- Matumizi ya mbolea za kemikali zaathiri samaki asilia. Kemikali zitokanazo na mbolea za viwandani na viuatilifu huathiri samaki na mazingira.
- Kutokana na uchafuzi wa mazingira samaki wa asili wamepungua kiasi kikubwa.
- Kipindi cha mvua tope na maji yenye sumu kutoka mashambani hutiririka hadi ziwani.
- Sheria inayozuia kilimo ndani ya mita 100 karibu na vyanzo vya maji haitekelezwi ipasavyo.
Pembezoni mwa wilaya ya Missenyi, mkoani Kagera nchini Tanzania, kipo kijiji cha Kashenye kinachopakana na Ziwa Victoria. Ziwa hili ndilo kubwa zaidi barani Afrika, na pili duniani, likiwa na maji baridi. Ziwa Victoria ndio chanzo cha Mto Naili. Lina shughuli nyingi za kiuchumi, hasa uvuvi wa samaki aina ya dagaa, sato, sangara na wengineo.
Amina Juma, mama wa watoto wanne, ambaye pia ni mjane, na anayejulikana zaidi kama Mama Koku, anaishi kijiji hiki, akijishughulisha na kilimo cha mbogamboga katika kitongoji jirani cha Kaishebo.
Mama Koku na watoto wake watatu wana wiki nzima hawajapata kitoweo cha samaki, na wamekuwa wakitumia mboga ya ‘Sukuma wiki’, mchicha na matembele.
Siku moja jioni baada ya kutoka shambani, Mama Koku anafungua fundo la kitenge chake alichokuwa amekipachika kwenye mlango wa chumba chake, anachukua noti pekee aliyokuwa amebaki nayo kama akiba ya nyumbani, TSh10,000 ($3.8), na kumpatia mtoto wake wa kiume, Ruta (11), akimbie mwaloni kununua samaki.
Kutokana na hamu ya kupata kitoweo cha samaki, mtoto anapiga mbio hadi mwalo wa Kabindi, na kama wasemavyo Waswahili, ‘ Mgaagaa na upwa hali wali mkavu’, kijana anajipatia samaki watatu aina ya sato, aliowaona wamenona, kwa TSh8,000.
Mama Koku anapokea samaki kwa furaha na kutayarisha mlo wa usiku. Hata hivyo, baadaye usiku, hali inakuwa si shwari tena kwani watoto wanaanza kulalamikia maumivu ya tumbo, kuharisha na pia kuhisi kizunguzungu, madhila yanayomkumba mama yao pia. Asubuhi wanaamkia zahanati ya kata na majibu ya daktari yanaonyesha wamekula chakula kinachodhaniwa kuwa na sumu.
Hata hivyo Mama Koku anasema daktari hakuthibitisha kama maradhi yaliyowatapa yalitokana na ulaji wa samaki ama la.

Matope na kemikali zenye sumu
Kitongoji cha Kaishebo, kilichoko kando ya Ziwa Victoria, ndiko Mama Koku na wakulima wengine wa mbogamboga na mahindi wanapata riziki zao za kila siku.
Kuwepo kwao hapo kunatokana na ukweli kuwa eneo hilo ni ardhi oevu, chepechepe na nyenye maji ya kunyunyizia mazao yao kama vile nyanya, vitunguu, kabichi na mazao mengine.
Ili waweze kupata mazao mengi na yenye ukubwa wa kuwavutia wanunuzi, wakulima wa mbogamboga hulazimika kutumia mbolea za viwandani na viuatilifu kwa ajili ya kuua wadudu.
Nyakati za mvua tope kutoka mashambani pamoja na maji yenye sumu kutokana na mbolea za viwandani zenye kemikali, hubebwa hadi ziwani.
Wavuvi, ambao pia wanahaha kujipatia riziki, huvua samaki bila kuwa na uhakika kama wako salama ama la, na kuwauza kwa wananchi wakiwemo hao hao wakulima kama Mama Koku.
“Ni mzunguko unaoogopesha sana. Ili kujipatia mazao mengi, wakulima hutumia madawa yenye kemikali zenye sumu na kuchafua ziwa. Samaki kutumia sumu hizo, na wavuvi, bila kufahamu, huwauza kwa hao hao wakulima. Mzunguko huo huendelea hivyo kila siku,” anasema Japhet James, mkazi wa kitongoji cha Kaishebo.
