mpya kwenye mchango wa jamii za wenyeji katika kufanikisha lengo la kimataifa la kulinda asilimia 30 ya bahari ifikapo mwaka 2030.
Jimmy Muranga kutoka Sokoke, kaunti ya Kilifi, Pwani ya Kenya, anakumbuka vizuri enzi za utoto wake, alipokuwa akikaa na babu yake na kuelezwa hadithi na kupewa mafunzo kuhusu utunzaji wa mazingira.
Wazee walimueleza jinsi maeneo mbalimbali ya bahari, mikoko na misitu ya pwani ilivyo na umuhimu mkubwa kwa maisha ya binadamu. Kupitia simulizi hizo, Muranga alijifunza kuwa mazingira si rasilimali za kutumia tu, bali ni urithi wa kulindwa kwa ajili ya vizazi vijavyo.
Nchini Kenya, ukanda wa pwani wenye urefu wa takriban kilomita 640 ni kitovu cha uchumi wa buluu unaojumuisha uvuvi, utalii, usafiri wa baharini na biashara nyingine zinazotegemea bahari. Karibu watu milioni nne wanaishi katika eneo la pwani, huku maelfu ya wavuvi na makumi ya maelfu ya kaya wakitegemea rasilimali za bahari kwa riziki zao. Hali hiyo inaifanya uhifadhi wa bahari kuwa muhimu si tu kwa mazingira bali pia kwa ustawi wa uchumi wa taifa.
Muranga, ambaye sasa ni mvuvi na pia mwenyekiti wa kikundi cha kijamii cha kulinda misitu cha Sokoke, ana jukumu la kuhakikisha kuwa anapitisha elimu hiyo kwa jamii, hasa kwa vizazi vichanga, ili ihifadhiwe kwa vizazi vijavyo.

Mikoko ni misitu ya kipekee inayostawi katika maeneo ya maji ya chumvi kwenye fukwe za bahari za kanda za kitropiki. Misitu hii huunganisha nchi kavu na bahari, ikifanya kazi muhimu katika kulinda mazingira na ustawi wa jamii za pwani.
“Zamani tulikuwa tukikalishwa na mababu zetu tukisimuliwa hadithi na kanuni za kijamii ambazo zilikuwa zinalinda mazingira. Kwa mfano, kuna misitu fulani tuliambiwa haiangaliwi, kwa hivyo tukipita hapo tulikuwa tunaogopa hatuwezi kuiangalia. Hivyo haikuwa rahisi kwa watu kuusongelea na kufanya uharibifu,” alisema Muranga.
Elimu hiyo asili haikuishia kwa misitu pekee, ilifika hadi baharini. Kulingana na Muranga, bahari ilichukuliwa kama eneo takatifu, lisilofaa kutumiwa visivyo. Endapo mtu angeiharibu basi angepata laana kutoka kwa roho za mababu au bahari.
Umuhimu wa mikoko unaonekana pia katika tafiti za kimataifa. Umoja wa Mataifa unasema mikoko ni miongoni mwa mifumo ya ikolojia yenye uwezo mkubwa zaidi wa kuhifadhi kaboni duniani, ikiwa na wastani wa tani 1,000 za kaboni kwa hekta katika miti na udongo wake. Aidha, mikoko huchukua kaboni kwa kasi inayoweza kuwa mara mbili hadi nne zaidi kuliko misitu mingi ya nchi kavu, huku ikilinda fukwe dhidi ya mawimbi na kuwa mazalia muhimu ya samaki.
Ili kuhakikisha kuwa kulikuwa na uvuvi endelevu, wazee waliweka marufuku ya kuvua wakati wa msimu wa kusi. Pia wavuvi walionywa wasivue katika maeneo yaliyokuwa na matumbawe. Hii ilitoa fursa kwa samaki kuzaana.
Wazee pia walitumia mitego maalum ya kuvua samaki iitwayo mugono. “Mugono, ulikuwa na umbo la mviringo ambapo samaki huingia ndani kupitia mlango maalumu, lakini hawezi kutoka. Mitego hiyo pia ilikuwa rafiki sana kwa bahari na viumbe vyake.
