- Mabadiliko ya tabianchi yanamwongezea mwanamke mzigo wa kazi na matatizo.
- Dhana ya jinsia kwenye mambo ya mabadiliko ya tabianchi inahitaji vitendo, na siyo nadharia tu.
- Mijadala kuhusu tabianchi iwe jumuishi ili kuzingatia uzoefu na changamoto halisi za wanawake na wanaume.
- Pengo kati ya sera na utekelezaji hukwamisha utekelezaji wa mipango mizuri.
Katika kipindi ambacho dunia inaendelea kukabiliwa na changamoto za mabadiliko ya tabianchi, mijadala mingi imekuwa ikijikita katika athari zake kwa ujumla, bila kuangalia namna makundi tofauti yanavyoathirika.
Katika kuadhimisha Siku ya Wanawake Duniani, Machi 8, 2026, Mongabay ilifanya mahojiano ya ana kwa ana na Leonard Chakupewa Soza, Mtaalamu wa Masuala ya Jinsia na Mazingira, ili kuchambua kwa kina uhusiano kati ya mabadiliko ya tabianchi na usawa wa kijinsia.
Mahojiano haya yanalenga kuangalia nafasi ya wanawake katika mipango na harakati za kukabiliana na athari hizo na kwa nini ni muhimu kuhakikisha sauti zao zinajumuishwa katika maamuzi, sera, mipango na sheria.
Yafuatayo ni mahojiano kati ya mwandishi wa Mongabay na Leonard Chakupewa Soza.

Mongabay: Mabadiliko ya tabianchi yanawaathiri vipi wanawake kwa namna tofauti na wanaume katika nchi zinazoendelea, zikiwemo za Afrika Mashariki?
Leonard: Ili kuelewa athari za mabadiliko ya tabianchi kwa wanawake, ni muhimu kuanza kwa kuangalia nafasi yao katika jamii. Wanawake katika nchi nyingi za Afrika ni kundi kubwa. Kwa mfano, katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2022 inaonyesha kati ya watu 61,741,120 waliohesabiwa. Wanaume walikuwa 30,053,130, sawa na asilimia 49 ya watu wote, huku wanawake wakiwa 31,687,990, sawa na asilimia 51. Asilimia 60 ya watu wanaojishughulisha na kilimo ni wanawake, ikimaanisha kwamba wao ndio wanaolisha taifa. Wanawake pia hubeba mzigo mzito wa malezi ya watoto na utunzaji wa wazee na wagonjwa.
Kutokana na mlundikano huo wa majukumu ya kifamilia na kijamii, wanawake huathirika zaidi pale mabadiliko ya tabianchi yanapotokea na kusababisha athari kama ukame, kupungua kwa mvua, kukauka kwa vyanzo vya maji, kutokea kwa mafuriko na mambo mengine yanayomuongezea mwanamke mzigo wa kazi na changamoto katika maisha yake ya kila siku.
Mongabay: Ni mifano gani halisi inayoonyesha namna mabadiliko ya tabianchi yanavyomuathiri mwanamke moja kwa moja?
Leonard: Ipo mingi, lakini nigusie miwili inayojirudia mara kwa mara na kuwaathiri wanawake katika nchi zenye kipato kidogo kama Tanzania. Mabadiliko ya tabianchi yanaposababisha vyanzo vya maji kukauka, wanawake huhangaika huku na kule kutafuta maji. Wale wa mjini hulazimika kununua madumu ya maji ya visima kwa bei kubwa wakati wale wa vijijini hutembea umbali mrefu kutafuta vyanzo vichache vya maji vilivyopo, wakati mwingine wakipita kwenye maeneo yasiyo salama kwao dhidi ya dhulma za kiutu. Wapo akinamama ambao wamefanyiwa ukatili wakiwa kwenye harakati za kusaka maji.