Essau Kayungi, Mwenyekiti wa Kitengo cha Usimamizi wa Ziwa Victoria (BMU) wa Kata Kashenye, anasema ni vigumu kuzuia mzunguko huo hatari kwa sababu wanunuzi wa samaki wana elimu ndogo ya kuwatambua samaki wenye sumu kwa vile hawaonyeshi dalili za wazi.
Kaishebo ni moja tu ya maeneo mengi yanayozunguka Ziwa Victoria, ambako shughuli za kilimo zinafanyika kwenye bonde la ziwa. Katika maeneo yote hayo, wako wakulima wa mbogamboga wengi ambao hutiririsha tope na sumu kwenye ziwa.
Maeneo mengine ambayo kilimo cha aina hiyo kinaendelea ni kando ya Mto Kagera, Mto Mwisa na Kyanyasabi katika Wilaya ya Misenyi mkoani Kagera. Mito hiyo pia humwaga maji kwenye Ziwa Victoria na kuleta madhara.
Uchafuzi wa Mto Mirongo ni chanzo kingine cha maji ambayo yanaathiri Ziwa Victoria.
Wadau wa mazingira nchini wamehusisha uchafuzi wa vyanzo vya maji na kupungua kwa samaki kwenye mito, maziwa na bahari nchini.
Dkt Anthony Tabu Munyaho, Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa Lake Victoria Fisheries Organization, aliwahi kunukuliwa na vyombo vya habari akisema kuwa changamoto kubwa zaidi ni uchafuzi wa vyanzo vya maji unaobadilisha mazingira wanamoishi samaki.
Athari za tope, sumu ziwani
Ingawa hakuna takwimu zozote zinazounganisha moja kwa moja tukio lililompata Mama Koku na wanae na sumu inayoingia ziwani kutokea kwenye mashamba ya mbogamboga yanayotumia mbolea na kemikali zenye sumu, hoja na tafiti mbalimbali vinabainisha ushahidi wa mazingira wa uhusiano huo.

Kulingana na taarifa za kitabibu, dalili kama kutapika na maumivu ya tumbo ni za kawaida na huonekana ndani ya dakika chache hadi masaa kadhaa baada ya kula samaki wenye sumu.
Taarifa zaidi zinasema sumu ya samaki huathiri mfumo wa mmeng’enyo wa chakula na neva kwa walaji na kusababisha maradhi kama vile kutapika, kuharisha na maumivu makali.
Melissa Friedman, katika makala yake ya kitaaluma, ijulikanayo kama Ciiguatera Fish Poisoning: Treatment, Prevention and Management-TCM, iliyochapishwa katika jarida la Marine Drugs, alieleza kuwa kuna uhusiano kati ya kula samaki wenye sumu na maradhi ya tumbo kama kuhara na kutapika.
Makala hiyo ilitahadharisha juu ya athari za vitendo vya kutiririsha tope litokanalo na shughuli za kilimo, hasa cha mbogamboga kando ya Ziwa Victoria. Kwa mujibu wa makala hiyo, vitendo hivyo licha ya kuathiri afya za walaji wa samaki, huchangia pia upungufu wa samaki.
Aidha, athari za kutiririshwa kwa tope na sumu zitokanazo na mbolea kwenye ziwa ni miongoni mwa mambo yaliyowahi kubainishwa na wataalamu kutoka Mradi wa Usimamizi wa Mazingira ya Ziwa Victoria (LVEMP).
Walisema shughuli hizi za kilimo huua chujio za maji na hivyo kuruhusu tope kuingia ziwani na kuwafanya samaki washindwe kuvuta hewa vizuri, na wakati mwingine kusababishia vifo vyao.
Sheria ipo, haitekelezwi
Licha ya vitendo hivyo kuendelea kufanyika, Sheria ya Usimamizi wa Mazingira ya mwaka 2004 inazuia kilimo ndani ya mita 100 karibu na vyanzo vya maji.
Egidius Mutalemwa, Afisa wa Mazingira wilayani Missenyi, katika mahojiano na Mongabay, alisema Mamlaka wilayani Missenyi kwa sasa ipo kwenye operesheni ya kuwaondoa watu waliovamia ardhi oevu katika tarafa ya Kiziba inayopakana na Ziwa Victoria. Alisema watu watakaokaidi amri hiyo watafikishwa mahakamani.
