- Mwanamke mmoja katika Wajir aliishi na mtoto wa duma kwa zaidi ya miaka miwili, akimlea kama sehemu ya familia yake katika mazingira magumu ya ukame.
- Wataalamu wa wanyamapori wanaonya kuwa malezi ya binadamu kwa wanyama wa mwitu husababisha “imprinting,” hali inayoweza kuhatarisha maisha ya binadamu na kumfanya mnyama ashindwe kuishi porini.
- Mamlaka ya Kenya Wildlife Service (KWS) ilimwondoa duma huyo baada ya mazungumzo ya siku tano, ikisisitiza kuwa ni kinyume cha sheria kumiliki mnyama wa mwituni bila kibali.
- Kisa hiki kinaangazia mvutano kati ya huruma ya kijamii na sayansi ya uhifadhi, huku kikitoa wito wa kuelimisha jamii zinazoishi karibu na wanyamapori kuhusu hatua sahihi za kuchukua wanapokutana na wanyama hao.
WAJIR, Kenya – Katika maeneo kame ya kaskazini mwa Kenya, maisha hayapimwi kwa saa au dakika, bali kwa uvumilivu wa nafsi dhidi ya mazingira. Hapa, katika Kaunti ya Wajir, ardhi imepasuka kwa jua kali, na upepo wa vumbi hubeba harufu ya jasho la mifugo na matumaini ya mvua isiyotabirika.
Maisha ya jamii za wafugaji ni mzunguko usiokwisha wa kutafuta malisho na maji. Lakini ndani ya moyo wa jangwa hili, kumeibuka hadithi inayopinga mantiki ya asili – ya upendo uliopitiliza, hatari iliyojificha, na mipaka inayofifia kati ya binadamu na mnyama mwitu mwenye kasi kubwa.
Ni hadithi ya Bishara Abdirahman Omar, mama wa watoto tisa, ambaye kwa zaidi ya miaka miwili alifanya jambo ambalo wengi wangeliona kama hukumu ya kifo. Mama huyu aliishi na duma ndani ya nyumba kama sehemu ya familia yake.
Bishara anakumbuka siku hiyo kwa uwazi kabisa, kana kwamba ilitokea jana. Ilikuwa ni asubuhi yenye joto kali, na yeye alikuwa akitembea porini kutafuta kuni na kuangalia mifugo yake.
Katika kichaka kimoja cha miiba, alisikia sauti dhaifu; kilio kidogo kilichofanana na kile cha mtoto wa paka aliyeishiwa nguvu. Aliposogea, alimkuta mtoto wa duma, akiwa mdogo kiasi cha kutoshea kwenye viganja vyake, macho yake yakiwa bado na ukungu wa upofu wa utotoni.
“Alikuwa hana msaada kabisa. Nilimwangalia, nikatazama huku na huko nikitarajia kumuona mama yake, lakini hapakuwa na dalili yoyote. Alikuwa ameachwa peke yake kufa kwa njaa au kuliwa na fisi,” Bishara alisimulia, huku akitazama upeo wa macho.
Kwa Bishara, hakuona mnyama hatari, bali aliona kiumbe aliyehitaji maziwa na joto. Bila kufikiria mara mbili, alimbeba na kumpeleka nyumbani kwake, uamuzi ambao ungebadilisha maisha ya familia yake na kuvuta hisia za ulimwengu wa uhifadhi.
Mwezi Aprili 2026, Mongabay ilitembelea familia ya Bishara huko Wajir, na kumpata akiwa na mumewe Rashid Abdi Hussein Abdi. Walikuwa wamehamia eneo jipya lenye nyasi nyingi kufuatia mvua za msimu. Mifugo yao, ikiwemo mbuzi, ng’ombe na ngamia, ilikuwa imetapakaa karibu na makazi yao ya jadi. Jua kali lilikuwa linamulika ngozi ya Bishara, ishara ya maisha magumu ya ukame.

Rashid aliketi karibu, akifuatilia kwa makini simulizi ya mkewe. Hakunena mengi, lakini uwepo wake ulionyesha kuwa familia nzima iliishi na mnyama huyo na kushuhudia ukuaji wake.
Hapo awali, Rashid, mwenye umri wa miaka 46, alikuwa ameambia mwandishi wa BBC kwamba yeye na mkewe walijua kuwa duma huyo hangewanufaisha kwa njia yoyote ile kama mifugo ingefanya. “Lakini niliamua kwamba kwa kuwa watu wanaua wanyama hawa, labda sisi tunapaswa kuwafuga badala yake na kuwa tofauti.”