Mfano mwingine ni kuhusu kukosekana kwa mvua. Mvua isiponyesha kabisa au ikichelewa, huathiri uzalishaji wa mazao na hivyo kupungua kwa mavuno. Hali hiyo inamfanya mwanamke atumie muda mwingi kuhakikisha familia yake inapata chakula. Kadhalika kipato chake hupungua, na hivyo kuongeza utegemezi wake. Mambo yote hayo huathiri ustawi wa mwanamke na kwa kiasi kikubwa humwongezea hatari ya kufanyiwa vitendo vya ukatili wa kijinsia.
Mongabay: Umesema mabadiliko ya tabianchi yanaweza kuchangia ongezeko la vitendo vya ukatili dhidi ya wanawake. Hebu fafanua uhusiano huo.
Leonard: Athari za mabadiliko ya tabianchi huchangia ongezeko la vitendo vya ukatili dhidi ya wanawake lakini si kwa njia za moja kwa moja. Umaskini na utegemezi ni baadhi ya athari za mabadiliko ya tabianchi. Mambo haya yanapomkabili mwanamke, humweka katika hatari kubwa ya unyanyasaji.
Aidha, ugumu wa maisha husababisha migogoro ya kifamilia isiyoisha ambayo huchochea ukatili wa majumbani. Kwa upande mwingine, majanga yatokanayo na mabadiliko ya tabianchi, kama mafuriko na maporomoko, husababisha watu kukosa makazi na hivyo kuhama, na katika mazingira ya uhamiaji, wanawake hukabiliwa na unyanyasaji na ukatili.
Mongabay: Lugha ya usawa wa kijinsia inazidi kusikika katika majadiliano na makubaliano kuhusu mabadiliko ya tabianchi. Hatua hii inakupa taswira gani?
Leonard: Ni hatua chanya inayoonyesha kwamba wanawake wanaendelea kutambulika kama wadau muhimu katika masuala ya tabianchi. Hatua hii pia inaashiria kwamba katika mipango, majadiliano na makubaliano ya masuala yanayohusu mabadiliko ya tabianchi, suala la usawa wa kijinsia limeendelea kutambuliwa rasmi kama kipengele muhimu kinachostahili kupewa kipaumbele.
Mongabay: Ni jambo jema kwamba lugha ya usawa wa kijinsia inaendelea kusikika. Je, uhalisia katika utekelezaji wa hilo ukoje?
Leonard: Japo lugha ya usawa wa kijinsia ipo kwenye mikakati, kampeni na makubaliano kuhusu masuala muhimu yanayohusu mabadiliko ya tabianchi, katika ngazi mbalimbali za kitaifa na kimataifa, bado utekelezaji wake umeendelea kuwa dhaifu kutokana na sababu mbalimbali.
Kwa maneno mengine tunaweza kusema kwamba mipango na makubaliano mara nyingi hubaki kwenye maandishi. Hatuoni usawa wa kijinsia katika masuala ya tabianchi, ukizingatiwa kwa vitendo na kiwango kinachotakiwa na kwa namna inayoleta manufaa kwa wanawake hasa wale walioko vijijini.

Mongabay: Ni vikwazo gani vinavyokwamisha ujumuishi wa kijinsia katika mipango na utekelezaji wa masuala ya mabadiliko ya tabianchi?
Leonard: Kuwepo kwa pengo kati ya sera na utekelezaji wake ni changamoto ya kwanza ambayo hukwamisha mipango mizuri kutekelezwa na kuleta manufaa. Hili hutokea pale ambapo nchi huafiki kuchukua hatua kadhaa lakini hukosa mifumo mizuri na madhubuti ya kutafsiri hayo makubaliano kuwa mipango na utekelezaji halisi. Kwa Tanzania, sera na mikakati inayoongoza masuala ya tabianchi ni pamoja na; Sera ya Taifa ya Mazingira ya 2021, Sera ya Mabadiliko ya Tabianchi pamoja na Mkakati wa Taifa wa Mabadiliko ya Tabianchi.
Changamoto nyingine ni ukosefu wa rasilimali za kuendesha programu zinazolenga kuimarisha usawa wa kijinsia katika masuala ya tabianchi.
