- Uuzaji wa bidhaa za wanyamapori kupitia mtandaoni kutoka kwa spishi zinazolindwa unashamiri kwenye Facebook. Jukwaa hilo lilikuwa mwenyeji wa zaidi ya robo tatu ya wanyamapori 22,000 na mizoga yao inayojulikana kuuzwa mtandaoni kati ya Aprili 2024 na Machi 2026,yenye thamani ya $65 milioni, kulingana na ripoti ya hivi majuzi.
- Watafiti waligundua kuwatakriban 84% ya wanyama wanaouzwa kwenye Facebook ni wale ambao biashara yao ya kimataifa imepigwa marufuku. Zaidi ya nusu yao walikuwa katika hatari ya kutoweka au viumbe hatarini sana.
- Muundo wa mtandao wa Facebook, makundi yake yaliyofungwa, watumiaji wasiojulikana, uchumaji wa mapato ya maudhui na kanuni za algoriti zinazosukuma maudhui yanayohusiana kwa watumiaji huifanya kuwa jukwaa la wasafirishaji haramu, watafiti wanasema. Sera rasmi ya jukwaa hilo inazuia uuzaji wa wanyamapori, lakini idadi ya wanyama wanaotolewa kwa ajili ya kuuzwa inaonyesha udhibiti hafifu.
- Ili kukabiliana na biashara hii kubwa ya mtandaoni, wataalamu wanatoa wito wa udhibiti mkali wa maudhui kwenye Facebook na mifumo mingine, pamoja na uangalizi bora na kuongezeka kwa ushirikiano kati ya mifumo ya mtandaoni na utekelezaji wa sheria.
Kwa kubonyeza tu kitufe au kutelezesha vidole kwenye simu, unaweza kununua karibu chochote mtandaoni, ikiwemo wanyama adimu au walio hatarini. Kuanzia nyara za kipekee za papa hadi ndege hai wa kigeni, pembe za faru au pembe za ndovu, wanunuzi wanaweza kwenda kwenye majukwaa ya biashara ya mtandaoni na kuzipata zote. Wasafirishaji hujificha nyuma ya skrini zao huku wakinufaika kutokana na mauzo ya mtandaoni ya spishi za wanyama wanaolindwa huku wanyama hawa wakipungua porini.
“Ni soko kubwa zaidi la wanyamapori,” alisema mtafiti wa biashara ya wanyamapori Chris Shepherd kutoka Kituo cha Biolojia Anuwai. “Ni rahisi, unaweza kufanya kazi bila kujulikana ukiwa nyumbani kwako. Hakuna gharama za kuanzisha duka.”
Biashara ya mtandaoni katika bidhaa haramu za wanyamapori inaendelea kukua, ikihusisha spishi zaidi na jiografia pana. Ni tasnia haramu inayoendeshwa na mitandao ya uhalifu iliyopangwa vizuri, na ni vigumu kushtaki. Kukamata wahalifu mtandaoni ni changamoto sana.
“Masoko ya wanyamapori yamehamia kutoka maeneo halisi hadi maeneo ya mitandaoni, na hiyo inaakisi mwelekeo mpana zaidi wa uchumi wa dunia,” alisema Simone Haysom, mkurugenzi wa programu za uhalifu wa kimazingira katika shirika lenye makao yake makuu Uswizi la Global Initiative Against Transnational Organised Crime.
Katika ripoti ya hivi karibuni, Haysom na mwenzake Russell Gray walichanganua data ya biashara ya wanyamapori mtandaoni kuanzia mwezi wa Aprili 2024 hadi mwezi Machi 2026. Waliangazia mataifa 10 katika mabara matatu, mahali ambapo uhalifu wa kimazingira na matumizi ya intaneti ni mkubwa, na kuyafanya kuwa mazingira yanayochochea biashara ya wanyamapori mtandaoni. Walipata bidhaa 266,535 za wanyamapori zilizochapishwa kwenye masoko 61 ya mitandaoni, yenye thamani ya takriban $66 milioni.
Takriban 75% ya karibu matangazo 22,000 waliyoyaona yalikuwa kwenye Facebook, jukwaa ambalo limejulikana kwa uuzaji wa wanyamapori hai, kama uchunguzi wa hivi karibuni wa Mongabay ulivyoonyesha.

