- Kila mwaka, Tuzo ya Mazingira ya Goldman huwaheshimu wanaharakati wa ngazi ya chini kutoka kila moja ya kanda sita za mabara yenye wakazi.
- Washindi wa tuzoza 2026 ni Iroro Tanshi kutoka Nigeria, Borim Kim kutoka Korea Kusini, Sarah Finch kutoka Uingereza, Theonila Roka Matbob kutoka Papua New Guinea, Alannah Acaq Hurley kutoka Marekani, na Yuvelis Morales Blanco kutoka Colombia.
Wanaharakati sita wa mazingira kutoka ulimwenguni kote walitunukiwa Tuzo ya Mazingira ya Goldman tarehe 20 Aprili. Ikitambulika kama “Tuzo ya Nobel ya Kijani,” Tuzo ya Goldman huwaheshimu wanaharakati kutoka kanda sita za mabara yenye wakazi. Kwa mara ya kwanza katika historia, washindi wote sita ni wanawake.
Washindi wa mwaka huu walipambana kulinda popo adimu nchini Nigeria kwa kutoa mafunzo kwa wanajamii kuhusu kuzuia moto katika maeneo ya nyika; walishinda kesi ya kihistoria mahakamani nchini Korea Kusini na kulazimisha serikali kuweka malengo madhubuti ya hali ya hewa; walisimamisha mradi wa kuchimba mafuta nchini Uingereza baada ya miaka kumi ya vita vya kisheria; waliishinikiza kampuni kubwa ya uchimbaji madini duniani kusafisha mgodi ulioachwa wenye sumu huko Papua New Guinea; walizuia mgodi mkubwa wa shimo wazi uliopendekezwa katika historia ya Marekani Kaskazini huko Alaska; na wakasaidia kusimamisha miradi ya uchimbaji mafuta kwa mbinu ya kupasua miamba nchini Colombia.
“Wakati tunaendelea kupigana kulinda mazingira na kutekeleza sera za hali ya hewa za kuokoa maisha nchini Marekani na duniani kote, ni wazi kwamba viongozi wa kweli wako miongoni mwetu,” alisema John Goldman, makamu wa rais wa wakfu wa mazingira wa Goldman. “Nimefurahi sana kuheshimu kundi letu la kwanza kabisa la wanawake sita, kwani hili ni onyesho kubwa la nafasi ambayo wanawake wanaendelea kuchukua katika jamii ya mazingira ulimwenguni.”
Washindi walitunukiwa katika hafla iliyofanyika San Francisco nchini Marekani tarehe 20 Aprili, iliyoandaliwa na mtangazaji wa Telemundo Vanessa Hauc, pamoja na burudani ya muziki kutoka kundi la Caminos Flamencos. Tukio hilo lilionyeshwa moja kwa moja kuanzia saa 5:30 asubuhi kwa saa za ndani (00:30 UTC tarehe 21 Aprili) kwenye chaneli ya YouTube ya Tuzo ya Goldman.
Tuzo ya Mazingira ya Goldman ilianzishwa mnamo mwaka 1989 na Richard na Rhoda Goldman. Washindi wa tuzo huchaguliwa na jopo la kimataifa la waamuzi kutoka kwa uteuzi wa siri unaowasilishwa na mtandao wa kimataifa wa mashirika ya mazingira na watu binafsi.
Hawa ndio washindi wa Tuzo ya Mazingira ya Goldman mwaka 2026:
Iroro Tanshi — Nigeria (Afrika)

Popo wa mkia mfupi mwenye umbo la mviringo wa kijani (Hipposideros curtus) hakuwa amerekodiwa popote duniani kwa miaka mitano wakati mwanaikolojia wa uhifadhi Iroro Tanshi alipogundua tena koloni dogo lililokuwa katika Hifadhi ya Wanyamapori ya Mlima wa Afi nchini Nigeria mwaka wa 2016. Ilikuwa ni mara ya kwanza kuthibitishwa kuonekana nchini katika kipindi cha miaka 45. Wiki mbili baadaye, moto wa mwituni ulipita eneo hilo na kukaribia kuliharibu.
Tukio hilo lilimpa motisha Tanshi, ambaye sasa ana umri wa miaka 41, mkurugenzi wa Shirika la Uhifadhi wa Mamalia Wadogo (SMACON). Alitumia miaka mingi kujenga mpango wa jamii wa kuzuia moto wa nyikani akitumia mbinu zinazofanana na programu za Huduma ya Misitu ya Marekani na mifano ya hatari ya moto kutoka Kusini Magharibi mwa Marekani.