Aidha, taarifa nyingi zilizopo hazionyeshi tofauti ya athari kati ya wanawake na wanaume. Kutokana na hilo, inakuwa vigumu kupanga sera zinazolenga mahitaji halisi ya kila kundi.
Tatizo jingine ni maazimio na makubaliano kuhusu masuala ya mabadiliko ya tabianchi na madhara yake kuelezwa kwa ujumla, bila kukumbuka kuwa hali ya kuathiriwa na mabadiliko ya tabianchi inatofautiana kati ya wanawake na wanaume.
Tanzania ina mfumo na sera inayotambua mabadiliko ya tabianchi lakini changamoto kubwa mara nyingi imekuwa kwenye utekelezaji, uratibu na ujumuishaji wa masuala kama usawa wa kijinsia katika vitendo.
Mongabay: Unasemaje kuhusu ushirikishwaji wa wanawake kwenye mipango na majadiliano kuhusu tabianchi?
Leonard: Ushirikishwaji wa wanawake katika dhana nzima bado ni mdogo. Majadiliano ya juu ya sera na miongozo kuhusu masuala ya tabianchi bado yanashirikisha wanawake kwa kiasi kidogo sana. Hilo husababisha mijadala kuhusu masuala mengi yanayowaathiri moja kwa moja kukosa msukumo, uzito na nguvu inayostahili.
Kadhalika, maamuzi yanayofanywa hayazingatii kikamilifu uzoefu na changamoto halisi za wanawake. Hii ni kwa sababu sura nyingi zinakuwa ni za wanaume, jambo linalopelekea upangaji wa mipango kufanywa kwa mitazamo ya walio wachache licha ya kwamba ina athari kwa wengi.
Kwa hali kama hiyo, inakuwa ni vigumu kwa wanaume kufikiria athari za mabadiliko ya tabianchi zinazowaathiri wanawake kwa kiwango ambacho wanawake wenyewe wangefanya. Hapa ndipo busara ya kutoa nafasi kwa sauti za wanawake inahitajika.
Mongabay: Je, mfumo dume una athari gani katika eneo hilo?
Leonard: Mfumo dume kwenye nchi nyingi, hasa zinazoendelea, bado ni changamoto na huathiri mambo mengi, ukiwemo utekelezaji wa maazimio yanayofikiwa kwenye majukwaa na mikutano inayojadili masuala ya mabadiliko ya tabianchi.
Ni vema tukakiri kwamba hata viongozi wetu bado wanaathiriwa na mfumo huo katika maamuzi na mashauri mbalimbali, kwani hata wao wanaendelea kuishi kwenye jamii hizo hizo zinazoshajiisha fikra kandamizi dhidi ya wanawake. Masuala kama uundwaji wa sera na utekelezaji wake ni miongoni mwa mambo yanayoathiriwa na mfumo dume.
Ukosefu wa uwajibikaji ni changamoto nyingine inayosababisha makubaliano yasitekelezwe kikamilifu. Tangu mikutano ya COP ilipoanza mwaka 1995, mataifa yanayoshiriki huafikiana maazimio lakini yaliyo mengi hayatekelezwi kutokana na tofauti katika sera za kiuchumi na uwajibikaji.
Siasa pia zimekuwa zikitawala sana na kufanya mipango mizuri inayoafikiwa isifanikiwe. Mathalani, mifuko ya majanga ya dharura katika nchi nyingi za Afrika, ni kwa ajili ya kugharimia ziara za viongozi kutathmini uharibifu na si manunuzi ya mahitaji ya kiutu kwa waathirika ambao kwa kiasi kikubwa huwa ni wanawake na watoto.
Teknolojia duni na kukosekana kwa takwimu sahihi kuhusu utekelezaji wa sera hizi, hufanya iwe vigumu kupima mafanikio na kuwawajibisha wahusika.
Mongabay: Umetaja mikutano ya COP; kwa kifupi mikutano hiyo ina umuhimu gani kwa wanawake katika nchi zinazoendelea?
Leonard: Huwezi kujadili masuala ya mabadiliko ya tabianchi bila kugusia mikutano hiyo ambayo nchi wanachama hukutana humo kila mwaka kujadili hatua za kupambana na mabadiliko ya tabianchi.
