- Green Climate Fund (GCF) imefungua ofisi za kikanda katika miji ya Nairobi na Abidjan ili kuongeza ufadhili wa miradi ya tabianchi barani Afrika.
- Miradi inayoungwa mkono na GCF nchini Kenya ina thamani ya $493 milioni na inalenga kuleta manufaa makubwa katika kukabiliana na athari za tabianchi na kupunguza uzalishaji wa hewa ukaa.
- Miongoni mwa mafufaa makubwa ya GCF ni pamoja na kuimarisha minyororo ya thamani ya kilimo inayostahimili mabadiliko ya tabianchi katika maeneo yenye ukame.
- Kikao cha bodi ya GCF kiliazimia kupunguza muda wa kuidhinisha miradi kutoka kiwango cha juu cha miaka mitatu hadi miezi tisa.
Green Climate Fund (GCF) kwa sasa una washirika 168 waliothibitishwa, baada ya kuongeza washirika 10 zaidi katika kikao cha bodi kilichofanyika katika makao makuu yake nchini Korea Kusini mwishoni mwa Machi 2026. Hii inaongeza idadi ya nchi zinazoendelea na wadau wanaoshirikiana na mfuko huo kubaini maeneo na njia bora zaidi ya kuleta mabadiliko chanya kwenye tabianchi.
Kwa mujibu wa taarifa ya GCF kwa Mongabay, kwa sasa mfuko huo unaunga mkono miradi minne nchini Kenya na miradi 23 ya kikanda inayohusisha nchi nyingi.
“GCF hutoa ufadhili kupitia washirika waliothibitishwa; taasisi za kifedha zilizoidhinishwa kufanya kazi na mfuko huu. Taasisi hizi zinakidhi viwango vya GCF na zinaendana na dhamira ya mfuko ya kuleta mabadiliko chanya katika kukabiliana na tabianchi,” alisema Catherine Koffman, Mkurugenzi wa Idara ya Kanda ya Afrika wa GCF.
Katika barua pepe kwa Mongabay, Rebecca Phwitiko, Mtaalamu wa Mawasiliano wa GCF (Vyombo vya Habari na Maudhui), alieleza kuwa maeneo makubwa wanayolenga kufanyia kazi yanajumuisha kuimarisha minyororo ya thamani ya kilimo inayostahimili mabadiliko ya tabianchi katika maeneo yenye ukame.
Mengine ni kurejesha maeneo ya malisho na vyanzo vya maji vilivyoharibika ili kuboresha upatikanaji wa maji na maisha ya watu, kupanua matumizi ya nishati jadidifu na nishati safi za kupikia, pamoja na kufungua fursa za ufadhili mseto kwa teknolojia rafiki kwa tabianchi kupitia taasisi za kifedha za ndani.
Miradi inayoungwa mkono na GCF nchini Kenya yenye thamani ya $493 milioni inalenga kuleta manufaa makubwa, “ikiwa ni pamoja na kuboresha usalama wa chakula, kuimarisha ustahimilivu wa maji, kupunguza uzalishaji wa hewa ukaa, na kuongeza upatikanaji wa nishati safi pamoja na huduma za kifedha’’. Phwitiko aliiambia Mongabay.
Miradi minne ya GCF inayotekelezwa nchini Kenya kwa ngazi ya nchi moja ni: KCB Bank Kenya Limited: Mradi unaoshughulikia suluhisho za kilimo kinachostahimili mabadiliko ya tabianchi kwa MSMEs na wakulima, Mamlaka ya Usimamizi wa Mazingira ya Kenya (NEMA): Mradi unaoshughulikia usalama wa maji ya Mto Upper Athi, Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO): Mradi unaoghulikia minyororo ya thamani ya kilimo kinachostahimili mabadiliko ya tabianchi, na International Union for Conservation of Nature: TWENDE: Mradi uaohusu mbinu za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi kwa kutumia mifumo ya ikolojia katika maeneo kame na yenye ukame kiasi. Mradi wa Benki ya KCB uliidhinishwa mwezi Machi.
Wakati huohuo, kikao cha bodi kiliamua kupitia upya muda wa kushughulikia na kuidhinisha miradi ya GCF kutoka kipindi cha miaka mitatu hadi miezi tisa.
“Mnamo mwaka 2025, GCF iliboresha mfumo wake wa uthibitishaji kama sehemu ya mageuzi makubwa yaliyolenga kuufanya mfuko huu kuwa na ufanisi zaidi na wenye matokeo chanya. Mchakato mpya ni wa haraka zaidi, ukilenga kukamilika ndani ya miezi tisa.
“Pia ni wazi zaidi na unaojibu mahitaji kwa haraka, huku ukiendelea kuzingatia viwango vya juu vya uwajibikaji wa kifedha, ulinzi wa mazingira na kijamii, pamoja na sera muhimu kama ile ya usawa wa kijinsia,” alisema Catherine.
Katika mkutano uliofanyika kwa nji ya mtandaoni uliohudhuriwa na takribani watu 20, wengi wao wakiwa waandishi wa habari na wanasayansi, GCF pia ilitangaza kufungua ofisi mbili mpya za kikanda, hatua inayodhihirisha kuimarika kwa jitihada za ufadhili wa miradi ya tabianchi barani Afrika.
“Kuanzishwa kwa ofisi hizi za kikanda kunaashiria mwanzo wa mbinu maalum zaidi za kufadhili miradi ya mabadiliko ya tabianchi, ikijumuisha kukabiliana na athari zake na kupunguza uzalishaji wa hewa ukaa, hasa katika nchi zilizo hatarini zaidi,” alisema Catherine.
Aliongeza kuwa ingawa walikuwa wakifanya kazi kwa mafanikio kutoka makao makuu yao nchini Korea Kusini, kusogea karibu zaidi na jamii kunamaanisha kuwahusisha zaidi katika maamuzi ya maeneo ambayo GCF itatoa ufadhili.
Ofisi ya Nairobi itahudumia Ukanda wa Afrika Mashariki na Kusini, huku ofisi ya Abidjan ikihudumia Afrika ya Kati na Magharibi.
Picha ya Bango: Catherine Koffman, Mkurugenzi wa Idara ya Kanda ya Afrika wa GCF (kushoto), wakati akihutubia waandishi wa habari katika mkutano wa wanahabari uliofanyika mtandaoni mwezi Machi,2026. Picha na Lynet Otieno, Mongabay.