Alisema familia yake ilimtunza duma huyo kwa muda wa miaka miwili na miezi mitatu. “Mnyama huyo alikuwa msumbufu mwanzoni, lakini mwishowe alitulia na akawa kama mmoja wa watoto,” alisema.
Katika utamaduni wa jamii ya Wajir, kusaidia kiumbe aliye katika taabu ni kitendo cha utu (birrimai).
Mazingira ya boma na changamoto ya ukame
Boma la Bishara liko katika mazingira ya Manyatta za kitamaduni za Kisomali. Hizi ni vibanda vya mviringo vilivyojengwa kwa miti, nyasi, na vitambaa vilivyochakaa. Katika mwaka wa 2022 hadi 2024, kaskazini mwa Kenya ilikumbwa na moja ya ukame mbaya zaidi kuwahi kurekodiwa.
Vyanzo vya maji vilikauka, na mifugo ilianza kufa kwa wingi. Katika hali hii ya uhaba wa chakula, uamuzi wa Bishara wa kugawa maziwa kidogo ya mbuzi yaliyopatikana kwa ajili ya duma huyu waliyemwita Abdullahi, ulikuwa ni kitendo cha kujitolea kikubwa.
Kwa mujibu wa Bishara, vumbi jekundu la Wajir lilikuwa likitanda kila mahali, na wakati wa mchana, duma huyo alikuwa akijificha chini ya vivuli vya vibanda hivyo. Alikuwa akilala kando ya watoto wadogo wa Bishara, akivuta hewa ile ile yenye joto na vumbi.

Kwa familia hii, Abdullahi hakuwa tu mnyama, bali mshirika katika safari ya kuvumilia ukame huo mkali. Rangi ya ngozi yake ya madoa meusi na ya dhahabu ilijichanganya vizuri na rangi ya ardhi ya Wajir wakati wa machweo, na kumfanya awe karibu asionekane na wageni.
Maisha ya ndani ya boma
Kwa miezi kadhaa, familia ya Bishara ilimlisha Abdullahi maziwa ya mbuzi kwa kutumia chupa, na wakati mwingine uji, kama njia moja ya kumpa joto kama mzazi. Abdullahi hakuwa mgeni; alikuwa akicheza na watoto tisa wa Bishara. Katika boma hilo la kitamaduni la wafugaji, si jambo la ajabu kuona mbuzi na kondoo wakizunguka, lakini uwepo wa duma ulibadilisha anga.
“Alikuwa kama mwanangu wa kumi,” Bishara anasema kwa tabasamu la huzuni. “Alikuwa ananifuata kila mahali. Nilipokuwa nikipika, alikuwa anakaa kando yangu. Nilipokuwa nikilala, alikuwa akijiviringisha miguuni pangu. Watoto walimzoea kiasi kwamba walicheza naye michezo ya kukimbizana,” anasema.
Kwa macho ya kawaida, hii ilionekana kama muujiza wa amani. Abdullahi alikuwa na tabia za kipekee; hakuwahi kuwadhuru au kuwashambulia watoto. Cha kushangaza zaidi ni kuwa hakuwahi kushambulia mifugo. Kwa Bishara, hii ilikuwa ishara kwamba mnyama huyo alitambua ukarimu wao. Lakini ukweli ni kwamba, Abdullahi alikuwa akipoteza silika yake ya asili, ya kuwa mnyama wa mwituni.
Abdullahi na fisi usiku
Usiku mmoja, hali ya hewa ilikuwa na utulivu wa kutisha. Ghafla, vicheko vya fisi vilianza kusikika kwa mbali, vikikaribia boma la mifugo la Bishara. Kawaida, fisi ni tishio kubwa kwa kondoo na mbuzi wa jamii za wafugaji.
Wakati ambapo mbwa wa boma walikuwa wakibweka kwa hofu, Abdullahi alisimama imara mlangoni mwa boma, mwili wake ukiwa umekaza na macho yake yaking’aa kama makaa ya moto usiku. Hakunguruma, lakini alisimama hapo kushuhudia fisi hao wakikimbia na kutokomea gizani baada ya mbwa kubweka kwa muda.
