- Wanaharakati wa mazingira na makundi ya kijamii wanapinga mpango wa kuhamishwa kwa Kituo cha Wanyama Yatima cha Nairobi, wakidai kukosekana kwa ushirikishwaji wa umma na kufunguliwa kwa kesi mahakamani kupinga leseni ya EIA.
- Wapinzani wanasema mpango huo utachukua takriban hekta 31 kutoka Nairobi National Park, na kuhatarisha bioanuwai, ikiwemo makazi ya faru weusi na mfumo wa ikolojia wa Athi-Kapiti.
- Kenya Wildlife Service inasema uhamisho unalenga kuboresha ustawi wa wanyama, kupunguza msongamano na kuanzisha kituo cha kisasa chenye viwango vya kimataifa vya uhifadhi na elimu.
- Mjadala umechochewa pia na mradi mkubwa wa Bomas International Convention Centre (MICE) wenye thamani ya $324 milioni, huku mahakama ikitarajiwa kusikiliza kesi hiyo Juni 30, 2026.
NAIROBI, Kenya – Huku dunia ikisherehekea Siku ya Kimataifa ya Bioanuwai, tangazo la kuhamishwa kwa kituo cha Nairobi Animal Orphanage linazua mjadala mkubwa kati ya Huduma ya Wanyamapori Kenya (Kenya Wildlife Service – KWS) na makundi ya wanaharakati wa mazingira ambao wameishutumu serikali ya Kenya kwa kutumia mamlaka yake kupita kiasi bila kuzingatia maoni ya wadau wengine.
Tayari kundi moja la utetezi nchini limewasilisha ombi mahakamani kutaka mahakama itoe amri kuizuia serikali kuhamisha Nairobi Animal Orphanage, kwa madai kuwa mpango huo ni njia ya kuficha njama za kugawa isivyo halali hekta 31 za ardhi kutoka Hifadhi ya Taifa ya Nairobi.
Shauri hilo liliwasilishwa na Kituo cha Sheria pamoja na taasisi ya Just Act katika Mahakama ya Mazingira na Ardhi, na likapewa kesi nambari E019 ya 2026. Walalamikiwa katika kesi hiyo ni KWS, Shirika la Bomas la Kenya, Wizara ya Ulinzi, Mamlaka ya Taifa ya Usimamizi wa Mazingira, Tume ya Taifa ya Ardhi, na Mwanasheria Mkuu wa Serikali.
Walalamikaji wanaitaka mahakama kusitisha leseni ya Tathmini ya Athari kwa Mazingira (EIA) nambari NEMA/ENVIS/CPR/LIC-0940, hatua ambayo itazuia ukataji wa msitu wa asili ndani ya hifadhi hiyo, ambayo ni makazi muhimu kwa faru weusi walio katika hatari kubwa ya kutoweka.
Katika hati ya kiapo iliyowasilishwa mahakamani, Kituo cha Sheria, kupitia kwa Mkurugenzi Mtendaji Wambua Kituku, ilishutumu serikali ya Kenya kwa kile ilichokiita matumizi mabaya makubwa ya fedha, pamoja na kukosekana kwa ushirikishwaji wa umma katika mpango wa kuhamisha kituo hicho cha wanyama.
“Mlalamikaji mbele ya mahakama hii anatafuta kulinda wanyamapori na mazingira dhidi ya unyonyaji usio na msingi na usio endelevu, akitimiza wajibu wake kama mwananchi kuhakikisha kuwa vizazi vijavyo vinarithishwa mazingira safi yenye afya na yenye uwiano wa kiikolojia.
“Naiomba mahakama kulinda imani ya umma katika rasilimali za asili na kuzuia hatua zinazotishia bioanuwai, uadilifu katika masuala yanayohusu ustawi wa vizazi vya sasa na vijavyo,” ilisema sehemu ya hati hiyo ya kiapo.

Mahakama imeainisha ombi hilo kama la dharura na imeziagiza taasisi zote sita zilizotajwa katika shauri hilo, kuwasilisha majibu yao kabla ya usikilizwaji wa kesi ya msingi uliopangwa kufanyika Juni 30, 2026.
Kwingineko, wataalamu wameonya kuwa kuhamishwa kwa kituo cha Nairobi Animal Orphanage kunaweza kuchelewesha muda wa urejeshaji wa sehemu ya nyanda za savana, ambapo takribani hekta 31 zitatengwa kutoka Nairobi National Park ili kupisha mradi huo.
