- Hong Kong na Singapore, vitovu viwili vya biashara ya wanyamapori barani Asia, viliingiza zaidi ya milioni mojaya ndege hai, karibu theluthi mbili kutoka Afrika kati ya mwaka 2006 na mwaka 2020, kulingana na uchambuzi mpya wa data ya forodha. Chiriku, wakiwemospishi zinazopungua porini, ziliongoza katika orodha.
- Zaidi ya theluthi mbili ya ndege hao walitoka nchi za Afrika ambako kanuni za usafirishajinje ya nchi ni dhaifu, zikiwemo Mali, Guinea, Tanzania na Msumbiji.
- Biashara hii kubwa ya ndege hai hupunguza idadi ya ndege wa porini na huenda ikaeneza magonjwa hatari au viumbe vamizi,watafiti wanasema.
- Wataalamu huhimiza nchi ziweke vikwazo vya kuagiza ndege hai, kutekeleza hatua kali zaidi za kuwaweka karantini na kupitisha orodha ambayo imeidhinishwa ya wanyama wa kufugwa ambao hawahatarishi viumbe hai au afya ya binadamu.
Ulimwenguni kote, watu hununua na kuwinda karibu nusu ya spishi 11,000 za ndege waliopo. Katika mabara ya Asia, Ulaya, Amerika Kaskazini na Amerika Kusini, ndege wa kuimba na kasuku ni ndege wa kufugwa nyumbani wanaotamanika sana. Wafugaji wa ndege hao hulipa pesa nyingi sana kwa spishi adimu au ndege wenye sauti nzuri ili kushindana katika mashindano ya uimbaji wa hali ya juu.
Wafugaji wa ndege aina ya vipanga na wawindaji wa michezo hukamata au kuua ndege wa porini. Matambiko ya imani za jadi katika Afrika Magharibi hujumuisha viwiliwili vya tai. Wanunuzi kutoka Marekani ya Kaskazini hutafuta hondohondo na ndege mvumaji waliokufa kama mapambo ya nyumbani. Orodha inaendelea.
Biashara hii kubwa inatisha zaidi ya spishi 200 za ndege kutoweka. Sasa, huku masoko ya mtandaoni yakiongezeka, wateja wanaweza kuagiza ndege kwa kubonyeza simu zao za mkononi kutoka mahali popote katika sayari.
Kusafirisha ndege kote ulimwenguni pia husambaza magonjwa hatari, kama vile homa ya ndege na virusi vwa circovirus, na wakati ndege wasio wa asili wanapotoroka au kuachiliwa, wanaweza kuongezeka kuwashinda spishi za asili.
“Kuna ukosefu wa ufahamu na kuthamini ukubwa wa biashara hii, na umakini mchache sana juu ya athari ambazo hii inaweza kuwa nayo kwa wakazi wa porini au hatari za kuenea kwa viumbe vamizi na magonjwa ya kuambukiza,” Rowan Martin ni mkurugenzi wa biashara ya ndege katika shirika lisilo la faida la World Parrot Trust. “Ikiwa watu hawajui kwamba hili linafanyika, basi tutawezaje kupunguza hatari zinazohusiana nayo?”
Katika kujaribu kuelewa ukubwa wa biashara ya ndege hai, Martin na wenzake walitumia hifadhidata ya Umoja wa Mataifa ya Comtrade (UN Comtrade), hifadhidata inayojumlisha taarifa za bidhaa zote zinazouzwa kati ya mataifa. Timu ilichanganua uagizaji wa ndege hai hadi Singapore na Hong Kong, vitovu vya biashara ya wanyamapori barani Asia kati ya mwaka 2006 na mwaka 2020. Pia walichunguza data ya uagizaji wa spishi mahususi kutoka Hong Kong na kuchapisha matokeo yao katika jarida la Conservation Biology.

Zaidi ya ndege milioni katika biashara, na inakua
Wakati Martin aliuita utafiti huo kuwa ni “picha ya biashara,” watafiti walinakili idadi kubwa ya ndege wanaoingia kwenye vibanda viwili vya biashara ya wanyamapori barani Asia, wengi wao kutoka Afrika: Zaidi ya ndege hai milioni moja katika kipindi cha miaka 15 ya utafiti waliingia katika vituo viwili. Singapore ilivuta karibu robo tatu yao.
