- Kwa kuruhusu wanyama kupita kwa uhuru, ushoroba umepunguza uvamiazi wa mashamba na hivyo kupunguza uhasama.
- Uwekezaji kwenye elimu umeleta matokeo chanya kitaaluma. Mwaka 2025, wanafunzi wa darasa la nne walifaulu wote kwa asilimia 100.
- Ongezeko la watu, shughuli za kilimo na wingi wa mifugo vinaathiri ushoroba na wanyama wanaoutumia.
- Elimu kwa wananchi na mashuleni itaongeza uelewa kuhusu umuhimu wa wanyamapori kwa serikali na kwa wananchi wenyewe.
Wakati miale ya jua asubuhi ikiangaza wilaya ya Babati kaskazini mwa Tanzania, watoto kutoka kijiji cha Sangaiwe wanapita katika njia zilizopo katikati ya misitu ya asili na kwingine mashambani. Ni umbali isiozidi nusu kilomita kuelekea shule ya Msingi Burunge. Katarina Claudi mwenye umri wa miaka 12, na rafiki yake Magdalena Gabriel ni miongoni mwa wanafunzi wa shule hiyo. Kutoka nyumbani kwao hadi hapo shuleni wanatumia dakika 20 tu.
Ukiwa katikati ya madarasa ya shule hiyo iliyopo kwenye mteremko wa mlima mdogo wenye mawe makubwa kwa madogo, utasikia sauti za watoto wakiimba na kukariri masomo yao zikiwa zimechanganyikana na sauti za ndege wa porini, na kutengeneza taswira ya kipekee ya maisha yanayoendelea pembezoni mwa moja kati ya mapito muhimu zaidi ya wanyamapori nchini Tanzania.
Ushoroba wa Kwakuchinja ni njia muhimu ya asili inayounganisha Hifadhi za Taifa za Tarangire na Ziwa Manyara. Wanyamapori kama tembo, nyumbu, pundamilia na twiga huutumia kuhama kwa uhuru kutoka sehemu moja kwenda nyingine kutafuta maji na malisho.
Manufaa ya ushoroba
Wilfred Mariani Makamu mwenyekiti wa hifadhi ya Burunge, anasema kuwepo kwa ushoroba kwa huo kumeleta manufaa makubwa si kwa uhifadhi tu, bali pia kwa jamii zinazozunguka hifadhi ya Burunge.
Anasema kutokana na kuwepo kwa ushoroba huo wananchi kwanza wananufaika na mapato yanayopatikana kupitia utalii ambayo kwa usimamizi mzuri wa Jumuiya ya Hifadhi ya Jamii ya Burunge, (Burunge WMA) hurudi moja kwa moja kwa wananchi kupitia njia mbalimbali ikiwa ni pamoja na miradi ya maendeleo, kielimu na kijamii.
Kwa mfano, kupitia ushoroba huo, shule mbili; sekondari ya Burunge na shule ya msingi Burunge, zimejengwa. Kadhalika, wananchi katika vijiji vya Vilima Vitatu na Sangaiwe wamenufaika kwa kujengewa ofisi.

Marian Mwaso, Mwenyekiti wa kijiji cha Sangaiwe, anasema kabla ya ujenzi wa shule hizo, watoto wa Sangaiwe na vijiji vingine Jirani walikuwa wakitembea umbali wa kilomita tano au zaidi kuelekea shule, lakini leo wanafika shuleni ndani ya dakika 20 tu kwa sababu shule zimejengwa karibu na makazi ya watu, ikiwa ni miongoni mwa manufaa ya ushoroba wa Kwakuchinja.
Katika Shule ya Msingi Burunge, uwekezaji huu kwenye miundombinu umeleta matokeo chanya kitaaluma, yanayojieleza yenyewe. “Darasa la nne (mwaka 2025) wanafunzi wetu wamefaulu wote kwa asilimia 100… Tulikuwa wa kwanza kikata,” anasema Mwalimu Mkuu Emanuel Mitaruni kwa furaha.