Hoja kuu inayotolewa na KWS ni kwamba mpango huo unalenga kuboresha ustawi wa wanyama ili kufikia viwango vya kimataifa, wakati wanaharakati wanadai kuwa uamuzi huo unasukumwa zaidi na maslahi ya kiuchumi.
Aidha, wanaopinga mpango huo wamehoji mipaka finyu iliopo kati ya haki za kiuchumi na za kimazingira, wakisema kuwa ahadi ya ajira 500 haiwezi kulinganishwa na athari kubwa itakayosababishwa na uwekezaji huo wenye thamani ya $324 milioni. Pia wameonya juu ya uwezekano wa kuongezeka kwa migogoro kati ya binadamu na wanyamapori, pamoja na kupungua kwa bioanuwai, hasa kwa makundi muhimu ya ndege wahamiaji wanaoingia na kutoka kwenye hifadhi hiyo.
Nairobi, mji mkuu wa Kenya, umejitangaza, si tu kama kitovu kikuu cha biashara, bali pia kwa umuhimu wake wa kiikolojia, ukiwa mji pekee kati ya miji mikuu barani Afrika wenye hifadhi ya wanyamapori ndani ya jiji. Nairobi National Park imekuwa ikiwapa watalii wa ndani na wa kimataifa fursa ya kushuhudia mandhari halisi ya asili, huku nyuma yake kukiwa na jiji linaloendelea kukua kwa kasi, likiwa na majengo marefu ya kisasa.
Hifadhi hiyo ina ukubwa wa kilomita za mraba 117, na ni sehemu ya mfumo mpana wa ikolojia wa Athi Kapiti. Mandhari yake yanajumuisha nyasi tambarare zilizo wazi, misitu ya acacia iliyotawanyika, misitu kando ya mito, mabonde ya miamba, na ardhi oevu ya msimu. Muunganiko huu wa mazingira huwezesha uwepo wa aina mbalimbali za mimea na wanyama.
Hifadhi hiyo ni makazi ya zaidi ya aina 100 za mamalia, wakiwemo simba, chui, duma, nyati, vifaru, twiga, pundamilia, na aina mbalimbali za swala. Pia, zaidi ya aina 500 za ndege zimerekodiwa katika hifadhi hiyo, jambo linaloifanya kuwa eneo muhimu kwa uhifadhi wa bioanuwai ya ndege, na kituo muhimu kwa ndege wahamiaji kutoka kanda ya Palearctic.
Nairobi Animal Orphanage imekuwa kimbilio la matumaini kwenye ukingo wa mji mkuu wa Kenya kwa zaidi ya miaka 60. Ilianzishwa mwaka 1964, ikiwa ya kwanza ya aina yake katika Afrika Mashariki, na imekuwa mahali muhimu pa kuwahifadhi wanyamapori walioumia, waliotelekezwa, au walio katika hali ya dhiki. Kituo hicho kipo ndani ya Nairobi National Park, ambayo ina mfumo wa ikolojia ya savana yenye hali ya mazingira ya mseto wa mjini na vijijini (peri-urban).
Mwaka 2013, KWS ilibuni mpango wa muda mrefu wa kuhamisha na kuboresha kituo hicho, ikiwa ni sehemu ya mkakati mpana wa kuboresha miundombinu na ustawi wa wanyama katika kituo hicho. Hata hivyo, utekelezaji wa mpango huo ulisalia katika hatua za awali kwa miaka kadhaa.
Mchakato rasmi wa utekelezaji ulianza baadaye, ambapo Oktoba mwaka 2025 KWS iliwasilisha Ripoti ya Tathmini ya Athari kwa Mazingira (EIA), ikieleza kwa kina mipango ya uhamishaji na uboreshaji wa kituo hicho. Ripoti hiyo ilikuwa sehemu muhimu ya hatua za kisheria zinazohitajika kabla ya kuanza kwa mradi.
Baada ya mapitio ya kitaalamu na mchakato wa udhibiti wa mazingira, Mamlaka ya Taifa ya Usimamizi wa Mazingira (NEMA) ilitoa leseni ya EIA mwezi Desemba 2025, ikiruhusu KWS kuendelea na utekelezaji wa mradi wa uhamishaji na uboreshaji wa kituo hicho.