Chiriku (Crithagra spp.), ndege wa nyimbo wenye manyoya yanayovutia macho, waliongoza orodha ya ndege walioletwa Hong Kong. Spishi mbili hasa, Chiriku wenye uso wa njano (C. mozambica) na nyuni mweupe (C. leukopigia) zilichangia asilimia 84 ya uagizaji uliorekodiwa kutoka Afrika kati ya mwaka 2015 na mwaka 2020.
Ingawa bado haziko katika hatari ya kutoweka, idadi ya spishi nne zinazotafutwa zaidi baada ya chiriku inapungua porini.
“Matokeo haya hayatushangazi vile, kwani tumekuwa tukizingatia mielekeo sawa,” alisema mtafiti wa biashara ya ndege Simon Bruslund kutoka Bustani ya Wanyama ya Copenhagen. Aliendelea kusema ameona tu ndege aina ya chiriku wenye koo nyeusi (C. atrogularis) kutoka Afrika wakitolewa kwa ajili ya kuuzwa katika soko nchini Indonesia.
Biashara ya wanyamapori inabadilika-badilika, na spishi zinazouzwa, njia za biashara na vitovu muhimu vya biashara hubadilika kwa wakati kulingana na kile wateja wanataka, viwango vya utekelezaji na faida. Bruslund, ambaye hakuhusishwa na utafiti huo, alisema hali hiyo inatumika hapa. “Biashara kwa hakika sio tuli na wasafirishaji hubadilika haraka kulingana na fursa.”
Takriban 14% ya aina za ndege zinadhibitiwa chini ya mkataba wa CITES, mkataba wa kimataifa ambao unadhibiti biashara ya mimea na wanyamapori. Takriban spishi 5,000 zinapatikana sokoni, lakini ni takriban spishi 1,600 tu ambazo zinalindwa chini ya mkataba wa CITES. Haijulikani ni ndege wangapi wanaovutwa au kuwindwa kutoka porini na hali gani inaharibu idadi ya watu, wataalam wanasema.
Ingawa data ya Comtrade si pana, inaweza kutofautiana na kukosa taarifa za spishi, zinaonyesha kiwango kikubwa cha biashara, hali inayotia wasiwasi kwa mataifa yanayosafirisha na kuagiza, watafiti waliandika. Bruslund alisema kwamba data yake ni “muhimu kwa kugundua mitindo mipya mapema.”

Afrika kitovu cha mauzo ya ndege hai
Karibu theluthi mbili ya ndege, asilimia 65, walitoka Afrika, wengi wao wakitoka porini, timu ya Martin ilipata. Walijumlisha takriban ndege 150,000 kutoka kwa aina 34 za spishi za ndege wa kuimba wa Kiafrika waliosafirishwa hadi Hong Kong, mojawapo ya maeneo machache barani Asia ambapo data ya kiwango cha spishi inapatikana kwa wanyamapori walioagizwa kutoka nje. Mali, Guinea, Tanzania na Msumbiji yalisafirisha ndege wengi zaidi.
“Ndege wa Kiafrika wanajulikana kwa sababu kumekuwa na udhibiti mdogo sana wa kanuni za mauzo ya nje,” Martin alisema. “Kuna wafanyabiashara wachache wakubwa wanaofanya kazi Afrika Magharibi, na mara nyingi biashara hizi za familia zina vifaa vikubwa vya kuwahifadhi ndege ambapo hukusanya ndege kabla ya kuwasafirisha nje, na mitandao ya kijamii imewezesha miunganisho kwa wanunuzi wapya.”
Kihistoria, Marekani na Umoja wa Ulaya zilikuwa sehemu kuu za mauzo ya ndege wa porini kutoka bara la Afrika. Takriban 70% ya ndege waliouzwa kihalali kati ya mwaka 1995 na mwaka 2005 walitoka Guinea, Mali na Senegal, huku wengi wakielekea EU, kulingana na utafiti wa mwaka 2017 katika jarida la Science Advances. Jumuiya ya EU ilipiga marufuku biashara zote za ndege wa porini mnamo mwaka 2005.