Tukio hili liliimarisha imani ya familia kuwa Abdullahi alikuwa zawadi kutoka kwa asili. Familia hii haikutambua kuwa kitendo hicho pia kilikuwa kikimuweka Abdullahi hatarini zaidi kwa kumfanya awe mlinzi wa binadamu badala ya kuwa mwindaji wa porini.
Mtazamo wa kisayansi
Wakati Bishara akiona upendo na ulinzi, wataalamu wa wanyamapori walikuwa wakiona bomu lililoweza kulipuka wakati wowote. Geoffrey Chege, mwanasayansi wa wanyamapori kutoka shirika la WWF-Kenya, anaeleza kuwa malezi haya ya binadamu yanatengeneza hali inayoitwa imprinting kwa Kiingereza.

“Duma anapolelewa na binadamu, anaanza kujitambulisha kama binadamu au kuwaona binadamu kama jamii yake. Hii ni hatari sana. Silika yake ya asili imejengwa juu ya kuvizia na kushambulia.
“Ingawa anaonekana mpole, homoni zake na ukuaji wake wa kibaolojia unamaanisha kuwa ni mnyama wa kuua. Siku moja harufu ya damu au harakati ya ghafla ya mtoto ingeamsha silika hiyo, na matokeo yake yangekuwa maafa,” Chege aliiambia Mongabay.
Zaidi ya hayo, kuna suala la utegemezi: Kwa sababu Bishara alimlisha Abdullahi nyama, uji na maziwa, mnyama huyo hakujifunza kuwinda. Katika ulimwengu wa duma, mama hufundisha watoto wake jinsi ya kuvizia, kukamata shingo ya mawindo, na kujiokoa na simba au fisi. Abdullahi alikuwa duma asiyejua asili yake ya kimaumbile.
Kwa mujibu wa taarifa iliyochapishwa na KWS, mnyama huyo aliyetolewa katika makazi ya familia ya Bishara alithibitishwa kuwa ni duma, jambo linaloendana na ushahidi wa picha na maelezo rasmi ya operesheni hiyo.
Takwimu za uhifadhi
Kubaini kwa usahihi idadi ya kitaifa ya duma bado ni changamoto kubwa kutokana na msongamano wao mdogo, tabia ya kusafiri maeneo makubwa, uhaba wa rasilimali, na ukosefu wa mbinu sanifu za utafiti.
Hata hivyo, kwa mujibu wa takwimu ya Kitaifa ya Wanyamapori (National Wildlife Census) ya mwaka 2025, idadi ya duma nchini Kenya inakadiriwa kuwa 605. Linasema makadirio yaliyopo yametokana na mchanganyiko wa mbinu rasmi na zisizo rasmi za utafiti.
Jamal Abdi Rashid, msimamizi wa Shirika la Huduma za Wanyamapori Kenya (KWS), kanda ya Wajir, anasema kwa jumla, kupungua kwa idadi ya jamii ya paka wakubwa kumehusishwa na kupoteza makazi, mwingiliano na binadamu, na mabadiliko ya tabianchi.
Sheria kuhusu umiliki wa wanyamapori
Sheria ya Uhifadhi na Usimamizi wa Wanyamapori ya mwaka 2013, hasa vifungu vya 95, 89 na 99, inasisitiza kuwa ni kosa kumkamata, kumiliki au kufuga mnyama wa mwituni bila kibali rasmi na mamlaka husika. Ni kosa la jinai linaloweza kupelekea faini ya kuanzia $7,746 (KSh1 milioni) hadi $154,919 (KSh20 milioni), au hata kifungo cha maisha gerezani. Lakini kwa jamii za Wajir, sheria hizi mara nyingi huonekana kama vitu vya kigeni vinavyotoka Nairobi.
Jamal anasema kuwa kisa cha Bishara kilikuwa na changamoto ya kipekee. “Hatuwezi kumchukulia Bishara kama mhalifu wa kawaida. Alifanya hivi kwa huruma. Lakini lazima tuseme ukweli; alikuwa anahatarisha kijiji kizima. Duma anapokuwa, mahitaji yake ya nyama huongezeka. Angeweza kuanza kuua mifugo ya majirani, na hilo lingesababisha mgogoro kati ya binadamu na wanyamapori.”
