- Wakati ujenzi wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (EACOP) ukikaribia kukamilika nchini Uganda na Tanzania, ripoti mpya imebaini athari za kimazingira zinazohusishwa na mradi huo.
- Bomba hilo linapita karibu au ndani ya mifumo nyeti ya ikolojia na njia za uhamaji wa wanyamapori, na linaweza kuwa na athari hasi kwa binadamu na mazingira.
- Hatari za bomba hilo zinaongezeka kutokana na maendeleo mapya ya mafuta na gesi katika eneo la Maziwa Makuu ya Afrika.
Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (EACOP) linaloanzia kwenye vitalu vya mafuta ya Ziwa Albert nchini Uganda hadi mji wa bandari wa Tanga nchini Tanzania, limeanza tena kuchunguzwa kwa karibu baada ya kutolewa kwa ripoti mpya inayobainisha maeneo ya bioanuwai na makazi ya wanyamapori ambayo bomba hilo linapitia au ambayo liko karibu nayo.
Kwa kutumia takwimu za ramani na makadirio ya thamani ya kiuchumi, ripoti ya Earth Insight, shirika lisilo la kiserikali lenye makao yake makuu nchini Marekani, inaonyesha kuwa bomba hilo lenye urefu wa kilomita 1,443 liko karibu na maeneo muhimu kwa maisha ya mamilioni ya watu na usalama wa maji, na pia sehemu ambazo hutumika kama njia za uhamaji wa wanyama.
Kutokana na uchambuzi huo, ripoti hiyo inahitimisha kuwa ujenzi wa bomba hilo tayari umeathiri jamii na mazingira, na kwamba usafirishaji wa mafuta utaleta hatari zaidi za muda mrefu.
EACOP ni mradi wa ubia kati ya kampuni ya TotalEnergies yenye asilimia 62 ya hisa, serikali za Uganda na Tanzania kila moja ikiwa na asilimia 15, pamoja na China National Offshore Oil Corporation (CNOOC) yenye asilimia 8. EACOP itasafirisha mafuta yanayochimbwa kutoka vitalu viwili kwenye bonde la Ziwa Albert: Kingfisher, linalomilikiwa na CNOOC; na Tilenga, linalomilikiwa na TotalEnergies.

Kwa mujibu wa Earth Insight, mradi huo unakaribia kukamilika na mafuta ya kwanza yataanza kusafirishwa mapema mwaka 2026.
“Linapita moja kwa moja katika maeneo ya viumbe walio hatarini kutoweka, na eneo muhimu zaidi ni la makazi ya kifaru mweusi,” Katie Boston wa Earth Insight, mtafiti mkuu wa utafiti huo, aliiambia Mongabay kwa njia ya simu.
Aliongeza kuwa bomba hilo linaweza kusababisha mgawanyiko wa makazi ya viumbe katika eneo la Kibale/Bukoora River Crossing, ambako ujenzi bado haujakamilika, na kuathiri viumbe kama kifaru mweusi, aina mbili za pangolini, mbwa pori wa Afrika na jamii kadhaa za nyani, wakiwemo sokwe aina ya Pan troglodytes schweinfurthii na nyani aina ya ashy red colobus (Piliocolobus tephrosceles).
Jamii na mashirika ya kiraia yamekosoa mambo kadhaa kuhusiana na mradi huo. Mambo hayo ni pamoja na mipango ya kuwahamisha wananchi, athari zinazoweza kutokea kwa mazao na ardhi za kilimo, pamoja na kiwango cha uzalishaji wa hewa ya ukaa kinachokadiriwa kufikia wastani wa tani milioni 34.5 za hewa ya ukaa kwa mwaka katika kipindi cha utekelezaji wa mradi ambacho ni zaidi ya miaka 25, kulingana na makadirio yaliyotolewa na taasisi ya Climate Accountability Institute.
Ripoti ya Earth Insight imeangalia maeneo kadhaa ambayo athari kwa bioanuwai zinaweza kuwa kubwa sana. Moja ya maeneo hayo ni kwenye kivuko cha mto Bukoora (Kibale).
“Inaonyesha jinsi athari za bomba hili zinavyoweza kuenea mbali zaidi ya eneo la mradi wenyewe,” alisema Boston.
Kwa kuwa eneo ambalo bomba linavuka mto liko umbali wa kilomita 12 tu kutoka Mfumo wa Ardhi Oevu wa Ghuba ya Sango kwenye kisiwa cha Musambwa-Kagera, eneo la ardhi oevu la mpakani linalotambuliwa chini ya Mkataba wa Ramsar, na kilomita 37 kutoka Ziwa Victoria, ambalo ni eneo la pili kwa ukubwa duniani la maji safi, kumwagika kwa mafuta kutoka kwenye bomba hilo kunaweza kusababisha madhara makubwa.
Mbali na kuchora ramani ya bomba la mafuta kuhusiana na maeneo ya bioanuwai, ripoti hiyo pia ilichunguza thamani ya kiuchumi ya baadhi ya maeneo hayo.
Boston alisema kuwa Eneo la Ramsar la Samuka linatoa huduma za mazingira zenye thamani inayokadiriwa kufikia dola za Marekani milioni 117.
Kwa mujibu wa kituo cha huduma za taarifa cha Ramsar, ingawa msongamano wa watu katika eneo hilo ni mdogo, linahudumia jamii kwa kutoa samaki, mimea ya dawa na malighafi za ujenzi na ufundi.
Diana Nabiruma kutoka Africa Institute for Energy Governance (Afiego), shirika la Uganda ambalo limekuwa likifanya kazi na jamii zilizoathiriwa na shughuli za kuwahamisha wananchi zinazofanywa na TotalEnergies kando ya bomba hilo, aliiambia Mongabay kuwa jamii zimeripoti kuwa vyanzo vya maji tayari vimechafuliwa na wananchi wameathirika.
