- Akiwa na umri wa miaka 13 pekee, Baraka Moruri tayari amepanda zaidi ya miti 7,600 na ana ndoto ya kufikia miti milioni moja kabla ya kutimiza miaka 18.
- Mshindi wa taji la Little Mr Environment Kenya anatumia kitabu chake Go Green With Baraka kuhamasisha watoto kushiriki katika uhifadhi wa mazingira.
- Baraka anasema watoto wanapaswa kupewa nafasi kubwa zaidi katika maamuzi kuhusu mabadiliko ya tabianchi kwa kuwa wao ndio watakaoishi na athari zake kwa muda mrefu zaidi.
- Licha ya changamoto za ufadhili na kubezwa kutokana na umri wake mdogo, anaamini watoto si wahanga wa tabianchi pekee bali pia sehemu muhimu ya suluhisho.
Ni saa moja asubuhi. Mbwa wawili aina ya Chihuahua wanaonekana kuwa waangalifu kwa uwepo wa mgeni kwenye lango la nyumba ya familia ya Moruri Baraka. Dakika chache baadaye, Baraka anashuka ngazi akiwa ameshika kichanuo mkononi na kujiandaa kwa mahojiano. Dada yake mdogo, ambaye bado hajatimiza miaka sita, anajiunga naye na mara kwa mara hujitosa kujibu baadhi ya maswali. Msichana huyo ni mmoja wa mashabiki wake wa karibu. Baraka, mwenye umri wa miaka 13, ameibuka kuwa mmoja wa watetezi vijana wa mazingira wanaotikisa mawimbi nchini Kenya
Baraka alianza kuwa na mapenzi na masuala ya mazingira tangu alipokuwa na umri wa miaka sita. Kufikia Machi 2026, tayari alikuwa amepanda zaidi ya miti 7,600 kwa msaada wa familia na marafiki zake. “Lengo langu halina kikomo. Nataka kupanda zaidi ya miti milioni moja kabla sijafikisha umri wa miaka 18,” anasema.
Mafanikio yake makubwa yamekuwa uzinduzi wa kitabu kiitwacho Go Green With Baraka, kinachosimulia shughuli zake za kuhifadhi mazingira kwa msaada wa familia yake. Kitabu hicho kimeandikwa kwa herufi kubwa na lugha rahisi ambayo mtoto anaweza kuielewa na kuhamasika kuitikia wito uliomo ndani yake.
Baraka anatumaini kuwa kitabu hicho kitaingizwa katika mtaala wa elimu wa Kenya lakini pia kitapatikana katika maduka mengi zaidi ya vitabu pamoja na majukwaa ya mtandaoni kama Amazon.


Baraka anatambulika kama mwanamazingira mdogo zaidi nchini Kenya na ndiye mshindi wa taji la Little Mr Environment Kenya na pia ni balozi wa mpango wa Plant Your Age, ulioanzishwa baada ya mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel, Profesa Wangari Maathai, kufariki dunia mwaka 2011, akiwa na umri wa miaka 71. Wakati huo, mwanaharakati wa mazingira Isaac Kalua, ambaye pia ni mshauri wa Baraka, alipanda miti 71 kwa heshima ya Wangari.
Baraka anasema msukumo wake wa kuendelea kutetea na kulinda mazingira unatokana na harakati za Wangari Maathai.
“Siku moja, nilipokuwa nafanya kazi ya darasani ya somo la Kilimo iliyohusisha kufanya utafiti kuhusu Profesa Wangari Maathai, nilitazama video ambayo ilionyesha jinsi alivyokuwa akinyimwa haki zake. Baadaye alipata Tuzo ya Amani ya Nobel kutokana na mchango wake katika uhifadhi wa mazingira, maendeleo endelevu na amani. Nilipata hamasa sana. Natamani kufikia mafanikio kama hayo. Kwa hakika alikuwa analinda mazingira kwa ajili ya vizazi vya sasa na vijavyo, kwa sababu alielewa athari za mabadiliko ya tabianchi katika siku zijazo,” anasimulia Baraka.
Kama mkulima, mfanyabiashara au msafiri anavyoweza kuathiriwa na hali ya hewa isiyotabirika, Baraka anasema watoto pia hupata wasiwasi wanaposhindwa kutabiri ni lini wataweza kutoka nje na kucheza. “Na wakati wa mafuriko au hali ya joto kali, hatuwezi kuzingatia masomo shuleni wala kushiriki katika shughuli za ziada za masomo,” anasema.