Akifanya kazi na vijiji 16 vinavyozunguka hifadhi ya hekta 1,000 (takriban ekari 25,000), alisaidia jamii kuandaa sheria za misitu na adhabu za kifedha kwa uchomaji haramu, na kuweka vituo vya hali ya hewa ili kutoa tathmini za kila siku za hatari ya moto. Mpango huo uliwapa mafunzo walezi 50 wa misitu walio na mikoba ya maji, vifaa vya GPS na redio za mawasiliano za njia mbili. Katika siku za hatari sana, watangazaji wa kijiji huzunguka kijiji asubuhi, wakitangaza tahadhari za kutochoma moto kwa upatu.
Tangu mapema mwaka wa 2022, walezi wamefanya doria katika zaidi ya mashamba 2,400 na kudhibiti mikurupuko 74 ya moto, na kuwazuia kuongezeka na kuwa moto wa nyikani usioweza kudhibitiwa. Eneo hilo la hifadhi, ambalo pia ni makazi ya sokwe, gorila na nyani walio katika hatari ya kutoweka, limeendelea kuhifadhiwa. Mpango huo umesaidia kulinda mazao na maisha ya takriban watu 27,000 katika jamii zinazozunguka. Kwa sasa Tanshi anafanya kazi ya kupanua mradi huo kote Nigeria na katika nchi nyingine.
Borim Kim — Korea Kusini (Asia)

Borim Kim, mwenye umri wa miaka 31, alianzisha shirika la Youth 4 Climate Action (Y4CA) baada ya wimbi la joto kali lililoweka rekodi mwaka 2018 huko mjini Seoul na kusababisha kifo cha mwanamke karibu na umri wa mama yake kutokana na ugonjwa wa joto ndani ya nyumba yake mwenyewe. Kim alihitimisha kuwa athari za mabadiliko ya tabianchi hazikuepukika kwa urahisi kupitia chaguo bora; badala yake, ziliwaathiri zaidi wale waliokuwa na rasilimali chache zaidi za kujilinda.
Shirika la Y4CA lilianza na migomo na kampeni za barua kwa watunga sheria, kabla ya Kim kuhamia mkakati wa kisheria. Mnamo mwezi Machi mwaka 2020, aliwaandaa vijana walalamishi 19 kuwasilisha malalamiko ya kwanza ya kikatiba yanayoongozwa na vijana huko Asia. Mashtaka zaidi yalifuatiwa kutoka kwa mashirika ya kiraia na, baadaye, kutoka kwa watoto wachanga waliowakilishwa na walezi wao katika kile kilichojulikana kama “Kesi ya Hali ya Hewa ya Watoto.” Shirika la Y4CA pia liliwasilisha “Muhtasari wa Ushiriki wa Umma” unaojumuisha ushuhuda kutoka kwa zaidi ya watu 5,200.
Mnamo mwezi wa Agosti mwaka 2024, Mahakama ya Kikatiba ya Korea Kusini iliamua malengo ya serikali ya hali ya hewa kuwa kinyume na katiba, na kuamuru bunge kuweka malengo ya kisheria ya kupunguza uzalishaji wa hewa chafu kwa kipindi cha 2031-2049. Jumuiya ya wataalam ya Korea Kusini ilikadiria uamuzi huo unaweza kuzuia kati ya tani metriki milioni 1,600 hadi tani milioni 2,100 za uzalishaji wa hewa ya ukaa. Uamuzi huo tangu wakati huo umechochea kesi za hali ya hewa zinazoongozwa na vijana nchini Japani na Taiwan.
Sarah Finch — Uingereza (Uropa)

Sarah Finch, mwenye umri wa miaka 62, alijikwaa katika uharakati wa hali ya hewa mnamo mwaka 2010 wakati tangazo katika gazeti la eneo hilo lilifichua pendekezo la kuchimba mafuta huko Horse Hill, eneo la mashambani katika Kaunti ya Surrey, kilomita 10 (maili 6) kutoka nyumbani kwake. Aligundua baadaye kidogo kuwa ni mojawapo ya miradi mingi ya maendeleo ya mafuta na gesi katika eneo la Weald, eneo lenye miti mingi kusini mashariki mwa Uingereza.
Finch alianzisha kikundi cha kujitolea cha Weald Action Group (WAG), na Baraza la Kaunti ya Surrey lilipoidhinisha mradi wa upanuzi wa Horse Hill mnamo mwaka 2019, aliamua kulipinga mahakamani. Alidai kuwa ukaguzi wa mazingira wa mradi ulizingatia uzalishaji kutoka kwa uchimbaji na ujenzi, lakini alipuuza takriban tani milioni 10.6 za hewa ya ukaa ambazo zingetokana na kuchoma mafuta yaliyotolewa. Baada ya kufeli kwa maombi mawili ya ukaguzi wa mahakama na kushindwa kwa Mahakama ya Rufaa mwaka wa 2022, kikundi cha WAG kilisonga hadi katika Mahakama ya Juu ya Uingereza, iliyofadhiliwa na Sheria ya Usaidizi ya Kisheria ya Mabadiliko.