Afiego imekuwa ikitetea utekelezaji wa haki wa mipango ya makazi mapya pamoja na utekelezaji sahihi wa hatua za kupunguza na kukabiliana na athari kulingana na ahadi zinazowalenga wananchi, maeneo oevu, misitu na wanyamapori. Shirika hilo linakamilisha ripoti mbili zitakazoangalia athari za EACOP kwa bioanuwai na mipango ya makazi mapya, ambazo zinatarajiwa kuchapishwa baadaye mwezi huu.

“Maeneo oevu yaliyoathiriwa na EACOP yana bioanuwai kubwa sana, na baadhi yake yana uhusiano na maeneo ya Ramsar,” Nabiruma aliiambia Mongabay, akiongeza kuwa kinyume na ahadi zilizotolewa na kampuni, jamii zimeripoti kuwa ujenzi wa bomba umesababisha uharibifu.
“Visima mbadala havikidhi viwango vinavyotakiwa. Mradi huu si tu kwamba unategemea rasilimali kutoka maeneo oevu, bali pia unatumia maji ya jamii,” alisema.
Udongo uliobaki kutokana na shughuli za uchimbaji wa mifereji uliachwa ndani ya makazi ya watu na karibu na maeneo oevu katika wilaya kama Hoima magharibi mwa Uganda, ambapo bomba linaanzia, na Kyotera katikati mwa Uganda, ambapo kituo kikuu cha kusukuma mafuta kinapatikana kabla ya bomba hilo kuvuka na kuingia Tanzania.
“Udongo huu umeingia kwenye maeneo oevu na kusababisha kujaa kwa mashapo,” alisema Nabiruma, akiongeza kuwa wamekuwa wakiona mapungufu katika utekelezaji wa hatua zilizokuwa zimeahidiwa katika tathmini mbalimbali zilizofanywa na kampuni.
Msemaji wa TotalEnergies, ambayo ilifanya mkutano wake mkuu wa mwaka wiki iliyopita mjini Paris, Ufaransa, alijibu Mongabay kwa maandishi akirejelea tafiti nyingi ambazo “zimefanywa kuchunguza athari za mradi huu katika ukanda huo unaotambuliwa duniani kwa bioanuwai yake ya kipekee na tajiri.”
Aliongeza kuwa njia ya bomba ilibuniwa ili kupunguza athari kwa bioanuwai na kwamba haipiti ndani ya maeneo yoyote yaliyohifadhiwa chini ya Ramsar au IUCN.
“Takriban asilimia 80 ya eneo lililotumika kwa bomba litarejeshwa katika hali yake ya asili,” alisema msemaji huyo, akiongeza kuwa TotalEnergies EP Uganda imejizatiti kuhakikisha kunakuwa na “matokeo chanya kwa bioanuwai” kupitia mradi wa Tilenga.
Kama ilivyo kwa EACOP, mradi wa Tilenga wa TotalEnergies umekumbana na upinzani mkali kutoka kwa mashirika ya kiraia nchini Uganda na duniani kote, ambayo yanakosoa mipango ya makazi mapya pamoja na mchango wake katika mabadiliko ya tabianchi kutokana na kutegemea uchimbaji wa mafuta ya kisukuku.
Satellite images reveal oil project surge in Ugandan park and wetland
Tathmini ya hivi karibuni iliyoagizwa na TotalEnergies ilihitimisha kuwa mpango wa makazi mapya kwa mradi wa mafuta karibu na Ziwa Albert umekamilika kwa mafanikio.
Hata hivyo, mashirika kama Afiego yalipinga hitimisho hilo, yakisema kuwa mradi huo umesababisha madhara makubwa ya kijamii na kiuchumi kwa wananchi, huku familia zilizoathirika zikikabiliwa na kupungua kwa ukubwa wa ardhi, kipato kidogo na ukosefu wa chakula.
“Kila mwanajamii ambaye Afiego amezungumza naye ana malalamiko,” alisema Nabiruma, akisisitiza kuwa ingawa wamebaini kasoro katika miradi ya Tilenga na EACOP, miradi hiyo haipaswi kuchanganywa kwa sababu kila mmoja una mifumo tofauti ya usimamizi wa kupunguza na kuzuia madhara.
TotalEnergies inakabiliwa na changamoto kadhaa za kisheria zinazohusiana na miradi ya Tilenga na EACOP. Changamoto hizo ni pamoja na kesi nchini Ufaransa chini ya sheria ya wajibu wa uangalizi (duty of vigilance), ambapo mashirika yasiyo ya kiserikali yanadai kuwa kampuni hiyo haikuchukua hatua za kutosha kuzuia hatari kwa haki za binadamu na mazingira, pamoja na mashauri mengine yanayopinga masuala ya upatikanaji wa ardhi, makazi mapya na fidia zinazohusiana na miradi hiyo.
Boston alisema kuwa Earth Insight inatoa wito wa kutathmini ikiwa EACOP inazingatia Mkataba wa Ushirikiano wa Bonde la Mto Nile, ulioridhiwa na Uganda, Tanzania, Burundi, Kenya, Ethiopia na Rwanda, ambao unasema kuwa nchi zote wanachama zinapaswa kuchukua hatua stahiki kuhakikisha kuwa miradi mikubwa ya miundombinu haiathiri usalama wa rasilimali za maji zinazovuka mipaka na uendelevu wa mazingira.
Picha ya bango: Korongo mdomo-kiatu (Balaeniceps rex), Hifadhi ya Taifa ya Murchison Falls, Uganda. Picha na Kyla Marino kupitia Flickr (CC BY 2.0).