- Wananchi walilalamikia mambo mengi, lakini hakuna hata moja liliwekwa kwenye ripoti.
- Tume imeleta mapendekezo ambayo kimsingi lengo lake ni kuua kabisa mashirika yanayofanya utetezi kwa jamii za asili za Wamaasai.
- Baadhi ya takwimu zilizotolewa na tume kuhusu ongezeko la mifugo “zilipikwa”.
- Mchakato wa tume haukulenga kusikiliza wananchi bali kuhalalisha maamuzi yaliyokwishafanyika.
Hili ni toleo la pili katika mfululizo wa makala kuhusu mgogoro wa Ngorongoro, Kaskazini mwa Tanzania. Soma toleo la kwanza hapa.
Baada ya tume mbili zilizoundwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan mwaka 2024, moja kuchunguza zoezi la kuhama kwa hiari kwa wakazi wa Ngorongoro na nyingine kuchunguza migogoro ya ardhi katika wilaya hiyo, kuwasilisha ripoti zake pamoja na kutoa mapendekezo, watu mbalimbali wametoa maoni yao.
Hawa ni pamoja na wenyeji wa wilaya ya Ngorongoro, wadau kutoka mashirika yasiyo ya kiserikali, Muungano wa Kutetea Haki za Wamasai (MISA), na wataalamu kutoka ndani na nje ya Tanzania. Baadhi wameyakataa mapendekezo ya tume hizo.
Charles Odero, Mwanaharakati na Mkurugenzi wa Shirika la Civil and Legal Aid Organization CILAO, ambaye amekuwa akipambania haki za binadamu katika eneo la Ngorongoro, anasema kuwa hajaridhishwa kabisa na mapendekezo ya tume zote mbili.
“Kama mdau sijaridhika na mapendekezo ya tume kwa sababu mbalimbali lakini moja ni kwamba yamehalalisha uporaji wa haki za jamii ya wafugaji wa asili (Wahadazabe, Wadatogana Maasai) ambao wanategemea ardhi ya Ngorongoro, Loliondo na Natron kama msingi na tegemeo la maisha yao,” anasema.

Akizungumzia suala la uhamaji wa hiari, Odero anakiri kuwa zoezi lilikuwa na kasoro nyingine na kushauri mapungufu hayo yaliyoainishwa na tume yafanyiwe kazi mara moja.
Pia alisisitiza kwamba haki itendeke hasa kwa wananchi ambao tayari walihama kutoka Ngorongoro. Anasema zile kaya ambazo wanaume walikuwa na wake zaidi ya watatu, basi zipewe haki ya nyumba, na siyo kuwekwa kwenye nyumba moja.
“Kama Tume imebaini hayo mapungufu, basi tunatarajia kuona Serikali ikichukua hatua mara moja kwa kuanza kurekebisha makosa hayo kwa wananchi ambao tayari wamehamishwa na wamepata madhila mbalimbali, kama waume wenye wake zaidi ya watatu kupewa nyumba moja, familia zenye vijana watatu waliooa kuhesabiwa kama kaya, bila kuwekwa kwenye fidia,” alisema Odero.
Waliodhalilisha wananchi wangewajibishwa
Dennis Moses, mwanasheria na mtetezi wa haki za ardhi katika wilaya ya Ngorongoro aliiambia Mongabay kuwa alikerwa na kitendo cha tume kutoeleza ni hatua gani zitakazochukuliwa dhidi ya watu waliosababisha zoezi la uhamaji kutokuwa shirikishi.
Dennis ambaye alikuwa mmoja wa mawakili walioongoza kesi ya Pori la Akiba la Parloleti iliyofunguliwa katika Mahakama ya Afrika Mashariki mwaka 2022 alisema alitarajia kusikia tume baada ya kubaini kasoro zilizofanywa, akitaka hao waliosababisha maumivu kwa wananchi wawajibishwe kwa kuchukuliwa hatua stahiki.
“Tangu mwanzo wa uhamishaji, wananchi tulisema kuwa zoezi hili siyo la hiari. Na sasa tume inayochunguza suala hili, imethibitisha hilo. Tume pia imesema Serikali ilikuwa ikitumia ushawishi badala ya kushirikisha.