Idadi kubwa ya spishi zinazotolewa mtandaoni, takriban 84%, zimepigwa marufuku kuuzwa kimataifa chini ya Mkataba wa Biashara ya Kimataifa ya Viumbe vya Pori vilivyo Hatarini kutoweka, yaani CITES. Zaidi ya nusu ya matangazo yote ya Facebook yalitoa wanyama walio hatarini kutoweka au walio katika hatari kubwa ya kutoweka ikiwa ni pamoja na kakakuona, sokwe wadogo, mumbi, kasa, swila na chui mawingu.
“Kuna kila kitu kwenye Facebook,” Gray alisema, akitoa mifano ya kwato za kakakuona, ngozi ya sokwe na pembe za ndovu zilizotiwa nakshi za sili wa baharini. “Ulimwengu hauko tayari kwa kiasi kikubwa cha biashara ya mtandaoni ya wanyamapori.”
Ingawa majukwaa ya Facebook, Etsy, Amazon na eBay yana sera zinazokataza uuzaji wa wanyama hai na bidhaa zao, mauzo ya mtandaoni yamekithiri na wanunuzi wanawanunua.
“Inafurahisha kuona ripoti nyingine ikitoka inayoweka biashara ya mtandaoni, na hasa masuala yanayohusu Facebook, kuangaziwa,” alisema Shepherd, ambaye amefanya kazi na majukwaa kama vile Etsy na eBay kukomesha biashara ya popo waliopakwa rangi (Kerivoula picta). Ripoti hii, alisema, inaonyesha kwamba Facebook ni “kitovu kikubwa cha biashara” kwa viumbe vilivyo hatarini. Shepherd hakuhusika katika uchapishaji wa ripoti hii.

Facebook ni jukwaa bora kwa wasafirishaji
Muundo wa Facebook hurahisisha uuzaji wa wanyamapori, waandishi wanasema. Mtu yeyote anaweza kufungua akaunti au kikundi cha faragha, cha wanachama pekee bila uthibitishaji wa kimwili au ukaguzi, mara nyingi kwa kutumia majina bandia au kuchapisha bila kujulikana. Watumiaji wanaweza pia kuwasiliana kwa faragha, kwa kutumia huduma yake ya ujumbe iliyosimbwa kwa njia fiche.
Lakini makundi ya Facebook, yanayoleta pamoja watu walio na mambo ya kawaida au mapendeleo ya pamoja (katika kesi hii, biashara ya wanyamapori), ni kitovu ambako wanunuzi na wauzaji wanaweza kujadiliana kupitia ujumbe wa kibinafsi, hivyo kufanya kuwa vigumu kwa wachunguzi kufuatilia.
Kwa sasa, algoriti za Facebook hufuatilia shughuli na maslahi ya watumiaji, na kupendekeza kurasa zinazofanana, anwani mpya, vikundi na maudhui yanayohusiana na biashara ya wanyamapori. Jukwaa pia huwaruhusu watumiaji kuchuma mapato kupitia maudhui yao: Wanaweza kupata pesa kwa kuunda maudhui kwa wateja wao wanaolipa.
Kabla ya kuibuka kwa vikundi vya Facebook, Haysom alisema biashara nyingi za wanyamapori mtandaoni zilipunguzwa kwa majukwaa ya mashabiki bila mpangilio au tovuti ambazo alizifananisha na “matoleo madogo ya Reddit” ambayo yalilenga spishi maalum au vikundi vya wanyama. Lakini sasa, hizo zimetoweka, alisema.
“Makundi ya Facebook kwa kweli yalibadilisha aina nyingi za tovuti kwenye mtandao kwa kutoa miundombinu hii ya bure iliyowezesha biashara hiyo kustawi,” Haysom alisema.

