- Tembo Pilipili imedhihirisha mafanikio ya dhana mbili zinazokinzana: uhifadhi na usalama wa watu na mali zao.
- Awali wenyeji waliwaona tembo kama maadui, lakini sasa wanaishi nao kwa amani.
- Idadi ya tembo imeongezeka kutokana na juhudi za uhifadhi na utekelezaji wa sheria kali dhidi ya ujangili.
- Kuchelewa kwa malipo ya kifuta jasho bado ni tatizo, mlolongo mrefu wa mchakato huwakatisha tamaa wananchi.
MANYARA, Tanzania – Emmanuel Mwita, mkulima katika Kijiji cha Vilima Viwili, wilayani Babati katika Mkoa wa Manyara, Kaskazini mwa Tanzania, anakumbuka uharibifu mkubwa aliokuwa akifanyiwa na tembo katika shamba lake la mahindi.
“Kuna wakati tembo walikuwa wanaingia na kula kila kitu, shamba lote linabaki kama uwanja. Sikuwa navuna kitu. Nilibaki na njaa tu,” anasema Mwita, na kuongeza: “Niliwachukia sana wanyama hao kwa kunirudisha nyuma.”
Matukio ya migogoro kati ya wanyama, hususan tembo, na binadamu mara nyingi yamekuwa yakisababisha hasara kwa wakulima, majeruhi na hata vifo kwa upande wa binadamu na kwa upande wa tembo. Wengine wamekuwa wakiuawa na wananchi waliokasirishwa na uharibifu wa wanyama hao.
Tembo Pilipili inavyooanisha dhana zinazokinzana
Katika kuoanisha dhana mbili ambazo kwa kawaida hukinzana; kupambana na wanyama waharibifu kwa upande mmoja na uhifadhi kwa upande mwingine, asasi ya Tembo Pilipili ilibuni mradi unaoendeleza uhifadhi wa wanyama walio hatarini kutoweka, hasa tembo, na papo hapo kuondoa migogoro baina ya tembo na binadamu.
Tembo Pilipili ni mradi ulioanzishwa mwaka 2021 ukilenga kutumia mbinu za kijamii kusaidia tembo na binadamu kuishi kwa pamoja bila migogoro. Ukiendeshwa na asasi inayojulikana kama Tembo Pilipili (TPP), mradi unafanya kazi katika maeneo yanayopakana na hifadhi za wanyama kama vile Tarangire, Ruaha, Selous, Serengeti na Mikumi.
Licha ya kudhibiti migogoro, mradi huo unasaidia wakulima kuzuia tembo wasiharibu mazao yao bila kuwadhuru.

Francis Ndemela, Meneja wa Mradi wa Tembo Pilipili, anasema: “Tulibuni mbinu hizi kwa ajili ya kusaidia uhifadhi na wakati huohuo kuondoa migogoro baina ya tembo na binadamu ambayo kwa kiasi fulani imekuwa ikileta uhasama baina ya wananchi na Serikali hasa pale wanyama walio hatarini kutoweka wanapouawa na wananchi walioharibiwa mazao yao,” anasema Ndemela.
Ndelema anasema kutokana na hali ya ukame, chakula kwenye maeneo ya hifadhi hupungua, hali inayowafanya tembo walazimike kwenda kwenye mashamba ya watu kutafuta chakula na maji.
“Lakini pia idadi ya tembo imeongezeka kutokana na juhudi za uhifadhi wa wanyama pori na uwepo wa sheria kali dhidi ya ujangili,” anasema Ndemela.
Taarifa za hivi karibuni kutoka kwa washirika wa uhifadhi zinakadiria kuwa idadi ya tembo nchini Tanzania inaweza kufikia karibu 60,000. Kulingana na mikakati ya kitaifa ya utunzaji wa tembo, idadi hiyo ya tembo nchini imefikiwa kutokana na kupungua kwa ujangili na juhudi zinazozingatia uhifadhi wa wanyama na hifadhi za misitu.
Kutokana na wingi huo, matukio ya wanyama wakali, wakiwemo tembo, kuvamia makazi na mashamba ya watu yamekuwa yakiongezeka. Hali hii inachangiwa si tu na hali ya ukame na kuongezeka kwa idadi ya tembo, bali pia kutokana na upanuzi wa makazi ya watu, kupungua kwa uoto wa asili, jambo linalosababishwa na uharibifu wa misitu na mabadiliko ya tabianchi.