Sambamba na hilo, alisema wanaendelea kutoa elimu ya utunzaji mazingira kwa wananchi ili wafahamu athari zilizopo na namna bora ya kutumia ardhi.

Kwa mujibu wa afisa huyo, kata zinazohusika na operesheni hiyo ni pamoja na Bugandika, Buyango, Ruzimga, Kitobo, Bwanjai, Gera, Ishozi, Ishunju, Kanyigo na Kashenye.
Licha ya Serikali kuja na mkakati wa kuwaondoa wakulima hao wanaokiuka taratibu, huenda ikapata pingamizi. Hiyo inatokana na ukweli kuwa wengi wa wanaolima maeneo hayo na kutumia mbolea na kemikali hizo, wanafanya hivyo kwa vile hawana namna nyingine ya kujipatia riziki.
“Nisipofanya hivyo nitapata wapi fedha ya kujikimu na kuwasomesha wanangu ilhali mimi ni mjane?” alisema Mama Koku alipoulizwa sababu za kutumia kemikali hizo na kulima eneo ambalo ni hatarishi kwa mazingira. Licha ya kukiri kutambua madhara ya matumizi ya kemikali, alisema hamna namna nyingine ya kuendesha kilimo chake.
Amos Nshekanabo, Diwani wa Kata ya Kashenye, aliiambia Mongabay kuwa kupitia Kamati ya Maendeleo ya Kata (WDC), wamekuwa wakiwahimiza wakulima kutolima karibu na vyanzo vya maji, na pia kuwashauri kutumia mbolea za asili kama samadi na mboji (mbolea ya biwi), kwa kilimo endelevu na kisicho na madhara.
Anasema ili kufanikisha hilo, wanatoa pia elimu ya ufugaji wa wanyama kwa lengo la kujipatia mbolea.
Matumizi ya mbolea za kemikali hasa zenye Naitrojeni na Fosforasi katika shughuli za kilimo kwenye bonde la ziwa pia ni chanzo kikubwa cha uharibifu wa mazingira.
Kwa mujibu wa taarifa kuhusu LVEMP III (2018-2022), uharibifu wa mazingira, uvuvi haramu, mabadiliko ya tabianchi na uchafuzi wa mazingira vimesababisha kupungua kwa samaki wa asili katika Ziwa Victoria, huku tafiti zikionyesha upatikanaji wa samaki kwa ujumla ukishuka kwa kiasi kikubwa, katika baadhi ya maeneo ukitajwa kufikia takribani asilimia 35.
Jumuiya ya Kimataifa ya Uhifadhi wa Mazingira (IUCN) imewahi kuonya kuhusu hatari ya kupungua kwa samaki katika Ziwa Victoria, wakiwemo kamba na kaa.
Dkt. Alex Wenaty Ngungulu, mtafiti kutoka Chuo Kikuu cha Kilimo, Sokoine, katika utafiti wake wa 2019, kupitia mradi wa Innovation and Markets for Lake Victoria Fisheries (IMLAF), alionya juu ya matumizi ya kemikali na uwezekano wa viuadudu kujipachika kwenye minofu ya samaki na kusababisha magonjwa yasiyoambukizwa.
Nini kifanyike
Baadhi ya wadau wanapendekeza umuhimu wa utekelezaji wa Sheria ya Usimamizi wa Mazingira ya mwaka 2004 inayozuia kulima ndani ya vyanzo vya maji, serikali kuongeza raslimali ngazi ya Halmashauri na kuwepo kwa ufuatiliaji wa kutosha, kama hatua muhimu za kukabiliana na changamoto hiyo.
“Kuendelea kutoa elimu kwa jamii ikiwemo juu ya matumizi ya mbolea ya samadi na mboji hasa katika maeneo yanayoweza kutiririsha maji kuelekea bondeni mwa ziwa, na kuchukua hatua za kisheria kwa wanaokaidi, ni miongoni mwa mambo yanayoweza kurejesha uhai wa ziwa Victoria,” anashauri Amos.
Picha ya Bango: Shughuli za kilimo kandokando ya ziwa husababisha hatari kwa viumbe wa majini na afya ya binadamu, kwani maji yanayotiririka kutoka mashambani hubeba mbolea na viuatilifu hadi ziwani na kuharibu mfumo wa ikolojia. Picha kwa hisani ya LVEMP.