“Kitendo cha wananchi kuondolewa huduma za kijamii, kufuta vijiji, kufuta vituo vya kupigia kura, vilikuwa vinalenga kuwaondoa wananchi kwa mateso.
“Lakini tume hizi zote hazikusema chochote, hazikueleza wahusika waliozuia huduma na kuwadhalilisha wananchi watachukuliwa hatua gani, alisema Dennis ambaye pia ni mkazi wa kijiji cha Endule katika tarafa ya Ngorongoro.
Kwa upande wake, Lanyori Kuya ambaye ni mkazi wa eneo la Alelilai anasema tume iliyoshughulikia suala la migogoro ya ardhi katika wilaya ya Ngorongoro iliegemea zaidi upande wa Serikali katika maoni na mapendekezo yake.
“Tume iliegemea upande mmoja. Kwa maoni yangu, matokeo ya uchunguzi huo ni kama wameweka nyama kwenye propaganda zilizokuwa zikiendeshwa tangu mwanzo. Hakuna sehemu ambayo tume ilichukua malalamiko ya wananchi.
“Sisi wananchi tulilalamikia mambo mengi sana, kwa mfano tulizungumzia suala la ardhi ya malisho kumegwa, tulieleza kuhusu Camp sites kujengwa kwenye maeneo ya malisho, lakini hakuna lalamiko hata moja tume imelizungumzia kwenye ripoti yake,” anasema Lanyori.
Eneo lingine ambalo wananchi wamelipinga ni kuhusu mapendekezo ya tume ya kuchunguza baadhi ya mashirika yasiyokuwa ya kiserikali. Tume ilidai kuwa baadhi ya mashirika huenda yanafanya ushawishi kwa wananchi ili kusiwe na utulivu katika eneo la Ngorongoro na ikapendekeza kuwa serikali iyachunguze.
Kuchunguza mashirika ni kutaka kuyaua
Hata hivyo, Odero, ambaye ni Mkurugenzi wa shirika la CILAO, amepinga vikali pendekezo la mashirika kuchunguzwa, akidai kuwa kufanya hivyo ni kunyamazisha mashirika yanayofanya kazi za utetezi wa haki za kiraia.
“Tume imeleta mapendekezo ambayo kimsingi lengo lake ni kuua kabisa mashirika yanayofanya utetezi kwa jamii za asili za Wamaasai, Wadatoga na Wahadzabe.
“Kama mmoja wa viongozi wa mashirika ya utetezi wa haki za binadamu, ninapinga vikali kabisa pendekezo hilo kwani taasisi hizi siku zote zinafanya kazi kwa mujibu wa sheria za nchi na kamwe kazi zetu zisichukuliwe kama ni uchochezi,” anasema Odero.
Kuhusu ukusanyaji wa taarifa, baadhi ya wananchi waliishutumu tume vikali wakisema haikujumuisha maoni yao.
“Wakati tume ya kushughulikia migogoro ya ardhi ilipofika katika eneo letu, ilitukataza sisi wananchi kurekodi mazungumzo baina yetu ili kuwe na kumbukumbu. Mimi nilihoji jambo hilo kwa sababu walipofika katika kata yangu (Alelilai) mimi nilikuwa mtu wa kwanza kutoa maoni lakini sikupewa majibu,” alisema Lanyori.
Maoni ya wananchi hayakuingizwa kwenye ripoti
Gabriel Kitende, mkazi wa Ngorongoro, alisema maoni yao hayakujuishwa kwenye ripoti. Alisema: “Tume zilikuja kutusikiliza sisi wananchi ili kujua kero zetu, lakini tumebaki midomo wazi kufuatia majibu ya tume hizi, mfano sisi wananchi, kero kubwa ni kunyimwa haki ikiwemo kufanyiwa uonevu ndani ya hifadhi. Sisi tunakamatwa, wakati mwingine mifugo inakamatwa, lakini haya hatujaona katika ripoti ya tume”.

Wananchi pia walipinga hoja kuhusu ongezeko la mifugo. Katika mazungumzo na Mongabay baadhi ya wakazi walisema hawajaridhishwa na takwimu zinazohusu ongezeko la idadi ya mifugo katika eneo la Ngorongoro.