Utafiti uliofanywa na African People and Wildlife unaonesha kuna takribani matukio 1,200 ya tembo kuvamia makazi ya watu na mashamba kwa mwaka nchini Tanzania. Idadi hii inaongeza tishio la uhifadhi na usalama wa watu na mali zao katika nchi ambayo idadi ya tembo na binadamu inakadiriwa kuwa tembo mmoja katika kila watu 10 tu.
Kwa mujibu wa Ndemela, mradi wa Tembo Pilipili unatekelezwa katika vijiji vinavyozunguka mbuga ya Mikumi katika Wilaya za Kilosa na Mvomero. Vijiji katika wilaya ya Kilosa ni: Vikweme, Mhenda na Kilangali wakati katika wilaya ya Mvomero ni Doma, Maharaka, Mkata, Mangae na Msongozi.
Maeneo mengine yanayonufaika na mradi huo ni mbuga ya Ruaha iliyoko Iringa Vijijini katika tarafa za Pawaga na Idodi kwenye kata za Mlowa na Kitisi; mbuga ya Tarangire; wilaya ya Babati katika kata za Nkait kwenye vijiji vya Kakoi, Mdori na Vilima Viwili; mbuga ya Ziwa Manyara, kata ya Magara katika kijiji cha Mayoka; Hifadhi ya Nyerere – wilaya ya Liwale kata za Mtawatawa na Mkutano; Pori la Akiba la Maswa – wilaya ya Bariadi kata za Matongo na Gilya pamoja na Ngorongoro Conservation Area iliyoko katika Wilaya ya Karatu.
Tembo Pilipili inafanyaje kazi?
Kwa mujibu wa Ndemela, mradi huo hutumia njia mbili: Pilipili na nyuki. Kwa upande wa pilipili, wakulima hukusanya pilipili na kuzisaga na kisha huzichanganya na mafuta machafu na hupaka mchanganyiko huo kwenye vitambaa ambavyo hufungwa kwenye kamba inayozunguka shamba. Harufu ya pilipili huwaudhi na kuwafanya wakimbie kutoka eneo husika bila kuleta madhara yoyote.

Kuhusu njia ya nyuki, Ndemela anasema: “Tunatengeneza mizinga ya kawaida halafu tunachukua tangawizi na kuiponda, kuiongezea maji na kupata juisi ambayo tunaipulizia ndani ya mizinga kwa kutumia kifaa cha kupulizia dawa. Harufu ya tangawizi huenea ndani ya mzinga. Mizinga ya nyuki hutundikwa kuzunguka mashamba. Hii huwafanya tembo waondoke kwa sababu kwa kawaida wanaogopa nyuki.”
Anasema ubunifu huu huwafanya nyuki wawe wakali zaidi na huwafuata tembo hata kwa umbali wa kilometa tano kutoka kwenye makazi yao.
Zaidi ya njia ya kutumia pilipili kwenye uzio wa mashamba na nyuki, njia nyingine wanayotumia ni kutengeneza tofali za pilipili. Anasema pilipili iliyochanganywa na kinyesi cha ng’ombe hutumika kutengeneza matofali ambayo huchomwa shambani nyakati za usiku na hivyo moshi wake kuwapalia tembo na kuwafanya wakimbie.
Manufaa ya Tembo Pilipili
Mwita ana shamba la mahindi lenye ukubwa wa ekari 10 ambapo mwaka wenye mavuno mazuri huweza kuvuna hadi magunia 100 ya kilogramu 100 kila moja. Hali hiyo ni tofauti na wakati hajaanza kuzuia tembo kwa kutumia pilipili. Kabla ya kujiunga na mradi huo, mavuno yake yalikuwa hayatabiriki kwa kuwa kuna wakati mahindi yake yalikuwa yakiliwa yote na tembo na hapati chochote.
Mwita ni mmoja wa wanufaika zaidi ya 11,000 wa mradi huo. Yeye na wakulima wenzake, licha ya mazao yao kutovamiwa lakini pia wamepata mafunzo ya uzalishaji pilipili na jinsi ya kuzitumia kwa ajili ya uhifadhi pamoja na ufugaji wa nyuki.
Alan Fidelis ni mnufaika mwingine wa mradi huo. Anakumbuka jinsi mwaka 2019, kabla hajaanza kutumia mbinu ya pilipili kulinda mashamba yake alivyokuwa akiteswa na wanyama hao.
Anasema kilichomuuma zaidi ni kwamba baada ya kuwasilisha malalamiko yake baada ya shamba lake la mpunga kuliwa lote na tembo, alisubiri kwa miaka mitatu kabla ya kupata kifuta jasho kutoka Serikalini.