Julius John Gabriel (40), mzazi anayeishi katika Kijiji cha Sangaiwe, anakumbuka kwa uchungu historia ya nyuma anapowatazama watoto wake wakitembea kwa usalama kuelekea madarasani. “Kipindi nikiwa nasoma tulikuwa tunatembea kama kilomita tano hivi kwenda ilipokuwa shule … sasahivi umbali ni nusu kilomita tu,” anasema.
Anaongeza kuwa mabadiliko haya yametokana moja kwa moja na kuwepo kwa ushoroba huo pamoja na usimamizi mzuri wa Burunge WMA. ambapo fedha zinazokusanywa kupitia utalii zimechangia ujenzi wa shule za Burunge.
Migogoro imepungua
Sambamba, huduma za kijamii, ushoroba huo umesaidia kupunguza migogoro kati ya hifadhi na wana jamii. Kwa kuruhusu wanyama kuwa na njia zao rasmi za kupita, uwezekano wa kuvamia mashamba au makazi ya watu umepungua na hivyo kupunguza pia uhasama.
Roman Alphonce, mfugaji na mjumbe wa kamati ya mifugo kijiji cha Vilima Vitatu anasema, migogoro haijapungua kwa sababu tu ushoroba upo, bali kutokana na usimamizi mzuri wa Burunge WMA, ambayo ni hifadhi ya jamii inayoundwa na vijiji 10 vinavyozunguka eneo la Kwakuchinja na wanajamii kuona manufaa ya uhifadhi.
Awali eneo linalozunguka ushoroba wa Kwakuchinja lilikuwa na migogoro kati ya binadamu na wanyamapori. Ongezeko la idadi ya watu na upanuzi wa shughuli za kibinadamu, hasa kilimo, makazi na ufugaji vilisababisha mwingiliano kati ya wanyamapori na wakazi wa maeneo jirani.
Wanyama kama tembo na pundamilia walikuwa wakivamia na kuharibu mazao ya wakulima, huku fisi na wanyama wengine wakali wakishambulia mifugo ya wafugaji. Hali hii ilileta uhasama. Hata hivyo, kwa sasa migogoro hiyo imepungua na wanyama na binadamu wanaishi kwa amani.
Mwalimu Mkuu wa shule ya msingi Burunge, Emanuel Mitaruni, anathibitisha uhalisia huu mpya wa kiikolojia ambao umekuwa sehemu ya ratiba yao ya kila siku. Anasema, “Tumeanza kuzoea, saa 1:30 usiku unatembea unakutana uso kwa uso na tembo na mnapishana,” anaeleza Mwalimu Emanuel akionyesha jinsi mipaka kati ya maisha ya binadamu na mazingira asilia inavyoingiliana kwa amani.

Mgao wa mapato
Burunge WMA imekuwa mfano hai wa jinsi rasilimali za wanyamapori zinavyoweza kuleta faida za moja kwa moja kwa wananchi, huku ikichochea maendeleo endelevu. Mfumo wake wa ugawaji wa mapato umefanikiwa kuleta usawa na kuimarisha miradi ya jamii katika vijiji vinavyozunguka hifadhi.
Emmanuel Duxo, Kaimu Katibu wa Jumuiya ya Uhifadhi wa Wanyamapori Burunge (JUHIBU), anafafanua jinsi mfumo huo unavyofanya kazi kisheria. Anasema, “Mgawanyo wa mapato kwa jumuiya na vijiji vinavyounda jumuiya ni asilimia hamsini kwa hamsini. Hii inamaanisha kuwa asilimia 65 ya mapato yanayokusanywa kutokana na utalii wa picha na uwindaji wa kitalii hupelekwa kwenye Jumuiya ya Burunge. Kati ya fedha hizo, nusu hubaki ndani ya taasisi kwa ajili ya uendeshaji, doria na ulinzi, huku nusu nyingine ikigawanywa sawa kwa vijiji kumi wanachama ili kufadhili miradi ya maendeleo”.
Mwenyekiti wa Kijiji cha Sangaiwe Marian Mwaso anasema awali kabla ya uwepo wa Burunge WMA, wananchi walilazimika kuchangia fedha kwa kila jengo la huduma za kijamii lililokuwa likijengwa. Anasema: “Kila ujenzi ukikaribia, mnaambiwa kaya yenu inatakiwa itoe TSh20,000 ($7.7) … ila kwa sasa hicho kitu hakipo tena. Jukumu letu sisi wanakijiji ni kutenga eneo tu.”
