- Jamii ya Baomo katika Kaunti ya Tana River inaishi kwa maelewano ya karibu na tumbili walio hatarini kutoweka kwa kutumia nyimbo za jadi, mawasiliano ya kijamii na mbinu zisizo na madhara.
- Hifadhi ya Jamii ya Ndera, iliyoanzishwa mwaka 2010, ina jukumu muhimu katika kulinda misitu, wanyamapori na rasilimali za ardhi kupitia usimamizi wa moja kwa moja wa wanajamii.
- Licha ya juhudi hizi, tumbili wanakabiliwa na changamoto kubwa kama ukataji miti, upanuzi wa kilimo, uwindaji haramu na athari za mabadiliko ya tabianchi.
- Ushirikiano kati ya jamii na watafiti, pamoja na matumizi ya teknolojia na mbinu ya One Health, unaongeza matumaini ya kuhifadhi spishi hizi na kuboresha uhusiano kati ya binadamu, wanyamapori na mazingira.
TANA RIVER, Kenya – Ni siku ya Jumamosi, majira ya asubuhi. Kwa mbali jua limeanza kuchomoza juu ya msitu wa Tana River, na kijiji cha Baomo kinaanza kuamka polepole. Ukimya wa asubuhi unapambwa na sauti za ndege.
Ili kuingia katika kijiji hicho, kilichozungukwa na msitu, kuna njia nyembamba inayokatiza msitu na mashamba, ambayo inaelekea Baomo. Njia hiyo ya asili imeundwa kupitia shughuli za kila siku za binadamu, magari, baiskeli na pikipiki zinazoitumia mara kwa mara. Pia kuna wanyamapori wanaotumia njia hiyo wakienda kutafuta maji na malisho.
Mongabay iliona kinyesi cha ndovu kilichokuwa kimesambaa barabarani na kukauka, huku vingine vikiwa bado vibichi na vikitoa harufu kali. Mbegu za mimea na majani yaliyosagika yalionekana ndani ya kinyesi hicho kilichokuwa ardhini. Kwa wakazi wa Baomo, kinyesi hicho si uchafu bali ni ujumbe kuwa wanaishi kwa ukaribu na wanyamapori wakubwa zaidi barani Afrika: ndovu.
Kijiji cha Baomo kilichoko katika Kaunti ya Tana River, pwani ya Kenya, kipo karibu na Mto Tana na kimezungukwa na msitu unaohifadhi wanyamapori mbalimbali, wakiwemo fisi, tumbili, ndovu, nyati, dikdik, nyani, twiga, ndege, nyoka na wanyama wengine.
Mpalawasi hawezi kukudhuru

Matawi ya miti yalipoanza kutikisika mbele yangu, Mwanahamisi Kandugu Sidi, mama wa umri wa miaka 65, aliyekuja kunipokea, aliniambia: “Mwanangu usiogope, wala usihofu. Hao ni tumbili ambao pia ni jamii yetu. Sisi kama jamii ya Pokomo tunawaita ‘Mpalawasi’. Hatakudhuru kabisa, anasubiri nimwimbie wimbo wake afurahie aende zake. Subiri nimwimbie: ‘Mpalawasi niagize kipala oh oh! Niagize kipala! Mpalawasi niagize kipala oh oh! Niagize kipala!’”
Mpalawasi ni aina ya tumbili ambaye kwa Kiingereza hujulikana kama Tana River Red Colobus (Piliocolobus rufomitratus), ambaye pia ameorodheshwa kuwa hatarini kuangamia duniani.
Kwa Mwanahamisi, wimbo huo unatoka katika jadi ya mababu zake. Anasema wimbo huo unakusudia kumwambia tumbili huyo amwonyeshe upendo.
“Mpalawasi wanaelewa lugha yetu ya kiPokomo. Sisi wanakijiji tukiwaona huwaimbia na wao hukaa wakituangalia, huku wakigusa utosi wao, ambao una manyoya yaliyolala vichwani kama vile wamevaa kofia. Wao hurukaruka na kuketi wakituangalia. Sasa tunaishi kama ndugu,” anasema Mwanahamisi.