Facebook inakataza uuzaji wa “bidhaa au sehemu yoyote” kutoka kwa wanyama walio hatarini na walio kwenye tishio, kama vile mfupa, meno, pembe, meno ya tembo, mizoga au wanyama hai. Mnamo mwaka wa 2019, pia ilianzisha arifa zinazojitokeza kwamba biashara ya wanyama walio kwenye hatari ya kutoweka ni kinyume cha sheria. Lakini kama ripoti mpya inavyoonyesha, bidhaa hizi bado zinatangazwa kwa wingi. Waandishi wanasema hiyo ni kwa sababu jukwaa la Facebook hufanya kazi duni ya kudhibiti maudhui.
Kwa kuwa ni asilimia 12 tu ya machapisho yaliyokuwa kwa Kiingereza, usimamiaji mwingi ulikuwa kwa Kiingereza. “Ni jukwaa la kimataifa, lakini [Facebook] haidhibiti kama jukwaa la kimataifa,” Haysom alisema.
Majukwaa mengine ya e-commerce “yanaonekana kuwa tayari zaidi” kudhibiti kile ambacho watumiaji huchapisha na kuondoa maudhui ambayo yanakiuka sera zao, Gray alisema. “Facebook haina udhibiti huo.” Katika uzoefu wake, alisema, “Iwapo unaripoti jambo ambalo ni kinyume cha sheria na linaenda kinyume na viwango vya jumuiya yao, wanakutumia tu ujumbe wa kiotomatiki wakisema kuwa hakikiuki viwango vya jamii, na hawauondoi.”

Tangu mwaka wa 2018, kampuni mama ya Facebook, Meta, imekuwa sehemu ya Muungano wa Kukomesha Usafirishaji Haramu wa Wanyamapori Mtandaoni, kundi la mashirika yaliyoundwa ili kukabiliana na biashara haramu ya mtandaoni. Katika ripoti yake ya hivi karibuni, muungano huo ulisema kuwa kati ya mwaka 2018 na mwaka 2025 uliondoa orodha za wanyamapori milioni 63.3 zilizopigwa marufuku na kuwazuia wauzaji. Lakini haikueleza kwa undani ni wapi orodha hizo ziliwekwa.
“Haujui ni kipi kimeondolewa na nani,” Haysom alisema. “Tunategemea Facebook kutuambia kilichoondolewa na kilichofanywa. Hakuna uangalizi huru.”
Kurasa mpya na vikundi vya mauzo ya wanyama vinaendelea kuonekana, ripoti inasema, zaidi ya nusu yao iliundwa baada ya Facebook kujiunga na muungano huo, kwa hivyo ufuatiliaji wa mara kwa mara unahitajika. Wakati Facebook inapozuia watumiaji au kufunga kikundi, wasafirishaji huwa haraka kuunda akaunti au kikundi kingine, Shepherd alisema. “Siwezi kudhania mtu yeyote kuacha kuuza wanyamapori haramu kwa sababu akaunti yao imeondolewa.”
Tangu kashfa ya Cambridge Analytica ilipotangazwa hadharani mnamo mwaka wa 2018, ikifichua data ya kibinafsi ya watumiaji milioni 87 kwa wahusika wa tatu kwa utangazaji wa kisiasa, jukwaa la Facebook limeimarisha ufikiaji wa data yake kwa kila mtu, pamoja na mashirika ya kiraia ambayo yanafuatilia biashara ya wanyamapori. “Kwa hivyo, hakuna njia ya kubinafsisha utafutaji na kudhibiti jukwaa kama mtu wa tatu,” Gray alisema.
Tangu hapo, jukwaa limeruhusu watumiaji kuchapisha bila kujulikana, hali iliyowasaidia wahalifu kushamiri, alisema. “Ni kama mtandao wa giza, kwa kweli. Hakuna tofauti halisi.”
Meta haikujibu maswali ya Mongabay kuhusu matokeo ya ripoti hiyo, au hata hatua inazochukua kukabiliana na usafirishaji wa wanyamapori katika majukwaa yake.


Wauzaji na Wanunuzi kwenye Facebook
Ripoti haikuangazia wasifu wa wanunuzi au wauzaji. Lakini uchambuzi wao unaonyesha, Gray alisema, kwamba watu wanaouza wanyama kwenye jukwaa la Facebook mara nyingi ni wawindaji haramu ambao huwinda kwa urahisi kitu cha ajabu na wanataka kukiuza. Ni namna wanavyofanya mawasiliano ya awali na walanguzi wa wanyamapori na wanunuzi.