“Iliundwa kwa namna kwamba samaki wadogo walikuwa na nafasi ya kupita na kutoka kupitia mianya iliyokuwapo, huku samaki wakubwa wakibaki ndani. Hivyo walikuwa wanavua samaki waliokomaa na kuwaacha wale wadogo waendelee kukua na kuzaliana kwa ajili ya kizazi kijacho,” Muranga aliiambia Mongabay.
Katika visiwa vya Zanzibar, vilivyoko Bahari ya Hindi, takribani kilomita 35 kutoka pwani ya Tanzania Bara, jamii katika eneo hilo zimekuwa zikitumia elimu asili kulinda na kusimamia rasilimali za baharini.
Mohammed Juma, Msimamizi Mshirikishi wa Utawala wa Rasilimali za Bahari katika Shirika la Mwambao Zanzibar, alisema utumiaji wa elimu asili katika kuhifadhi mazingira ya baharini sio jambo jipya katika jamii za eneo hilo. Shirika hilo linahamasisha na kusaidia jamii kutunza rasilimali za bahari ili waweze kufaidika nazo, na kuhakikisha kwamba zinabakia kuwa salama kwa kizazi cha sasa na kizazi kijacho.
“Kabla ya kuanzishwa kwa mifumo ya kisasa ya usimamizi na uhifadhi wa mazingira ya bahari, wazee wetu walikuwa tayari wameweka kanuni na desturi zilizolenga kulinda rasilimali za bahari. Kwa mfano, ukienda kwenye misitu, walikuwa wakikuambia kwamba aina fulani ya miti usikate, sehemu fulani usiende. Hata baharini walikuwa na mbinu zao. Wavuvi walielewa nyakati za kuvua aina fulani ya viumbe wa baharini na nyakati za kuviacha ili viweze kuzaliana na kuongezeka,” alieleza Juma.
Juma alisema kwa kawaida, vipindi vya uhifadhi vilihusishwa na matukio muhimu ya kijamii na kitamaduni. Jamii zilifunga maeneo ya uvuvi kabla ya sherehe kubwa ili kuhakikisha kuwa wakati wa kufungua maeneo hayo kunakuwa na mavuno mengi yatakayokidhi mahitaji ya wanajamii.
Mbali na kuimarisha uhifadhi wa mazingira, alisema mfumo huo uliimarisha mshikamano wa kijamii. Wanajamii walishiriki kwa pamoja katika kusimamia maeneo yaliyohifadhiwa na walifaidika kwa pamoja baada ya maeneo hayo kufunguliwa.
“Tulikuwa tunafanya sana wakati jamii zinajiandaa kwa shughuli kama sherehe za Eid, shughuli za kimila na matukio mengine ambayo hufanyika kila mwaka katika jamii zetu. Tulikuwa tunafaidika kwa sababu kwanza inaleta jamii pamoja, pili, mazao yanakuwa mengi wakati tunafungua sehemu za kuvua baharini,” alisema Juma.
Juma alisema kwa sasa wanatumia elimu asili pamoja na mbinu za kisasa katika kuhifadhi bahari na kuhakikisha uvuvi endelevu wa pweza.
“Kwa upande wa jamii ninayotokea, kwenye masuala ya uhifadhi wa pweza tulikuwa tunatunza kwa muda wa mwezi mmoja. Lakini sasa tumejaribu kupatiwa ujuzi na utaalamu mpya ambao unatuwezesha kuhifadhi kwa muda wa miezi mitatu, jambo ambalo linatoa mazao bora zaidi na kuboresha ikolojia ya bahari,” alisema Juma kwenye mahojiano na Mongabay.
Kulingana na Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO), bahari ni mfumo mkubwa zaidi wa ikolojia wa sayari ya dunia unaodhibiti hali ya hewa na kuwezesha maisha kwa mabilioni ya watu.
Takwimu za Shirika la Hali ya Hewa Duniani zinaonyesha kuwa bahari hufunika takriban asilimia 71 ya uso wa dunia na hubeba karibu asilimia 97 ya maji yote duniani. Pia takriban asilimia 40 ya watu duniani wanaishi ndani ya kilomita 100 kutoka pwani na hutegemea bahari kwa chakula, ajira na riziki zao, jambo linaloonyesha umuhimu wa kulinda mifumo ya ikolojia ya baharini.
