- Ripoti mpya imebaini kuwa asilimia 100 ya miamba ya matumbawe, misitu ya mikoko na maeneo muhimu ya bayoanuwai katika pwani ya Kenya yamo ndani ya maeneo yaliyotengwa kwa shughuli za mafuta na gesi.
- Bonde la Lamu limetajwa kuwa kitovu cha upanuzi huo, huku miradi minane ya mafuta ikipangwa kuanza katika eneo hilo.
- Watafiti wanaonya kuwa shughuli za mafuta na gesi zinahatarisha bayoanuwai ya baharini, uvuvi na jamii za pwani.
- Ripoti hiyo imetolewa kabla ya mkutano wa Our Ocean Conference mjini Mombasa, huku kukiwa na wito wa kulinda maeneo muhimu ya bahari.
Ripoti mpya imebainisha kuwa asilimia 100 ya miamba ya matumbawe, misitu ya mikoko, maeneo ya hifadhi za baharini pamoja na maeneo muhimu ya bayoanuwai katika ukanda wa pwani ya Kenya yamo ndani ya maeneo yaliyotengwa kwa shughuli za utafutaji wa mafuta na gesi. Maeneo hayo pia ni sehemu za bahari ambazo ni muhimu kiikolojia na kibayolojia.
Ripoti hiyo iliyopewa jina la Fossil Fuel Threats to the Ocean: Marine Life and Coastal Communities at Risk ilitolewa leo, siku chache kabla ya mkutano wa 11 unaohusu masuala ya bahari, mkutano wa ‘Our Ocean Conference’ unaotarajiwa kufanyika kuanzia Juni 16 hadi 18 mjini Mombasa, Kenya.
Ripoti hiyo inaeleza kuwa upanuzi wa shughuli za mafuta na gesi baharini unaweza kusababisha madhara makubwa yatokanayo na uchimbaji wa visima, umwagikaji wa mafuta, uchimbaji wa kina cha bahari pamoja na kuongezeka kwa shughuli za usafirishaji wa meli.
Bonde la Lamu limetajwa kuwa eneo linalopewa kipaumbele, ambapo miradi minane ya mafuta inayotarajiwa kuanza baadaye mwaka huu, imepangwa kutekelezwa katika ukanda huo wa pwani wenye historia na utajiri mkubwa wa kiikolojia.
“Uchambuzi wetu unaonesha kuwa asilimia 100 ya Miamba ya matumbawe na misitu ya mikoko katika eneo hili imefunikwa na vitalu vya mafuta na gesi. Kwa asilimia 100, maeneo haya ni ya hifadhi za baharini na pwani lakini pia ni muhimu kwa bayoanuwai,” ripoti hiyo imeeleza.
Katika ripoti hiyo, Kenya imetajwa kuwa ni miongoni mwa nchi ambazo zinaendelea kuhamasisha uwekezaji mkubwa katika sekta ya mafuta na gesi. Ripoti hiyo ilitolewa na shirika la Earth Insight kwa ushirikiano na mashirika 12 ya kiraia, ikiwa pia ni sehemu ya maandalizi ya maadhimisho ya Siku ya Bahari Duniani yanayofanyika Juni 8. Utafiti huo umehusisha nchi 11.
Hadi mwaka jana, juhudi za Serikali ya Kenya kuendeleza miradi ya mafuta na gesi baharini zilikumbana na upinzani kutoka kwa mashirika mbalimbali. Miongoni mwa hatua hizo yalikuwa maandamano yaliyofanyika katika ukanda wa pwani wakati wa Siku ya Mazingira Duniani mwaka 2025.
Katika kampeni iliyopewa jina la “Coastline, Not Oilline”, shirika la Natural Justice pamoja na washirika wake, walibainisha athari za kimazingira na kijamii zinazoweza kusababishwa na mipango mipya ya utafutaji wa mafuta katika eneo la Lamu.
“Shughuli hizi zinazopendekezwa zinatishia bayoanuwai ya baharini, maeneo ya urithi wa kihistoria na maisha ya jadi ya jamii zinazotegemea rasilimali za pwani,” ilisema taarifa iliyochapishwa kwenye tovuti ya taasisi hiyo.

Muturi wa Kamau kutoka Kenya Oil and Gas Working Group, kikundi kazi kinachoshughulikia masuala ya rasilimali za mafuta na gesi nchini Kenya, alisema: “Kenya inajiandaa kufungua maeneo nyeti ya kiikolojia kwa ajili ya utafutaji wa mafuta na gesi za kisukuku wakati huohuo ikiwa mwenyeji wa mkutano wa kimataifa unaolenga kulinda bahari. Swali kubwa hapa ni hili: Ni kwa gharama gani tuko tayari kuhatarisha mifumo hii ya ikolojia na maisha ya jamii za pwani ambazo zimeitegemea vizazi na vizazi?”