“Kama watamwinda kakakuona, wanafanya nini naye? Jamii hata hawatainunua kwa sababu wanajua ni haramu, au hawana uwezo wa kuinunua. Kwa hivyo, jambo la kwanza watakalofanya ni kwenda kwa kikundi kinachoitwa ‘pangolins for sale’ kwenye Facebook,” Gray alisema. “Kisha mtu atajitolea kumnunua. Na kuanzia hapo, wanawasiliana na mtandao mkubwa wa walanguzi wa wanyamapori.”
Lakini vikundi hivi si wanunuzi na wauzaji tu: Kampuni za usafirishaji mizigo na kampuni za dhamana za kifedha (escrow) hutangaza huduma zao kwa wafanyabiashara na mawakala ambao hujumlisha wanyamapori kabla ya kuwasafirisha nje kwa kiwango kikubwa. Mara mtu anapopata kikundi, algoriti hufanya kazi ya kuwaonyesha kadhaa zaidi ili kuongeza mwonekano wao, kuwasaidia kujenga miunganisho.
“Sisi hatuangalii tu masoko, pia tunaangalia uundaji wa mitandao … wawindaji haramu wanaounganishwa na mawakala,” Haysom alisema. “Kwa kweli unahitaji watu wachache tu kuunda mtandao wa kimataifa wa usafirishaji wa wanyamapori na kufanya uharibifu mkubwa.”
Baadhi ya wawindaji haramu wanaingiza pesa maradufu, wanapata pesa kupitia uchumaji wa mapato wa Facebook kwa waundaji wa maudhui huku wakiuza wanyama adimu, wanaolindwa. “Wanawawinda wanyamapori walio hatarini kutoweka, na wanachapisha shughuli zao kwenye jukwaa la Facebook na pia kufanya mauzo yao kupitia akaunti hizo,” Gray alisema. “Huu ni mwelekeo ulioanzishwa au unakuwa mtindo.”
Haja ya kanuni kali zaidi
Ripoti hiyo inataka kuwepo kwa kanuni zinazozuia taratibu za majukwaa kuongeza maudhui yanayohusiana na biashara haramu ya wanyamapori. Aidha inataka ufuatiliaji bora wa machapisho, hasa yale ambayo hayako kwa Kiingereza. Pia ni muhimu, waandishi wanasema, kwa Facebook kufungua usimamizi wake kwa uangalizi huru na kuratibu na utekelezaji wa sheria ili kuwanasa walanguzi.
“Tunahitaji udhibiti wenye meno,” Haysom alisema. “Kujidhibiti haijafanya kazi … na hakuna uwezekano wa kufanikiwa kikamilifu.” Alitoa Sheria ya Huduma za Dijitali ya Jumuiya ya EU kama mfano. Sheria hii ya mwaka 2022 inaamuru mifumo ya mtandaoni kuthibitisha wauzaji na kuondoa maudhui haramu. “Sidhani kama ni jambo gumu kuelewa.”
Majukwaa ya Facebook na Instagram kwa sasa yanachunguzwa katika jumuiya ya Bara Ulaya kuhusu kanuni za algoriti zinazohimiza tabia za uraibu kwa watoto na kwa kutotii sheria hiyo. Hivi majuzi Meta ilipatikana na hatia na Tume ya Ulaya kwa kushindwa kuzuia watoto walio na umri wa chini ya miaka 13 kuingia kwenye majukwaa yake.
Licha ya ripoti na tafiti kwa wingi kufichua biashara haramu ya wanyamapori kwenye Facebook, Meta haijawajibishwa nchini Marekani, ambako ndiko makao yake makuu, kwa sababu ya ulinzi chini ya Kifungu cha 230 cha Sheria ya Uadilifu ya Mawasiliano ya Marekani. Sheria ya mwaka 1996 inazuia kampuni za huduma za mitandao ya Marekani kuwajibika kwa maudhui yaliyotumwa na watumiaji, isipokuwa pale ambapo maudhui hayo yanakiuka sheria ya jinai ya shirikisho ya jinai ya shirikisho na serikali inaweza kuonyesha uthibitisho kwamba kampuni ilifanya hivyo kimakusudi.