Zaidi, shirika hilo linasema kuwa bahari inachukua takriban asilimia 90 ya joto la ziada la dunia. Shughuli za uchumi wa baharini huzalisha mapato ya mabilioni ya dola na kutoa chakula kwa mabilioni ya watu.
Lakini mabadiliko ya tabianchi, na uvuvi usio endelevu ni miongoni mwa sababu ambazo zimeathiri bahari na kuongeza hatari ya majanga kwa mamilioni ya watu duniani.
Mbali na athari za mabadiliko ya tabianchi, Shirika la Hali ya Hewa Duniani linasema kuwa uvuvi kupita kiasi, uchafuzi wa mazingira na ongezeko la joto baharini vinatishia riziki za takriban watu milioni 600 duniani wanaotegemea mifumo ya bahari kwa maisha yao.
Kutokana na hatari hizo, wakereketwa wa maswala ya uhifadhi wa mazingira wamekuja na mbinu mbalimbali za kulinda bahari, ikiwemo matumizi ya elimu asili.
Ujumuishaji wa elimu asili ni mojawapo ya mapendekezo yaliyotolewa katika kongamano la Our Ocean lililofanyika jijini Mombasa, Kenya, na ambalo lilikuwa la kwanza kuandaliwa Afrika.
Elimu asili hujumuisha mbinu mbalimbali zinazotofautiana kimaeneo dunia nzima, lakini lengo ni kuilinda na kuitunza bahari.
Katika maeneo ya pwani ya Afrika Kusini, jamii za kiasili zimeishi kwa uhusiano wa karibu sana na bahari, huku elimu asili na tamaduni za kulinda mazingira ya bahari zikiwa msingi wa juhudi zao za uhifadhi.
Wataalamu wa UNESCO wanasema mifumo ya “blue carbon” kama mikoko, nyasi za baharini na maeneo ya chumvi inaweza kuhifadhi kaboni mara mbili hadi nne zaidi kuliko misitu ya nchi kavu. Hata hivyo, karibu nusu ya maeneo ya asili ya mifumo hiyo duniani tayari yamepotea tangu karne ya 19 kutokana na shughuli za binadamu na mabadiliko ya tabianchi.
Neville van Rooy, kutoka shirika la Green Connection, linalopigania haki ya mazingira nchini Afrika Kusini, alisema jamii bado zina nafasi kubwa katika kulinda mazingira kupitia elimu asili.

“Jamii asili zinajua mazingira yao vizuri sana. Watakuambia ikiwa ni vizuri au vibaya kuvua sehemu fulani, na wataeleza sababu za kufanya au kutofanya shughuli fulani katika maeneo au nyakati fulani,” alieleza Rooy.
Kulingana na Rooy, kutokana na umbali wa huduma muhimu kama hospitali kwa jamii kadhaa za wavuvi eneo hilo, walitumia mbinu asili za uhifadhi wa bahari kujipatia dawa hasa wanapoumwa na nyoka. Hali hiyo ilisababisha jamii hiyo ya wavuvi kutenga eneo maalum ambalo wavuvi hawakuruhusiwa kuvua kwa sababu ni eneo la kutafuta tiba.
Kwa kufanya hivyo, Rooy alisema hakuna mtu aliyekiuka. “Jamii moja ya wavuvi ilikuwa mbali sana na huduma za matibabu. Kwa hivyo mtu alipoumwa na nyoka, kuna viumbe au mimea ya baharini ambayo huvunwa na kutumika kama tiba. Kwa hivyo eneo hilo la bahari lilikuwa limetengwa hususan kuvuna tiba hiyo,” alisema Rooy.
Katika visiwa vya Pohnpei na Chuuk, vilivyoko katika Federated States of Micronesia (FSM), jamii za kiasili zimekuwa zikiishi kwa uhusiano wa karibu sana na mazingira ya bahari na ardhi kwa kuzingatia tamaduni zao, huku wakilinda mazingira hayo.