Mara zote Baraka hutafuta taarifa mpya kuhusu mabadiliko ya tabianchi. Tukio baya zaidi aliloshuhudia ni mafuriko ya Machi 2026 nchini Kenya, ambayo kwa mujibu wa OCHA yaliua watu 110 na kuwafanya watu 34,700 kuyahama makazi yao. Kilichomhuzunisha zaidi kuhusu namna janga hilo lilivyoshughulikiwa, ni kushindwa kuwaona marafiki zake.
“Hatukuweza kuwaona marafiki zetu. Janga liliua watu wengi. Kwa namna fulani lilinifanya nitambue kwamba Kenya inahitaji kuchukua suala la mabadiliko ya tabianchi kwa uzito zaidi kwa sababu mafuriko yanachochewa na mabadiliko ya tabianchi na shughuli za binadamu, athari ambazo zinaweza kupunguzwa kupitia maandalizi na hatua za kukabiliana nazo,” aliiambia Mongabay.
Baraka anaendelea kueleza kuhusu maandalizi ya kukabiliana na majanga. Anasema: “Tungeweza kufanya mengi kuzuia vifo vilivyotokana na (mafuriko ya Machi 2026), hasa kwa kufungua na kusafisha mifereji ya maji iliyoziba.” Pia anafuatilia kwa karibu mambo yanayoendelea jijini Nairobi, ambako mifereji mibovu na iliyoziba ilisemekana kuchangia kuongezeka kwa athari za mafuriko.

Kwa sasa, Baraka ana wasiwasi kuhusu watu wanaoamini kwamba majanga yanayosababishwa na mabadiliko ya tabianchi ni adhabu kutoka kwa Mungu. Hata hivyo, anasisitiza kwamba sayansi inaonyesha shughuli za binadamu ndizo zinazochangia mabadiliko ya tabianchi.
“Katika kitabu cha Biblia cha Mwanzo, mwanadamu ameagizwa kulima na kuitunza ardhi kama msimamizi wa mazingira. Lakini tunafanya kinyume chake kupitia ukataji miti ovyo, uvunaji wa mbao na kutopanda miti mipya kuchukua nafasi ya ile iliyokatwa. Kwa hiyo ni adhabu kwa sababu tunakiuka amri ya Mungu,” anasema, huku akisisitiza umuhimu wa kuzingatia sayansi ya mabadiliko ya tabianchi.
Baraka amemshawishi nyanya yake kuhusu umuhimu wa kulinda mazingira. Sasa nyaya yake ametenga eneo maalumu la ardhi kwa ajili ya kupanda miti na huwaalika watoto kumtembelea ili washiriki katika upandaji miti.
“Kwa namna fulani anapambana na mabadiliko ya tabianchi kwa sababu nilitumia muda kumweleza kuhusu sayansi inayohusika. Kwa mtazamo wangu kila mtu katika familia yangu, pamoja na marafiki ambao wamekuwa wakihudhuria matukio yangu, wanafahamu kuhusu mabadiliko ya tabianchi. Hali ni hiyo pia katika baadhi ya shule kama White Star na Hillcrest School, ambako nimesaidia kupanda miti,” anasema.

Hata hivyo, safari yake kama ilivyo kwa wanaharakati wengine wa mazingira si rahisi. Changamoto kubwa inayomkabili Baraka ni kubezwa na baadhi ya watu kutokana na umri wake mdogo. “Watu hawaamini kizazi hiki (Alpha), lakini niko hapa kuthibitisha kuwa wamekosea na kuwakumbusha kwamba hata watoto wana mawazo mazuri na wanaweza kuwa vinara wa hatua za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi,” anasema.
Novemba mwaka 2023, Baraka, familia yake pamoja na marafiki zake waliandaa matembezi kuhusu mabadiliko ya tabianchi, ambayo, kwa mujibu wake, yalijumuisha burudani na mafunzo muhimu. Siku hiyo walipanda zaidi ya miti 2,000.
Baraka pia anafahamu changamoto ambazo wakulima hukabiliana nazo kutokana na kutotabirika kwa hali ya hewa. “Katika kipindi ambacho kawaida huwa cha ukame, mvua hunyesha, na misimu iliyokuwa ya mvua sasa imegeuka kuwa vipindi virefu vya ukame. Wakulima hawajui ni wakati gani wa kupanda mazao. Hili linaathiri usalama wa chakula,” aliiambia Mongabay.