Fedha hizi zimeleta mabadiliko makubwa na yanayoonekana wazi. Kwa mujibu wa Afisa Habari wa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) Beatus Maganja, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2022/23 pekee, Burunge WMA ilipokea zaidi ya TSh2 bilioni ($767,763) kutokana na mapato ya utalii wa picha na uwindaji wa kitalii. Fedha hizo ziligawanywa kwa vijiji vyote kumi vinavyounda WMA ya Burunge.
Mwananchi mmoja kutoka kijiji cha Sangaiwe alisema awali walikuwa hawapati chochote kutokana namaliasili na kwamba kipato chao kilikuwa kinatokana na uuzaji wa mawe na pombe za kienyeji.
Changamoto
Revocatus Meney, Afisa mtafiti kutoka Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori Tanzania (TAWIRI-Kanda ya Kaskazini) na mratibu wa mradi wa ufuatiliaji wa tembo, mfumo ikolojia wa Tarangire na Manyara, anasema ushoroba wa Kwakuchinja umekuwa ukipungua siku hadi siku.
Anasema katika miaka ya 1970, ushoroba huo ulikuwa na ukubwa wa takriban kilomita za mraba 600, ukitoa nafasi ya kutosha kwa uhamaji wa wanyama pori usio na kikwazo chochote. Leo, anasema, shinikizo kutokana na ongezeko la watu, shughuli za kilimo, makazi mapya, na wingi wa mifugo vimeubinya ushoroba huu kwa kiasi kikubwa.
Meney, ambaye amekuwa akifuatilia kwa ukaribu mabadiliko haya ya kiikolojia, anasema kutokana na ongezeko la watu, ushoroba umemegwa na hivyo kupungua na kubakia kilomita za mraba 274.45.
Anasema matokeo halisi ya hali hiyo ni pamoja na kuvurugwa kwa hali ya asili iliyokuwepo. “Hii sehemu ya upande wa juu kutoka Makuyuni (Wilaya ya Monduli), ambayo imekuwa kwenye hatari kwa sababu binadamu wamefungua shughuli pale, hususan za makazi na shughuli za kilimo,” anasema Meney.

Licha ya kubinywa huku kwa sehemu kubwa ya ushoroba wa Kwakuchinja, wanyama bado wanapambana kutumia njia iliyobaki kupita. Ruth Philemon, Afisa Mhifadhi Daraja la Kwanza kutoka Taasisi ya Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA-Kanda ya Kaskazini), anasisitiza kuwa mapito haya bado ni hai na “ukweli kwamba bado wanyama wanapita kutoka eneo moja kwenda eneo lingine kwa ajili ya kutafuta mahitaji yao ya kila siku ni ushahidi tosha wa uhai huo.”
Katikati ya ushoroba huu kunapita barabara ya lami inayounganisha Arusha na Babati, barabara ambayo licha ya kuwa mhimili muhimu wa kiuchumi kwa taifa na kwa wasafiri, imekuwa ni hatari kwa wanyamapori wanaojaribu kuvuka kwenda upande mwingine.
Kelele za magari na mwanga mkali nyakati za usiku vimewalazimu wanyama kubadili tabia zao za asili, jambo linalopelekea ajali zinazogharimu maisha yao.
“Ili kukwepa harakakti za binadamu wakati wa mchana, wanyama kama pundamilia, nyumbu, impala, na hata ndege wakubwa kama mbuni wanaanza kupita kwenye lile eneo kuanzia majira ya saa tatu usiku mpaka saa kumi na moja alfajiri,” anaeleza Meney.
Changamoto nyingine inayoukabili ushoroba wa Kwakuchinja ni ongezeko la idadi ya mifugo. Meyer anasema ongezeko hili huenda likaharibu uhifadhi wa ushoroba iwapo hakutakuwa na usimamizi mzuri wa mifugo na elimu kwa jamii inayozunguka eneo hilo.
“Ikiwa mapito haya yataachwa yazibwe kabisa, madhara yatakuwa zaidi ya wanyama kukosa maji. Itakuwa ni janga la kinasaba (genetic isolation) ambapo wanyama watajifungia kwenye visiwa vya kiikolojia. Hali hii inaweza kusababishia vifo kwa vizazi vyao vya asili. Kujifungia pia husababisha wanyama wa familia moja kujamiiana,” anasema Meyer.
