- WRTI imehamia mfumo wa CBET ili kuwajengea wahitimu ujuzi wa vitendo unaohitajika sokoni.
- Wahitimu 499 walitunukiwa vyeti, huku mpango wa RPL ukitambua ujuzi wa uzoefu.
- Ufadhili wa masomo na juhudi za upandaji miti zinaimarisha ajira kwa vijana na uhifadhi wa mazingira.
Taasisi ya Utafiti na Mafunzo ya Wanyama pori ya Kenya (WRTI) imefanikiwa kuhamia katika mfumo wa elimu na mafunzo unaozingatia umahiri (Competency-Based Education and Training), ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuandaa wataalamu ambao hawaelewi tu uhifadhi, bali pia wana ujuzi wa vitendo wa kulinda wanyama pori na rasilimali asilia za Kenya.
Mkurugenzi na Mtendaji Mkuu wa WRTI, Patrick Omondi, alielezea hatua hiyo kama sehemu ya juhudi za kitaifa za kuimarisha uwezo wa kitaalamu katika uhifadhi na usimamizi wa wanyama pori, sambamba na kuhamia kutoka mfumo wa nadharia kwenda katika mbinu za vitendo zinazoendana na mahitaji ya soko la ajira.
Omondi alitangaza mabadiliko hayo wakati wa mahafali ya 23 ya taasisi hiyo yaliyofanyika Machi 27, ambapo wahitimu wapatao 499 walitunukiwa vyeti. Mhitimu mmoja ambaye alifariki dunia kabla ya mahafali hayo, alitunukiwa cheti kwa heshima.
“Tumepitia upya mitaala yetu ili kuhakikisha inabaki kuwa na uhalisia, na tunaendelea kuimarisha ushirikiano na wadau muhimu ili kuongeza ubora wa mafunzo na kuongeza fursa za ajira kwa wahitimu wetu.
“Mapitio yanayoendelea ya programu za ngazi ya tano yataendelea kutuunganisha na mfumo wa kitaifa wa TVET na kuwezesha wanafunzi wetu kuendelea na masomo kwa urahisi,” alisema Omondi katika hafla hiyo iliyohudhuriwa na wadau wa uhifadhi kutoka serikalini, sekta binafsi na mashirika yasiyo ya kiserikali.
Baadhi ya wanufaika wa kozi fupi zilizozinduliwa hivi karibuni, zinazolenga kuwajengea uwezo wataalamu wa sekta ya wanyamapori, ni pamoja na waongoza watalii, ambao wanatarajiwa kuthibitishwa na Mamlaka ya Udhibiti wa Utalii ya Kenya (TRA).
Ili kuhimiza ushirikiano kati ya uhifadhi rasmi na ule unaoongozwa na jamii, hasa jamii za asili, WRTI pia imetangaza kuanza kutekeleza mpango unaoitwa “Utambuzi wa Ujuzi Uliopatikana kwa Uzoefu” (Recognition of Prior Learning), ambao utatambua rasmi ujuzi uliopatikana kupitia uzoefu wa vitendo.
Omondi alisema: “Mpango huu ni muhimu sana hasa kwa watu wanaofanya kazi katika hifadhi zinazosimamiwa na jamii, waongoza watalii, na sekta nyingine zisizo rasmi ndani ya sekta ya wanyama pori. Kwa kuthibitisha ujuzi huu, tunaongeza fursa za ajira, kukuza ushirikishwaji, na pia kuimarisha uwezo wa jumla wa nguvu kazi.”
WRTI pia ni miongoni mwa wanufaika wa ufadhili wa serikali kupitia Mfuko wa Utalii Tourism Revolving Fund, ambao utawezesha wanafunzi wenye uhitaji kupata mikopo ya masomo, fursa ambayo hapo awali ilikuwa ikitolewa kwa wanafunzi wa vyuo vikuu vya umma pekee.
“Wizara imeanzisha Mfuko wa Mzunguko wa Utalii unaofadhiliwa na Mfuko wa Utalii na kusimamiwa na Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu (HELB). Lengo la mpango huu ni kusaidia wanafunzi wenye uhitaji wanaosoma kozi za uhifadhi na utalii.
“Wanafunzi wa taasisi hii ni wanufaika wa utaratibu huu. Hata hivyo, fedha zilizotengwa bado ni kidogo ukilinganisha na uhitaji, na tunaiomba Serikali kuongeza ufadhili zaidi,” alisema Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati Sylvia Museiya, katika taarifa aliyoisoma kwa niaba ya Waziri wa Utalii, Rebecca Miano.

“Hadi sasa, zaidi ya $26,247 (KSh15 milioni) zimeshatolewa, jambo lililopunguza mzigo wa kifedha kwa wanafunzi na kuwezesha vijana wengi zaidi kufuata taaluma katika sekta ya wanyamapori,” alisema Omondi.
Kama kituo cha kitaifa cha ukuzaji miche ya miti, WRTI pia kinashiriki katika mpango wa serikali wa kupanda miti bilioni 15, ambapo tayari kimepanda miche zaidi ya 260,000 ya miti ya asili katika maeneo mbalimbali ya uhifadhi nchini.
WRTI ni shirika la serikali lililoanzishwa mwaka 2013 kwa lengo la “kuratibu tafiti kuhusu wanyama pori na kutoa takwimu na taarifa za kina zitakazosaidia kupatikana kwa suluhisho za kisayansi zinazochangia kwenye maamuzi ya sera, mbinu za usimamizi, na ubunifu katika utengenezaji wa bidhaa na utoaji wa huduma zinazotegemea rasilimali za wanyama pori.”
Majukumu yake mengine ni “kuimarisha uwezo katika uhifadhi na usimamizi wa wanyama pori kupitia mafunzo.”
Picha ya bango: Shamra shamra wakati wa mahafali ya 23 ya Taasisi ya Utafiti na Mafunzo ya Wanyama pori ya Kenya (WRTI). Picha na Lynet Otieno, Mongabay.