Ripoti ya Africa Climate Awareness Report 2023 iliyoangalia uelewa kuhusu mabadiliko ya tabianchi miongoni mwa jamii za Afrika inatia matumaini, inasema: “Wengi wa washiriki walikuwa wanafahamu namna ambavyo mabadiliko ya tabianchi yanaathiri mataifa yao, huku asilimia 65 wakiona athari hasi hasa kwenye upatikanaji wa chakula. Uelewa kuhusu kuongezeka kwa mafuriko na ukame ulifikia asilimia 57.”
Hata hivyo, ripoti hiyo inaonyesha tofauti za kiwango cha uelewa kati ya makundi mbalimbali ya watu. “Kwa ujumla, watu wazima walikuwa na uelewa mkubwa zaidi kuhusu athari za mabadiliko ya tabianchi kuliko vijana.”
Kiu ya Baraka ni kuona watoto wengi zaidi wakishiriki kikamilifu katika hatua za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi. “Viongozi wasituache nyuma. Sisi pia tuna mawazo na nguvu za kusaidia kupambana na mabadiliko ya tabianchi,” anasema.


Pia anatamani kuhudhuria mkutano wa COP31 ili kuwasilisha ujumbe huo kwa viongozi wa dunia katika mazungumzo ya kila mwaka kuhusu tabianchi. “Mimi si mtoto pekee ninayetetea hatua za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi. Tukifanya kazi kwa uthabiti, watoto wengi zaidi watapata matumaini,” anasema.Jitihada za Baraka zinaakisi mwelekeo mpana zaidi wa kuongezeka kwa uelewa wa mabadiliko ya tabianchi barani Afrika.
Ripoti ya mwaka 2025 ya Afrobarometer yenye jina “Adapting to a Changing Climate, the Importance of Climate Literacy”, inayosisitiza umuhimu wa “kufahamu kiwango cha uelewa wa umma na mitazamo ya watu kuhusu sababu za mabadiliko ya tabianchi” ili kutengeneza sera bora, inaonyesha kwamba “kwa wastani katika nchi 38, zaidi ya nusu ya wananchi (asilimia 56) wanasema wamewahi kusikia kuhusu mabadiliko ya tabianchi.”
Ripoti hiyo inaonyesha kuwa kiwango cha juu zaidi cha uelewa kilirekodiwa nchini Seychelles kwa asilimia 91, Mauritius kwa asilimia 83, Gabon kwa asilimia 79, Malawi kwa asilimia 77, na Cabo Verde kwa asilimia 76. Kiwango cha chini zaidi cha uelewa kilirekodiwa katika nchi za Mauritania kwa asilimia 31 na Nigeria asilimia 27.
Ili kuziba mapengo haya ya maarifa kati ya nchi na makundi mbalimbali ya watu, wadau kadhaa wanafanya juhudi za kuongeza uelewa kuhusu mabadiliko ya tabianchi na kuhamasisha hatua za kukabiliana nayo, mara nyingi wakiongozwa na mikataba na makubaliano ya kimataifa.
Kenya ni miongoni mwa nchi zilizotia saini Mkataba wa Umoja wa Mataifa wa Haki za Watoto wa mwaka 1989, ambao unaongozwa na misingi minne mikuu: kutobagua, kuzingatia maslahi bora ya mtoto, haki ya kuishi na kuendelea kukua, na kuheshimu maoni ya mtoto.
Utafiti unaonyesha baadhi ya sababu zinazowazuia vijana kushiriki kikamilifu katika hatua za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi kuwa ni pamoja na uhaba wa fedha, ukosefu wa maarifa na uelewa wa kutosha, kukosekana kwa utashi wa kisiasa, elimu duni kuhusu masuala ya kifedha, upatikanaji mdogo wa masoko pamoja na fursa finyu za huduma za kifedha.
Hali hii inaonekana pia katika kisa cha Baraka, ambapo hakuna chanzo cha wazi cha ufadhili wa miradi yake. “Karibu kila kitu anachofanya Baraka hufadhiliwa na mimi. Mwanzoni sikuwa na uelewa wa kutosha kuhusu mabadiliko ya tabianchi na nilimsaidia tu kufuata kile alichokipenda. Lakini sasa ninaanza kuona umuhimu wa kile anachofanya na gharama zinazohusika. Ninashukuru marafiki wachache na taasisi zinazotoa miche ya miti na kusaidia kwa njia mbalimbali mara kwa mara. Lakini tunahitaji msaada zaidi,” anasema Lawrine Moruri, mama mzazi wa Baraka.