Nikirejea kwenye swali, iwapo mikutano hiyo ina umuhimu kwa wanawake kutoka nchi zenye kipato cha chini ama la, jibu langu ni ndiyo. Kwenye mikutano hiyo ni fursa ambapo mataifa washiriki huchukua hatua na maamuzi kadhaa yanayolenga kuinua wanawake katika mapambano ya athari za mabadiliko ya tabianchi.
Katika mikutano hiyo pia kuna hatua na maazimio yanayotolewa ambayo yanajibu maswali na changamoto za wanawake na wasichana hasa kutoka katika nchi zinazoendelea. Ukubwa wa athari za mabadiliko ya tabianchi, ikiwa ni pamoja na kuathiri dunia nzima, ni zaidi kwa mataifa ya ulimwengu wa tatu, na waathirika wakubwa ni wanawake.

Mongabay: Je, COP30 ilikuwa na upekee gani kwa wanawake wa vijijini?
Leonard: COP30, iliyofanyika Novemba 2025 nchini Brazil, ilikuwa na umuhimu mkubwa kwa wanawake. Katika mkutano huo, pamoja na mambo mengine, nchi zilipendekeza mpango maalumu wa kufadhili hatua za kijinsia wa Bellem (Bellem Gender Action Plan) kwa ajili ya usaidizi wa kiuchumi kwa wanawake wa jamii asilia na wale wa mataifa yaliyoathiriwa sana na athari za mazingira barani Afrika. Hatua hii pekee inaonyesha umuhimu wa mkutano huo.
Kadhalika, nchi zilikubaliana kuhusu suala la usaidizi wa kifedha wa moja kwa moja katika majanga – asilia (Women-Responsive Climate Finance) – mpango unaolenga kuwezesha mashirika yasiyokuwa ya kiserikali yanayojihusisha na miradi ya wanawake katika mataifa masikini wanaojishughulisha na shughuli za kilimo-ikolojia na matumizi ya nishati safi.
Mambo mengine muhimu katika mkutano huo yalikuwa makubaliano kuhusu suala la ulinzi kwa wanaharakati wa mazingira (environmental human rights defenders) na uhakika wa taarifa na ushahidi.
Ukitafakari kwa makini, mambo yote hayo yaliyokuwa sehemu ya mkutano huo, yana manufaa kwa wanawake hasa wale wa vijijini. Kwa mfano, usaidizi wa kifedha utamwezesha mwanamke kuanzisha miradi ya kumwezesha kujiongezea kipato cha ziada na kufanya kilimo endelevu. Pia, kupitia miradi hiyo ataongeza ujuzi katika kukabiliana na athari za tabianchi na kushiriki kikamilifu kwenye maamuzi ya kijamii na kimazingira.
Aidha, kitendo cha washiriki wa COP30 kuwatambua wanawake kama mabalozi katika mapambano ya athari za mabadiliko ya tabianchi na kauli kwamba bila wanawake, jitihada haziwezi kuleta matunda, ni kitu kikubwa sana kwao. Mwanamke anaposikia kwamba kitu anachokifanya, hata kama ni kidogo, kimetambuliwa, inampa moyo wa kufanya vizuri zaidi.
Mongabay: Ni ujumbe gani ungependa kumaliza nao?
Leonard: Nasisitiza kwamba licha ya makubaliano kwenye mambo makubwa na yenye manufaa kwa wanawake, bado kuna pengo kati ya makubaliano na utekelezaji. Bila kupiga hatua kutoka kwenye maneno kwenda kwenye vitendo, bado dhana ya jinsia kwenye mambo ya mabadiliko ya tabianchi itabaki kuwa nadharia tu.
Picha ya bango: Upandaji wa mazao yenye mizizi inayosaidia kuboresha muundo wa udongo na mzunguko wa virutubisho ni miongoni mwa shughuli zinazofanywa na wanawake katika kulinda mazingira. Picha kwa hisani ya Global Platforms Tanzania.