Mnamo Juni mwaka 2024, mahakama ilitoa uamuzi wa 3-2 kwa upande wa kikundi cha WAG, ikipata kwamba mamlaka ya kupanga lazima zitathmini athari kamili ya hali ya hewa ya chini ya mkondo wa mradi wowote wa uchimbaji wa mafuta kabla ya kutoa kibali. Kituo cha Horse Hill kilisitisha uzalishaji mnamo Novemba mwaka 2024. Athari hizo zilionekana haraka. Ndani ya miezi kadhaa, serikali ya Uingereza ilivuta uungaji mkono wake kwa maendeleo makubwa mawili ya mafuta ya Bahari ya Kaskazini, mgodi wa makaa ya mawe uliopangwa ulipoteza kibali chake, na serikali ikatangaza kupiga marufuku leseni mpya za mgodi wa makaa ya mawe. Kufikia mwisho wa mwaka, “hukumu ya Finch” ilikuwa imechangia kucheleweshwa au kughairiwa kwa miradi na uzalishaji wa pamoja unaokaribia tani milioni 400 za hewa ya ukaa.
Theonila Roka Matbob — Papua New Guinea (Visiwa na Mataifa ya Visiwa)

Theonila Roka Matbob, mwenye umri wa miaka 35, alikulia katika kivuli cha mgodi wa shaba na dhahabu wa Panguna katika Kisiwa cha Bougainville, mojawapo ya shughuli kubwa zaidi za uchimbaji wazi wa madini duniani wakati wa miaka yake ya shughuli. Mgodi huo ulifanya kazi kutoka mwaka 1972 hadi mwaka 1989 chini ya kampuni tanzu ya kampuni kubwa ya uchimbaji madini ya Anglo-Australian Rio Tinto. Wakati huo, ilitupa wastani wa tani 150,000 za taka za madini kwa siku katika mito ya karibu, wakati jamii za mashinani zilipokea 1.4% tu ya mapato.
Wakati wakazi walipopingana dhidi ya uharibifu wa mazingira, vita vya kikatili vya wenyewe kwa wenyewe vilifuata na kusababisha vifo vya hadi watu 20,000. Baba ya Matbob alikuwa miongoni mwa wale waliouawa, na Matbob alitumia miaka sita ya utoto wake katika kambi ya wakimbizi. Rio Tinto iliachana na mgodi huo mwaka wa 1989, na mwaka wa 2016 ilitenga hisa zake huku ikikanusha jukumu la kusafisha. Miongo kadhaa baadaye, mifumo ya mito ya Jaba na Kawerong imesalia ikiwa imechafuliwa, huku vizazi vya jamii za chini ya mto vikiripoti magonjwa ya ngozi, magonjwa ya kupumua na matatizo ya ujauzito.
Mnamo mwaka 2020, Matbob alikuwa mlalamishi mkuu katika malalamiko ya haki za binadamu na wanajamii 156 dhidi ya kampuni ya Rio Tinto, iliyowasilishwa na Kituo cha Kitaifa cha Mawasiliano cha Australia kwa Maadili ya Biashara Husika. Mwaka huo huo alishinda kiti katika bunge la Bougainville.
Malalamiko hayo yalisababisha Rio Tinto kufadhili tathmini huru ya athari, iliyokamilishwa mwaka wa 2024. Mnamo mwezi wa Novemba mwaka 2024, kampuni ilitia saini mkataba wa maelewano na serikali ya Bougainville ikikiri rasmi madhara ya mgodi huo na kujitolea kurekebisha, ikiwa ni pamoja na kupanuliwa kwa upatikanaji wa maji safi na mfumo wa tahadhari ya mapema kwa hatari za ardhi kama maporomoko na mitikisiko. Ni ishara ya kwanza ya uwajibikaji ambayo jamii imeona katika miaka 35.
Alannah Acaq Hurley — Marekani (Kaskazini Marekani)

Alannah Acaq Hurley, mwenye umri wa miaka 40, alikulia Saguyaq (Clark’s Point) kwenye fuo za Bristol Bay ya Alaska, ambapo nyanyake alipitisha mafundisho ya Asilia ya Yup’ik yaliyokita mizizi katika ardhi na maji. Ghuba hiyo na sehemu zake za maji hutegemeza makazi makubwa zaidi duniani ya samaki aina ya salmoni mwenye mnofu mwekundu (Oncorhynchus nerka), huku samaki milioni 50 hivi wakizaa huko kila mwaka, wakidumisha tamaduni za Wenyeji, mifumo ikolojia, na tasnia ya uvuvi yenye thamani ya $2.2 bilioni.
