- Hadithi ya Mariana inaonyesha mgongano kati ya maisha na uhifadhi: anategemea biashara ya mkaa kujikimu licha ya kujua inaathiri misitu.
- Misitu ni muhimu kwa maisha na uchumi, ikisaidia mabilioni ya watu duniani kwa chakula, dawa, nishati na kipato.
- Tanzania inapoteza misitu kwa kasi kubwa (hekta 400,000–470,000 kwa mwaka), ikichochewa na umaskini, utegemezi wa kuni na mkaa, pamoja na ongezeko la watu.
- Athari za ukataji miti ni pamoja na kupungua kwa rutuba ya udongo, ukame, kupungua kwa maji, uharibifu wa bioanuai na kudorora kwa maisha ya jamii.
Hili ni toleo la kwanza katika mfululizo wa makala kuhusu uharibifu wa misitu Tanzania. Soma toleo la pili hapa.
Ni Alfajiri, siku ya Jumamosi, Mariana anadamkia kwenye kibanda chake cha kuuza mkaa ili kupakua mkaa kutoka kwenye magunia na kuuweka kwenye mifuko midogo midogo ili ifikapo asubuhi, awe tayari kuwauzia wateja wa rejareja.
Anafahamu mkaa unaharibu misitu, lakini hana njia nyingine ya kupata riziki ya kila siku kwa ajili yake na watoto wake watatu. Kwa Mariana, kila mfuko anaouza, ni chakula kwa watoto wake, lakini kwa upande wa uhifadhi, ni kifo kwa misitu zaidi katika eneo lake.
Hadithi ya Mariana ni kielelezo cha kweli kinachoonyesha hali halisi inayoendelea kwenye jamii mbalimbali nchini Tanzania, ambazo licha ya jitihada na miradi mbalimbali inayoendelea kulinda na kuhifadhi misitu, bado wanaendelea kukata miti kwa matumizi mbalimbali.
Kwa Mariana na jamii nyingi nchini, kuacha kukata misitu ni kuchagua uhifadhi badala ya uhai wao. Hii ina maana kwamba hatua hiyo itawafanya wapoteze njia pekee ya kujipatia riziki.
Misitu ni msingi wa maisha bora kwa wanadamu na viumbe hai vingine, na pia husaidia kujenga uhusiano wa kutegemeana baina ya mifumo mbalimbali ya maisha.
Kwa mujibu wa Shirika la Chakula na Kilimo Duniani (FAO), misitu ni nyezo muhimu ya kuondoa umaskini katika jamii zenye kipato cha chini au zisizokuwa na kipato cha kueleweka, kwani huzikinga na majanga mbalimbali ya kiuchumi na kimazingira.
Kulingana na Benki ya Dunia, maisha ya watu wapatao bilioni 1.6, ambayo ni zaidi ya asilimia 25 ya watu maskini duniani, hutegemea misitu katika maisha yao, hasa katika kupata chakula, dawa, maji, mbao na miti ya kujengea nyumba pamoja na biashara ya mazao ya misitu ambayo huwapatia fedha.

Benki ya Dunia, katika Ripoti yake inakadiria kuwa takribani watu bilioni moja ulimwenguni hupata dawa moja kwa moja kutoka misituni kwa ajili ya matatizo mbalimbali ya kiafya.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, kati ya asilimia 40 hadi 50 ya dawa zenye thamani ya $108 bilioni kwa mwaka, hutokana na mimea iliyoko katika misitu ya asili.
Aidha, katika nchi nyingi zinazoendelea, misitu ni chanzo cha uhakika cha kuni na mkaa ambavyo hutumika kama vyanzo muhimu vya nishati ya kupikia.
Taarifa za Serikali inaonyesha misitu huchangia takriban asilimia 90 ya mahitaji ya nishati katika nchi hizo.
“Faida na umuhimu wa misitu haviwezi kuelezwa kwa upana wake. Itoshe kusema kuwa misitu ni muhimu kwa uchumi wa mtu mmoja mmoja, familia, jamii na nchi kwa ujumla,” anasema Jafar Kideghesho, Mtafiti katika masuala ya misitu, katika andiko lake, Hali na Mwelekeo wa Ukataji Miti Ovyo Nchini Tanzania, Sababu zake, Athari zake na Hatua za Kuchukua (Realities of Deforestation in Tanzania – trends, drivers , implications and way forward).
Pamoja na manufaa haya, misitu inaendelea kuharibiwa, hali inayotishia kutoweka kwake nchini Tanzania.
Ukataji misitu Tanzania: Hali ikoje?
Ukataji wa misitu nchini Tanzania unaelezwa kuwa ni janga la kimazingira linaloathiri mamilioni ya watu, hasa wale waishio vijijini ambao idadi yao, kulingana na takwimu za Benki ya Dunia, inakadiriwa kuwa ni kati ya asilimia 65 na 70 ya Watanzania wote.