Wanasema takwimu za tume hazina uhusiano na matukio ya ukame ambayo yamekuwa yakiikumba Ngorongoro katika miaka iliyopita ambapo jamii ilipoteza mifugo mingi.
Wengine walidai kwamba takwimu zilizotolewa na tume kuhusu ongezeko la mifugo, zilipikwa.
Julius Laitayok, mkazi wa kijiji cha Alelilai, anasema kuwa takwimu za mifugo pamoja na watu zilizotolewa hazina usahihi wowote.
Anasema: “Tawimu hizi hazina ukweli. Na ukiangalia tume zote zimependekeza kuwa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro iandae utaratibu maalum wa kuwasajili wenyeji, huu ni ushahidi kuwa serikali haiamini katika takwimu zake”.
Kwa upande mwingine Dennis Moses anasema takwimu za idadi ya mifugo iliyoongezeka siyo za kweli kwani kwa miaka na miaka wakazi wa Ngorongoro wamekuwa wakipoteza mifugo yao kutokana na ukame na kiangazi kikali kwa hiyo idadi ya mifugo imekuwa ikipungua.
“Hizo takwimu siyo za kweli kwa sababu ripoti ya jamii ya mwaka 2022 ilionyesha kuwa idadi ya mifugo iliyokuwepo mwaka 1959 imezidiwa na ile ya mwaka 2022 kwa idadi ya mifugo mitatu tu.
“Mwaka 2022 watu walipoteza sana mifugo katika nyanda za juu za Ngorongoro ikiwemo Nainokanoka na Alelilai…mwaka jana watu walipoteza mifugo katika eneo la Endulen na Kakesio. Maelfu ya mifugo ya na kufa lakini tume haikusema kama mifugo ilikufa,” alidai Dennis.
Aliongeza kuwa ripoti ya Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro ya mwaka 2017, ilionyesha kuwa wakazi wa Ngorongoro walipoteza mifugo kwa asilimia karibu 70 na kwamba siyo kweli kuwa mifugo imeongezeka kwa kiasi ambacho wanasema katika ripoti yao.
Mongabay ilifanikiwa kuona ripoti hiyo iliyochapishwa kwa ushirikiano kati ya Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro na German Cooperation (GIZ) ikisema kuwa mwaka 2017, zaidi ya ng’ombe 77,389, kondoo 78,490 na mbuzi 72,881 walikufa katika eneo la Ngorongoro pekee.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, mifugo iliyokufa ni asilimia 70 ya mifugo yote iliyokuwepo kwa kipindi hicho. Ripoti pia inataja kuwa mwaka 2009, asilimia 71 ya mifugo ilikufa katika kijiji vya Nainokanoka, Sinon na Sendui.
Kuhusu suala la kuondolewa kwa mfumo wa ardhi mseto, hatua iliyopendekezwa na tume, baadhi ya taarifa za vyombo vya habari zilisema kwamba iwapo ikitekelezwa, italeta taharuki kwa wananchi badala ya kutatua kilio chao ambacho ndicho kilipelekea tume hizo kuundwa.
Pia taarifa hizo zilidai kuwa mapendekezo haya kama yatatekelezwa, basi yatahalalisha watu kuondolewa kwa nguvu.
Mabadiliko ya sheria
Tume iliyokuwa ikichunguza mgogoro wa ardhi ilipendekeza mabadiliko ya sheria ili kuondoa dhana ya Ardhi Mseto (Multiple Land Use), mfumo ambao uliruhusu shughuli za binadamu na uhifadhi kwa pamoja.
Kuhusu pendekezo la eneo la Ziwa Natron kupandishwa hadhi na kuwa Pori la Akiba, wananchi walidai likitekelezwa, litaathiri wananchi wa Wilaya tatu za Ngorongoro, Longido na Monduli.
Msimamo wa MISA kuhusu Tume za Rais ripoti ya Ngorongoro

Muungano wa kutetea haki za Wamasai, Maasai International Solidarity Alliance (MISA), wao pia wamekuwa na mtazamo wao kuhusiana na matokeo ya uchunguzi wa tume hizo pamoja na mapendekezo yao.
