- Uchache wa maafisa wa mazingira kuanzia ngazi ya mtaa hukwamisha mapambano dhidi ya uchimbaji holela wa mawe.
- Sheria zipo, lakini kuna udhaifu mkubwa kwenye usimamizi na utekelezaji wake.
- Mtazamo wa watu juu ya kutumia rasilimali zilizo karibu nao kujitafutia riziki umekuwa mwiba.
- Elimu ya mazingira kwa wachimbaji na jamii, uwekaji wa maeneo rasmi ya uchimbaji, na matumizi ya teknolojia rafiki vipewe kipaumbele.
Hili ni toleo la pili la mfululizo wa makala kuhusu uchimbaji holela wa mawe jijini Mwanza. Soma toleo la kwanza hapa.
Licha ya kuwepo kwa Sera ya Taifa ya Mazingira ya mwaka 2021, Sheria ya Usimamizi wa Mazingira ya mwaka 2004 pamoja na mikakati mbalimbali ya usimamizi wa mazingira, ikiwemo Mpango Kabambe wa Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (2022-2032), bado uchimbaji holela wa mawe umeendelea kuwa jinamizi linalowaumiza wakazi jijini Mwanza.
Akizungumzia sababu za hali hiyo kuendelea, Laurent Kitogo, Afisa wa Mazingira kutoka Environmental Management and Economic Development Organization (EMEDO), anataja udhaifu katika usimamizi pamoja na utekelezaji wa sheria kuwa kikwazo kikubwa.
“Sheria ni eneo moja na usimamizi wake ni jambo jingine. Tunazo mamlaka kuanzia ngazi za mitaa, vijiji na maeneo yote ambayo watu wanaishi. Sheria imeelekeza kabisa kwamba kutakuwa na maafisa wa mazingira kuanzia ngazi ya mtaa, lakini ukiangalia kwa uhalisia ulivyo, utaona maafisa wa mazingira wanaanzia ngazi ya halmashauri. Huwezi kumkuta afisa wa mazingira katika ngazi ya kata,” anasema.
David Joseph, Mkuu wa Idara ya Maliasili na Mazingira jijini Mwanza, anasema kuwa katika Halmashauri ya Jiji la Mwanza hakuna eneo lililotengwa kwa ajili ya uchimbaji wa mawe, na kwamba wanaochimba, baadhi wanakuwa wanasawazisha viwanja vyao kutokana na kuwa na asili ya miamba, au ni wavamizi ambao wameona hiyo kama fursa ya ujasiriamali.
“Watu wanachimba mawe katika miktadha kuu miwili. Moja, asili ya Mwanza ni milima, na sehemu nyingi zina mawe. Hata kama ni tambarare, utakuta kuna mawe…kwa hiyo watu wengine wanachimba yale mawe ili kusawazisha viwanja vyao…hayo mawe yakiwa mengi, wanayatumia kujenga wenyewe na mengine kuyauza. Pili, kuna wavamizi ambao wanaona sehemu kama hizo ni fursa za ujasiriamali. Wanatumia rasilimali zilizopo kwenye maeneo yao kinyume na utaratibu,” anasema.
Anasisitiza kuwa Halmashauri haina eneo rasmi ambalo limepimwa kwa ajili ya shughuli hiyo.

Kwa mujibu wa David, miongoni mwa jitihada za kupambana na biashara hiyo imekuwa kuwakamata wale waliovamia na kujihusisha na shughuli ya uchimbaji wa mawe. “Hao (wachimbaji mawe kiholela) ni wavamizi. Tunawakamata, kuwashtaki na kuwatoza faini kuanzia $1,151 (TSh3 milioni) mpaka $19,185 (TSh50 milioni) kwa kosa moja,” anasema.
Licha ya jitihada hizo, mtazamo wa watu juu ya kutumia rasilimali zilizo karibu nao kujitafutia riziki umekuwa mwiba na kuendelea kuchochea biashara hiyo.