Siku tano za mazungumzo na operesheni ya uokoaji
Taarifa zilienea kuhusu “mwanamke wa duma,” na hatimaye KWS wakalazimika kuchukua hatua mnamo Oktoba 2025. Hata hivyo, kumuondoa mnyama huyo haikuwa kazi rahisi; ilikuwa ni operesheni iliyohitaji diplomasia, heshima kwa utamaduni, na uelewa wa kisaikolojia.

Wakati maofisa wa KWS walipofika boma la Bishara, walikaribishwa na hali ya wasiwasi. Bishara na familia yake walikuwa tayari kumlinda Abdullahi kwa gharama yoyote ile. Kwao, kumchukua duma huyo ilikuwa sawa na kumteka nyara mtoto wa familia.
Hapo ndipo nafasi ya wazee wa jamii ilipokuwa muhimu. Sheikh Mukhtar, kiongozi wa kidini na kijamii, alishiriki katika mazungumzo hayo magumu. “Ilibidi tutumie busara. Tulimweleza Bishara kuwa Abdullahi alihitaji kuwa na duma wenzake. Tulimwambia kuwa ikiwa duma huyo angemdhuru mtu mbeleni, damu hiyo ingekuwa juu ya mikono yake,” Sheikh Mukhtar aliiambia Mongabay.
Ilichukua siku tano za mazungumzo chini ya kivuli cha miti ya acacia. Kila siku, Bishara alikuwa akilia, akimkumbatia Abdullahi, ambaye sasa alikuwa mkubwa na mwenye nguvu. Hatimaye Bishara alikubali kumuachilia mnyama huyo. Siku ya kuondoka, boma zima lilijaa huzuni. Abdullahi alipewa dawa ya usingizi, akawekwa kwenye ngome na kusafirishwa hadi Nairobi Safari Walk, kwa mujibu wa KWS.
Maisha mapya katika hifadhi
Abdullahi sasa anaishi katika Naserian Wildlife Conservancy. Hapa si pori la wazi kabisa, bali ni mazingira yaliyodhibitiwa ambapo wataalamu wanajaribu kumrudisha katika hali yake ya asili; mchakato unaojulikana kama rewilding.
Mchakato huu ni mgumu na wa gharama kubwa. Wataalamu wanapunguza mawasiliano ya binadamu na mnyama huyo wakitumia njia za kiufundi kumfanya aanze kuwinda mwenyewe.
“Ni kama kumfundisha mtu mzima lugha ambayo hajawahi kuisikia,” anasema mmoja wa walinzi wa hifadhi hiyo, ambaye hakutaka jina lake litajwe. “Abdullahi bado anatafuta binadamu kila anapoona gari, akiwa anategemea kupewa chakula. Itachukua miaka, na labda hatawahi kuweza kuishi porini peke yake bila msaada,” anaelezea.
Huu ndio ulikuwa upande wa pili wa huruma ya Bishara. Kwa kumuokoa mnyama huyo, alimfanya asiweze kuwa mnyama kamili tena.
Ongezeko la matukio na changamoto ya magonjwa
Jamal anathibitisha kuwa visa hivi vinaripotiwa takriban mara nne kwa mwaka katika vichaka vya Wajir. “Wiki chache kabla ya operesheni ya Abdullahi, tuliwaokoa watoto wengine wa chui, lakini walifariki kutokana na magonjwa na lishe isiyofaa waliyopewa na binadamu,” aliiambia Mongabay.
Jamal anasema: “Katika kipindi cha ukame wa mwaka kuanzia 2022 hadi 2024, kulirekodiwa mwingiliano mkubwa kati ya wanyamapori na binadamu katika maeneo ya makazi. Hali hii ilisababishwa na wanyama kulazimika kutafuta maji na chakula karibu na boma za wafugaji”.
Upendo usiofutika
Miezi kadhaa baadaye, kidonda cha kutengana bado ni kibichi moyoni mwa Bishara. Mongabay ilipomtembelea, bado kulikuwa na harufu ya Abdullahi kwenye baadhi ya matandiko yake ya zamani. “Watu wananiambia alikuwa mnyama hatari, lakini mimi niliona roho yake. Alikuwa akinifariji nikiwa na huzuni,” Bishara anasema huku akifuta machozi kwa ncha ya vazi lake.
“Sijuti kumchukua. Najua sheria inasema ni vibaya, lakini Mungu anajua nia yangu. Natamani tu ningeweza kumtembelea, nimuite jina lake ‘Abdullahi’, na nione kama bado ananikumbuka.”