Katika tamko “Msimamo wa MISA kuhusu tume mbili za Rais” walipinga vikali mapendekezo ya tume zote mbili wakidai kuwa hayazingatii maoni ya wananchi na kwamba yanaweza kuongeza migogoro badala ya kuitatua.
Katika tamko hilo lililotolewa Machi 18, 2026, siku tano baada ya kuwasilishwa kwa ripoti za tume hizo Machi 12, 2026, MISA ilisema kuwa baada ya kufanya tathmini ya kina, wamefikia uamuzi wa kuyakataa mapendekezo ya tume hizo, lilisema tamko la MISA lililokaririwa na vyombo mbalimbali vya habari.
Miongoni mwa hoja zilizotolewa na MISA katika tamko lao ni kwamba mchakato wa tume hizo ulikuwa na kasoro tangu mwanzo, na kwamba haukulenga kusikiliza wananchi bali kuhalalisha maamuzi yaliyokwishafanyika wakati malalamiko ya wakazi, hayakufanyiwa kazi.
“Tangu mwanzo, masharti ya kazi ya tume yaliundwa ili kuhalalisha maamuzi yaliyokuwa tayari yamefanyika. Tume zote mbili zilijikita zaidi katika namna ya kutekeleza uhamishaji kutoka Tarafa ya Ngorongoro badala ya kushughulikia matatizo yaliyowasilishwa na wakazi,” limeeleza tamko hilo.
MISA walisema kuwa ripoti za tume hazikuwa na uhuru wala siyo za kuaminika katika kutathmini hali halisi ya wananchi wa Ngorongoro, Loliondo, Sale na Msomera.
Inadai kuwa tume hizo kwa kiasi kikubwa zilitegemea nyaraka za sera zilizowahi kupingwa na kurudia sababu ambazo zimekuwa zikitumika kuhalalisha kuondolewa kwa wafugaji wamasai katika ardhi yao ya asili.
Aidha, tamko hilo la MISA limeeleza kuwa hitimisho la tume hizo liliegemea kwenye takwimu zenye upungufu na upendeleo.
“Hitimisho lililotolewa linategemea makadirio yaliyopitiliza ya idadi ya watu, matumizi ya takwimu zisizo sahihi kuhusu binadamu, mifugo na wanyamapori, pamoja na migongano mikubwa ya kimaslahi ya taasisi, huku likipuuza ushahidi wa kisayansi unaopinga na mitazamo ya serikali,” limefafanua tamko hilo.
Katika hatua nyingine, MISA wamepinga vikali hoja kwamba uwepo wa Wamasai (watu) ni tishio kwa uhifadhi wa mazingira, ikisisitiza kuwa jamii hizo zimeishi kwa muda mrefu kwa kushirikiana na wanyamapori.

“Kwa vizazi vingi, sisi Wamasai tumeishi Ngorongoro kwa mfumo wa kuishi pamoja na wanyamapori. Maisha yetu ya ufugaji si tishio kwa uhifadhi, kinyume chake, maarifa yetu ya jadi na mifumo ya matumizi ya ardhi ya kijamii imekuwa ikiendeleza mfumo huu wa ikolojia kwa karne nyingi,” lilieleza tamko hilo.
Katika sehemu nyingine, MISA walikemea kitendo cha tume hizo kutoihoji serikali kwa kuondoa baadhi ya huduma za kijamii katika eneo la Hifadhi ya Ngorongoro, jambo lililopelekea baadhi ya wakazi kukubali kuondoka kutokana na kukosa huduma muhimu.
MISA pia wamelaani ukimya wa tume hizo kuhusu madai ya unyanyasaji dhidi ya Wamasai, ikisema hali hiyo inaashiria upendeleo. Pia imeeleza wasiwasi wake kuhusu matukio ya hivi karibuni ya ukamataji wa wakazi na kuamriwa kuondoka katika maeneo yao ili kupisha shughuli za utalii.
Kuhusu Ziwa Natron, MISA wamepinga vikali mapendekezo ya kuligeuza kuwa hifadhi ya wanyamapori, ikisisitiza kuwa eneo hilo ni ardhi ya vijiji kwa mujibu wa sheria za Tanzania.