Anasema mustakabali wa ushoroba wa Kwakuchinja, na nyingine nchini Tanzania, unategemea sana utashi wa kisera na nia ya dhati ya kushirikisha jamii.
Mikakati ya kitaifa
Ruth Philemon, Afisa Mhifadhi Daraja la Kwanza kutoka TAWA-Kanda ya Kaskazini, anasema Kwakuchinja ni mfano tu wa mapambano mapana zaidi yanayoendelea nchini kote kurejesha ushoroba 20 za wanyamapori zilizotambuliwa kama kipaumbele cha kitaifa.

Kulingana na Ruth, Serikali, ikishirikiana na taasisi mbalimbali, inachukua hatua madhubuti kuhakikisha ushoroba za wanyamapori zinalindwa na kurejeshwa katika asili yake ili wanyama waendelee kuzitumia kama zamani.
Licha ya mipango ya kurejesha maeneo haya, TAWA inawekeza nguvu kubwa katika kuelimisha jamii na kuimarisha ulinzi.
Ruth anabainisha kuwa wanatoa elimu kwa wananchi na mashuleni ili waelewe umuhimu wa wanyamapori, kwani kuwepo kwao kunasaidia kupata wawekezaji na hatimaye kuingiza mapato kwa serikali na kwa wananchi wenyewe.
Alisema ili kudhibiti uharibifu unaotokana na shughuli za kibinadamu kama vile ukataji miti na uingizaji wa mifugo, mamlaka inachukua hatua kali. Miongoni mwa hatua hiyo ni kufanya doria kuzuia uharibifu wa mazingira na kuwatia mbaroni wanaokiuka taratibu na sheria za zilizopo.
Ushoroba nyingine
Licha ya Kwakuchinja, ushoroba katika maeneo mengine katika nchi nyingine ikiwemo nchi jirani ya Kenya, zimekuwa na manufaa makubwa kwa uhifadhi na pia kwa jamii zinazozunguka hifadhi. Kwa mfano Amboseli Wildlife Corridors, Kenya kwa kuruhusu wanyamapori kama tembo kusafiri kati ya maeneo mbalimbali wakitafuta maji na malisho, husaidia kudumisha bioanuwai, kuzuia kutengwa kwa wanyama (genetic isolation), na kuimarisha mifumo ya ikolojia kwa kusambaza mbegu na virutubisho kwenye udongo.
Aidha, ushoroba huo hunuifaisha jamii kwa njia mbalimbali, ikiwa ni pamoja na kuwapa fursa ya kushiriki katika shughuli za uhifadhi, kunufaika na sehemu ya mapato yatokanayo na utalii pamoja na kupata huduma za kijamii kupitia miradi ya maendeleo na kijamii kama elimu na ajira. Ushirikishwaji huo pia huchangia kupunguza migogoro kati ya binadamu na wanyamapori, kwa kuwa jamii hupata motisha ya kulinda mazingira badala ya kuyaharibu.
Ushoroba mwingine ambao una manufaa kwa wananchi na uhifadhi ni Masai Mara, Kenya ambao kwa kurahisisha uhamaji wa wanyama katika maeneo mbalimbali umesaidia kudumisha uwiano wa ikolojia na kulinda bioanuwai. Aidha kwa kutoa njia maalum za kupita wanyama, ushoroba huo umesaidia kupunguza migogoro kati ya binadamu na wanyamapori.
Kwa upande wa jamii, ushoroba huo huwanufaisha wananchi kiuchumi. ambapo kupitia shughuli za utalii, wananchi hupata ajira kama waongoza watalii, wahudumu wa hoteli na walinzi wa hifadhi, hali inayochangia kuongeza kipato chao. Ushoroba huo pia umetoa fursa kwa wananchi kufanya biashara ndogondogo kama uuzaji wa bidhaa za asili na kazi za mikono.
Picha ya Bango: Tembo kwenye ushoroba wa Kwakuchinja, upande wa Ziwa Manyara. Picha na Isack Dikson, Mongabay.