Bishara anawakilisha kundi la watu wanaoishi pembezoni mwa hifadhi za taifa nchini Kenya, ambao huruma yao mara nyingi hukutana na ukuta wa sheria na sayansi.
Muktadha wa kikanda na uhifadhi wa Pan-Afrika
Kisa cha Bishara na Abdullahi kinagusia mjadala mpana zaidi katika Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) kuhusu jinsi ya kusimamia rasilimali za wanyamapori huku kukiwa na ongezeko la idadi ya watu.
Katika nchi kama Tanzania na Uganda, migogoro ya binadamu na wanyamapori imeongezeka kutokana na ukame na kupungua kwa maeneo ya asili, na pia ongezeko la idadi ya watu wanaoishi karibu nao. Sheikh Mukhtar anasema hadithi hii ya Wajir inatukumbusha kuwa bila sera madhubuti zinazoshirikisha jamii moja kwa moja, juhudi za uhifadhi zinaweza kuonekana kama ukandamizaji.
Uhifadhi unahitaji bajeti kubwa ambayo mara nyingi ni changamoto kwa mataifa ya EAC, na mengine barani Afrika, yanayopambana na madeni ya nje na dharura za ukame. Lakini hadithi hii pia inaonyesha uwezekano wa “uhifadhi wa kijamii,” ambapo wenyeji wanakuwa walinzi badala ya kuwa maadui wa wanyamapori.
Mafunzo kwa jamii na dunia
Jamal anasema kisa hiki ni somo kwa dunia kuhusu uhifadhi katika karne ya 21. “Kadiri makazi ya binadamu yanavyozidi kuingiliana na maeneo ya wanyamapori, visa kama hivi vitaongezeka. Kuna haja kubwa ya kuelimisha jamii za pembezoni kuhusu nini cha kufanya wanapopata wanyama walioachwa. Badala ya kuwachukua, wanapaswa kutoa taarifa kwa KWS mara moja,” Jamal anasema, na kuongezea: “Kwa jamii zinazoishi maeneo haya, si kitu cha ajabu kwamba mtawaona wanyama wa mwitu, lakini tunawahimiza wanapoingilia makazi yenu mpige ripoti kupitia wazee”.
Chege pia anatoa maoni: “Huruma ya binadamu ni kitu kizuri. Lakini inapogusa wanyama wakubwa, inaweza kuwa hatari. Tunapaswa kuheshimu “umbale” wa wanyamapori”.
Kwa mujibu wa Sheikh Mukhtar, operesheni ya kumuokoa Abdullahi “ilifanikiwa kwa sababu serikali ilishirikiana na wazee wa kijamii. Hii inaonyesha kuwa uhifadhi hauwezi kufanikiwa bila kuhusisha jamii”.
Je, ni upendo au ni dhambi?
Baada ya matembezi ya Mongabay nyumbani mwa Bishara, swali linabaki: Je, alikuwa akiokoa maisha ya duma huyo au bila kujua alikuwa anahatarisha maisha yake ya porini?
Kwa Bishara, jibu ni rahisi. “Nilimsaidia tu… alikuwa peke yake. Nimejifunza sasa, lakini sina majuto. Ningependa kumuona tena”.
Leo hii, duma Abdullahi anatazama nyasi ndefu za Naserian, akitafuta silika alizopoteza, huku kule Wajir, mwanamke mmoja akitazama mwezi na kumuombea kiumbe aliyemlea kama mwanawe. Safari ya kurudi porini ni ndefu, lakini kumbukumbu ya upendo huo itabaki milele katika mchanga wa kaskazini mwa Kenya.

Hitimisho la kitaalamu
“Kisa hiki kinaonyesha umuhimu wa kuimarisha elimu ya uhifadhi wa kijamii,” Chege aliiambia Mongabay.
Jamal, kwa upande wake, alisema: “Suluhisho la kudumu linategemea uelewa wa jamii kuwa wanyama wanapaswa kubaki katika mazingira yao ya asili. Kitendo cha Bishara kilitokana na huruma, lakini kisayansi, mwingiliano huu unahatarisha usalama wa raia na kudhoofisha juhudi za kulinda spishi zinazotoweka.”
Picha ya bango: Duma Abdullahi akiwa nyumbani kwa Bishara kabla ya kuchukuliwa na maafisa wa KWS. Picha kwa hisani ya KWS.