“Tunapinga kauli kwamba Ziwa Natron ni Eneo la Hifadhi ya Wanyamapori (GCA). Eneo hili lina vijiji 26 na zaidi ya watu 70,000, na kwa mujibu wa sheria za Tanzania, hakuna GCA inayoweza kuanzishwa katika ardhi ya vijiji,” sehemu ya tamko la MISA ilieleza.
Wamesisitiza msimamo wao wa kupinga uhamishaji wa aina yoyote kutoka katika maeneo yao. “Tutaendelea kusimamia haki yetu ya kubaki na kuishi katika maeneo haya,” limeeleza tamko hilo, huku likitoa wito kwa serikali kutambua na kulinda haki zao.
Namna ya kupata suluhisho kutoka wananchi
Wakizungumzana Mongabay, wakazi na wadau wa Ngorongoro wametoa maoni yao kuhusu nini kifanyike ili kupata suluhisho la kudumu la mgogoro wa Ngorongoro.
Wanasema, kwanza Serikali inatakiwa iendelee kuzungumza na wananchi ili kuwa na makubaliano yanayozingatia maslahi ya makundi yote yanayoguswa na mgogoro huu.
“Wadau tukae tuzungumze na tukubaliane kuhusu namna ya kuendesha mambo kwa kuheshimiana. Tunahitaji utalii, uhifadhi, nyama, maziwa, ngozi na ustawi wa Wahadzabe, Wamaasai na Wadatoga.
“Ukiondoa kimoja vyote vinatoweka kwani uwepo wa jamii hizi ndani ya Ngorongoro, Loliondo, Lake Natron ni kichocheo cha ulinzi wa maeneo hayo na wanyama waliopo,” anasema Odero.
Kwa upande wa Gabriel anasema endapo serikali itaondoa wakazi wa Ngorongoro, eneo hilo litaharibika. Anasema: “Ukisema unataka kulinda urithi wa Dunia, unaulindaje kwa kuwafukuza Wamasai? Ukitaka kuharibu Ngorongoro, basi ondoa watu.
“Utabakiwa na mchanga tu. Wanyama, vyanzo vya maji na misitu vyote vitatoweka. Wananchi wa Ngorongoro ndiyo waliolinda urithi wa eneo hilo siku zote. Kama serikali inataka kulinda urithi huu, izungumze na wananchi”.
Maoni ya wataalamu huru kutoka Uganda, Kenya na Tanzania
Kuhusiana na mapendekezo ya tume hizo mbili, wataalamu mbalimbali kutoka Tanzania pamoja na nje ya nchi wametoa maoni yao.
Akizungumzana Mongabay, Mkurugenzi wa Mamlaka ya Usimamizi wa Mazingira nchini Uganda (NEMA), Dr. Akankwasah Barirega alikiri kwamba ongezeko la watu na mifugo litaleta ushindani wa kutumia rasilimali zilizopo.
“Kwa sababu ardhi inabaki kama ilivyo, huku idadi ya watu ikiongezeka, ni wazi kuwa kutakuwa na ushindani wa maeneo bila shaka. Hata ukisema utasimamia ongezeko la wanyama, lakini ongezeko la mifugo pamoja na watu litaleta ugomvi wa kupambania rasilimali iliyopo.
“Ni muhimu serikali kufanya maamuzi kabla malengo ya muda mrefu ya uhifadhi hayajapotea. Ni rahisi kuhamisha mifugo na watu, lakini siyo rahisi kuhamisha wanyamapori,” alisema Dr. Akankwasah.
Akizungumzia uhamaji, alisema suala hilo linatakiwa kuangaliwa kwa makini ili kuepuka matokeo hasi yanayoweza kuleta athari kwa maisha na uchumi wa kaya zinazohamishwa.
Michael Onduto, Mtaalamu wa Sayansi ya Mazingira kutoka nchini Kenya, anasema kitaalamu inaonekana jamii za asili zina mchango mkubwa sana katika kutunza ikolojia ya eneo hilo.