Kwa mujibu wa FAO, kuanzia mwaka 2015 hadi 2020, Tanzania imekuwa ikipoteza kati ya hekta 400,000 hadi 470,000 za misitu kila mwaka.
Kulingana na takwimu hizo, mikoa inayoongoza kwa ukataji miti ovyo ni Dodoma, Manyara, Singida, Simiyu, Geita na Kilimanjaro.
Kadhalika, Taasisi ya Kimataifa ya Mazingira, Global Forest Watch, inakadiria kuwa kati ya kipindi kinachoanzia mwaka 2000 hadi 2020, Tanzania ilipoteza ekari za misitu zipatazo 3.82 milioni (au asilimia 11 ya misitu yake ambayo ni takriban hekta 48.1 milioni, au asilimia 55 ya ardhi yote ya Tanzania).
Taarifa zaidi zinaonyesha kasi ya ukataji ovyo wa misitu nchini Tanzania inakadiriwa kuwa asilimia moja kwa mwaka, kiwango ambacho ni mara mbili ya wastani wa ulimwengu.
Kulingana na takwimu za Benki ya Dunia, ukataji miti ni janga la kimazingira linaloathiri mamilioni ya watu nchini Tanzania hasa wale waishio vijijini, ambao idadi yao, inakadiriwa kuwa ni kati ya asilimia 65 na 70 ya Watanzania wote.
Petro Nyiti ni mtaalamu wa misitu kutoka kampuni ya Reforest Africa, shirika linalofanya kazi katika mikoa ya Iringa na Morogoro nchini Tanzania kuhamasisha wananchi vijijini kutunza misitu na kuivuna kwa namna endelevu ili kuendelea kunufaika nayo.
Anasema kuwa upotevu huu wa misitu unachangiwa kwa kiasi kikubwa na ongezeko la watu, utegemezi wa nishati ya mkaa na kuni pamoja na umaskini.
Ongezeko la watu, kwa upande wake, linachochea mahitaji ya chakula, makazi mapya, miundombinu ya maendeleo, mahitaji ya vifaa vya ujenzi, na hata samani za maofisini na majumbani.
Mambo mengine yanayochangia uharibifu wa misitu ni upanuzi wa shughuli za kilimo, ufugaji wa kuhamahama pamoja na uvunaji holela wa mazao ya misitu kama mkaa, mbao na milingoti.
Sababu nyingine ni watendaji wa serikali na mamlaka nyingine kutosimamia sheria za misitu ipasavyo, na hivyo kutoa mwanya kwa wafanyabiashara haramu wa mazao ya misitu.
“Hapa kijijini tulikuwa na msitu mkubwa wa Bondwa, lakini watu wamekata miti mingi kiasi kwamba ule ukijani uliokuwa unaonekana haupo tena. Hatuna uhakika lini tutapata mvua na hata rutuba ya udongo imepungua.

“Kinachotushangaza ni kwamba serikali ya kijiji haiwachukulii hatua wahalifu hawa ambao wengi hutoka nje ya kijiji chetu,” anaeleza Felician Oscar, mkazi wa kijiji cha Makole, kata ya Mgeta, Wilaya ya Mvomero, Mkoani Morogoro.
Mwenyekiti wa kijiji cha Makore, Simba Dimoso anakiri kuwepo kwa uharibifu wa msitu, lakini anasema ni vigumu kuwakamata wahalifu. Anasema: “Hawa watu wengi hupita njia za milimani ambako hakuna barabara. Siyo rahisi kuwafuatilia na kuwakamata. Lakini baadhi ya wanakijiji wanawafahamu watu hao, na ni wajibu wa kila mmoja kuzuia uhalifu huu,” anasema Dimoso.
Upotevu wa misitu Tanzania: Nini kimejificha?
Wataalamu na wananchi mbalimbali waliohojiwa na Mongabay kwa nyakati tofauti walieleza sababu mbalimbali zinazochangia upotevu wa misitu nchini.
Miongoni mwa sababu kuu zilizotajwa ni pamoja na utegemezi wa nishati ya mkaa na kuni, pamoja na ongezeko la watu walilosema linachochea mahitaji ya chakula, makazi mapya, miundombinu ya maendeleo, mahitaji ya vifaa vya ujenzi, na hata samani za maofisini na majumbani.
Simon Lugazo, mtaalamu wa kujitegemea wa masuala ya misitu, ambaye amewahi pia kufanya kazi na taasisi ya Tanzania Forest Conservation Group, anasema kuwa jamii za vijijini zinategemea sana nishati ya kuni kwa kupikia, na baadhi ya wananchi wanashughulika na utengenezaji mkaa kwa ajili ya kuuza kwa watumiaji wa mijini, kwani matumizi ya mkaa vijijini ni madogo sana.