Kwa wakazi wa Baomo, tumbili si wageni. Ni majirani wa kila siku, wakazi wa muda mrefu wa misitu ya asili inayozunguka kijiji hiki cha pembezoni mwa Mto Tana. Hapa pia kuna tumbili ambaye ameorodheshwa kuwa hatarini kuangamia. Anaitwa Tana River Crested Mangabey (Cercocebus galeritus) au “Karao magongo” kwa kiPokomo.
Wanapoambiwa wasiharibu mazao, hutii
Tumbili hawa hupatikana katika Kaunti ya Tana River pekee. Kwa mujibu wa wakazi wa Baomo, wana uwezo wa kusikia na kuelewa wanaposemeshwa, kwani wanapoambiwa wasiharibu mazao, hutii na kuondoka.
“Kila tunapotumia njia ya mazungumzo, au kugonga mitungi pamoja, tumbili hao huogopa na kwenda. Hapa hatuwaui wala kuwadhuru. Hata siwezi kuhamia kwingine ama katika kaunti nyingine humu nchini. Siwezi kuwasaliti hawa wanyama; nitaendelea kuishi nao hapa hapa,” anasema Mwanahamisi.
Anawapa mafunzo ambayo yamepitishwa kwa miaka mingi, kutoka kizazi kimoja hadi kingine.
“Nina wajukuu saba na wote hao ninawapitisha kwenye mafunzo ya jadi ambayo nami pia nilijifunza kutoka kwa wazazi wangu. Nawafundisha jinsi ya kuishi na hawa tumbili,” anasema Mwanahamisi.
Kalian Egarise, ambaye anajihusisha na ukulima, aliambia Mongabay kuwa wao hutumia mbinu za kijamii kuzuia uvamizi wa mashamba yao unaofanywa na wanyamapori wengine pamoja na nyani. Anasema huzungushia ua mashamba yao kuzuia wanyama wadogo, wakiwemo mpalawasi na karao magongo kuyavamia.

“Tunatumia miti midogo midogo kuzungusha ua katika mashamba yetu, ili kuzuia wanyama wadogo kuvamia mashamba yetu. Lakini kuzuia uvamizi wa ndovu, tunatumia waya. Pia huwa tunawasha moto kandokando ya mashamba ili kufukuza wanyama hao. Sisi hatuwadhuru. Hapa utalii unaweza kuimarika sana kwa sababu tunawalinda sana wanyama. Hii ndio imetupelekea kuunda Hifadhi ya Jamii ya Ndera,” anasema Egarise.
Wakazi wa Baomo bado wanaheshimu tumbili kama sehemu ya urithi wa asili.
Mwaka 2010, Hifadhi ya Jamii ya Ndera, ambayo ni kilomita za mraba 150 (hekta 15,000), iliundwa na jamii ikapewa jukumu la kusimamia rasilimali zao kwa njia endelevu. Hifadhi hiyo inahusisha vijiji vitano ambavyo ni Baomo, Kitere, Mnazini, Mvungeni na Kinyadu.
Msimamizi wa kijiji cha Baomo, Saidi Komora, amesema baadhi ya rasilimali zinazohifadhiwa ni pamoja na wanyamapori, misitu na ardhi. “Hii ardhi ya Ndera ni ya jamii. Wao hufanya mikutano miwili kwa mwezi ili kuzungumzia jinsi ya kulinda hifadhi hiyo,” anasema.

Kwa wakati mmoja, akiwa na umri wa miaka 13, Komora alikuwa anajihusisha na uwindaji haramu. Kwa sasa, yeye ni mwanaharakati wa kutetea wanyama hao wa pori.
“Nilikuwa mwindaji haramu sugu. Nilifanya hivyo tangu nikiwa darasa la saba nikitafuta ada ya shule. Niliendelea hivyo hadi nikamaliza kidato cha nne. Siku moja nilikamatwa na maafisa wa kulinda wanyamapori wa KWS. Ilinibidi niombe msamaha na nikawaahidi kuwa nitatoa hamasa kwa jamii kuhusu umuhimu wa kuhifadhi wanyama hawa. Pia nilitembea katika vijiji vyote vitano kuhamasisha watu juu ya umuhimu wa kuwatunza wanyama na misitu. Hivyo ndivyo maisha yangu yalivyobadilika,” Komora anasimulia.
Walikuwa wawindaji haramu wamebadilika
Komora na wenzake saba ambao hapo awali pia walikuwa wawindaji haramu, wamebadilika na wanajihusisha na ukulima. Anasema: “Wanakijiji waliona uwajibikaji wangu na namna nilivyobadili mwenendo wangu… ndio maana niliteuliwa kuwa kiongozi katika masuala ya hifadhi.”
Dhado ni askari wa jamii anayelinda Hifadhi ya Jamii ya Ndera. Yeye ni miongoni mwa vijana 12 waliochaguliwa na wakazi wa Baomo kulinda rasilimali yao tangu mwaka 2017. Askari hao wanatoka kwa kila kijiji na wamewezeshwa kwa mafunzo kutoka Manyani, iliyoko katika Kaunti ya Taita-Taveta.