KWS inasema kuwa uamuzi huo unaambatana na hitaji la kuboresha ustawi wa wanyama, kushughulikia changamoto za miundombinu na msongamano, pamoja na kuimarisha viwango vya kimataifa vya uhifadhi na elimu ya wanyamapori.
KWS na hatua ya uhamishaji
KWS ilianzishwa chini ya Sheria ya Uhifadhi na Usimamizi wa Wanyamapori (Wildlife Conservation and Management Act) Na. 47 ya Sheria za Kenya. Taasisi hii ilianzishwa mwaka 1989, na kwa sasa inaongozwa na Sheria ya Uhifadhi na Usimamizi wa Wanyamapori ya mwaka 2013. KWS ina jukumu la kuhifadhi na kusimamia wanyamapori nchini Kenya, kutekeleza sheria husika, pamoja na kusimamia hifadhi za taifa, mapori ya akiba, na maeneo ya hifadhi.
KWS ilieleza kuwa uamuzi wa kuhamisha kituo hicho ulitokana na changamoto za kiutendaji na miundombinu, ambazo zimesababisha msongamano wa wanyama, kuongezeka kwa msongo wa mawazo kwa wanyama kutokana na mabanda ya zamani, pamoja na wasiwasi kuhusu ustawi wao.
“Msongamano wa wageni, hasa kutoka kwa wanafunzi na makundi ya ziara, umeathiri uwezo wa kituo na uzoefu wa wageni kwa ujumla. Nafasi ndogo pia imezuia maendeleo ya vituo vya elimu na utafiti, jambo linalopunguza matokeo chanya ya programu za uhamasishaji kuhusu uhifadhi. Mapungufu katika ustawi wa wanyama, pamoja na changamoto za uendeshaji na usimamizi, vinaonyesha hitaji la haraka la kuwa na kituo cha kisasa kilichojengwa mahsusi kwa madhumuni hayo,” ilisema sehemu ya ripoti hiyo.
Chini ya mradi huo, Nairobi Animal Orphanage itahamishwa kutoka eneo lake la sasa la ekari 5 lililo karibu na makao makuu ya KWS, hadi eneo la hekta 31 ndani ya Nairobi National Park. Mpango wa maendeleo pia unajumuisha ujenzi wa daraja la watembea kwa miguu litakalounganisha korido ya hekta 9 kati ya eneo jipya la kituo hicho na Nairobi Safari Walk.
Kupinga hoja za wanaharakati wa mazingira
Makundi mbalimbali ya wanaharakati yameeleza wasiwasi wao, yakiishutumu serikali ya Kenya kwa kufanya mchakato wa uhamishaji wa Nairobi Animal Orphanage kwa usiri.
Akshay Vishwanath, Mkurugenzi Mtendaji wa Public Interest Litigation and Advocacy for the Environment (PILAE), amehoji mantiki ya kutenga hekta 40 kutoka Nairobi National Park, akisema tayari hifadhi hiyo imeathirika na miradi mingine ya serikali.
“Tayari hifadhi imepoteza sehemu ya ardhi na imeathirika kwa kiasi kikubwa kutokana na barabara ya Southern Bypass, SGR Phase 1 na 2, na Inland Container Depot Road. Kituo cha wanyama kinaweza kujengwa mahali popote bila kuathiri malengo yake. Kwa nini kijengwe ndani ya hifadhi?” aliuliza.

Vishwanath pia alikosoa mchakato wa ushirikishwaji wa umma uliofanywa na KWS, akisema haukufikia viwango vinavyotakiwa kisheria wala kuzingatia ipasavyo maoni ya wadau wa hifadhi hiyo.
“Baada ya kikao cha awali cha wadau mwezi Oktoba mwaka 2025, KWS ilikataa kushiriki kwenye mazungumzo zaidi kuhusu mradi huo. Friends of Nairobi National Park waliomba mikutano mara nne kati ya Oktoba 2025 na Februari 2026, lakini maombi yote yalipuuzwa na KWS. Wazo zuri si zuri ikiwa linakiuka sheria,” aliongeza.

Hata hivyo, KWS imekanusha madai hayo. Katika taarifa yake, taasisi hiyo ilisema: “Madai ya Friends of Nairobi National Park kwamba msitu wa juu (upland forest) ndani ya Nairobi National Park unaharibiwa ni ya kupotosha, hayana msingi, na yanachochewa na hisia.”