Kwa jicho la kitaaluma na haki za binadamu, hali hii (mgogoro) inaonyesha mvutano kati ya njia za utunzaji wa mazingira na mtazamo wa utunzaji mazingira unaohusisha jamii.
Licha ya kuwa ongezeko la watu na mifugo lina misingi ya kisayansi, lakini ushahidi unaonyesha kuwa kutenga jamii za asili ni njia isiyo endelevu.
Njia za kiutamaduni za jamii kama Wamasai na mbinu zao za ufugaji zimeleta mizania sahihi kwenye suala la uhusiano wa wanyama, na kuwaondoa wao kutapunguza uimara wa jamii na mazingira wa jamii husika.
Akieleza namna bora ya kuhakikisha kuna ushiriki wa jamii hizi, Onduto anasema kuwa Serikali, jamii, pamoja na wadau wa mazingira, kwa pamoja wanatakiwa kupanga na kufanya maamuzi ili kuimarisha maelewano na kuaminiana.
“Njia ya ushirikishwaji wa jamii katika utunzaji inatakiwa kupewa kipaumbele, na kuhakikisha kuwa jamii hizi zinahusika katika kupanga na kusimamia. Usimamizi wa pamoja ambapo jamii, serikali na wadau wanashirikiana katika kufanya maamuzi, kutapunguza migogoro na kuongeza imani baina yao,” anasema Onduto.

Leonard Chakupewa, Mtaalamu wa Mazingira kutoka Tanzania anasema ongezeko la idadi ya watu pamoja na idadi ya mifugo kwa namna yoyote ile lazima vitaleta athari hasi au chanya.
“Kunapokuwa na ongezeko la watu, moja ya mambo ambayo huanza kuonekana ni kuharibika kwa makazi ya wanyama, kwasababu watu wanavyoishi wanahitaji kuchangamana na wakati mwingine, wanahitaji njia kutoka sehemu na kufika sehemu, Barabara zitajengwa ambazo watu watatumia kuingia na kutoka kwenye hifadhi kwa kutumia vyombo vya moto.
“Sasa shughuli hizi zote zinapofanyika katika yale maeneo nyeti kama mazalia ya wanyamapori au makazi yao, hupelekea maeneo hayo kuharibika,” anasema Leonard.
Anasisitiza kuwa jamii hizi zinahitaji kuhusishwa ipasavyo kuleta suluhisho. Anasema ni vema wananchi wenyewe waulizwe wanaonaje kuhusu uhifadhi wakati idadi yao na mifugo yao inapoongezeka.
“Nasisitiza sana jambo la ushirikishwaji wa jamii zenyewe kupitia majukwaa mbalimbali kama vikao vya wazi, mabaraza lakini pia uandaaji wa vikao. Vyote vizingatie kuheshimiana na kusikilizana. Mambo haya yanapokelewa kwa mitazamo mingi, kwa hiyo matumizi ya nguvu au vitisho si mazuri.
“Njia hizi zinaweza kuondoa watu lakini si nzuri katika kuleta utengamano na utu. Hawa ni Watanzania wenye akili na utashi ambao wanaweza kusikiliza, kupendekeza na kushauri. Nafikiri kuna umuhimu wa kujadiliana kwa pamoja,” anasema Leonard.
Msimamo wa Serikali
Akipokea ripoti za tume hizo mbili, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan aliahidi kufanyia kazi mapendekezo na kasoro zilizoelezwa katika ripoti za tume hizo.
“Taarifa hizi pia zimetupa taswira ya uhamaji wa hiari kutoka Ngorongoro kwenda vijiji vya Msomera, Kitwai B na Saunyi na maeneo mengine.
“Nasi tumezisikia changamoto, tumesikia kwamba serikali tulifanya zoezi kwa nia njema lakini tulikosea baadhi ya maeneo. Hayo sasa ndiyo maeneo ya kukaa, kutafakari na kurekebisha,” alisema Rais Samia wakati akipokea ripoti.
Picha ya Bango: Upana wa ardhi ya Ngorongoro unawapa nafasi wafugaji kufuga kwa uhuru. Kutokana na suala la mifugo kuongezeka, ushindani unaongezeka kati ya eneo la malisho ya mifugo na maeneo ya uhifadhi. Picha na Dominic Allen.