“Hawana chanzo mbadala cha nishati. Watu wanavyoongezeka ndivyo hitaji la nishati linavyoongezeka na kimbilio la jamii za vijijini ni kuni na mkaa.
“Ongezeko la watu linachochea ongezeko la vijana ambao wanahitaji kujiajiri au kuajiriwa ili kujikimu kiuchumi. Ajira iliyo rahisi kwao ni kuchoma mkaa na kuuza au kuuza kuni, kwani haihitaji ujuzi wowote na haina gharama ya uwekezaji,” Lugazo aliiambia Mongabay.
“Tukumbuke pia kuwa watu wanahitaji chakula, hivyo pamoja na matumizi ya kuni na mkaa kama vyanzo vya mapato, wanavijiji hukata misitu ili kupata mashamba kwa ajili ya uzalishaji wa chakula,” aliongeza.
Michael Mdalahela kutoka kijiji cha Viwanja Sitini katika Halmashauri ya Mlimba katika Wilaya ya Kilombero, naye anaunga mkono hoja za wenzake kwamba ukosefu wa kipato cha uhakika ndiyo unawasukuma kufanya biashara hizo.
Kwa maoni yake, ukiondoa kilimo, hakuna chanzo kingine cha mapato kwa ajili ya wakazi wa kijiji hicho, hivyo ili waweze kuishi hawana budi kuvamia misitu ili kutengeneza mkaa na kukata kuni.
“Tegemeo letu kubwa ni kilimo kinachotupatia mazao ya chakula na ya biashara. Lakini siku hizi kilimo hakiaminiki kwani wakati mwingine mvua zinakuwa chache kiasi ambacho mazao hayawezi kustawi.
“Wakati mwingine pia mvua zinakuwa nyingi na kusababisha mafuriko ambayo huharibu kabisa mazao. Katika hali kama hii, tunakuwa hatuna tegemeo la maisha bali kuingia msituni,” anasema Mdalahela.
Kwa upande wake, Ignace Weluka ambaye ni mtaalamu wa misitu kutoka Shirika la Maendeleo Endelevu Rukwa aliiambia Mongabay kuwa ufugaji wa kuhamahama unaohusisha makundi makubwa ya mifugo, umesababisha uharibifu mkubwa wa msitu wa Lyamba lya Mfipa katika mkoa wa Rukwa.
“Mifugo inaachiwa kuzurura ovyo na hivyo kuharibu uoto wa asili na mazingira kwa ujumla. Hali hii imeathiri ubora wa msitu na imesababisha mmomonyoko wa ardhi na kutoweka kwa huduma za kiikolojia zinazotokana na misitu,” anasema Weluka.
Rashid Nambalamoto, mkazi wa kijiji cha Viwanja Sitini katika Halmashauri ya Mlimba. Anasema: “Kwa asili, wenyeji wa vijiji vya Halmashauri ya Mlimba walikuwa ni wakulima na wavuvi tu. Lakini katika miaka ya hivi karibuni kumetokea wimbi la wafugaji na makundi makubwa ya ng’ombe ambao hawana utaratibu wa malisho.
“Makundi hayo yamefanya uharibifu mkubwa wa vyanzo vya maji na mazingira kwa ujumla na kusababisha mfarakano mkubwa baina ya wageni na wahamiaji”.

Kutokana na hali hiyo, anasema: “Hakuna msitu ambao uko salama; misitu yote imevamiwa na makundi ya ng’ombe ambao wanaharibu kabisa uoto wa asili. Wachungaji pia hukata sehemu kubwa ya misitu ili kutengeneza njia ya kupitisha mifugo yao ambayo huingia hata mashambani. Hali hii imekuwa tishio siyo tu kwa misitu, bali pia kwa mazingira kwa ujumla”.
Sababu nyingine inayotajwa ni kitendo cha watendaji wa Serikali na mamlaka nyingine kutosimamia sheria za misitu ipasavyo na hivyo kutoa mwanya kwa wafanyabiashara haramu wa mazao ya misitu kuendelea kufanya uharibifu.
“Hapa kijijini kwetu tulikuwa na msitu mkubwa wa Bondwa, lakini watu wamekata miti mingi kiasi kwamba ule ukijani uliokuwa unaonekana na kuvutia, haupo tena.
“Kwa sasa hata rutuba ya udongo wetu imepungua na hatuna uhakika tufanye nini ili hali irejee kama ilivyokuwa mwanzo,” anasema Felician Oscar, mkazi wa kijiji cha Makole, kata ya Mgeta Wilaya ya Mvomero, Mkoani Morogoro.
Anasema kinachowashangaza wengi ni kwamba Serikali ya kijiji haiwachukulii hatua wahalifu wanaokata miti ambao wengi hutoka nje ya kijiji chetu, na kwamba hawafahamu nini kimejificha nyuma ya pazia.