Taarifa hiyo iliendelea kusema: “Uhamishaji na uboreshaji wa Nairobi Animal Orphanage ni mpango halali, uliopangwa kwa umakini, na unaoangalia mbele, kwa madhumuni ya kuboresha uhifadhi wa wanyamapori, ustawi wa wanyama, elimu ya uhifadhi, pamoja na uzoefu wa wageni.”
Prof Karanja Njoroge, mwanaharakati wa mazingira na mjumbe wa bodi ya Friends of Karura Community Forest Association, pia aliishutumu KWS kwa kufanya mambo kwa usiri, na akauliza kuhusu muda uliochaguliwa wa kuhamisha kituo hicho.
“Kulikuwa na kiongozi mwandamizi nchini ambaye hivi karibuni alisema kwamba Nairobi National Park iko mahali pasipofaa. Kiongozi huyo alisema eneo hilo linapaswa kubadilishwa kuwa makazi ya watu. Hivyo basi, inafanya mtu kujiuliza, je, yeye alikuwa anajua kitu gani ambacho sisi hatukujua?” alisema Njoroge.
Ujenzi unaendelea
Karibu na Nairobi Animal Orphanage, ujenzi unaendelea katika Bomas International Convention Centre (BICC), ukiwa na lengo la kujitangaza kama kitovu kikuu cha mikutano, motisha, makongamano na maonyesho (MICE). Mradi huu wenye thamani ya $324 milioni (KSh41.9 bilioni) unatarajiwa kuhudumia wajumbe 11,000 kwa wakati mmoja. Eneo jipya la kituo cha wanyama litakuwa umbali wa takribani kilomita 1.5 kutoka BICC.

Ripoti ya tathmini ya athari za mazingira iliyoandaliwa na KWS inaonyesha kuwa kutakuwa na eneo la maegesho karibu na lango la kuingilia kituo hicho, lenye uwezo wa kupaki magari 1,300. Muundo wa kituo kipya cha Nairobi Animal Orphanage unajumuisha eneo la maegesho lenye ukubwa wa hekta 3.2.
Uhusiano kati ya kituo hicho na BICC unaonekana wazi katika michoro ya usanifu wa jengo hilo la mikutano. Leseni ya Mamlaka ya Kitaifa ya Usimamizi wa Mazingira yenye nambari NEMA/ENVIS/CPR/LIC/0940 inaonyesha kuwa eneo la maegesho limewekwa kwa namna ambayo itarahisisha ufikaji kwenye kituo cha BICC na kituo cha wanyama.

Mamlaka ya Kitaifa ya Usimamizi wa Mazingira ilitoa leseni Desemba 3, 2025, ikiruhusu KWS kubadilisha matumizi ya hekta 31 za ardhi iliyokuwa imefunikwa na miti asilia, kwa ajili ya uhamishaji wa kituo hicho.
Makundi ya wanaharakati yanadai kuwa sababu halisi ya uhamishaji huo si ustawi wa wanyama, bali ni maslahi ya kibiashara yanayohusiana na hadhi ya eneo hilo kama kituo cha MICE.
“Eneo la maegesho la ukubwa huu linaonekana kupita kiasi kwa kituo cha wanyama, na tunaamini limekusudiwa kuhudumia BICC. Maombi rasmi ya mara kwa mara ya kupata ripoti ya EIA, leseni ya EIA, na michoro ya ujenzi wa BICC yamepuuzwa,” alisema Akshay Vishwanath.
Nobert Nyandire, mhifadhi wa mazingira kutoka Chuo Kikuu cha Cambridge, alisema kuwa ingawa uboreshaji wa kituo hicho ni muhimu, mchakato ulipaswa kuwajumuisha wadau wote ili kujenga uelewa wa pamoja.

“Kuna wadudu wa asili na mimea katika eneo ambalo kituo kinahamishiwa, ambavyo ni muhimu katika mfumo wa ikolojia wa Nairobi National Park. Usumbufu huu unaathiri uadilifu wa uhifadhi,” aliongeza.
Nyandire, ambaye pia ana shahada ya uzamili ya mipango kutoka Chuo Kikuu cha Nairobi, aliitaja Nairobi National Park kama hifadhi ambayo imekuwa ikizidishwa zaidi na ukuaji wa haraka wa mji wa Nairobi.
“Serikali ya Kenya inapaswa kuzingatia misingi bora ya matumizi ya ardhi na kuanzisha miundombinu katika maeneo ambayo tayari yameharibiwa au yenye umuhimu mdogo wa kiikolojia. Kwa sasa, hifadhi muhimu ya kaboni inaendelea kupunguzwa, na inaonekana kama hifadhi hii imechukuliwa kama chaguo rahisi zaidi,” Nyandire aliiambia Mongabay.