Hususan Mali, ilichukua jukumu kubwa katika usafirishaji wa ndege wa porini katika miaka ya hivi karibuni. Martin alisema wamepokea ripoti kwamba ndege ambao wamenaswa kwingineko Afrika Magharibi mara nyingi husafirishwa kutoka Mali wakiwa na vibali vya ulaghai vinavyodai kuwa walitoka huko. Kwa mfano, utafiti wake uligundua Mali iliwasafirisha kasuku wa kijivu wa kiafrika (Psittacus erithacus) kabla ya biashara hiyo kupigwa marufuku, ingawa ndege hawa si asili ya nchi hiyo.

Mwaka 2007, Ghana iliondoa spishi 114 za ndege kutoka kwenye mkataba wa CITES Kiambatisho cha III, ambacho hudhibiti mauzo ya nje kwa vibali kutoka nchi hiyo na kufuatilia biashara halali inayotokea huko. Ilikuwa mojawapo ya ufutaji mkubwa kama huu hadi sasa, na imefanya biashara ya ufuatiliaji kuwa ngumu sana.
“Aina hii ya spishi ziliuzwa kabla ya kufutwa kwa orodha, lakini tulikuwa na nambari halisi … Baada ya kufutwa, biashara hiyo ikawa ‘isiyoonekana,’ lakini iliendelea,” Bruslund alisema.
Katika utafiti wa mwaka 2025, yeye na wenzake waliandika kwamba uagizaji wa spishi za Kiafrika kutoka Marekani zilizoondolewa kutoka kwenye CITES uliongezeka mara 14 kwa wastani, ikitoka kutoka karibu sifuri mnamo mwaka 2006 hadi karibu 40,000 mnamo mwaka 2007 na kushuka hadi takriban 20,000 mnamo mwaka 2008.
Utafiti huu wa sasa uligundua kuwa uagizaji wa ndege hadi Hong Kong na Singapore uliongezeka baada ya mwaka wa 2006, na ndege zaidi wakiwasili kutoka Afrika. Martin anahusisha kuongezeka kwa utajiri na uwezo wa kumudu watu wa tabaka la kati barani Asia, pamoja na ongezeko la watu na mitandao ya kijamii ambayo inachochea mahitaji ya wanyama vipenzi wa kufugwa na miunganisho zaidi ya ndege ambayo hurahisisha usafiri.
Kufikia mwaka 2018, biashara ilianza kupungua, labda kutokana na sababu nchi kama Tanzania zilipiga marufuku usafirishaji wa wanyama pori miaka miwili iliyopita, na kwa upande mwingine wa biashara hiyo, Singapore ilisimamisha uagizaji wa ndege wa mapambo kutoka nchi zilizokuwa na milipuko ya mafua ya ndege hivi karibuni. Idadi inayopungua ya ndege maarufu inaweza pia kuwa imejumuishwa, ingawa hakuna anayejua kwa uhakika.
Majukwaa ya mitandaoni yamepanua zaidi biashara. Utafiti wa mwaka 2022 wa Martin na wenzake ulionyesha aina 83 za ndege wa Kiafrika wanauzwa mtandaoni, na watumiaji kutoka Asia Kusini na Mashariki ya Kati walihusika zaidi na machapisho ya kuuza ndege kwenye Facebook.
Martin alisema matokeo hayo yalichochea uchunguzi zaidi kuhusu biashara ya ndege nchini Bangladesh, ambayo ilikuwa ikiagiza viumbe kadhaa vilivyoko kwenye hatari ya kutoweka kutoka ulimwenguni kote. Mnamo mwaka 2024, mkataba wa CITES ulipendekeza kwamba Bangladesh isitishe biashara ya ndege wote waliyoorodheshwa kwenye CITES kimataifa. Nchi ilijibu kwa kusitisha uagizaji wa ndege wote wa kigeni.