Anasema tumbili hao wamepungua kwa kuwa wanatorokea maeneo mengine kutokana na shughuli za ukulima katika kijiji. Pia uhaba wa mvua unaochangiwa na mabadiliko ya tabianchi umesababisha tumbili hao kukosa malisho na wengine wanaliwa na wanyama kama vile nyani na chatu.
“Wakazi wengi walivamia msitu na kukata miti ili kuandaa maeneo kwa ajili ya mashamba. Hatua hii iliharibu sana makazi ya tumbili hao. Hiyo ni kama miaka 10 iliyopita. Tuliingilia kati na kuwapa wenyeji mafunzo kuhusu uhifadhi wa misitu,” anasema Dhado.
Hifadhi ya kijamii ya Ndera imezungukwa na misitu ya Sifa, Kimbu, Kambini, Luthenye, Buluchani, Lalafitu, Baratiro, Lemu, Boboa na Changaraweni. Misitu ya Lalafitu, Kimbu na Sifa ni makao ya tumbili hao, na pia ni misitu ambayo jamii haiwezi kumruhusu mtu yeyote kuivamia na kukata miti kwa minajili ya mkaa au mbao ama kuandaa mashamba.
Said Roba Hirbae ni mtaalamu wa nyanjani katika msitu wa Tana River kwenye Taasisi ya Utafiti wa Primata nchini Kenya (KIPRE). Taasisi hii imepewa jukumu la kushughulikia utafiti wa afya ya binadamu kupitia utafiti wa magonjwa ya wanyama, hasa Primata na pili kulinda na kuhifadhi Primata nchini Kenya.

KIPRE inashughulikia spishi 21 za Primata nchini, zikiwemo mpalawasi na karao magongo, ambao wote wako katika hatari zaidi kuangamia duniani. Hili ni shirika la kipekee linalofanya utafiti wa Primata na uhifadhi hawa tumbili nchini Kenya.
Kufuatilia tumbili ndani ya msitu
Hirbae anasema kazi yake kubwa ni kufuatilia tumbili hao kwa ukaribu ndani ya msitu akiangalia chakula ambacho wanakula.
“Kitu tunachoangalia katika chakula wanachokula ni miti wanayoitumia. Tunaichukua miti hiyo waliyokula, tunaikausha halafu tunaiandaa kwa ajili ya kuiwasilisha kwenye Makumbusho ya Kitaifa ya Kenya. Baadhi ya miti wanayopenda kula ni pamoja na mbuyu, mkoma, mtari, mkuru na mguvu. Hii ni baadhi ya miti ambayo inaliwa sana,” Hirbae anaiambia Mongabay.
Sambamba na hilo, wanafanya zoezi la kujua idadi ya tumbili hao kila mara ili takwimu ziweze kuwafahamisha kuhusu ongezeko au upungufu wa wanyama hao, na pia kufahamu mienendo, tabia na uwepo au ukosefu wa chakula chao msituni.
Kipindi cha kiangazi kilichoendelea kwa zaidi ya miezi kumi hadi Februari kilichangia kuongeza shinikizo kwa malisho yao na pia kuongeza uwindaji haramu wa tumbili hao katika maeneo ya Tana ya chini.
Pia KIPRE inatumia teknolojia ya GPS ili kuangalia jinsi tumbili hao wanavyotembea na ni maeneo gani ya misitu wanakwenda kila siku, na kwa nini. Na pia wanaangalia mwenendo wa kitabia wanapokuwa juu ya miti au wanapokuwa wanakula matunda na mizizi ardhini.
“Mimi huanza kufuata tumbili hao kuanzia asubuhi saa kumi na mbili na nusu na nafanya hivyo hadi saa kumi na moja jioni. Kesho yake nitaenda pale kwa usaidizi wa kubonyeza GPS. Hawa wanyama wanatembea mwendo wa kasi sana,” anasema.
Mpalawasi ni nadra kushuka chini; wao ni warukaji hodari kutoka kwenye mti mmoja hadi mwingine, ila wao hushuka pale wanapolazimika kuvuka kwenda kwenye upande mwingine wa msitu. Karao magongo nao hutumia muda wao sana ardhini.
Licha ya umuhimu wake wa kiikolojia, Mpalawasi na Karao magongo wanakabiliwa na vitisho vingi, vikiwemo uharibifu wa makazi yao ya asili, ongezeko la shughuli za binadamu na mabadiliko ya matumizi ya ardhi katika Bonde la Mto Tana.
Mkusanyiko wa changamoto hizi umesababisha shirika la IUCN kuorodhesha tumbili hawa kama spishi iliyo hatarini kutoweka, na unatoa wito wa dharura kwamba juhudi madhubuti za uhifadhi ni lazima zichukuliwe kabla hazijapotea kabisa.
“Spishi hii ipo katika hali ya kutoweka, kwa sababu mabadiliko ya tabianchi yanachangia na pia idadi ya wanakijiji imeongezeka. Hata misitu ambayo ingeweza kubeba hawa wanyama imeanza kukatwa kwa ajili ya mashamba.
“Sasa hivi msituni kumekuwa na madoa. Kwa mfano, ukitoka vijiji kama Kajitupe kuelekea Mchelelo hadi Sifa, misitu imeshikana, lakini ukielekea kijiji cha Kiliwalani, ni mashamba. Misitu ambayo ilikuwa inaficha hawa wanyama ni kama inaisha kwa sasa,” anasema Hirbae.
Hirbae anaongeza kuwa Karao magongo amepungua sana kufuatia kukatwa kwa miti. Anasema: “Mimi naona kuwa mangabey ameathirika sana kwa kuwa anatembea mita 800 kila siku porini, ikilinganishwa na mpalawasi ambaye anaruka mitini. Inakadiriwa wanaruka kati ya mita 150 hadi 200 kila siku”.
Spishi hii imeainishwa na shirika la kimataifa la IUCN kuwa katika hatari kubwa ya kutoweka, kulingana na orodha yake ya viumbe vilivyo hatarini ya mwaka 2019. Mpalawasi na Karao magongo ni miongoni mwa nyani 25 walio katika hatari kubwa ya kutoweka.