Mwenyekiti wa kijiji cha Makore, Simba Dimoso anakiri kuwepo kwa uharibifu wa msitu lakini anasema ni vigumu kuwakamata wahalifu. Anasema: “Hawa watu wengi hupita njia za milimani ambako hakuna barabara. Siyo rahisi kuwafuatilia na kuwakamata,” anasema Dimoso.
Anaongeza kuwa baadhi ya wanakijiji wanawafahamu watu hao wanaokata misitu ovyo, lakini hawaonyeshi jitihada za kuwadhibiti, ingawa ni wajibu wa kila mmoja kuzuia uhalifu huu.
Kupungua Misitu: Athari kwa mazingira na jamii
Jafar Kideghesho, Mtafiti katika masuala ya misitu, katika andiko lake, hali na Mwelekeo wa Ukataji Miti Ovyo Nchini Tanzania, Sababu zake, Athari zake na Hatua za Kuchukua (Realities of Deforestation in Tanzania – trends, drivers , implications and way forward), anasema athari za ukataji miti ovyo haziishii kwenye uharibifu wa mazingira tu bali huenda mbali na kuathiri uchumi wa jamii kwani misitu ni chanzo muhimu cha kipato na ajira hivyo hupunguza fursa za mtu mmoja mmoja au familia kujiingizia kipato au kupata ajira.
“Ukataji miti ovyo unapoteza uoto wa asili na hivyo kuchochea mmomonyoko wa udongo. Inakadiriwa kuwa asilimia 61 ya ardhi ya Tanzania imeingia katika hali ya jangwa na hivyo haina uwezo wa uzalishaji wa mazao ya kilimo,” anaeleza Kideghesho.
Anafafanua kuwa ukataji miti pia una athari kubwa kwa jamii zinazotegemea misitu moja kwa moja kwani licha ya kuharibu nyenzo muhimu za maisha, hupunguza uzalishaji wa chakula na upatikanaji wa maji.
Anasema uharibifu na upotevu wa misitu pia huwalazimisha watu kuhama na kutafuta maisha mapya baada ya mfumo wa maisha waliyozoea kuvurugwa na hivyo kukosa mahitaji muhimu.
Kideghesho anataja athari nyingine zinazosababishwa na ukataji miti ovyo kuwa ni kilimo kukosa tija kutokana na upotevu wa rutuba unaosababishwa na kutoweka kwa misitu, upungufu wa mvua, ukame, ongezeko la joto na pia huongeza makali ya athari za mabadiliko ya tabianchi ambayo huharibu bioanuai.
Nambalamoto, mkazi wa kijiji cha Viwanja Sitini katika Kata ya Mlimba Wilaya ya Kilombero anasema kufungua mashamba msituni kunakofanywa na wakulima wadogo hata kama ni shamba dogo la ekari moja, kunachangia uharibifu wa misitu.
Bila miti, hakuna ardhi yenye rutuba
Anafafanua: “Mara msimu wa mvua unapokwisha, mashamba hukauka kwani udongo hauwezi kuhifadhi unyevunyevu kwa kuwa hakuna tena mtiririko wa maji unaopita chini kwa chini kutoka msituni. Shida tunayoipata sasa hivi ni kwamba hatuna miti, ardhi haina rutuba na uzalishaji wa kilimo umepungua,” anasema Ndambalamoto.

Uharibifu wa misitu pia huathiri ustawi wa wanyama. Kwa mujibu wa taarifa ya Serikali 20, Tanzania ina aina mbalimbali za wanyama na mimea ambayo baadhi yake haipatikani sehemu nyingine yoyote ulimwenguni na kwamba upotevu wa misitu ambayo ndiyo makazi na vyakula vya wanyama hao umekuwa tishio la baadhi yao kutoweka.
“Misitu ya asili inabeba jukumu kubwa la kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, kujenga uchumi endelevu wa jamii na kuchochea ustahimili wa jamii katika kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi,” anaeleza Mchomvu.
Kwa ujumla, Kideghesho anasema kutoweka kwa misitu hakuathiri miti peke yake bali huharibu mazingira, huathiri bioanuai na vyanzo vya maji, na huvuruga uchumi na maisha ya jamii hasa zile zinazotegemea misitu moja kwa moja kwa maisha yao.
Ripoti za utafiti zinaonyesha kuwa matumizi ya kuni, mkaa na nishati nyingine chafu husababisha vifo vya watu kati ya 22,000 na 39,000 kila mwaka, wengi wao wakiwa wanawake na watoto. Vifo hivyo husababishwa na kuvuta hewa chafu (indoor air pollution).
Picha ya Bango: Biashara ya mkaa inatajwa kama sababu kubwa inayochochea watu kukata miti. Picha kwa hisani ya Ecohubmap.