Msafiri Heneliko, mchimbaji wa mawe jijini Mwanza, anasema kazi hiyo ya kupasua mawe imegeuka kuwa ajira kwa vijana wengi. “Unaposema huu ni uharibifu, una maana tusifanye kazi kama hizi? Sawa, kwa upande wako tunaharibu, lakini kwetu sisi, hiyo ni ajira,” anahoji Msafiri.
Wananchi wanahofia kutoa taarifa
Changamoto nyingine katika kukabiliana na uchimbaji holela wa mawe ni kwamba wananchi, ambao ndiyo waathirika wakubwa wa kadhia hii, hawajitokezi kuripoti wala kutoa malalamiko kwa mamlaka husika.
Kwa hiyo, licha ya Sheria ya Usimamizi wa Mazingira ya mwaka 2004 kueleza bayana wajibu wa kila raia, wananchi wengi hawajatimiza wajibu huo. Baadhi wanadai kuwa hawaripoti matukio hayo kutokana na hofu ya kuingia kwenye migogoro au uhasama na wenzao.
Rahma Harris, ambaye nyumba yake imepakana na eneo la uchimbaji, anaeleza kuwa licha ya nyumba yake kupata nyufa na kuwa hatarini kutokana na mmomonyoko wa udongo, bado hana ujasiri wa kutoa taarifa. “Sasa utamwambia nini mtu ambaye anachimba eneo lake? Sitaki kuwaongelea hawa watu. Naogopa kujiingiza kwenye uhasama,” anasema.
Hali hiyo inadhihirika pia kupitia maelezo ya Winifrida Buganda, mkazi wa Nyakagwe A, anayeeleza namna viongozi wa mitaa wanavyokwama kusimamia utekelezaji wa sheria hizo. “Serikali za mitaa au wenyeviti, sawa wanasimamia, lakini saa nyingine hata wao wanaogopa,” anaeleza Buganda, katika mahojiano na Mongabay.
Kuhusu udhibiti wa miradi, ukiwemo wa uchimbaji mawe, kifungu cha 81 cha Sheria ya Usimamizi wa Mazingira ya mwaka 2004, kimeweka sharti la lazima la kufanya Tathmini ya Athari kwa Mazingira (TAM) kabla ya kuanza kwa mradi au shughuli yoyote yenye uwezekano wa kuathiri mazingira.
Kuhusu hili, Mkuu wa Idara ya Maliasili na Mazingira David Joseph anasema: “Tathmini ya athari kwa mazingira haifanywi tu kila eneo; ina taratibu zake. Si kila unapochimba ufanye tathmini. Sheria haipo hivyo. Kwa mfano, kusawazisha viwanja haihitaji tathmini kwa sababu zoezi hilo lina vigezo vyake. Kama anajenga labda ghorofa, au eneo la kihistoria, au la hifadhi, au mtu anajenga hoteli au karibu na ziwa, hapo ni lazima tathmini ya athari kwa mazingira na jamii ifanywe”.
Licha ya matakwa hayo ya kisheria, bado uchimbaji wa mawe umeendelea kufanyika katika maeneo mbalimbali jijini Mwanza.

Katika kufuatilia suala hili, Mongabay ilifika katika ofisi ya Mtendaji wa Kata ya Buhongwa, moja ya maeneo ambayo shughuli za uchimbaji wa mawe zimekithiri. Hata hivyo, juhudi za kupata maelezo au ufafanuzi kutoka ofisi hiyo hazikufanikiwa, kwani viongozi hawakuwa tayari kutoa ushirikiano wala kuzungumzia kwa kina hali halisi ya utekelezaji wa sheria katika eneo hilo.
Tathmini ya athari kwa mazingira
Mitazamo inayokinzana kuhusu suala la tathmini ya athari kwa mazingira, ni kikwazo kingine. Wakati suala la kufanyika kwa tathmini ya athari kwa mazingira, ni takwa la kisheria kwa mujibu wa kifungu cha 81 cha Sheria ya Usimamizi wa Mazingira ya mwaka 2004, likilenga kuangalia madhara yanayoweza kusababishwa na shughuli husika kwenye mazingira, Mkuu wa Idara ya Maliasili na Mazingira jijini Mwanza anasema tathmini haifanyiki kila eneo, na kwamba ina taratibu zake.
