- Satelaiti husaidia kubaini matukio ya moto mapema na kuuzima kabla ya kuleta madhara.
- Juhudi hizo zimesaidia kupunguza matukio ya moto kwa asilimia 11 kwa mwaka.
- Watetezi wa mazingira wataka watu waelimishwe ili walinde maeneo yanayowazunguka.
Katika juhudi za kubaini matukio ya moto mapema na kuudhibiti kabla ya kuenea na kusababisha madhara makubwa katika hifadhi za misitu, Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania unafanya ufuatiliaji wa moto nchi nzima kwa kutumia teknolojia ya satelaiti.
Hayo yamesemwa na Waziri wa Maliasili na Utalii Ashatu Kijaji wakati akiwasilisha hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka 2026/2027 mnamo Mei 15, katika kikao cha bajeti kinachoendelea katika mji mkuu wa nchi, Dodoma.
Kijaji alisema kupitia juhudi hizo, matukio ya moto yamepungua kwa wastani wa asilimia 11 kwa mwaka. Aidha, ukubwa wa maeneo yanayoathirika na moto kila mwaka unaendelea kupungua.
Katika hotuba yake, Waziri alisema pia kuwa Wakala umesafisha njia za kuzuia moto zenye urefu wa kilomita 2,723, kusimamia minara 17 ya kuangalizia moto pamoja na vituo saba vya kufuatilia na kudhibiti moto katika maeneo ya hifadhi, huku ukidhibiti matukio 92 ya moto.
Waziri huyo aliongeza kuwa Wakala umetoa mafunzo ya mbinu za kukabiliana na kudhibiti moto kwa vikosi 45 vyenye jumla ya watu 705. Vilevile, mafunzo yametolewa kwa wananchi 20,297 kutoka vijiji 245 vinavyopakana na hifadhi za misitu na mashamba ya miti yaliyopo katika maeneo mbalimbali nchini.
“Wakala utaendelea kuzuia na kupambana na matukio ya moto kwa kufanya kampeni 295 za kuzuia moto katika vijiji 337 pamoja na kuunda vikundi 49 vyenye jumla ya watu 588 kwa ajili ya kuzuia na kudhibiti moto kwenye hifadhi za misitu,” Kijaji alisema katika hotuba yake.
Aidha, kwa mujibu wa Kijaji, Wakala utafungua kilomita 114 za njia mpya za kuzuia moto na kusafisha kilomita 4,376 za njia za kuzuia moto katika mashamba 26 ya miti.
“Vilevile, Wakala utaendelea kusimamia minara 19 ya kuangalizia moto na kujenga minara mipya mitatu katika mashamba ya miti Silayo na Buhigwe pamoja na Msitu wa Hifadhi ya Mazingira Asilia Pugu/Kazimzumbwi,” alisema.
Sauti za watetezi wa mazingira
Kufuatia kauli hiyo ya Kijaji, watetezi wa masuala ya uhifadhi na mazingira wameitaka serikali kutilia mkazo elimu kwa wananchi, hasa wale wa vijijini ili kukomesha tabia hiyo ambayo inaendelea kuleta wasiwasi kuhusu athari zake za muda mrefu kwa mazingira.
“Wananchi inabidi waelimishwe na kufahamu kwamba uchomaji moto katika hifadhi na misitu una athari kubwa kwa mazingira, wanyama na pia bioanuwai,” alisema Joachim Maganga, Mwasisi na Mwenyekiti wa Mazingira ni Uhai, taasisi isiyo ya kiserikali inayojishughulisha na uhifadhi wa mazingira katika maeneo ya vijijini.
Amesema wananchi wengi wanaposikia kuhusu uchomaji wa misitu hudhani athari zake ni kwa miti tu. Hawafahamu kwamba kitendo hicho kinaharibu pia makazi ya viumbe mbalimbali, wakati mwingine wanyamapori, ndege na wadudu muhimu katika mfumo wa ikolojia.
“Madhara ya vitendo hivyo hayaathiri kizazi chao tu bali hata kizazi kijacho,” aliongeza Joachim.
Peter Mayalla, Katibu Mkuu wa taasisi hiyo, anasema iwapo wananchi wataelimishwa na wakawa na uelewa wa kutosha, wao wenyewe watakuwa walinzi wa maeneo yanayowazunguka.
“Tujifunze kwa wenzetu wa kata za Mlimani na Boma huko Manispaa ya Morogoro. Baada ya kuhamasika, waliamua kuwa walinzi katika kudhibiti vitendo vya uchomaji moto wa misitu ya asili na Hifadhi ya Milima ya Uluguru,” alisema Peter.
Miongoni mwa mifano inayoleta kumbukumbu ya huzuni kuhusu uchomaji moto ni tukio lililotokea Desemba 2025, ambapo moto mkubwa wa porini uliozuka katika eneo la Mount Hanang uliharibu zaidi ya hekta 170 za msitu na kuzua hofu kubwa miongoni mwa wakazi.
Queen Sendiga, Mkuu wa Mkoa wa Manyara, ambaye aliongoza operesheni ya dharura, alinukuliwa na vyombo vya habari akisema serikali imetuma zaidi ya wanamgambo 200 pamoja na mamia ya wananchi kujitolea kusaidia kuzima moto huo.
Kwa mujibu wa taarifa za vyombo vya habari moto huo ambao chanzo chake hakikuthibitishwa ulizuka ndani ya Hifadhi ya Asili ya Mount Hanang na ilikuwa vigumu kuudhibiti kutokana na miteremko mikali, upepo mkali na milipuko mipya ya moto iliyokuwa ikijitokeza mara kwa mara kwenye korongo makubwa.
Picha ya bango: Waziri wa Maliasili na Utalii Ashatu Kijaji wakati akiwasilisha hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka 2026/2027 mnamo Mei 15, katika kikao cha bajeti kinachoendelea katika mji mkuu wa nchi, Dodoma.