- Asilimia ya ada zinazolipwa na watalii huelekezwa moja kwa moja kwenye uhifadhi, ikiwemo doria za kuzuia uvuvi haramu.
- Mtazamo kuhusu usalama ni moja ya vigezo muhimu vinavyoamua iwapo mtalii atachagua eneo fulani kutembelea.
- Kinapotokea kifo chenye utata cha mtalii, ni hatari kubwa kuwa na pengo kwenye mawasiliano.
Mnamo Aprili 09, Ashley Robinson, mwenye umri wa miaka 31, Mmarekani aliyekuwa kwenye kisiwa cha Unguja na mchumba wake kwa ajili ya mapumziko, alifariki hospitalini alipokimbizwa baada ya kukutwa akiwa mahututi katika villa aliyokuwa anaishi. Chanzo cha kifo hicho bado kimegubikwa na utata. Tukio hilo limewagusa watu mbalimbali kwa namna tofauti. Kwa familia na rafiki zake, kifo hicho kimeleta majonzi makubwa.
Kifo hicho pia kimekuwa pigo kwa wafuasi wake mitandaoni, kwa sababu Ashley alikuwa ni mtu maarufu kwenye mitandao ya kijamii, aliyetumiwa na taasisi mbalimbali kama influencer kutokana na nguvu ya ushawishi aliyokuwa nayo. Kwa wadau wa sekta ya utalii na uhifadhi wa mazingira, kifo cha mtalii kinaibua maswali mazito kuhusu mustakabali wa sekta hizo.
Baada ya kutokea kwa kifo hicho, Zuberi Chembela, ambaye ni Naibu Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai katika jeshi la polisi Zanzibar, alikaririwa na vyombo vya habari akisema wanamshikilia mchumba wa marehemu Ashley Joseph Isaac McCannon, na kwamba wamechukua pasi yake ya kusafiria, wakati uchunguzi ukiendelea.
Kwa mujibu wa Chembela, tayari familia ya Ashley imeteua taasisi maarufu ya uchunguzi wa vifo vya ghafla na vyenye utata, ili kutafiti chanzo cha kifo hicho kwa kushirikiana na serikali ya Zanzibar, kwa lengo la kubaini kama alijiua au aliuawa.
Kifo cha Ashley kinahusiana vipi na uhifadhi?
Hubert Kilangali, mmoja wa watafiti wa utalii Zanzibar, anasema kuwa kwa mujibu wa utaratibu uliowekwa na Biodiversity Finance Initiative (BIOFIN), asilimia 45 ya kila ada inayolipwa na mtalii kule Zanzibar inakwenda katika kuimarisha na kulinda uhifadhi.
BIOFIN ni mpango wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) uliozinduliwa 2012 kwa lengo la kuzisaidia nchi kuchambua matumizi ya fedha za bayoanuai na kubuni njia mpya za kuzipata na kuzisimamia.
Ripoti ya BIOFIN iliyochapishwa Septemba mwaka 2025 imeonyesha jinsi ilivyotekeleza majukumu yake ya kuisaidia Zanzibar kupata mapato zaidi kutokana na utalii na jinsi asilimia 45 ya mapato hayo yanayotokana na ada zinazolipwa na watalii yanavyopaswa kutumiwa kwenye uhifadhi.
Ripoti hiyo imeelekeza kuwa kwa kila ada inayolipwa na mtalii, asilimia 45 ielekezwe moja kwa moja kwenye juhudi za uhifadhi ikiwemo doria za kuzuia uvuvi haramu na upandaji wa matumbawe. Asilimia 30 hurudishwa kwa jamii na uvuvi endelevu, na asilimia 25 huenda katika hazina kuu ya taifa.
Kilangali anasema: “Kutokana na kiasi cha mchango kinachotolewa na kila mtalii katika kuchangia uhifadhi, mtalii anapofuta safari, karibu nusu ya fedha ambazo zingetumika kwenye doria dhidi ya wavuvi haramu pia hupungua”.
Anasema kuwa watalii wakipungua kwa asilimia 10 pekee, Hifadhi ya Mnemba inapoteza uwezo wa kufadhili boti za doria kwa takribani siku 40 kwa mwaka, mwanya ambao unaweza kutumiwa na wavuvi haramu.
