- Familia zinazoishi katika maeneo yasiyo salama, zisaidiwe ili zisiendelee kujiweka kwenye hatari.
- Mipango ya matumizi ya ardhi izingatie uhalisia wa mazingira na uimarishwe utekelezaji wa sheria zote.
- Kamati za majanga katika ngazi zote ziimarishwe ili ziweze kuitikia dharura kwa haraka kabla madhara hayajawa makubwa.
- Upandaji miti na uhifadhi wa maeneo oevu utasaidia kupunguza kasi ya maji ya mvua na kuzuia udongo kuteleza.
Aprili 22 ni siku ambayo mataifa 193 duniani yanaadhimisha ‘Earth Day’ kwa kufanya mambo mbalimbali, wengine wakipanda miti, kusafisha mazingira, kuondoa takataka za plastiki kwenye mifereji na shughuli nyingine zinazodhihirisha wajibu wa kila mmoja katika kulinda na kutunza mazingira.
Lakini katika kitongoji cha Wage, kijiji cha Dimilo, kata ya Kibungo Juu, mkoani Morogoro, zaidi ya kaya 15 zinaadhimisha siku hiyo bila kuwa na makazi baada ya kuzikimbia nyumba zao kufuatia maporomoko ya tope yaliyokumba eneo lao hivi karibuni.
Huko wilayani Rungwe, wanasherehekea siku hii huku wakiwa na majonzi mazito kufuatia kupoteza ndugu na jamaa zao zaidi ya watu 20 waliofariki katika maporomoko yaliyosababishwa na mafuriko yaliyotokea Machi 15, 2026.
Kutokea kwa maporomoko ni miongoni mwa majanga yaliyoelezwa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) katika taarifa yake kuhusu mwelekeo wa mvua za masika Machi-Mei, 2026.
Katika taarifa hiyo, Mkurugenzi Mkuu wa TMA, Dkt. Ladislaus Chang’a alisema maeneo yanayopata misimu miwili ya mvua kwa mwaka (kanda ya Ziwa Victoria, nyanda za juu Kaskazini-mashariki, Pwani ya kaskazini pamoja na maeneo yaliyopo kaskazini mwa mkoa wa Kigoma) katika kipindi cha miezi hiyo, vipindi vifupi vya mvua kubwa vingeweza kujitokeza na kusababisha mafuriko na maporomoko ya ardhi.
Alisema matukio hayo yangeweza kuleta uharibifu wa miundombinu na mazingira, milipuko ya magonjwa, pamoja na upotevu wa mali na maisha.
Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC ) nalo lilitoa tahadhari kuhusu hatari ya mvua kubwa na maporomoko ya ardhi ambayo yangeweza kusababisha uharibifu mkubwa.
Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Immaculate Semesi, akizungumza na vyombo vya habari, alisisitiza umuhimu wa kuchukua tahadhari mapema wakati matukio ya hali mbaya ya hewa yanayochochewa na mabadiliko ya tabianchi yakiendelea kuongezeka.
Wakiongea na Mongabay kwa nyakati tofauti, baadhi ya watalaam wa mazingira walisema kwa vile mabadiliko ya tabianchi yanaendelea kutokea na kuleta athari kubwa ni vema kukawa na mipango inayowajengea uwezo wananchi ili wafahamu namna ya kuchukua tahadhari.
Vifo vya Maporomoko: Tunajikwamua vipi?
Frankline Masika, anasema ni muhimu kuweka na kusimamia mipango ya matumizi ya ardhi inayozingatia uhalisia wa mazingira na kuimarisha utekelezaji wa sheria zote zinazolinda vyanzo vya maji na miteremko mikali.

Jambo la pili anasema ni vema wananchi wakahimizwa kukaa mbali na maeneo yasiyo salama. Anasema: “Ni vema watu wakahimizwa kukaa mbali na maeneo yenye historia ya mito au maziwa kusinyaa na kutanuka ili kuepuka madhara yanayotabirika”.