Katika utafiti huo, Kenya imetajwa pamoja na Australia, Cameroon, Indonesia, Jamaica, Norway na Trinidad na Tobago kama miongoni mwa nchi ambazo “zinaendelea kuhamasisha uwekezaji mkubwa katika sekta ya mafuta na gesi.” Nchi nyingine zilizotajwa ni Argentina, Alaska, Mexico na Tanzania.
“…miradi hiyo inaonyesha jinsi upanuzi wa shughuli za mafuta na gesi usivyoishia kwenye visima au vitalu vya baharini pekee, bali unahusisha mifumo mikubwa iliyounganishwa ya mabomba ya kusafirisha mafuta na gesi, bandari, vituo vya kusafirisha bidhaa nje ya nchi, tafiti za mitetemo ya ardhi, njia za usafirishaji wa meli, mitambo ya uchakataji pamoja na miundombinu mingine ya nchi kavu inayohusiana na shughuli hizo.
“Ikiwa itatekelezwa, miradi hii inaweza kuzifanya nchi kutegemea miundombinu ya mafuta na gesi kwa miongo mingi ijayo huku ikiongeza shinikizo kwa bayoanuwai, maisha ya watu wa pwani na uthabiti wa hali ya hewa,” imeeleza ripoti.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, kuendelea na miradi ya mafuta kutahatarisha zaidi mfumo wa ikolojia ya pwani ambayo tayari inakabiliwa na mabadiliko ya tabianchi.
“Shughuli zote hizi za mafuta na gesi za kisukuku zinatishia sekta ya uvuvi, maisha ya watu wa pwani, jamii za asili, mamalia wa baharini, miamba ya matumbawe, misitu ya mikoko, nyasi za baharini na mifumo mingine ya ikolojia ambayo tayari iko chini ya shinikizo kutokana na mabadiliko ya tabianchi,” imeeleza.
Utafiti huo unaeleza umuhimu wa miamba ya matumbawe na misitu ya mikoko kwa mifumo ya ikolojia ya pwani: “Miamba ya matumbawe na misitu ya mikoko ni maeneo muhimu ya kuzaliana na kulelea viumbe wa baharini, yanayosaidia sekta ya uvuvi, kulinda mwambao dhidi ya mmomonyoko wa ardhi na dhoruba, pamoja na kuhifadhi kiwango kikubwa cha kaboni ya baharini (blue carbon) inayosaidia kudhibiti mabadiliko ya tabianchi.
“Uharibifu wa mifumo hii hautachochea tu kupotea kwa bayoanuwai na kusambaratika kwa mifumo ya ikolojia, bali pia utapunguza uwezo wa eneo hili kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi na kuongeza hatari kwa maeneo ya pwani.”
Watafiti pia wameangalia athari zinazoweza kuzikumba jamii za wenyeji. “Kwa jamii za Pwani, athari zake zinaweza kuwa kubwa na za kutisha. Maelfu ya wavuvi na kaya zinazotegemea rasilimali za baharini hutegemea miamba ya matumbawe, misitu ya mikoko na mifumo ya ikolojia ya pwani kwa ajili ya usalama wa chakula, kipato, utambulisho wa kitamaduni na maisha yao kwa ujumla,” imeeleza ripoti hiyo.

Ripoti hiyo imekuja wakati Kenya ikiendelea kuhamasisha uchumi wa buluu kama moja ya nguzo za maendeleo ya kiuchumi, hususan katika sekta za uvuvi, utalii na biashara ya usafirishaji wa baharini.Ripoti hiyo imehitimisha kuwa maendeleo ya mafuta na gesi baharini yanaendelea katika “baadhi ya maeneo muhimu zaidi ya baharini duniani kwa upande wa ikolojia,” yakiwemo Kenya na Tanzania.
“Inasikitisha kuona matokeo ya utafiti huu na ukubwa wa mipango ya upanuzi wa miradi ya mafuta na gesi za kisukuku inayotishia afya na mustakabali wa bahari yetu,” alisema Tyson Miller, Mkurugenzi Mtendaji wa Earth Insight.
“Ahadi za nchi mbalimbali kulinda asilimia 30 ya bahari ifikapo mwaka 2030 zinatoa fursa muhimu ya kuzuia utoaji wa vitalu vipya vya mafuta na gesi ili kulinda maeneo ya sasa na ya baadaye ya hifadhi za baharini, njia za nyangumi na mamalia wengine wa baharini, pamoja na afya ya miamba ya matumbawe, nyasi za baharini, misitu ya mikoko na jamii zinazozitegemea,” anasema.
Picha ya Bango: Ramani inayoonyesha maeneo ambako utafiti ulifanyika duniani, ikionyesha jinsi nchi zinavyoendelea kuhamasisha uwekezaji mkubwa katika sekta ya mafuta na gesi. Ramani kwa hisani ya Earth Insight.