Hilo mara nyingi ni vigumu kulithibitisha. “Serikali ingehitaji ushahidi kwamba Meta ilikuwa ikifanya zaidi ya kuandaa chapisho hilo,” Gray alisema. “Ndio maana, kiutendaji, swali sio, ‘Je, wanyamapori haramu waliuzwa kwenye Facebook?’ Ni, ‘Je, Facebook yenyewe ilishiriki katika uhalifu huo kwa kujua?'”

Lakini maamuzi ya hivi majuzi ya mahakama huko California na New Mexico yamedai kuwa Meta inawajibika kwa maudhui yake, haswa kwa madhara kwa afya ya akili ya watoto. Baraza la mahakama huko New Mexico liliongezea kusema kwamba Meta ilificha ilichokifahamu kuhusu unyanyasaji wa kingono kwa watoto kwenye jukwaa, na hivyo kuendeleza madhara hayo kwa kujua.
Gray alisema anatumai watunga sera wa Marekani wanaona hitaji la kanuni zinazowajibisha majukwaa ya mtandaoni kwa shughuli zingine za uharibifu. “Biashara ya mizoga ya wanyamapori inaposonga hadi kwenye biashara ya kidijitali, itakuwa vigumu katika siku zijazo kuidhibiti.”
Shepherd alisema majukwaa yanahitaji kusonga mbele zaidi ya kuondoa machapisho. “Hiyo ni kukwaruza tu. Kinachotakiwa kufanywa ni ufuatiliaji: Watu hawa wako wapi? Wako wapi wanyama hawa wanaouzwa?” Alisema. “Hatua za utekelezaji zinapaswa kuchukuliwa.”
Alisema majukwaa ya mtandaoni sharti yashirikiane na vyombo vya sheria ili kuwanasa wasafirishaji na kuwafikisha mahakamani. “Wanahitaji kwenda zaidi ya kusumbua vikundi hivi vya wafanyabiashara na kuzingatia kuwashtaki watu hawa, kuwakamata watu hawa na kuwaondoa kwenye biashara.”
Muda unayoyoma kwa vitendo. Biashara hiyo kubwa inachangia kile kinachoitwa Kipindi cha Sita cha Kutoweka kwa wanyama wengi, na spishi nyingi ziko katika matatizo makubwa, zikikaribia ukingoni.
“Meta inahitaji kujiuliza ni jukumu lipi linataka kuchukua katika mchakato huo. Je, inataka kuwa jukwaa kuu ambapo biashara hiyo imejikita na kupunguzwa, au inataka kuweka kielelezo cha namna ya kukabiliana na biashara changamano ya mtandaoni?” Haysom aliuliza.

Picha ya bango: Simbamarara wa Bengal kutoka Rajasthan, nchini India. Uwindaji haramu ni mojawapo ya vitishio vikubwa kwa simbamarara, kutoka spishi ya paka aliye hatarini kutoweka barani Asia. Picha © Thomas Fuhrmann kupitia iNaturalist (CC BY-NC 4.0).
Spoorthy Raman ni mwandishi katika Mongabay, anayeangazia mambo yote ya porini kwa uzingatio maalum juu ya wanyamapori wasiojulikana sana, biashara ya wanyamapori, na uhalifu wa mazingira.
Nukuu:
Salas-Picazo, R. I., Ramírez-Bravo, O. E., Meza-Padilla, I., & Camargo-Rivera, E. E. (2023). The role of social media groups on illegal wildlife trade in four Mexican states: A year-long assessment. Global Ecology and Conservation, 45, e02539. doi:10.1016/j.gecco. 2023.e02539
Ceballos, G., Ehrlich, P. R., & Raven, P. H. (2020). Vertebrates on the brink as indicators of biological annihilation and the sixth mass extinction. Proceedings of the National Academy of Sciences, 117(24), 13596–13602. doi:10.1073/pnas.1922686117
Habari hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza hapa kwa lugha ya Kiingereza mnamo tarehe 5/05/2026