Licha ya hayo, kuna nuru inachomoza gizani. Uwepo wa hifadhi ya kijamii ya Ndera umewafanya tumbili hao kuwa salama, na wanavijiji wanashirikiana kufanya maamuzi kabla ya kugusa hifadhi ya wanyama hao. Kadhalika, wanajamii wameanza juhudi za kurejesha mazingira, na pia kuendelea kuhamasishwa juu ya umuhimu wa kuwahifadhi.
Mengine yanayotia moyo ni ufugaji wa mbuzi wa kisasa aina ya Gala na ukuzaji wa mbegu zinazonawiri na kutoa mavuno kwa mvua kidogo inayopatikana kufuatia mabadiliko ya tabianchi.
KIPRE pia imeanza mbinu ya One Health inayoangalia mwingiliano na uhusiano uliopo kati ya afya ya binadamu, afya ya wanyamapori na mifugo kwa lengo la kukabiliana na magonjwa, hasa yale yanayosambaa kutoka kwa wanyama hadi kwa binadamu.
Thamani ya kinyesi cha tumbili
“Tunakusanya kinyesi cha tumbili hao, tunaweka Formaline na Ethanol halafu tunapeleka kwenye maabara kwa ajili ya uchunguzi zaidi. Kisha tunakwenda kwa jamii kuchukua takwimu na pia wanakubali kutupa kinyesi chao ili kwenda kupima. Zoezi hili litatusaidia kujua milipuko hii ya magonjwa inatokea wapi kila mara. Mradi huu umekuwa ukiendelea kwa muda wa miaka mitatu sasa,” anafafanua Hirbae.
“Tumbili hawa ni muhimu sana, na wameanza kukimbilia katika misitu midogo midogo kwa sababu makazi yao sasa imeanza kuharibiwa na ukataji wa miti kwa sababu ya mashamba. Ninawashauri wakaazi wa Ndera, kutoharibu makazi ya hawa tumbili na wanyamapori kwa jumla,” Hirbae anatamka.
Wakati safari ya Mongabay katika eneo hili ilikamilika, ilikuwa dhahiri kuwa kuna uwezekano mkubwa wa mwanadamu na wanyamapori kuishi kwa maelewano.
Katika nyimbo za jadi zinazopitishwa toka kizazi kimoja hadi kingine, kuna hekima ya kale inayotukumbusha kwamba uhifadhi hauanzi kwa sheria pekee, bali kwa uhusiano wa karibu, heshima na utamaduni.
Kadri misitu ya Tana inavyoendelea kukabiliwa na shinikizo la kibinadamu na mabadiliko ya tabianchi, mustakabali wa mpalawasi na karao magongo utategemea zaidi maamuzi ya leo: kulinda au kupoteza.
Na pengine, katika sauti za kina mama kama Mwanahamisi wanapoimba, kuna tumaini kwamba kizazi kijacho hakitasimulia hadithi za viumbe waliopotea, bali kitaendelea kuziimba wakiwa hai, jirani zao wa kila siku.
Picha ya bango: Tana River Mangabey wakiwa katika msitu mmoja katika Kaunti ya Tana River. Picha na Northern Rangelands Trust.