“Nililima mpunga ekari tatu na mazao yalipokomaa kabla sijavuna, tembo waliingia na kula mazao yote. Niliripoti kwa Ofisa Ugani ambaye alikuja shambani na kupiga picha na kuondoka nazo.
“Baada ya siku chache, wakaniita ofisini na kusema kuwa Serikali itatoa kifuta machozi ambacho ni kiasi kidogo cha fedha. Lakini fedha hizo zilikuja baada ya miaka mitatu pamoja na hasara niliyokuwa nimeingia,’’ anasema Fidelis. Anasema wakati anafuatilia malipo yake aliambiwa kwamba utolewaji wa fedha hutegemea uwepo wa bajeti.
Mkuu wa Kitengo cha Maliasili na Uhifadhi wa Mazingira Wilaya ya Iringa John Mtimbanjayo ambaye anashughulikia masuala ya migogoro kati ya wanyama na binadamu, anasema malipo ya kifuta jasho huchelewa kutokana na mlolongo mrefu wa mchakato wenyewe ambao huanzia kijijini, kwenda wilayani na kisha wizarani.
Anasema kuwa mchakato huo hujumuisha kujaza fomu, kupiga picha ya athari za shamba na picha ya mkulima kuwekwa kwenye fomu husika na kisha kuwasilisha wilayani ambapo pia maofisa wilayani huhitaji kujiridhisha kwa kutembelea eneo husika.
Baada ya maofisa ngazi ya wilaya kujiridhisha, huwasilisha madai wizarani lakini hufanya hivyo baada ya kuwa wamekusanya madai mengi kwa pamoja ili kupunguza gharama.
“Hata wizarani nao huhitaji kwenda hadi kijijini kujidhirisha na hii, kutembelea wilaya zote zanye athari na kuiridhisha, inachukua muda mrefu. Mambo yote yanaweza kukamilika, lakini ikiwa bajeti haitoshi, itabidi malipo yasubiri,’’ anasema.
Kwa mujibu wa Kanuni ya Kifuta jasho kwa uharibifu unaosababishwa na Wanyama wakali ya mwaka 2024 (Wildlife Conservation Dangerous Animals Damage Consolation Regulation 2024), kifuta jasho hutofautiana kulingana na umbali liliko shamba kutoka kwenye hifadhi.
Kwa shamba lililo chini ya kilometa moja kutoka kwenye hifadhi halilipwi kifuta jasho chochote. Kilometa 1 hadi nne hulipwa TSh75,000 ($30); kilometa 4 – 5 hulipwa TSh112,000 ($45) wakati shamba lililo zaidi ya kilometa 5 hulipwa TSh150,000 ($60) kwa eka.
Mtanziko wa Fidelis ni kama ule wa Franco Stondo wa Mikumi, ambaye pia ni mnufaika wa mradi wa Tembo Pilipili ambaye alikaribia kukata tamaa kulima katika kijiji chake kilichopakana na Hifadhi ya Taifa ya Mikumi.

Stondo anasema wao walikuwa wakitumia njia nyingine za kienyeji kulinda mashamba yao dhidi ya tembo kama vile kupiga madebe, kumulika tochi na kuwasha moto lakini hakukuwa na mafanikio makubwa. “Kwa kweli tulikuwa tunawachukia sana tembo na kuwaona kama maadui zetu,” anasema.
Asasi ya Tembo Pilipili iliwapa mafunzo Stondo, Fidelis, Mwita na wenzake jinsi ya kulinda mashamba yao kwa kutumia njia hizi za asili na zisizo na gharama kubwa.
“Tangu nimeanza kutumia pilipili, tembo hawaharibu tena mashamba,” anasema Fidelis ambaye hulima alizeti, mahindi, maharage na pilipili.
Kijiji cha Muhenda kilichopo Wilaya ya Kilosa mkoani Morogoro kinapakana na Hifadhi ya Taifa ya Mikumi ambayo pia inajulikana kwa kuwa na tembo wengi.
Manufaa katika uhifadhi na kiuchumi
John Mtimbanjayo, aliyekuwa mratibu wa mradi wa Tembo Pilipili katika Halmashauri ya Kilosa anasema kuwa mradi huo umesaidia kwa kiasi kikubwa kupatanisha mamlaka za uhifadhi na wananchi baada ya uhusiano kuwa mbaya kwa muda mrefu kutokana na wananchi kuua wanyama kwa upande mmoja na wanyama na kuharibu mashamba yao kwa upande mwingine.