Hata hivyo, Juvenary Matagili ambaye ni mtaalam wa mazingira anasema kutofanya tathmini hupelekea kukosekana kwa mipango sahihi ya mazingira. Anasema: “Kukosekana kwa TAM kunamaanisha hakuna tathmini ya hatari, hakuna mipango ya kupunguza athari, na hakuna ufuatiliaji. Hii husababisha shughuli kufanyika kiholela bila kuzingatia kanuni za uhifadhi wa mazingira, na kuongeza kasi ya uharibifu wa ardhi, maji na bioanuai”.
Changamoto nyingine inazotajwa kukwamisha jitihada zao ni idadi ndogo ya maafisa pamoja na kutokuwa na gari za ukaguzi (patrol).
Eradius Erasto, Mhandisi Mazingira kutoka Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) Kanda ya Victoria-Mashariki, anasema katika ngazi za chini, yaani serikali za mitaa kuna kamati za mazingira, lakini hazina taaluma ya kutosha kwenye masuala hayo, hivyo kutoa mwanya kwa uchimbaji holela wa mawe kuendelea.
“Kamati za mazingira zinatakiwa kubaini mapungufu yote kuhusu mambo ya mazingira, lakini wanashindwa kufanya hivyo kutokana na kukosekana kwa uwezeshwaji wa kitaaluma. Zinaweza zikawa kamati lakini ufahamu wao wa masuala ya mazingira ukawa chini,” anasema Mhandisi Eradius, akizungumza na Mongabay.
Ili kuziba pengo hilo, Eradius anasema kuwa wamekuwa wakitoa elimu kwa kamati hizi ili ziweze kutekeleza majukumu yao ipasavyo katika maeneo yao.
Nini kifanyike kudhibiti uchimbaji holela wa mawe
Katika juhudi za kupambana na uchimbaji holela wa mawe, Juvenary ameshauri Serikali kuimarisha utekelezaji wa sheria za mazingira na madini, pamoja na kuhakikisha kila mradi unafanya TAM.
“Serikali inapaswa kuimarisha utekelezaji wa sheria za mazingira na madini. Lakini pia inatakiwa kuhakikisha kila mradi unafanyiwa Tathmini ya Athari kwa Mazingira kabla ya kuanza,” anasema.
Aidha, anashauri kutolewa kwa elimu ya mazingira kwa wachimbaji na jamii, kuweka maeneo rasmi ya uchimbaji yenye udhibiti, kuhamasisha matumizi ya teknolojia rafiki kwa mazingira pamoja na kufanya urejeshaji wa mazingira, kama kupanda miti na kurejesha ardhi baada ya uchimbaji.
Anasema hatua nyingine zinazoweza kusaidia ni kuongeza ukaguzi na adhabu kwa wanaokiuka sheria zilizowekwa. “Hatua hizi kwa pamoja hujenga usimamizi endelevu na kupunguza madhara ya uchimbaji holela,” anashauri Juvenary Matagili, ambaye ni mtaalamu wa mazingira.
David anashauri kila mwananchi kuendelea kutimiza wajibu wa kulinda na kutunza mazingira. Anasema: “Suala la mazingira sio la afisa tu, wala si la Mkurugenzi wa Jiji; ni la kila mtu. Sheria imesema, kila raia, kila kikundi, kila taasisi ina wajibu wa kutunza na kuhifadhi mazingira kuanzia anapoishi hadi sehemu nyingine zote”.
Anasema ni muhimu kwa Serikali kuendelea kushirikiana na taasisi zisizo za kiserikali na wadau wengine kutoa elimu na maonyo dhidi ya uchimbaji holela wa mawe.
Picha ya Bango: Katika mtaa wa Bulale jijini Mwanza, shughuli za uchimbaji holela wa mawe zimeacha mashimo pembezoni mwa barabara na majengo ya biashara. Picha na Dominic Allen, Mongabay.