Kituo cha wanyama, hifadhi na kituo cha mikutano
Kulingana na International Fund for Animal Welfare, Kenya ilirekodi zaidi ya matukio 26,641 yaliyothibitishwa rasmi ya migogoro kati ya binadamu na wanyamapori nchini kote kati ya Julai 2023 na Juni 2025.
Jijini Nairobi, wakazi wa Lang’ata na Rongai waliripoti kuonekana kwa simba, chui, nyati na fisi wanaozurura, wanaodhaniwa kuvuka kutoka Nairobi National Park.
Njoroge ameeleza uwezekano wa kuongezeka kwa migogoro hiyo kutokana na kutengwa kwa hekta 31 za ardhi. “Tunapaswa kuwa na mjadala wa kupanua hifadhi, si kuendelea kupunguza ardhi yake wakati tayari wanyama wanakabiliwa na msongamano,” aliiambia Mongabay.
Hata hivyo, KWS imesema itafanya urejeshaji wa mazingira kwa hatua, kwa kutumia mimea asilia ili kurejesha muundo wa makazi na kuimarisha mfumo wa ikolojia.
Brian Awuonda, mwanasheria wa mazingira na haki ya tabianchi, amesema hatua ya KWS ni sehemu ya mjadala mpana duniani kuhusu mgongano kati ya haki za kiuchumi na haki za mazingira. “Hoja inayojitokeza ni kwamba haki ya mazingira inahusiana na haki ya kuishi, kwa sababu ubora wa mazingira ya mtu unaathiri moja kwa moja maisha yake. Kwa muktadha huo, tunatafuta kuelewa, kati ya haki za kiuchumi na za mazingira, ipi ina uzito zaidi?”

Kuhusu madai ya kukosekana kwa ushirikishwaji wa umma, Awuonda aliiambia Mongabay kuwa KWS ilitegemea mwongozo wa vyombo mbalimbali vya kisheria, ikiwemo Sheria ya Uhifadhi na Usimamizi wa Wanyamapori, na Sheria ya Usimamizi na Uratibu wa Mazingira na akabainisha kuwa mpango huo ulianzishwa mwaka 2013 na umejadiliwa kwa zaidi ya muongo mmoja.
“KWS ilipaswa kutoa tangazo rasmi la serikali (gazeti la serikali) katika vyombo vya habari vinavyosambazwa kitaifa kama njia mojawapo ya chini ya ushirikishwaji wa umma. Lakini kwa sasa, mapitio ya kimahakama ndiyo njia bora ya kumaliza mvutano huu. Mahakama itaamua kama uamuzi huo ulikuwa wa busara, wazi na unaoweza kuhalalishwa,” alisema.
Uhamishaji wa Nairobi Animal Orphanage ni mchakato muhimu unaoonyesha mjadala wa Kenya kuhusu uhifadhi wa mazingira katika miji. Ikiwa hatua hiyo itasababisha kupungua kwa ukubwa wa hifadhi kwa ajili ya miundombinu kama maegesho, inaweza kuwa ishara ya mwanzo ya kuporomoka kwa uadilifu wa hifadhi hiyo. Kwa upande mwingine, ikiwa ahadi ya KWS ya kujenga kituo cha kisasa cha kiwango cha kimataifa itatekelezwa, kituo hicho kinaweza kuingia katika karne yake ijayo kama mfano bora wa usimamizi wa kisasa wa wanyamapori.
Picha ya bango: Eneo lililofyekwa kwa ajili ya ujenzi ndani ya hifadhi, huku ujenzi wa Kituo kipya cha Bomas (Bomas International Convention Centre) ukionekana upande wa pili wa barabara. Picha kwa hisani ya PILAE.
Nukuu
Nairobi National Park Management Plan (2020-2030)
Wildlife Census Methodology – WRTI/KWS
Impact of Urbanization on NNP – ResearchGate
https://new.kenyalaw.org/akn/ke/act/2013/47/eng@2022-12-31
https://nairobipark.org/athi-kapiti-ecosystem/
https://new.kenyalaw.org/akn/ke/act/2013/47/eng@2022-12-31
https://new.kenyalaw.org/akn/ke/act/ln/2009/61/eng@2022-12-31
