- Mfumo umerahisisha uwasilishwaji wa taarifa sahihi na kuepuka udanganyifu.
- Uwazi na uwajibikaji vimeongezeka, sasa inawezekana kufuatilia kila muamala.
- Sasa malipo ya fidia yatachukua siku sabahadi 14, tofauti na miezi sita hadi 12 ya awali.
Wizara ya Maliasili na Utalii imeanzisha mfumo wa Problem Animals Information System (PAIS), mahsusi ulioundwa kusimamia taarifa za matukio ya wanyamapori wakali pamoja na kuratibu na kuwezesha ulipaji wa vifuta jasho/machozi kwa wananchi wanaoathirika na matukio hayo.
Hayo yamesemwa na Waziri Ashatu Kijazi wakati akiwasilisha hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka 2026/2027, Mei 15, katika kikao cha bajeti kinachoendelea makao makuu ya nchi, Dodoma.
Amesema mfumo huo wa kisasa umerahisisha ukusanyaji, uwasilishwaji wa taarifa sahihi na kuepuka udanganyifu. Umeboresha pia uchakataji na utunzaji wa taarifa za matukio ya uharibifu wa wanyamapori wakali na waharibifu.
Vilevile, mfumo umerahisisha malipo ya kifuta jasho na machozi kwa wananchi waliopata madhara ya wanyamapori wakali na waharibifu.
“Kwa sasa taratibu za malipo zinachukua siku saba hadi 14 tofauti na taratibu za awali ambapo malipo yalikuwa yakichukua miezi sita hadi 12,” amesema.
Sambamba na hilo, waziri amesema mfumo umeongeza uwazi na uwajibikaji kwani unawezesha kufuatilia kila muamala.
Kwa mujibu wa Waziri, hadi kufikia Aprili mwaka 2026, Wizara imelipa kiasi cha TSh8,149,314,750 ($3,134,351) ikiwa ni kifuta jasho na machozi kwa wananchi 22,696 waliopatwa na madhara ya wanyamapori katika Halmashauri za Wilaya 81 ikilinganishwa na 43 katika kipindi kama hiki cha Mwaka wa Fedha 2024/2025 ambapo jumla ya TSh4,604,909,750 ($1,771,119) zililipwa kwa wananchi 16,939.

Taarifa hiyo ya Kijazi kuhusu maboresho kwenye utaratibu wa malipo ya fidia huenda ikawa mkombozi kwa wananchi ambao wamekuwa wakitumia muda mrefu kufuatilia malipo yao huku baadhi yao wakikata tamaa kutokana na mlolongo mrefu uliopo.
Alan Fidelis aliwahi kunukuliwa na Mongabay akieleza jinsi alivyoteseka kufuatilia madai yake.
Alisema kilichomuuma zaidi ni kwamba alipowasilisha malalamiko yake baada ya shamba lake la mpunga kuliwa lote na tembo, alisubiri kwa miaka mitatu kabla ya kupata kifuta jasho kutoka Serikali.
Anasema wakati anafuatilia malipo yake aliambiwa kwamba utolewaji wa fedha hutegemea uwepo wa bajeti.
Mkuu wa Kitengo cha Maliasili na Uhifadhi wa Mazingira Wilaya ya Iringa John Mtimbanjayo ambaye anashughulikia masuala ya migogoro kati ya wanyamapori na binadamu aliiambia Mongabay kuwa malipo ya kifuta jasho huchelewa kutokana na mlolongo mrefu wa mchakato wenyewe ambao huanzia kijijini, kwenda wilayani na kisha wizarani.
Alisema kuwa mchakato huo hujumuisha kujaza fomu, kupiga picha ya athari za shamba na picha ya mkulima kuwekwa kwenye fomu husika na kisha kuwasilisha wilayani ambapo pia maofisa wilayani huhitaji kujiridhisha kwa kutembelea eneo husika. Baada ya maofisa ngazi ya wilaya kujiridhisha, huwasilisha madai wizarani lakini hufanya hivyo baada ya kuwa wamekusanya madai mengi kwa pamoja ili kupunguza gharama.
“Hata wizarani nao huhitaji kwenda hadi kijijini kujidhirisha na hii, kutembelea wilaya zote zenye athari na kuiridhisha, inachukua muda mrefu. Mambo yote yanaweza kukamilika, lakini ikiwa bajeti haitoshi, itabidi malipo yasubiri,” anasema.
Kwa mujibu wa Kanuni za kifuta jasho kwa uharibifu unaosababishwa na wanyamapori wakali ya mwaka 2024 (Wildlife Conservation (Dangerous Animals Damage Compensation) Regulations, 2024), kifuta jasho hutofautiana kulingana na umbali liliko shamba kutoka kwenye hifadhi.
Kwa shamba lililo chini ya kilomita moja kutoka kwenye hifadhi halilipwi kifuta jasho chochote. Kilomita 1 hadi nne hulipwa TSh75,000 ($30); kilomita 4–5 hulipwa TSh112,000 ($45) wakati shamba lililo zaidi ya kilomita 5 hulipwa TSh150,000 ($60) kwa ekari moja.
Picha ya bango: Baadhi ya wanyama wanaopatikana katika mbuga nchini Tanzania. Picha kutoka tovuti ya TANAPA.