Aidha anasema kuwa kamati za majanga katika ngazi za wilaya na vijiji lazima ziimarishwe kwa kupewa rasilimali fedha, vifaa vya kisasa vya uokoaji, na mafunzo ya utayari ili ziweze kuitikia dharura kwa haraka kabla madhara hayajawa makubwa.
Vilevile, anashauri kuimarishwa kwa mifumo ya utoaji wa taarifa za tahadhari kwa kutumia teknolojia ya SMS, redio za jamii, na mitandao ya kijamii ikiwa ni hatua muhimu itakayohakikisha taarifa zinawafikia wananchi kwa lugha rahisi na kwa wakati.
Kwa upande wa maendeleo, Masika anasema ni vyema kuwekeza kwenye miundombinu yenye ustahimilivu kama barabara, madaraja, na mifereji mikubwa inayoweza kustahimili shinikizo la maji mengi kipindi yanapotokea mafuriko.
“Hatua hizi ziende sambamba na uhamasishaji wa mbinu za kilimo rafiki, kama matumizi ya matuta na mbegu zinazostahimili ukame, ili kuzuia mmomonyoko wa udongo na kuimarisha usalama wa chakula,” anasema.
Kuhusu urejeshaji wa mifumo ya ikolojia, anasema hilo linaweza kufanyika kupitia upandaji miti na uhifadhi wa maeneo oevu na kwamba hatua hizo zitasaidia kupunguza kasi ya maji ya mvua na kuzuia udongo kuteleza.
Hata hivyo alisema jitihada hizi zinahitaji ushirikiano wa karibu kati ya serikali za mitaa, asasi za kiraia, na wadau wa kimataifa ili kuhakikisha kuwa bajeti na sera za maendeleo zinajumuisha mikakati madhubuti ya kupunguza hatari za majanga.
Leonard Chakupewa Soza anasema ili kukabiliana na majanga hayo ni muhimu watu wakaelimishwa juu ya njia endelevu, nyepesi na rafiki za kujihami na athari za mabadiliko ya tabianchi.
Akitoa mifano ya nchi jirani za Burundi na Rwanda, anasema wananchi wameelimishwa namna ya kutumia njia rafiki ambazo kwa kiasi kikubwa zinawasaidia kujikinga na majanga.
“Hizo nchi kutokana na ardhi yao kuwa na milima mingi, huwa wana siku maalum kwa ajili ya shughuli za maendeleo na miongoni mwa mambo wanayoyafanya siku hiyo ni kukata mifereji inayokatiza maeneo ya vilima ili maji yasishuke moja kwa moja kwenye mabonde na kwenda kwenye nyumba zilizo mabondeni na badala yake yapite kwenye mifereji na kuingia kwenye korongo lililo karibu ambalo huyapeleka kwenye vyanzo vingine vya vikuu vya maji”.
Anasema hiyo husaidia kupunguza mmomonyoko unaoweza kutokea kwenye maeneo ya milima na kusababisha majanga makubwa kwa wale wanaoishi kwenye mabonde,” anasema.
Sambamba na hilo la elimu, yeye pia anashauri jitihada ziwekwe kuwahimiza wananchi wanaoishi katika maeneo korofi kama mabondeni, kwenye mikondo ya maji, kwenye miteremko mikali na kwingine ambako ni rahisi kuathiriwa na majanga kama mafuriko na maporomoko, wahamie sehemu salama.
“Kuna familia zinazoishi maeneo yasiyo salama, ni vema zikasaidiwa ili wasiendelee kujiweka kwenye hatari. Wengine hawana uwezo wa kupata maeneo mengine wala kujenga nyumba nyingine. Wananchi kama hao wagawiwe maeneo yaliyo salama na kusaidiwa kujenga nyumba za gharama nafuu,” anasema.
Vifo vya watu 89
Itakumbukwa kuwa, mnamo Desemba 3 mwaka 2023, takriban watu 89 walipoteza maisha baada ya kutokea kwa maporomoko ya udongo katika Mlima Hanang mkoani Manyara baada ya mvua kubwa kunyesha. Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Serikali ya Tanzania na kukaririwa na vyombo vya habari sababu iliyopelekea maporomoko hayo ni kumeguka kwa sehemu ya mlima huo ambao ulikuwa na miamba dhoofu iliyonyonya maji na kusababisha mporomoko na hivyo kutengeneza tope.
