- Utafiti umebaini kuwa maeneo yaliyohifadhiwa nchini Ethiopia yalipunguza kwa kiasi kikubwa ukataji miti na upanuzi wa kilimo kati ya mwaka 2000 na 2020, ikionyesha utendakazi wa uhifadhi wenye nguvu zaidi kuliko ilivyotarajiwa.
- Utafiti pia unabainisha kuwepo kwa “mchangamano wa maslahi”, huku jamii zinazoishi karibu na maeneo mengi ya hifadhi zikikabiliwa na usalama mdogo wa chakula na ustawi, wakati sehemu ndogo ya maeneo yalipata matokeo ya “kunufaishana” kwa watu na asili.
- Matokeo ya “kunufaishana” kwa watu na asili yalitokea katika maeneo yaliyohifadhiwa ambapo malengo ya uhifadhi yaliwiana kwa karibu zaidi na mifumo ya maisha ya wenyeji, walisema waandishi, na kuna uwezekano wa kuhitaji zaidi ya kuongeza tu bajeti za maeneo yaliyohifadhiwa.
- Watafiti wanasema kuna baadhi ya tahadhari muhimu kwa makadirio yao, kama vile tofauti ya muda wa data ya mazingira na ustawi pamoja na uwezekano wa kuwepo kwa vigezo vingine ambavyo havikujumuishwa katika uchanganuzi.
Utafiti mpya uliochapishwa katika jarida la Nature unaonyesha kuwa maeneo ya hifadhi ya Ethiopia yalipunguza kasi ya ukataji miti na upanuzi wa kilimo, huku yakisaidia kudumisha nyanda za malisho. Lakini utafiti pia unapendekeza kuwa faida zile zile za uhifadhi zinaweza pia kuhusishwa na kupungua kwa usalama wa chakula na ustawi kwa jamii zilizo karibu, huku ukisisitiza baadhi ya tahadhari katika matokeo yao.
Utafiti huo, uliofanywa kwa ushirikiano kati ya watafiti nchini Ethiopia na Uingereza, na Mamlaka ya Uhifadhi wa Wanyamapori ya Ethiopia, ulitathmini matokeo ya kimazingira na kijamii katika maeneo 25 yaliyohifadhiwa nchini Ethiopia katika kipindi cha mwaka wa 2000-2020. Walipima kiwango cha misitu, upanuzi wa kilimo, nyanda za malisho, usalama wa chakula, utofauti wa lishe na ustawi wa nyenzo.
Ingawa maeneo yaliyohifadhiwa yalikuwa na ufanisi mkubwa katika kupunguza uharibifu wa mazingira licha ya shinikizo kubwa kutoka kwa ukuaji wa idadi ya watu, upanuzi wa kilimo, na mahitaji ya ardhi, watafiti waligundua mchangamano wa maslahi (trade-offs) kati ya matokeo ya mazingira na kijamii katika tathmini zao.
Maeneo 12 yaliyohifadhiwa yalikuwa na matokeo mazuri ya kimazingira kwa gharama ya ustawi wa jamii. Wakati huo huo, maeneo matano kati ya maeneo yaliyohifadhiwa yalikuwa na matokeo ya “faida kwa wote” kwa uhifadhi wa bioanuwai na ustawi wa jamii na maeneo matatu yaliyohifadhiwa yalikuwa na matokeo ya “hasara kwa wote”.
“Ethiopia ina utajiri wa viumbe hai, lakini pia inakabiliwa na changamoto kubwa kuhusu umaskini, usalama wa chakula na mahitaji ya ardhi,” alisema Sophie Jago, mwandishi mkuu wa utafiti na msaidizi wa utafiti katika Bustani za Kifalme za Mimea za Kew (Royal Botanic Gardens, Kew) nchini Uingereza.
“Ukweli kuwa maeneo yaliyohifadhiwa yanatoa faida zinazoweza kupimika kwa asili katika muktadha huu ni muhimu … Matokeo magumu ni kwamba mafanikio haya ya mazingira yamekuja na gharama kwa jamii zilizo karibu, haswa karibu na usalama wa chakula.”

Waandishi walisisitiza tahadhari muhimu kwa makadirio yao ya athari za maeneo ya hifadhi ya Ethiopia. Utafiti unatumia tofauti za muda kwa data ya mazingira na ustawi, kutokana na data ya kitaifa iliyopatikana. Pia wanakiri kuwa huenda kulikuwa na vigezo vingine ambavyo havikujumuishwa katika uchanganuzi. Lakini, utafiti huo ulisema, uchanganuzi wa unyeti unaonyesha utofauti kama huo utalazimika kuwa na nguvu isiyo ya kawaida na kwamba wanaamini kuwa matokeo ni thabiti kwa ujumla.
“Ustawi wa nyenzo pia ulipungua kwa kiasi kikubwa katika uchanganuzi wetu mkuu, lakini matokeo hayo hayakuwa thabiti katika uchambuzi wa uthabiti, kwa hivyo tunaifasiri kwa uangalifu zaidi,” alisema Wendawek Abebe, mwandishi mwenza wa utafiti kutoka Chuo Kikuu cha Addis Ababa.