Collins Otieno, mkurugenzi wa Africa Youth Climate Fund, anaeleza kuwa tatizo hili ni la kimfumo na linaanzia ngazi za juu ambako fedha nyingi za tabianchi zinapaswa kutoka. Anasema kiasi cha fedha za kimataifa za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi kinachowafikia watoto na vijana, ni chini ya asilimia moja, jambo analolihusisha kwa kiasi fulani na ukosefu wa uwezo wa kuelewa na kusimamia mifumo ya ufadhili.

Tatizo lingine ni ukosefu wa uwezo wa kushughulikia kiasi kikubwa cha fedha. “Hili ni suala la taasisi na linapaswa kuongozwa na sera au mifumo ya kisheria. Utatumia njia ipi kupokea fedha ikiwa hakuna muundo rasmi wa kuzisambaza? Katika ngazi ya kitaifa pia kuna wizara mbalimbali zinazofanya kazi kila moja kivyake, hata kama zote zinahusika kwa namna fulani na masuala ya watoto,” anasema Otieno. Anaongeza: “Tuna mfumo ambao umeundwa kuwapuuza vijana na watoto, kuanzia ndani ya familia hadi katika jamii kwa ujumla.”
Otieno anapendekeza kuwepo kwa taasisi ya kati ya kusimamia na kufikisha fedha za tabianchi kwa watoto. “Tunahitaji sera ambazo zinaweza kubadilisha mfumo unaowezesha mamlaka katika usimamizi wa fedha za tabianchi kuwa mikononi mwa wachache. Fedha bado zinashikiliwa na Hazina ya Taifa, lakini tunahitaji mifumo inayowezesha upatikanaji wake kiurahisi,” anasema Otieno.
Anasema watoto na vijana wanapaswa kushiriki katika mijadala kuhusu fedha za tabianchi. “Kwa sasa Afrika inajadili mifumo mbalimbali ya fedha za tabianchi (katika SB64), lakini ni nani atakayelipa madeni haya? Watoto ndio watakaolipa kupitia kodi katika siku zijazo,” anasema.
Baraka anaonekana kutofahamu sana changamoto za kifedha zinazomzunguka, na katika mahojiano yote hatilii mkazo suala la fedha. Ana ndoto kubwa zaidi, ikiwemo kuanzisha shule itakayokuwa kinara wa uhifadhi wa mazingira. Anaamini kuwa uelewa kuhusu mabadiliko ya tabianchi shuleni unaweza kuboreshwa zaidi.
Kumekuwa na juhudi za kuingiza elimu ya mabadiliko ya tabianchi katika mitaala ya shule za umma nchini Kenya. Makubaliano yaliyotiwa saini kati ya mashirika matatu mwaka 2024, yalilenga kuongeza ujumuishaji wa elimu ya tabianchi katika elimu ya awali, ingawa utekelezaji wake bado unaendelea.
Kwa mujibu wa Dorcas Aid, shirika la kimataifa lisilokuwa la serikali, “Shule ni sehemu muafaka kwa ajili ya miradi inayolenga kuleta mabadiliko kwa kuwa zinatoa mazingira mazuri ambayo watoto wanaweza kujifunza na kushiriki kikamilifu katika shughuli kama upandaji miti.”

Baraka anasema anapotembelea shule, huwaelezea watoto kuhusu mabadiliko ya tabianchi kwa njia rahisi na yenye kuwafurahisha. Watoto huuliza maswali mengi. Anasema hata katika maeneo yasiyo na nafasi ya kupanda miti, “Nawaeleza njia nyingine za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, ikiwa ni pamoja na kutumia magari ya umeme, kuzima taa na kufunga mabomba ya maji yasipotumika. Pia kuna mimea ya ndani ya nyumba inayoweza kusaidia katika kupunguza athari za mabadiliko ya tabianchi.”
Juma Ignatius, Mshauri Mkuu wa Sera wa Kimataifa katika shirika la World Vision International, anasema ushiriki wa watoto katika harakati za kukabiliana na tabianchi unapaswa kujumuisha uwezo wa kushawishi sera.