Kwa mujibu wa taarifa iliyochapishwa kwenye tovuti ya UNICEF, mafuriko na maporomoko ya ardhi yaliyotokea Afrika Mashariki mwezi Mei mwaka 2024 yaliathiri karibu watu milioni moja katika nchi za Burundi, Kenya, Somalia na Tanzania, kufuatia mvua kubwa zisizo za kawaida zilizochochewa na hali ya tabianchi ya El Niño ya 2023–24.
Maafa hayo licha ya kusababisha vifo vya watu, yalisababisha uharibifu wa nyumba, shule na miundombinu, pamoja na upotevu wa mazao na mifugo. Maelfu ya familia walilazimika kuhama makazi yao na kuishi katika makazi ya muda, huku walioko hatarini zaidi wakiwa ni wale wanaoishi karibu na mito na maeneo yasiyo na huduma bora za maji na usafi.
Kwa ujumla, hali hii inaonyesha jinsi mabadiliko ya tabianchi yanavyozidisha majanga na kusisitiza umuhimu wa hatua za muda mrefu za kuimarisha ustahimilivu wa jamii, kupunguza uzalishaji wa gesi chafu na kuongeza uwekezaji katika maandalizi na kukabiliana na majanga ya tabianchi, taarifa hiyo inasema.
Serikali ya Tanzania imekuwa ikichukua hatua kadhaa ikiwa ni pamoja na kuwasisitiza wananchi wanaoishi maeneo hatarishi kuhamia sehemu salama. Lakini pia watalaam mbalimbali wametoa ushauri wao na namna ya kupunguza athari hizo.
Mara kadhaa viongozi wa Serikali wamekuwa wakisisitiza jamii kutoka maeneo yenye mafuriko kuhamia maeneo salama na kutoa wito wa kuimarishwa kwa uwezo wa kitaifa wa kujiandaa na kukabiliana na maafa.
Hivi karibuni, TMA ilihimiza Idara ya Usimamizi wa Maafa, kwa kushirikiana na wadau mbalimbali nchini, kuendelea kuratibu na kutekeleza mipango ya kupunguza athari zinazoweza kujitokeza.
Aidha, Sekta ya Mazingira pamoja na Kamati za Usimamizi wa Maafa katika ngazi za mikoa, wilaya, kata/shehia, na kijiji/mtaa zinashauriwa kuchukua hatua stahiki, ikiwa ni pamoja na kutoa elimu kuhusu maafa kwa kuzingatia sera, sheria, taratibu na miongozo itakayosaidia katika kuzuia/kupunguza athari, kujiandaa, kukabiliana na kurejesha hali pindi maafa yatakapotokea
Hivi karibuni, NEMC iliwataka wananchi kuzingatia miongozo ya mazingira, kuepuka kujenga katika maeneo hatarishi ya mafuriko na maporomoko, pamoja na kufuatilia taarifa za hali ya hewa. Baraza hilo pia lilisisitiza umuhimu wa kutekeleza kikamilifu Sheria ya Usimamizi wa Mazingira ya mwaka 2004 na kuzingatia mipango sahihi ya matumizi ya ardhi ili kuzuia uharibifu wa mazingira.
Kama kauli mbiu ya mwaka 2026 ya Earth Day, “Nguvu Yetu, Sayari Yetu” Soza anasema wananchi na wadau wote, kila mmoja kwa nafasi yake ana wajibu wa kutumia uwezo wao kuchukua hatua stahiki kulinda dunia wanayoishi.
Picha ya bango: Watanzania wahimizwa kuwa waangalifu dhidi ya athari za mabadiliko ya tabianchi na kuhakikisha usalama wao kila mvua inaponyesha kupita kiasi, ili kujiepusha na maporomoko. Picha na Franklin Masika, Mongabay.