- Kupitia jaribio hili, hapandi miti tu; anapanda ndani yetu ujasiri na azma ya kuvuka mipaka yetu katika urejeshaji wa misitu.
- Wengi wanaona uhifadhi kama suala la kupanda miti tu, lakini uhifadhi pia ni suala la kiuchumi.
- Kile alichofanya Hillary kinaweza kufanywa na kijana mwingine yeyote.
Kijana mwenye umri wa miaka 29 ambaye ni mwanaharakati wa masuala ya mazingira, ameweka rekodi mpya ya dunia kwa kupanda miti 23,326 ndani ya saa 24, akivunja rekodi ya awali ya Guinness ya kupanda miti 23,060.
Hillary Kiplagat Kibiwott alianzia zoezi hilo katika Kituo cha Misitu cha Kessup kilichoko katika kaunti ya Elgeyo-Marakwet, tarehe 22 Aprili, 2026 chini ya uangalizi mkali wa wawakilishi wa Guinness World Records, Huduma ya Misitu ya Kenya (Kenya Forest Service) pamoja na wahudumu wa afya. Alikamilisha zoezi hilo Alhamisi, tarehe 23 Aprili.

Timu yake kuu ilijumuisha vijana waliokuwa wakichimba mashimo katika eneo la msitu lililoharibiwa lenye ukubwa wa ekari 30 na kumpa miche ya miti, pamoja na baba yake ambaye alimwelekeza na kumsaidia wakati wa zoezi hilo.
Akihamasishwa na umati wa watu waliokuwa wakiimba na kushangilia huku wakitaja jina lake, wakiwemo wanafunzi wa shule za msingi, Hillary alipanda wastani wa miche 16 kwa dakika. Zoezi hilo lilikuwa likirushwa moja kwa moja mtandaoni.
Wakati anafikia mwisho wa zoezi hilo, alikuwa amechoka sana kiasi kwamba alisafirishwa kwa gari la wagonjwa, lakini alirejea baada ya zaidi ya saa moja akiwa tayari kuzungumza na waandishi wa habari na umati uliokuwa ukimsubiri. Alisema lengo lake lilikuwa kuonyesha kuwa mpango wa kupanda miti bilioni 15 uliozinduliwa na Rais wa Kenya, William Ruto, unawezekana.
Kuhusu changamoto wakati wa zoezi hilo, alitaja ardhi yenye milima, joto kali la mchana na baridi ya usiku kuwa baadhi ya mambo yaliyompa wakati mgumu.
Familia yake ilijisikia fahari kuhusu mafanikio ya kijana huyo. Baba yake, Moses Komen, alisema: “Kijana huyo ana mtazamo chanya wa maisha. Wakati wa zoezi hili tulikuwa wote ili kumtia moyo na kumuunga mkono.” Mama yake alisema Hillary amekuwa mtu asiyekata tamaa na ameendeleza hulka hiyo tangu udogo wake. “Kwake huwa hakuna kitu kisichowezekana.”

Awali, Hillary alikuwa ameweka lengo la kupanda miti 24,000. “Kufikia asubuhi nilikosa nguvu. Sikuwa nataka hata kula. Nilianza kwa nguvu lakini nikapoteza uwezo kadri muda ulivyopita. Nashukuru Mungu kwa kile nilichofanikiwa kufanya,” alisema.
Hata hivyo, ili kumpa moyo, Chris Kiptoo, Katibu Mkuu wa Hazina ya Kenya na mlezi wa Mpango wa Uhifadhi wa Kaptagat, alisema: “Sir Winston Churchill aliwahi kusema, ‘Mafanikio si kitu cha mwisho. Kushindwa si mwisho. Ni azma ya kuendelea ndiyo muhimu.’’
Hillary, ambaye pia ni mwanzilishi mwenza wa Green Earth Foundation, ana jina lenye maana ya kipekee. Siku alipoanza zoezi hilo, Kiptoo alitoa maelezo kuhusu jina lake, akisema: “Jina lake, Kibiwott, kwa lugha ya Kalenjin, linamaanisha aliyezaliwa wakati wa msimu wa mvua. Katika jamii nyingi za Kenya, msimu huo huashiria hatua za maamuzi na ni wakati wa kupanda.
“Kupitia jaribio hili la kuvunja rekodi, hapandi miti tu; anapanda ndani yetu ujasiri na azma ya kuvuka mipaka yetu katika urejeshaji wa misitu, na kutuchochea kufikiria upya kinachowezekana katika hatua za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.”
Eneo la Elgeyo-Marakwet katika Bonde la Ufa nchini Kenya, hivi karibuni lilikumbwa na maporomoko ya ardhi ambayo yalihusishwa kwa sehemu na mabadiliko ya tabianchi pamoja na mabadiliko ya matumizi ya ardhi, ikiwemo ukataji miti kwa miongo kadhaa. Janga la maporomoko ya hivi karibuni katika Bonde la Kerio lilitokea Novemba 1, 2025 na kusababisha vifo vya watu zaidi ya 31.
Akimpongeza Hillary kwa “kuonyesha ari na kujitolea kwa dhati katika uhifadhi wa misitu,” Mhifadhi Mkuu wa Misitu Alex Lemarkoko alisema: “Jaribio hili la rekodi sasa linasubiri kuthibitishwa na Guinness Wo rld Records.”
Kabla ya Hillary, aliyeshikilia rekodi ya dunia alikuwa Antoine Moses, aliyepanda miti 23,060 kwa siku moja huko La Crete, Alberta, Kanada, tarehe 17 Julai 2021.
Sasa Hillary anapanga kupanda miti zaidi katika kaunti zote 47 za Kenya. Mmoja wa watu waliokuwepo kwenye tukio hilo la upandaji miti alisema: “Kile alichofanya Hillary kinaweza kufanywa na kijana mwingine yeyote. Wengi wanaona uhifadhi kama suala la kupanda miti tu, lakini uhifadhi pia ni suala la kiuchumi.”
Picha ya bango: Hillary Kibiwott, kijana wa Kenya mwenye umri wa miaka 29 ambaye ameweka rekodi mpya ya dunia ya kupanda miti, akiwa kwenye gari lililozungukwa na watu wanaomuunga mkono. Picha na Uzalendo TV.