Tangu mwaka wa 2001, mfumo wa ikolojia umekuwa ukitishiwa na Mgodi wa Pebble unaopendekezwa, mradi mkubwa wa shaba na dhahabu kwenye vyanzo vya maji ambao ungekuwa na shimo lenye upana wa kilomita 4 (maili 2.5), kilomita 160 (maili 100) za barabara mpya, na bwawa kubwa zaidi la udongo la kuhifadhia taka duniani. Wanasayansi walikadiria uharibifu wa karibu kilomita 160 za mito ya salmoni na hekta 850 (ekari 2,100) za ardhi oevu.
Hurley alipanga kwa mara ya kwanza dhidi ya mgodi kama mwanafunzi wa chuo kabla ya viongozi wa kikabila kumchagua mnamo 2013 kama mkurugenzi mkuu wa shirika la United Tribes of Bristol Bay (UTBB), akiwakilisha mataifa 15 ya kikabila yanayotambuliwa na serikali. Muungano huo ulijengwa kwa makusudi, ukiunganisha vikundi vya wenyeji asili, vyama vya wavuvi wa kibiashara na mashirika ya kitaifa ya mazingira.
Kampeni ya shirika la UTBB ilitoa zaidi ya milioni moja ya maoni ya umma kwa Shirika la Ulinzi wa Mazingira la Marekani (EPA). Hurley alitoa ushahidi mbele ya bunge la Congress mwaka wa 2019. Mnamo Novemba mwaka 2020, Kikosi cha wahandisi wa jeshi kilikataa kibali cha maji cha mgodi huo. Shirika la UTBB liliendelea kusisitiza serikali, na Januari mwaka 2023 shirika la EPA lilitumia mamlaka yake ya kura ya turufu, mara ya 14 tu katika historia yake, kuzuia mradi huo kabisa. Hurley na shirika la UTBB sasa wanafanya kazi kuratibu ulinzi huo kuwa sheria.
Yuvelis Morales Blanco — Colombia (Marekani Kusini na Kati)

Yuvelis Morales Blanco, mwenye umri wa miaka 24, alikulia katika jamii ya Afro-Colombia ya Puerto Wilches kwenye kingo za Mto Magdalena, katika familia ya wavuvi ambayo ilitegemea afya ya mto huo ili kuishi. Alitazama vuno la samaki wa babake wakipungua mwaka baada ya mwaka huku mafuta yakimwagika kutoka kwa miundombinu ya karibu ya Ecopetrol ikichafua maji. Mnamo mwaka wa 2018, mlipuko katika uwanja wa mafuta wa kampuni ya Lizama ulipeleka mafuta ghafi kutiririka kwenye vijito viwili vya Magdalena, na kulazimisha karibu familia 100 kuhama na kuua maelfu ya samaki na wanyama wengine.
Wakati dalili za uchimbaji kwa kupasua miamba kwa shinikizo la maji zilipoanza kuonekana katika njia yake ya chuo kikuu, Morales Blanco alijiunga na shirika la Alianza Colombia Libre de Fracking na kuanzisha Aguawil, shirika la vijana ambalo lilikwenda nyumba hadi nyumba huko Puerto Wilches kuelezea hatari za miradi ya majaribio ya Ecopetrol iliyopendekezwa ya Kalé na Platero iliyoletwa mtoni. Kampeni hiyo ilikua, na kufikia kilele cha maandamano makubwa ya barabarani mnamo Desemba mwaka 2020. Ushahidi wake kwenye mkutano wa hadhara mnamo Januari mwaka 2021 ulisambazwa sana. Pia ilimfanya kuwa shabaha: Wanaume waliojihami kwa silaha walitokea nyumbani kwake mapema mwaka 2022, na kumlazimisha kutafuta hifadhi nchini Ufaransa.
Uhamisho wake wa hadhi ya juu ulisaidia kuinua suala hilo kuwa ajenda muhimu katika uchaguzi wa rais wa mwaka 2022 wa Colombia. Mshindi wa mwisho, Gustavo Petro, alitangaza kuwa hakuna miradi ya kupasua miamba itakayoendelea chini ya usimamizi wake, na Ecopetrol ilisimamisha kandarasi zake mnamo Septemba mwaka 2022. Mnamo mwezi Agosti mwaka 2024, Mahakama ya Kikatiba ya Colombia iliamua kuwa miradi hiyo ilikuwa imekiuka haki ya jamii ya Afro-Colombia ya kupata ridhaa ya jamii mapema, kwa hiari na kwa ufahamu kamili. Tangu wakati huo, hakuna miradi ya kupasua miamba kwa shinikizo la maji iliyoendelea popote nchini Colombia.
Picha ya bango: Washindi wa mwaka 2026 wa Tuzo ya Mazingira ya Goldman. Picha kwa hisani ya Goldman Environmental Prize.
Habari hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza hapa kwa lugha ya Kiingereza mnamo tarehe 20/04/2026