- Global Energy Monitor ilitoa mapitio yake ya kila mwaka ya matumizi ya makaa ya mawe duniani, ikisema uzalishaji wa nishati ulipungua kidogo mwaka wa 2025.
- Ingawa matumizi yake kwa ujumla yalipungua, uwezo wa kuzalisha umeme kwa kutumia makaa ya mawe uliongezeka kwa 3.5%, hasa kutokana na miradi mipya nchini Uchina na India.
- Katika Jumuiya ya Ulaya (EU), karibu 70% ya mipango ya kufunga mitambo ya makaa ya mawe kwa mwaka wa 2025 ilishindwa kutekelezwa, kwa kiasi fulani kutokana na wasiwasi juu ya kukatika kwa nishati.
- Marekani iliongoza kwa ongezeko la uzalishaji wa umeme wa makaa ya mawe, huku uingiliaji kati wa sera ukichangia ongezeko hilo la 13%.
Matumizi ya makaa ya mawe duniani kote yaliendelea kupungua mnamo mwaka 2025, lakini kulikuwa na ongezeko la uwezo wa kuzalisha umeme kwa kutumia makaa ya mawe, kulingana na ripoti ya kila mwaka ya kikundi cha uchambuzi wa data Global Energy Monitor. Uzalishaji wa umeme kutoka kwa makaa ya mawe kwa ujumla ulipungua kwa 0.6% mwaka jana, lakini uwezo wa akiba wa mitambo ya makaa ya mawe unaoweza kutumika wakati wa mahitaji makubwa ya umeme uliongezeka kwa 3.5%.
Sehemu kubwa ya ongezeko hilo ilitokea nchini Uchina, ambapo uwezo wa ziada wa kuzalisha umeme kwa kutumia makaa ya mawe unazidi kuchukuliwa kuwa chaguo mbadala ili kuhakikisha usalama wa nishati. Wakati Uchina iliongeza gigawati 78.1 za uwezo wa nishati ya makaa ya mawe mnamo 2025, matumizi yake halisi ya nishati ya makaa ya mawe yalipungua kwa 1.2%.
Kupungua huku kulidhihirika wazi kwani kulikuja huku kukiwa na ongezeko la jumla la mahitaji ya nishati ya Uchina. Kulingana na ripoti hiyo, zaidi ya 90% ya ongezeko hilo la mahitaji ya nishati lilikidhiwa na nishati ya upepo na jua badala ya makaa ya mawe. Wakati Uchina inasalia kuwa mtumiaji mkubwa zaidi wa makaa ya mawe duniani, mahitaji yake zaidi ya nishati yanatimizwa kwa njia mbadala.
India ilirekodi ongezeko la pili kwa ukubwa la uwezo wa nishati ya makaa ya mawe mnamo mwaka 2025, lakini pia ilionyesha harakati kuelekea gridi safi zaidi. Pamoja na nyongeza za rekodi za nishati ya jua na upepo, nishati jadidifu zilichangia zaidi ya nusu ya uwezo wa jumla wa nishati nchini kwa mara ya kwanza.
Christine Shearer, mtafiti mkuu wa ripoti ya kimataifa ya nishati ya makaa ya mawe, alisema sehemu kubwa ya uwezo mpya wa makaa ya mawe ulioongezwa nchini India na Uchina uliidhinishwa miaka iliyopita, kabla ya mwelekeo wa soko la nishati jadidifu kubadilika.
“Hadi kufikia wakati mitambo hii yote ya makaa ya mawe ilianza kufanya kazi mnamo mwaka 2025, vyanzo mbadala vya nishati kama jua na upepo vilikuwa tayari vimekuwa nafuu zaidi nchini Uchina na India,” alisema. “Kwa hivyo, unaona mwisho wa wimbi la zamani la uwekezaji likifika kwenye soko ambalo tayari limesonga mbele. Swali kuu ni jinsi watunga sera na kampuni za huduma za umeme zitakubali kwa haraka mabadiliko hayo na kuanza kupanga sera na uwekezaji kulingana na hali mpya ya soko.”