“Pia tungeweza tu kutathmini matokeo ambayo data ya kuaminika ya kiwango cha kitaifa ilipatikana. Tulipima eneo la misitu, upanuzi wa kilimo, nyanda za majani, usalama wa chakula, utofauti wa lishe na ustawi wa nyenzo.”
Yana ufanisi zaidi kuliko wakosoaji wengi wanavyodhani
Kuthibitisha kisababishi, watafiti walitumia mbinu ya majaribio, njia ambayo inakadiria kile kingelitokea iwapo eneo halingelindwa kwa kulinganisha na maeneo sawa yasiyohifadhiwa. Pia walilinganisha makazi yalioko karibu na maeneo yaliyohifadhiwa na makazi yanayofanana yalioko mbali zaidi.
“Maeneo yaliyohifadhiwa hayawekwi kwa kubahatisha. Mara nyingi yapo katika maeneo ya mbali zaidi, kwenye miinuko ya juu, au kwenye ardhi ambayo haifai kwa kilimo,” alisema Abebe. “Ikiwa tutalinganisha tu maeneo yaliyohifadhiwa na yasiyohifadhi<wa, tunaweza kupata picha ya kupotosha ya athari zao.”
Kulingana na waandishi, hawakulinganisha tu matokeo kabla na baada ya maeneo yaliyohifadhiwa kuanzishwa kwani hii ilimaanisha kuwa wangeweza tu kuzingatia maeneo yaliyohifadhiwa yaliyoundwa baada ya mwaka 2000 (wakati data ya serikali ilikuwa thabiti), ambayo inawakilisha robo tu ya maeneo yaliyohifadhiwa ya Ethiopia.

Watafiti walizingatia maeneo yaliyohifadhiwa kama yalikuwepo mwaka wa 2000 ili kutathmini utendaji wao chini ya mfumo wa sasa wa serikali ya Ethiopia. Walikagua mabadiliko ya mazingira kati ya mwaka wa 2000 na 2020/21, huku matokeo ya ustawi wa kaya yakipimwa kati ya mwaka wa 2011 na 2016. Ingawa hii ilikuwa muda mfupi ambao unaweza kukosa matukio ya muda mrefu, walisema waandishi, ulikuwa muda mrefu zaidi ambao wangeweza kufuatilia.
Utafiti huo uligundua kuwa maeneo yaliyohifadhiwa yalipunguza upotevu wa misitu kwa takriban 25% na upanuzi wa kilimo kwa karibu 44% ikilinganishwa na mandhari sawa na isizohifadhiwa. Maeneo yaliyohifadhiwa pia yalipunguza kasi ya ubadilishaji wa makazi na kupunguza upotevu wa nyasi.
Kulingana na waandishi, matokeo ya utafiti yanapendekeza maeneo ya hifadhi ya Ethiopia yanafanya kazi kwa ufanisi zaidi kuliko “wakosoaji wengi” walivyodhani, licha ya wasiwasi wa muda mrefu juu ya uwezo dhaifu wa kitaasisi na vikwazo vya kifedha.
Ila matokeo ya kijamii ni tofauti sana
“Maeneo yaliyohifadhiwa mara nyingi hutoa faida kwa viumbe hai na dunia nzima, wakati gharama zina uwezekano mkubwa wa kuhisiwa na watu wanaoishi karibu nao,” Jago alibainisha.
Jamii zinazoishi ndani ya kilomita 10 (maili 6.2) za maeneo yaliyohifadhiwa zilipata upungufu wa usalama wa chakula ikilinganishwa na makazi yanayofanana kitakwimu yalio mbali zaidi. Vipimo vya ustawi wa nyenzo pia vilipungua, ingawa anuwai ya lishe haikuonyesha mabadiliko dhahiri. Watafiti wanakadiria athari hiyo ilikuwa sawa na upotevu wa takriban miezi milioni 3.9 ya upatikanaji wa chakula cha kutosha kwa kaya za jamii zilizoishi karibu na maeneo yaliyohifadhiwa katika kipindi cha utafiti.
Kulingana na watafiti, athari hizi zinaweza kutokea kwa sababu jamii hupoteza ufikiaji wa ardhi na rasilimali, au, wakati mwingine, kwa sababu mamlaka za mazingira hazifanyi kazi vya kutosha na jamii kurekebisha maisha yao.
“Kwa ujumla, wakati kuna tahadhari muhimu [katika utafiti], ushahidi kwamba makazi karibu na maeneo ya hifadhi yalipata matokeo mabaya zaidi ya usalama wa chakula ni mkubwa,” alisema Abebe.

Bado, watafiti wanaonya dhidi ya kutafsiri matokeo kama ushahidi kwamba uhifadhi unapaswa kuachwa.
