- Kenya imeandika historia kwa kupokea swala wa milimani (Mountain bongos) wanne adimu waliorejeshwa kutoka bustani za wanyama Ulaya, ikiwa ni hatua muhimu ya uhifadhi wa spishi hii iliyo hatarini kutoweka.
- Wanyama hao ni sehemu ya juhudi za kimataifa za kuzaliana na kurejesha idadi yao porini, zikihusisha ushirikiano kati ya taasisi za uhifadhi za Kenya na Ulaya.
- Mradi huu unalenga kuongeza idadi ya swala hao nchini Kenya, ambako wanapatikana kiasili lakini wamepungua sana kutokana na uharibifu wa makazi na uwindaji haramu.
- Kurejeshwa kwao kunatarajiwa kuimarisha juhudi za uhifadhi wa bioanuwai na pia kuchangia sekta ya utalii wa wanyamapori nchini.
Wiki hii Kenya imepokea kundi la swala wa milimani walio katika hatari kubwa ya kutoweka, wakitokea Jamhuri ya Czech ambako walikuwa wakihifadhiwa chini ya usimamizi wa Bustani ya Wanyama ya Zoo Dvůr Králové.
Urejeshaji wa swala hao wanne dume, waliokulia katika bustani mbalimbali za wanyama chini ya mpango wa uhifadhi nchini Uingereza, ni hatua muhimu katika juhudi za Kenya kurejesha wanyama ambao kiasili wana nguvu na hupenda kuzunguka milimani kwa uhuru katika makazi yao ya asili.
Hatua hii pia inaendana na mkakati wa kitaifa wa urejeshaji wa mwaka 2019–2023 unaolenga kuokoa spishi hiyo iliyokuwa hatarini kutoweka, juhudi ambazo zimeendelea hata miaka kadhaa baadaye. Swala hao watahifadhiwa katika Kituo cha Uhifadhi wa Wanyamapori cha Mount Kenya (MKWC), kilichopo katika maeneo ya milimani ya Laikipia.
Uhamisho huo uliongozwa na wataalamu kutoka Bustani ya Wanyama ya Chester nchini Uingereza, kwa ushirikiano na Huduma ya Wanyamapori Kenya (KWS) pamoja na Chama cha Ulaya cha Bustani za Wanyama na Hifadhi za Majini.
Akizungumza wakati wa kupokea swala hao waliowasili kwa ndege ya mizigo ya KLM katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Jomo Kenyatta jijini Nairobi, Waziri Mkuu Msaidizi na Waziri wa Mambo ya Nje na Masuala ya Diaspora, Musalia Mudavadi, alisema kuwa simulizi ya swala wa milimani inaakisi hali pana ya mazingira nchini humo.
Alisema: “Waliwahi kustawi katika misitu ya milimani, kuanzia Aberdares hadi Mlima Kenya, Mau na Eburu, lakini sasa spishi hii ya kipekee inakabiliwa na ukweli mchungu wa kuwa katika hatari ya kutoweka kabisa.”
Wadau wengine kadhaa waliokuwepo ni pamoja na Waziri wa Utalii na Wanyamapori Rebecca Miano, Mkurugenzi Mkuu wa KWS Erustus Kanga, Balozi wa Jamhuri ya Czech Nicol Adamcova, pamoja na wawakilishi wa MKWC, Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Kenya, na shirika la ndege la KLM.
Siku iliyofuata, Huduma ya Wanyamapori Kenya (KWS) ilitoa taarifa kwa umma kuhusu hali ya wanyama hao: “Swala wanne wa milimani wamewasili salama katika Kituo cha Uhifadhi wa Wanyamapori cha Mlima Kenya alfajiri ya leo. Kwa sasa wameanza kuzoea mazingira chini ya uangalizi wa karibu, hatua ambayo ni tulivu lakini muhimu katika kuimarisha idadi yao na kulinda mustakabali wao,” KWS ilisema katika taarifa yake.
Kupitia Mpango wake wa Kurejesha Swala wa Milimani porini, MKWC kwa sasa ni makazi ya zaidi ya swala 100. Kulingana na mkakati wa Kenya, hifadhi hizi zinatumika kuwasaidia wanyama hao kurejesha silika za kuishi porini kabla ya kuwaachia waendelee na maisha katika mazingira yao ya asili. Swala wa milimani huishi kwa takribani miaka kati ya 12 hadi 22.
Mpango wa Kitaifa na Mpango Kazi wa urejeshaji wa swala, ulibuniwa ili kutoa mwongozo kuhusu ongezeko la idadi ya spishi hii, ukiwa na malengo ya kuongeza idadi kutoka swala 96 waliokuwa porini na 77 katika kwenye kituo cha MKWC mwaka 2019, hadi kufikia angalau 750 ifikapo mwaka 2069. Mkakati huo pia ulijumuisha hatua mahsusi za kukabiliana na vitisho vinavyoathiri spishi hiyo.
Shirika la Uhifadhdi wa Mazingira (IUCN) limeonyesha uwezekano wa kuendelea kupungua kwa idadi ya swala hawa, jambo linashinikiza uwepo wa hatua za makusudi kutoka kwa serikali ya Kenya na washirika wake ili kukabiliana na vitisho dhidi ya wanyama hao.
Swala wa milimani ndiye swala mkubwa zaidi, mzito zaidi na mwenye rangi nyingi za kuvutia miongoni mwa swala wa misitu ya Afrika, na hupendelea maeneo yenye vichaka vizito na vilivyofungana. Hula aina mbalimbali za majani.
Kupungua kwa idadi ya wanyama hawa kumehusishwa na kupungua kwa makazi yao, uwindaji haramu, hata katika kipindi cha ukoloni, pamoja na sababu za asili kama magonjwa, mawindo, sumu ya baadhi ya mimea na mapigano kati yao wenyewe.
“Hii (kurejea kwa swala wa milimani kutoka walikokuwa wamefungiwa) ni wakati wa matumaini, wajibu na dhamira mpya ya kulinda mustakabali wa mojawapo ya mamalia wakubwa adimu zaidi duniani,” alisema Kanga.
Picha ya Bango: Swala wa milimani aliye hatarini kutoweka akiwa kwenye Bustani ya Chester, Cheshire, Uingereza. Picha kwa hisani ya Chester Zoo.