“Watoto wataishi muda mrefu zaidi kuliko kizazi cha sasa cha watu wazima. Hatuwezi kufanya chochote bila wao. Hili si tatizo la Kenya pekee. Hata katika matukio makubwa ambapo watoto huonekana kuwakilishwa, mara nyingi utawakuta kwenye mijadala wakitumia maandishi yaliyoandaliwa na watu wazima,” anaiambia Mongabay.
Anasema kimataifa, baadhi ya majukwaa kama mikutano midogo ya COP ambayo huwaunganisha watoto na watunga sera, yameonyesha mafanikio. “Nilikutana na mtoto kutoka Visiwa vya Solomon nchini Brazil katika moja ya mikutano hiyo, ambaye alikuwa na uwezo mkubwa wa kujieleza. Kulikuwa pia na mtoto kutoka Tanzania. Lakini mara nyingi mipango hiyo inaongozwa na mashirika ya kiraia badala ya serikali,” anasema.
Juma anapendekeza kuwepo kwa sera ya kudumu inayohakikisha mataifa yanapoandaa misimamo ya nchi wakati wa mikutano ya COP au Mikutano ya Mawaziri wa nchi za Afrika kuhusu mazingira, sauti za watoto lazima zisikike. “Mabadiliko ya tabianchi huwaathiri watoto kwa namna tofauti. Mkulima atakuwa na wasiwasi kuhusu misimu ya kupanda, lakini kwa mtoto, suala ni jinsi hali ya hewa inavyomwezesha kucheza na kuendelea na maisha yake ya kila siku,” anasema.
Watafiti wanapendekeza uwekezaji katika kujenga maarifa, ujuzi na rasilimali zinazohitajika ili vijana washiriki kikamilifu katika hatua za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi. “Badala ya kupunguza thamani ya mchango wao, ni muhimu kuzingatia maoni, mitazamo na uzoefu wao wakati wa kuunda sera jumuishi. Sera inaweza kutamka kwamba angalau asilimia 40 ya wanachama katika kila mpango au taasisi inayohusiana na tabianchi wawe vijana ili kuhakikisha mitazamo yao inazingatiwa katika utungaji wa sera,” wanasema.
Kwa sasa Kenya inaimarisha sera zitakazowezesha watoto kushiriki katika shughuli kama ubingwa wa mazingira, kama inavyoonekana katika Rasimu ya Sera ya Watoto ya Kenya. “Kwa kutambua changamoto za kipekee zinazowakabili watoto nchini Kenya, sera hii inalenga kushughulikia masuala kama umaskini, tofauti za kiafya, vikwazo vya elimu, pamoja na athari za ukatili na unyanyasaji. Lengo letu ni kuunda mazingira ambayo kila mtoto anaweza kustawi, akifaidika na haki zake za msingi za kuishi, kukua, kulindwa na kushiriki,” anaeleza Carren Ageng’o katika waraka huo.
Katika wito wake wa kuomba kuidhinishwa kwa sera hiyo, Alfred Mutua anasema: “Sera ya Watoto ya Kenya ya mwaka 2025 si waraka wa kawaida tu; ni ahadi kwa watoto wetu na wito kwa watu wote kuchukua hatua.”

Takwimu za UNICEF zinaonyesha idadi ya watoto wenye umri wa chini ya miaka 18 nchini Kenya ilikuwa 24,943,382 kufikia mwaka 2025. Kazi ya Baraka inaweza kuonekana kama tone la maji baharini ikilinganishwa na juhudi za Kenya kupanda miti bilioni 15 ifikapo mwaka 2030. Hata hivyo, anasema mwaka 2026 anataka kutoka kwenye uhamasishaji hadi hatua ya utekelezaji.
Hataki watoto waonekane tu kama kundi lililo hatarini kutokana na athari za mabadiliko ya tabianchi, bali kama wadau muhimu katika kutafuta na kutekeleza suluhisho za tabianchi ndani na nje ya nchi.
Baada ya mahojiano, Baraka anaondoka kwenda kucheza na marafiki zake. Ni picha ya kawaida ya utoto. Hata hivyo, nyuma ya tabasamu lake kuna ujumbe mzito: watoto si wahanga wa mabadiliko ya tabianchi pekee, bali pia wanaweza kuwa sehemu ya suluhisho.
Picha ya bango: Baraka akiwa anacheza nyumbani kwao Nairobi. Picha kwa hisani ya Lawrine Moruri.