“Hii haimaanishi kwamba uhifadhi haupaswi kutokea,” alisema. “Inamaanisha uhifadhi unahitaji kuungwa mkono vyema, kufadhiliwa vyema na kubuniwa kwa njia ambazo hupunguza gharama za kijamii na kuboresha matokeo kwa jamii zilizo karibu.”
Jinsi ya kupata “matokeo ya kunufaishana” zaidi
“Baadhi ya maeneo yaliyohifadhiwa katika utafiti yanaonekana kutoa matokeo bora kwa binadamu na asili, jambo linalopendekeza kuwa mchangamano huu wa maslahi hauwezi kuepukika na kuna mahali tunaweza kujifunza,” Jago alibainisha.
Kulingana na utafiti, matokeo haya yenye uwiano zaidi yalielekea kutokea ambako malengo ya uhifadhi yaliwiana kwa karibu zaidi na mifumo ya maisha ya wenyeji.
“Kuunda matokeo ya kunufaishana kuna uwezekano kuhitaji zaidi ya kuongeza tu bajeti za eneo lililohifadhiwa,” alisema Wendawek. Utafiti uligundua kuwa maeneo yaliyohifadhiwa yenye bajeti kubwa yalihusishwa na matokeo yenye nguvu zaidi ya mazingira, lakini si lazima kuboreshwa kwa ustawi wa jamii zilizo karibu.
Watafiti wanapendekeza hii inaweza kuwa ni kwa sababu taasisi zinazosimamia maeneo yaliyohifadhiwa zinafadhiliwa na kupewa mamlaka ya kulinda bayoanuwai badala ya kuboresha moja kwa moja maisha ya jamii zinazozunguka maeneo hayo.
Pengo hilo, waandishi wanahoji, linaonyesha kizuizi kikubwa ndani ya mifumo mingi ya uhifadhi.
“Matokeo muhimu ni kwamba wasimamizi wa maeneo yaliyohifadhiwa hawawezi kutatua changamoto hizi peke yao,” Jago alisema, “Uhifadhi wa haki na unaofaa utahitaji msaada kutoka kwa serikali, wafadhili na mashirika yanayofanya kazi katika uhifadhi, usalama wa chakula, maisha na maendeleo.”
Kufikia Septemba mwaka 2024, maeneo yaliyohifadhiwa yanachukua takriban 9.4% ya eneo la ardhi la Ethiopia. Utafiti huonya kwamba upanuzi unaweza kuwa mgumu zaidi kwa sababu mifumo mingi ya ikolojia muhimu na isiyo na uwakilishi duni inaingiliana na ardhi ambayo tayari inatumika kwa kilimo na malisho. Zaidi ya hayo, shinikizo juu ya ardhi linaweza kuongezeka huku idadi ya watu nchini ikitarajiwa kuwa karibu mara dufu ifikapo 2050.

“Kupanua maeneo yaliyohifadhiwa bila kwanza kushughulikia ufanisi, uwezo wa usimamizi na athari za ndani kunaweza kufanya uhifadhi kuwa mgumu kuudumisha,” watafiti walisema.
Utafiti unapendekeza hii inazua changamoto kubwa ya kisera kwa Ethiopia: kupanua uhifadhi kunaweza kufaidi viumbe hai, lakini pia kunaweza kuongeza shinikizo kwa maisha ya vijijini isipokuwa athari za ndani zitashughulikiwa kwa ufanisi zaidi.
Mekbeb E. Tessema, mtaalamu huru wa bioanuwai, mshauri wa mabadiliko ya hali ya hewa na mazingira na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Kifikra ya Uhifadhi wa Wanyamapori ya Ethiopia, alisema utafiti unatoa baadhi ya ushahidi wenye nguvu zaidi kufikia sasa juu ya mchangamano wa maslahi kati ya uhifadhi na riziki nchini Ethiopia.
Kulingana na Tessema, matokeo hayo yanafaa hasa wakati nchi zinafuata lengo la kimataifa la bayoanuwai la kulinda 30% ya ardhi na bahari ya Dunia ifikapo 2030.
“Katika muktadha wa lengo la kimataifa la 30×30, utafiti huo unatuma ishara ya onyo: upanuzi wa uhifadhi ambao unapuuza gharama za kijamii unahatarisha kudhoofisha uendelevu wa kiikolojia na kisiasa,” alisema.
Picha ya bango: Watoto wadogo kutoka kijiji cha Rira wanasimama kando ya barabara karibu na nyumba yao duni ndani ya Hifadhi ya Kitaifa ya Milima ya Bale. Picha na Solomon Yimer ya Mongabay.
Habari hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza hapa kwa lugha ya Kiingereza mnamo tarehe 10/06/2026.
Balancing elephant conservation and community needs: Q&A with award-winning ranger Fetiya Ousman
Nukuu:
Jago, S., Gizaw, G., Genanaw, B., Langley, J., Lulekal, E., White, J. D. M., . . . Borrell, J. S. (2026). Trade-offs between nature and people in Ethiopia’s protected areas demonstrate challenges in translating global conservation targets into national realities. Nature Ecology & Evolution. https://doi.org/10.1038/s41559-026-03047-9