Uchina bado ina gigawati (GW) 1,243.3 za uwezo wa kuzalisha umeme kwa kutumia makaa ya mawe zaidi ya nchi nyingine zote duniani zikijumlishwa, lakini nishati jadidifu zinachukua sehemu inayoongezeka ya muundo wake wa jumla wa nishati. Kulingana na Shearer, wakati makaa ya mawe yalichukua 55% ya jumla ya uzalishaji wake wa umeme mnamo mwaka 2025, nishati jadidifu kama vile upepo, jua na umeme wa maji zilitoa 35%.
Lakini uwezo wa mitambo mipya na iliyorejeshwa katika matumizi ya makaa ya mawe nchini Uchina ulifikia kiwango cha juu zaidi kuwahi kurekodiwa mwaka 2025, ikionyesha wasiwasi juu ya kutegemewa kwa vyanzo vya nishati mbadala hata kama nchi inabadilika kuelekea kuongezeka kwa matumizi yake.

Ripoti hiyo ilitoa picha mseto ya utegemezi wa makaa ya mawe duniani kote na tofauti za eneo. Idadi ya nchi zinazojenga au kupendekeza mitambo mipya ya makaa ya mawe ilishuka kutoka 38 hadi 32 mwaka wa 2025. Baada ya Brazil na Honduras kuahidi kusitisha matumizi yao ya makaa ya mawe, Amerika Kusini sasa haina miradi mipya ya makaa ya mawe inayopendekezwa.
Mpito thabiti wa Jumuiya ya Ulaya kutoka kwa makaa ya mawe pia unaendelea. Mwaka jana, makaa ya mawe yaliwakilisha 10% tu ya jumla ya uwezo wa kuzalisha umeme, chini kutoka 30% mwaka wa 2000, na kwa mara ya kwanza umeme zaidi ulitolewa na nishati jadidifu kama upepo na jua kuliko nishati ya mafuta.
Hata hivyo, karibu 70% ya mipango ya kufunga mitambo ya makaa ya mawe katika Jumuiya ya Ulaya iliyoratibiwa mwaka 2025 haikutekelezwa, ikionyesha mwelekeo mpana wa kimataifa. Usumbufu katika masoko ya nishati uliosababishwa kwanza na uvamizi wa Urusi nchini Ukraine na sasa mvutano wa kijeshi unaohusisha Iran, Israel na Marekani umezifanya baadhi ya serikali kusita kuondoa uwezo wao wa makaa ya mawe, zikihofia kuwa huenda zikahitajika iwapo kutakuwa na uhaba wa mafuta.
Shearer alisema athari ya jumla ya bei ya juu ya makaa ya mawe na mafuta mengine yanayosababishwa na mzozo wa kijeshi unaohusisha Iran itakuwa kuchochea kupitishwa zaidi kwa nishati jadidifu.
“Mgogoro huo unaimarisha somo la msingi kwamba utegemezi wa nishati ya mafuta inayouzwa kimataifa huleta hatari ya kiuchumi na kijiografia. Hiyo inaweza kuongeza kasi ya uwekezaji katika nishati jadidifu kwa muda mrefu,” alisema.
Huku matumizi ya makaa ya mawe yalipungua kwa kiwango cha kimataifa, nchi iliyoongoza kwa ongezeko hilo ilikuwa Marekani, ambayo iliona uzalishaji wa umeme wa makaa ya mawe ukiongezeka kwa 13%. Marekani ilikuwa nchi pekee yenye uchumi mkubwa iliyoripoti ongezeko la matumizi ya makaa ya mawe. Hali hiyo ilikuwa matokeo ya moja kwa moja ya uingiliaji kati wa sera za utawala wa Trump na mabadiliko katika motisha za nishati safi.