“Mara nyingi ilionekana kama Serikali inathamini zaidi Wanyama kuliko wananchi wake kwa kuwa kuna sheria kali dhidi ya ujangili na kudhuru wanyama. Kutokana na uhaba wa rasilimali, hata wananchi wakitoa taarifa za uvamizi wa tembo katika mashamba yao, inachukua muda mrefu sana hadi wahifadhi kufika na kuwafukuza. Mradi kama Tembo Pilipili ni suluhisho.
“Manufaa ya mradi huu ni mtambuka kwa kuwa zaidi ya kusaidia uhifadhi na kuongeza usalama wa wakazi na mali zao, umekuwa pia na manufaa mengi kiuchumi,” anaeleza Francis Ndemela.
Wakulima zaidi ya 11,000 wamejengewa uwezo wa kulima pilipili na kuunganishwa kwenye vikundi na kupewa fursa za mikopo kwa ajili ya kazi nyingine za uzalishaji mali.
“Ukulima wa pilipili kwa ajili ya uhifadhi umeleta pia manufaa ya kiuchumi kutokana na zao hilo kuwa la biashara,” anasema Ndemela.
Alan Fidelis ambaye ni mkulima anasema yeye na wenzake wanaolima pilipili wamekuwa wakiuza zao hilo kwenye kiwanda cha kusindika pilipili cha Dabaga na kujipatia fedha ambapo kilo moja ya pilipili ya unga huuzwa kwa bei ya TSh5,000 ($2).
“Katika msimu mmoja wenye misimu 10 ya pilipili naweza kupata kati ya TSh5,000,000 ($1,950) na TSh6,000,000 ($2,340), fedha ambazo kabla ya mradi huu nilikuwa sizipati,” anasema.
Mradi huu umewaunganisha wakulima katika maeneo yao katika vikundi 168 na kuwasaidia kupata mikopo kutoka Vision Fund ambako tayari TSh572 milioni zimetolewa kama mikopo ya masharti nafuu kwa ajili ya uzalishaji.
Ndelema anasema kuwa pamoja na uhifadhi, kuna matokeo chanya katika uchumi wa wakulima wanaoishi kando mwa hifadhi. Anasema wakulima hao si tu kwamba kwa sasa wanapata mazao zaidi, bali pia wanapata fursa nyingine za kiuchumi.

Kwa mujibu wa Ndelama, kwa sasa mradi huo unatekelezwa kwenye maeneo yanayopakana na hifadhi. Hata hivyo wana mpango wa kuuendeleza katika sehemu nyingine nchini pindi rasilimali zitakapopatikana.
Changamoto
Mtimbanjayo anasema changamoto kubwa iliyopo ni kwamba wahifadhi wanashindwa kufika kwa haraka pale wanapoarifiwa kuwa wanyama wamevamia maeneo ya makazi ya watu na kufanya uharibifu kwenye mashamba. Anasema hatua hiyo inawafanya wananchi wawe na hisia kwamba Serikali inathamini zaidi wanyama kuliko watu na mali zao.
“Kwa mfano wilaya ya Kilosa ina kilometa za mraba 12,000 na wahifadhi ni wachache. Inakuwa si rahisi kwao kuitikia wito kwa wakati kunapotokea changamoto ya uvamizi wa wanyama. Jambo hili, kwa bahati mbaya, husababisha wananchi wadhani kuwa Serikali inathamini wanyama kuliko wao, hisia ambazo si za kweli,” anasema Mtimbanjayo.
Uzoefu wa nchi nyingine
Ulinzi wa mazao dhidi ya tembo bila kuwadhuru ni mbinu inayotumika sehemu mbalimbali za Afrika na katika bara la Asia.
Kwa mujibu wa tovuti ya National Geographic, nchini Kenya na Uganda mbinu ya pilipili hutumika pamoja na taa na milio ya kengele au mabati kufukuza tembo mashambani.
Nchini Zambia kuna mradi unaofanana na Tembo Pilipili ambapo pilipili huzungushiwa kwenye mashamba na matofali ya pilipili kuchomwa nyakati za usiku ili kufukuza tembo.
Mtandao wa Uhifadhi Wanyamapori (WCN) unaeleza mafanikio ya mradi wa kudhibiti tembo kuvamia mashamba nchini Zambia katika maeneo yanayopakana na Hifadhi ya Taifa ya Luangwa. Wakazi wamekuwa wakitumia mbinu mbalimbali kudhibiti tembo, ikiwemo uzio wa pilipili kuzunguka mashamba yao.
Picha ya Bango: Meneja Mradi wa Tembo pilipili, Francis Ndelema akionesha jinsi ya kuzungushia wigo wa kitambaa chenye pilipili shambani. Picha kwa hisani ya Mradi wa Tembo Pilipili.