Kifo hicho kuathiri utalii kwa muda, ni wazi na pia kitaathiri pato la Zanzibar, ambalo kwa kiasi kikubwa hutegemea utalii. “Kifo tata cha mtalii ni lazima kitakuwa na matokeo hasi ya muda mfupi au mrefu kama jambo hilo halitashughulikiwa vyema,” anasema Kilangali.
Kwa mujibu wa jarida la Tanzania Affairs, toleo la 142 lililochapishwa Oktoba 2025, utalii ndio injini ya mapato ya Zanzibar na fedha. Utalii unachangia karibu asilimia 30 ya uchumi wa Zanzibar.
Kifo tata cha mtalii huibua maswali kuhusu suala la usalama. Kuhusu hilo, Kilangali anafafanua kuwa mtazamo kuhusu usalama ni moja ya vigezo muhimu vinavyoamua iwapo mtalii atachagua eneo fulani kutembelea au kukaa.
Anasema hofu haishii kwa watalii wanaokusudia kutembelea visiwani humo tu, bali hata kwa wenye mahoteli. Kilangali alisema kwa uzoefu wake, baada ya matukio ya vifo vyenye utata, mahoteli mengi hushuhudia uhifadhi wa nafasi (bookings) zikipungua kwa muda.
Waendeshaji watatu wa hoteli zilizoko Nungwi na Mnemba waliiambia Mongabay kwamba walipokea maombi ya wateja kadhaa kughairi uhifadhi wa nafasi walizokuwa wamefanya ndani ya masaa 48 tu, baada ya taarifa ya kifo chenye utata cha Ashley kusambaa mnamo Aprili 09.
“Wateja wamekuwa wakiuliza: Je, tutakuwa salama? Polisi wana uwezo?” amesema meneja mmoja wa hoteli bila kutaka kutajwa jina, kwa madai kuwa wamiliki wa hoteli wamewakataza maofisa wao kuongea na waandishi wa habari kuhusu suala la kifo hicho.
Nini kifanyike kinapotokea kifo chenye utata
Kilangali, amesema kila kinapotokea kifo chenye utata cha mtalii wa kigeni, ni hatari kubwa kunapokuwa na “pengo la mawasiliano”.
Anasema kuchelewa kutoa taarifa rasmi na za kuaminika kunazusha nadharia za kuwepo kwa njama, jambo linaloharibu sifa zaidi ya tukio lenyewe.
Mtafiti huyu wa utalii ameshauri kuwa pale mtalii anapofariki katika mazingira yasiyo ya kawaida, nchi mwenyeji, balozi husika, na chombo huru cha kimataifa kama Interpol wafanye tathmini ya pamoja ndani ya saa 72.
“Lengo ni ripoti ya haraka na ya kuaminika kimataifa ili kulinda mnyororo wa thamani, ambayo ni mtalii → ada → doria → miamba hai → Watalii Zaidi,” anasema.
Kuhusu ushirikiano katika uchunguzi, Mwanahamisi Katundu, mkazi wa Chakechake Pemba, ameshauri timu ya pamoja ya wataalamu wa ndani na nje kwa ajili ya uchunguzi wa kitaalamu pale tukio tata linalohusu raia wa kigeni linapotokea, ili ripoti iwe ya kuaminika na sifa ibakie salama.
Na kama ripoti ya BIOFIN inavyoonyesha, uaminifu huo ndio unalipa mishahara ya walinzi wa bahari na kununua miche ya matumbawe.
Kifo cha mtalii mmoja ni msiba wa kibinadamu kwanza, na unaleta maumivu makali kwa familia na marafiki.
Uchunguzi, ushirikiano ndiyo njia pekee ya kuhakikisha Bahari ya Hindi, Mnemba, Jozani, na Stone Town vinaendelea kupokea wageni – na walinzi, kwa mujibu wa Kilangali.
Picha ya Bango: Ashley Robinson, Mmarekani aliyefariki Aprili 9 mwaka huu wa 2026 akiwa kwenye mapumziko kwenye kisiwa cha Unguja yeye na mchumba wake.