Mnamo mwaka wa 2025, serikali ya Marekani iliamuru mitambo mitano ya makaa ya mawe katika majimbo manne kuendelea kufanya kazi licha ya mipango ya kuifunga. Zaidi ya $600 milioni za fedha za umma zilitumika katika kuboresha na kupanua maisha ya vifaa vya makaa ya mawe nchini Marekani, uamuzi ambao ripoti ilisema unachangia kupanda kwa bei ya umeme majumbani.
Nje ya Uchina na India, miradi iliyopendekezwa ya makaa ya mawe mnamo 2025 mara nyingi ilikuwa ya mitambo maalumu ya kuzalisha umeme kwa matumizi ya viwanda husika kama uchimbaji madini au usindikaji wa madini. Nchini Indonesia, uwezo wa makaa ya mawe ulipanda hadi gigawati (GW) 20 mwaka jana, hasa kuhudumia viwanda vya nikeli na alumini, na gigawati (GW) 14 za ziada kwa sasa zinaendelea kujengwa.

Wakati mataifa ya Kiafrika kwa ujumla yanawakilisha sehemu ndogo ya matumizi ya makaa ya mawe duniani, Zimbabwe na Zambia zilitangaza jumla ya gigawati (GW) 5.2 za uwezo mpya wa makaa ya mawe uliopangwa, ambazo kimsingi zinalenga kuendesha viwanda vyao vya uchimbaji madini.
Kwa ujumla, Zimbabwe ina kiwango cha nne kwa ukubwa duniani cha miradi ya makaa ya mawe iliyo katika hatua ya maendeleo, kikiwa na gigawati (GW) 8.6.
“Serikali zote mbili, linapokuja suala la viwanda, zina mtazamo wa kutojua kabisa aina ya nishati wanayotumia,” alisema Kudakwashe Manjojo, mshauri wa masuala ya mpito wa nishati katika shirika la hali ya hewa na nishati la Power Shift Africa, lenye makao yake makuu nchini Kenya. “Kwa hivyo kimsingi, nishati yoyote ni nishati nzuri.”
Zimbabwe ni mojawapo ya wazalishaji wa juu wa lithiamu duniani. Manjojo alisema inashangaza kwamba inaposafirisha nje nyenzo kwa vyanzo vya nishati mbadala, inalazimika kutumia makaa ya mawe kwa shughuli zake za viwandani. Huku ukame unaohusiana na hali ya hewa ukipunguza kiwango cha umeme unaotokana na maji nchini Zimbabwe, alisema kuongezeka kwa uzalishaji katika migodi ya makaa ya mawe inayomilikiwa na Uchina ni sababu kubwa katika matumizi ya nchi hiyo ya mafuta kwa ajili ya kuzalisha umeme.
“Takriban miaka minne au mitano iliyopita, Uchina ilisema haitakuwa ikijenga migodi mipya ya makaa ya mawe barani Afrika, lakini hilo halikuzuia kuongeza uzalishaji katika migodi ya makaa ya mawe iliyokuwapo tayari,” alisema.
Katika muda mrefu, Manjojo alisema ana wasiwasi kutegemea makaa ya mawe kutakuwa kikwazo kwa Zimbabwe. “Makaa ya mawe yanafifia, sawia na mafuta na gesi, sote tunajua nishati mbadala ni nafuu, lakini miji ya uchimbaji wa makaa ya mawe itabeba mzigo mkubwa wa mpito huo wa nishati, na hilo linaweza kuwa na athari kubwa za kiuchumi na kijamii,” alisema.
Picha ya bango: Kiwanda cha kuzalisha umeme kwa kutumia makaa ya mawe cha Mill Creek katika jimbo la Kentucky nchini Marekani kinamilikiwa na kuendeshwa na Louisville Gas & Electric. Picha na Willian Alden kupitia Flickr (CC BY-SA 2.0).
Habari hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza hapa kwa lugha ya Kiingereza mnamo tarehe 21/05/2026