‘Inayotisha’ viumbe hai na hatari za afya ya umma
Kwa kanuni chache na ufuatiliaji mdogo wa idadi ya ndege wanaonunuliwa na kuuzwa, biashara kubwa ya ndege wa porini inadhuru viumbe hai barani Afrika. Ndege ni muhimu kwa mazingira kwani huchavusha maua, kutawanya mbegu, kudhibiti vijidudu na kufufua mandhari.
Bruslund alisema masomo ya viwanjani “yanakosekana sana,” hususan katika Afrika Magharibi. “Kwa idadi inayoonekana ya ndege katika biashara ya ndege hai … inakubalika sana kwamba wengi wanaweza kuwa katika matatizo halisi.”
Pamoja na wengi, kama si wote, ndege wanaouzwa kutoka porini, Martin alisema hakuna data ya kubainisha iwapo kiwango hiki cha biashara ni endelevu. “Hakuna ripoti za vituo vikubwa vya kuzalisha ndege hawa, na kwa kweli hakuna kichocheo cha kiuchumi cha kukuza hii kwa sababu wanaweza kunaswa kwa urahisi zaidi porini.”
Mamilioni ya ndege waliojaa katika nafasi ndogo, wakisafirishwa na kuuzwa chini ya hali zenye usumbufu, mara nyingi zisizo na afya, wanaweza kueneza magonjwa hatari kwa ndege waliofungwa na wale wa mwituni, na yamkini kwa wanadamu.
Ugonjwa hatari wa virusi vya circovirus, unaojulikana pia kama ugonjwa wa mdomo na manyoya ya ndege, unatia wasiwasi: Virusi hivyo vilianzia Australia na vimeenea ulimwenguni kote kupitia biashara ya ndege. Psittacosis, ugonjwa mwingine wa bakteria katika kasuku, unaweza kuambukizwa hadi kwa wanadamu na kusababisha homa ya mapafu. Ugonjwa hatari wa mafua ya ndege, ambao umeenea duniani kote, ni wasiwasi mwingine mbaya. Masoko wazi ya ndege hujulikana kuwa maeneo yenye virusi.
“Ni hali nzuri kwa uhamisho wa usawa wa vimelea kati ya aina tofauti za spishi,” Martin alisema. “Hatari za usalama wa viumbe ni za kutisha sana.”
Wakati ndege wasio wa asili wanatolewa au kutoroka, wanaweza kuwa vamizi. Kwa mfano, kasuku huko New Zealand na kimelea fumbwe mkia-mwembamba (Vidua macroura) katika sehemu za Marekani, Karibiani na Hawaii, walioletwa kama wanyama wa kufugwa, wanashindana na ndege wa asili. Kasuku mdogo mwenye shingo ya rangi angavu (Psittacula krameri), aliyeletwa Ulaya kama mnyama kipenzi wa kufugwa, amesababisha kupungua kwa kiasi kikubwa kwa wanyamapori asilia.

Waandishi wa utafiti wanapendekeza kuwa nchi zinazouza bidhaa nje ziangalie upya sera zao za biashara na kuruhusu biashara ikiwa tu manufaa yanazidi hatari kwa mazingira na afya ya binadamu. Nchi zinazoagiza ni sharti ziimarishe hatua za karantini, ziweke ukomo wa idadi na kuhakikisha ndege wanaoingizwa wanapatikana kihalali, waandishi waliandika.
“Nchi nyingi zimeiondokea biashara ya ndege wa mwituni kwa sababu ya hatari na changamoto zinazowezekana za usimamizi bora,” Martin alisema.
Hata hivyo, kuweka vituo vya karantini kunahitaji pesa na wafanyikazi waliofunzwa ili kuhakikisha kuwa itifaki zote za kutengwa zinafuatwa ipasavyo na uwepo wa uangalizi wa kutosha. “Hilo si jambo dogo,” Martin alisema. Ingawa vifaa hivi vitasaidia, ndege wanaosafirishwa kinyume cha sheria bado watakuwa katika hatari kubwa kwa afya ya wanyama na binadamu.
