- Mahakama ya Mazingira na Ardhi ya Isiolo imeidhinisha kesi dhidi ya BP kuendelea kusikilizwa kikamilifu kuhusu madai ya uchafuzi wa mazingira.
- Walalamikaji 299 kutoka Kargi na Kalacha wanadai taka za sumu kutoka uchimbaji wa mafuta (1985–1993) zilichafua maji ya ardhini, kusababisha vifo vya zaidi ya watu 500 na mifugo mingi.
- Taka hizo zinadaiwa kuwa na kemikali hatari kama radiamu, aseniki, risasi na nitrati, zilizotupwa bila usalama na kampuni ya Amoco (iliyonunuliwa na BP).
- Kesi inaungwa mkono na PARAAN na inaweza kuwa mfano muhimu kwa madai mengine ya uchafuzi wa mafuta kaskazini mwa Kenya.
Mahakama ya Mazingira na Ardhi mjini Isiolo Kenya, imeamuru kwamba kesi ya hatua ya ngazi ya juu dhidi ya kampuni kubwa ya mafuta ya Uingereza ya BP inaweza kuendelea kusikizwa kikamilifu. Katika kesi hiyo, inadaiwa kuwa taka za sumu zilizoachwa kutokana na uchimbaji wa mafuta katika miaka ya 1980 zilichafua maji ya ardhini kaskazini mwa Kenya, na kuua zaidi ya watu 500 na maelfu ya mifugo.
Kesi hiyo, iliyofunguliwa Februari na walalamikaji 299 katika Mahakama ya Mazingira na Ardhi mjini Isiolo, ilifikishwa mahakamani na wakazi wa Kargi na Kalacha, makazi mawili yaliyoko katika kaunti ya Marsabit.
Inadaiwa katika kesi hiyo kuwa shughuli za uchimbaji wa mafuta zilizofanywa kati ya mwaka 1985 na mwaka 1993 kaskazini na kaskazini-magharibi mwa Kenya na Shirika la Amoco, ambalo lilinunuliwa na BP mwaka wa 1998, vichafuzi hatari na sumu vilimwagwa kwenye mazingira, na kuchafua maji ya ardhini ambayo jamii hutegemea kwa kunywa na kwa mifugo yao.
Hati za korti zinadai kuwa taka za kuchimba visima zilizo na isotopu za radiamu, aseniki, madini ya risasi na nitrati, zilitupwa kwenye mashimo yaliyoachwa wazi au ambayo hayakuwekwa katika hali inayotakiwa kiusalama.
Katika kesi hiyo, washitakiwa ni pamoja na kampuni ya British Petroleum PLC ambayo ni mshitakiwa wa kwanza, huku wengine 11 wakiwa ni Shirika la Kitaifa la Mafuta la Kenya; mawaziri wa mazingira, maji, afya na madini; Mamlaka ya Rasilimali za Maji; serikali ya kaunti ya Marsabit; mwanasheria mkuu; Mamlaka ya Kitaifa ya Usimamizi wa Mazingira; Mamlaka ya Udhibiti wa nishati ya Nyuklia ya Kenya pamoja na Taasisi ya Utafiti wa Matibabu ya Kenya.
Ofisi ya Waandishi wa Habari ya BP iliiambia Mongabay kupitia barua pepe kwamba haikuwa na maoni yoyote juu ya kesi hiyo. Uamuzi wa Mahakama Kuu wa mwezi Aprili hauwajibishi wahusika lakini unafuta kizingiti cha kisheria ili kesi ya msingi iweze kusikilizwa kikamilifu.
Walalamikaji 299 waliotajwa huenda wakawa tu wawakilishi au sehemu ndogo tu ya wale walioathirika. Kesi hiyo inaungwa mkono na Muungano wa Wafugaji wa Kuvumilia na Kukabiliana na hali ngumu katika Mataifa (PARAAN), mtandao wa mashirika ya kiraia 37 kutoka kaunti tisa za Kenya na nchi tatu za Afrika Mashariki. Mratibu wa PARAAN, Liban Golicha, aliiambia Mongabay kuwa shirika hilo lilifikia uamuzi wa kuwa sehemu ya sakata hilo baada ya shirika mwanachama katika kanda hiyo kuwaletea ushahidi kutoka kwa jamii hiyo.
“Hii ilikuwa dhuluma ya muda mrefu na ya kihistoria ambayo ilitokea zamani,” Golicha alisema. “Tulikuja kuwaunga mkono, kuwasaidia kupata ridhaa ya jamii na kuwezesha timu ya kisheria kutembelea tovuti na kusaidia kuratibu wadau wengine.”
Kulingana na Golicha, kesi hiyo, haiko peke yake. Madai ya aina hiyo ya utupaji wa taka za sumu na kampuni za uchimbaji mafuta, yameibuliwa pia katika kaunti zingine kaskazini mwa Kenya zikiwemo Garissa, Wajir na Isiolo. Shirika la PARAAN limeanza kupokea maswali kutoka kwenye maeneo hayo kuhusu namna ya kufuatilia hatua mbalimbali za kisheria…
“Iwapo hatua hii itafanikiwa, litakuwa funzo muhimu.” Kwa sasa, shirika la PARAAN linashughulikia kesi ya Kargi na Kalacha kama jaribio,’’ alisema Golicha.
Picha ya Bango: Wakazi wa Kalacha wakati wa mkutano na wawakilishi wa mashirika ya kiraia na wanasheria mnamo Februari, 2026. Picha kwa hisani ya Zeitun.