Mwanabiolojia wa bahari na mtetezi wa utamaduni na mazingira kutoka visiwa hivyo, Nicole Yamase, ambaye pia ni “Mkurugenzi wa Athari” kutoka shirika la OneReef, alisema elimu ya asili ina jukumu kubwa katika kuelewa uhusiano wa binadamu na mazingira.

Kulingana na Yamase, katika jamii za FSM, hasa Chuuk, walitumia mbinu za kufungwa kwa muda kwa maeneo ya uvuvi ili kuruhusu mazingira kujirejesha.
Zaidi, alisema mbinu hiyo hutumika kama sehemu ya mila za kijamii, hasa wakati wa matukio ya msiba au maombolezo. Wakati mtu anapofariki, jamii inaweza kufunga maeneo ya bahari na ardhi kama ishara ya heshima na pia kama njia ya kuhifadhi rasilimali.
“Kwa mfano, mtu akifariki, jamii itaweka jani la mnazi eneo la nchi kavu au baharini kuashiria kwamba eneo hilo limefungwa. Muda wa kufungwa hutegemea nafasi ya marehemu katika jamii, ambapo viongozi wa hadhi ya juu huweza kupewa muda mrefu zaidi wa heshima na ulinzi wa eneo, kama mwezi mzima.
“Baada ya kipindi hicho, jamii hukusanyika pamoja kuvua samaki maeneo hayo na kufanya sherehe kubwa kusherehekea maisha ya aliyefariki,” alieleza Yamase.
Hata hivyo, alisema kuna hatari ya mbinu asili za kulinda mazingira ya bahari kuangamia endapo hazitanakiliwa na kutumiwa na vizazi vya sasa. Katika juhudi za kulinda mazingira ya bahari Barani Afrika na dunia nzima kwa ujumla, wataalamu wa sayansi ya bahari wanasema kuna haja ya kujumuisha elimu asili na teknolojia ya kisasa, pamoja na kuzingatia sheria za kitaifa na kimataifa.
Daktari Nina Wambiji, mwanasayansi wa uvuvi wa baharini kutoka Taasisi ya Utafiti wa Bahari na Uvuvi Kenya (KMFRI), ambaye pia ni makamu wa rais wa Western Indian Ocean Marine Science Association (WIOMSA), alisema uhifadhi wa mazingira ya bahari unahitaji mashauriano ya karibu na washikadau mbalimbali na kujumuisha mbinu za asili na za kisasa.

Kulingana na Wambiji, mbinu za kisasa za kuhifadhi mazingira ya bahari, ikiwemo teknolojia ya upandaji wa matumbawe katika maeneo yaliyoharibika ili kurejesha uhai wa miamba ya baharini, pamoja na matumizi ya satelaiti kufuatilia uchafuzi wa maji na mabadiliko ya mazingira, zinasaidia kuona kinachoendelea baharini na kuja na mbinu za kutoa suluhu.
Aidha, alisema maeneo madogo ya uhifadhi yanayosimamiwa na jamii yana mchango mkubwa, na yakijumuishwa yanaweza kuleta matokeo makubwa zaidi ya kitaifa na kikanda hasa katika juhudi za kuafikia mpango wa 30x30.
Lengo la 30x30 ni ahadi ya kimataifa ya kulinda na kuhifadhi angalau asilimia 30 ya bahari na ardhi ya dunia ifikapo mwaka 2030. Mpango huu unalenga kurejesha afya ya viumbe vya baharini, kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, na kulinda riziki za jamii za wavuvi.
Aidha juhudi zaidi za kimataifa ambazo tayari zimeanza kufanya kazi ni pamoja na mkataba wa kimataifa wa Biodiversity Beyond National Jurisdiction (BBNJ). Huu ni mkataba muhimu wa kihistoria wa Umoja wa Mataifa wa kulinda bahari kuu, ulioanza kutumika rasmi tarehe 17 Januari 2026.
Lengo la BBNJ ni kusimamia uhifadhi na matumizi endelevu ya viumbe vya baharini na kufanikisha ahadi ya 30×30.
Picha ya bango: Kongamano la 11 la Our Ocean liliofanyika jijini Mombasa, Kenya kati ya tarehe 16 na 18 Juni 2026. Picha na Malavika Vyawahare, Mongabay.