Kujiingiza katika biashara haramu ni changamoto ngumu ya kimataifa. Bruslund anapendekeza usajili na uhifadhi wa kumbukumbu za ndege wote wa porini waliozuiliwa. “Inaonekana kama jambo la kuwajibika kufanya,” alisema. Korea Kusini, Singapore na baadhi ya nchi za Jumuiya ya Ulaya (EU) zinajaribu “orodha chanya” ya wanyama ambao wanaweza kufugwa kama kipenzi. Inaweza kufanya biashara kuwa endelevu kwa kuruhusu uuzaji wa wanyama wanaofugwa pekee na wale ambao sio wavamizi au kuhatarisha afya.
“Hilo lingeruhusu fursa ambapo biashara hii inaweza kuchangia uhifadhi badala ya kinyume chake,” Bruslund alisema.

Picha ya bango: Chiriku mwenye rangi ya njano kutoka Afrika Kusini. Ndege huyo ndiye anayeongoza orodha ya ndege wa mwituni wanaosafirishwa kutoka Afrika hadi Asia. Picha Hakimiliki © ya tjeerd kupitia iNaturalist (CC BY-NC 4.0).
Spoorthy Raman ni mwandishi wa Mongabay, anayeangazia mambo yote ya porini kwa uzingatio maalum juu ya wanyamapori wasiojulikana sana, biashara ya wanyamapori, na uhalifu wa mazingira.
Nukuu
Lees, A. C., Haskell, L., Allinson, T., Bezeng, S. B., Burfield, I. J., Renjifo, L. M., . . . Butchart, S. H. (2022). State of the World’s birds. Annual Review of Environment and Resources, 47(1), 231–260. doi:10.1146/annurev-environ-112420-014642
Trail, P. W. (2022). Dying for love: Illegal international trade in hummingbird love charms. Conservation Science and Practice, 4(6). doi:10.1111/csp2.12679
Challender, D. W. S., Cremona, P. J., Malsch, K., Robinson, J. E., Pavitt, A. T., Scott, J., . . . Hoffmann, M. (2023). Identifying species likely threatened by international trade on the IUCN Red List can inform CITES trade measures. Nature Ecology & Evolution, 7(8), 1211–1220. doi:10.1038/s41559-023-02115-8
Davies, A., Andersson, A. A., Martin, R. O., Inglis, S., & Dingle, C. (2026). Using customs data to understand overlooked trade in non‐CITES birds between Africa and Asia. Conservation Biology, e70265. doi:10.1111/cobi.70265
Reino, L., Figueira, R., Beja, P., Araújo, M. B., Capinha, C., & Strubbe, D. (2017). Networks of global bird invasion altered by regional trade ban. Science Advances, 3(11), e1700783. doi:10.1126/sciadv.1700783
Jürgens, J., Staerk, J., Bruslund, S., Nielsen, R. O., & Conde, D. A. (2025). CITES Appendix III matters: Hidden impacts of CITES deletions on global bird trade. Biological Conservation, 310, 111365. doi:10.1016/j.biocon.2025.111365
Martin, R. O., Senni, C., & D’Cruze, N. C. (2018). Trade in wild-sourced African grey parrots: Insights via social media. Global Ecology and Conservation, 15, e00429. doi:10.1016/j.gecco.2018.e00429
Davies, A., Nuno, A., Hinsley, A., & Martin, R. O. (2022). Live wild bird exports from West Africa: insights into recent trade from monitoring social media. Bird Conservation International, 32(4), 559–572. doi:10.1017/s0959270921000551
Newmark, W. D., Mkongewa, V. J., Amundsen, D. L., & Welch, C. (2020). African sunbirds predominantly pollinate plants useful to humans. The Condor, 122(2). doi:10.1093/condor/duz070
Kang, E. G., Han, J., Shim, Y. J., Lee, D. N., Choi, K., & Yeon, S. (2025). Psittacine beak and feather Disease: global spread, international trade, and conservation challenges. Animals, 15(20), 2947. doi:10.3390/ani15202947
Dutta, S., & Ray, U. (2025). Psittacosis, an uninvited guest. Journal of Global Infectious Diseases, 17(2), 104–107. doi:10.4103/jgid.jgid_113_24
Habari hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza hapa kwa lugha ya Kiingereza mnamo tarehe 15/04/2026