- Zaidi ya kasa 350 wamehifadhiwa kwenye viota maalum Zanzibar ili kuwalinda dhidi ya vitisho kama ujangili na shughuli za kibinadamu, lakini wataalamu wanasema hatua hiyo pekee haitoshi kukabiliana na kupungua kwao.
- Utafiti mdogo uliopo unaonyesha idadi ya kasa imepungua kwa kiasi kikubwa katika miaka ya hivi karibuni, huku maeneo yaliyokuwa na kasa wengi yakishuhudia kupungua kwa kasi.
- Ingawa juhudi za kimataifa za uhifadhi zimechangia kuongezeka kwa idadi ya kasa wa kijani duniani, vitisho kama mabadiliko ya tabianchi, uvuvi, na uharibifu wa makazi bado vinaendelea kuwaathiri Zanzibar.
- Wataalamu wanasisitiza umuhimu wa ushirikishwaji wa jamii, utafiti wa kina, na hatua madhubuti za uhifadhi ili kurejesha idadi ya kasa na kulinda mifumo ya ikolojia ya bahari.
ZANZIBAR, Tanzania – Nchini Tanzania, katika visiwa vya Zanzibar, zaidi ya kasa 350 wamehifadhiwa katika viota maalum kwenye fukwe, hatua ambayo wataalamu wanadai ni muhimu katika kuwalinda dhidi ya ujangili, wanyama wanaowinda, na shughuli nyingi za kibinadamu zinazoendelea katika maeneo ya pwani.
Hata hivyo, wahifadhi wa mazingira wanaonya kwamba kulinda viota pekee hakutatosha kubadili kile wanachoeleza kuwa ni kupungua kwa kiasi kikubwa kwa idadi ya kasa, hasa katika pwani ya kaskazini-mashariki ya Unguja, ambako hapo awali kulishuhudiwa kasa wengi.
Casper Morch, ambaye ni mwanaikolojia na msimamizi wa miradi wa Taasisi ya Under the Wave iliyopo Zanzibar, anasema kuna utafiti mdogo sana wa kisayansi kuhusu kasa wa baharini Zanzibar, lakini idadi ya kasa imepungua mara dufu katika miaka ya hivi karibuni.
Morch anasema: “Tunajua kumekuwa na upungufu mkubwa wa kuonekana kwa kasa. Zamani wapiga mbizi walikuwa wanaona kasa 30 hadi 40 kwa wiki, lakini sasa wanajiona wenye bahati wakiona hata mmoja tu.”

Taasisi ya Under the Wave, ikishirikiana na mamlaka za Zanzibar, ilianza uhifadhi wa kasa mwaka 2020, mwaka ambao walibaini kuwa idadi ya kasa ilikuwa ikipungua kwa kasi.
“Tulianzisha mara moja viota (aquaria) ambavyo hadi sasa vina kasa takribani 350. Lakini hawawezi kuzaliana kama walivyokuwa wakiishi kwenye makazi yao ya asilia. Hili ni jambo tunalolitambua na tutahakikisha wanarejea na kuwa salama,” anasema Morch.
Taasisi hiyo inasema kasa wanahitaji kurudi walipotoka, lakini hilo litakuwa salama pale ambapo wanajamii wakiwemo wavuvi wataelimika zaidi.
Pwani ya Zanzibar imekuwa sehemu muhimu ya maisha ya kasa wa kijani, ambao kwa sasa amepunguzwa katika orodha ya International Union for Conservation of Nature (IUCN) Red List kutoka hadhi ya “aliye hatarini kutoweka” hadi “asiye na wasiwasi mkubwa.”
Oktoba 2025, Shirika la Kimataifa la Uhifadhi wa Mazingira (IUCN) lilieleza kuwa kutokana na juhudi endelevu za uhifadhi, kasi ya kupungua kwa idadi ya kasa imepungua maradufu duniani.
Kwa mujibu wa taasisi hiyo, tathmini ya spishi hiyo ya kasa wa kijani, iliyofanyika Desemba 2024 ilionyesha kuwa idadi ya kasa hao duniani imeongezeka tangu miaka ya 1970 na hivyo kutolewa kwenye orodha ya spishi zilizo hatarini kupotea.
Orodha hiyo ilianzishwa mwaka 1964, na ni mojawapo ya vyanzo vya kina zaidi duniani vya taarifa kuhusu hali ya hatari ya kutoweka kwa spishi za wanyama, kuvu na mimea. Hadi sasa inajumuisha spishi 172,620, na kati ya hizo 48,646 ziko katika hatari ya kutoweka.
IUCN inasema kuwa kwa miongo kadhaa, vitisho kama upotevu wa makazi, mabadiliko ya tabianchi, uchafuzi wa mazingira, spishi vamizi, uvuvi wa kibiashara na biashara haramu ya wanyamapori vimeendelea kuchangia kupungua kwao.
Hata hivyo, juhudi za uhifadhi zinataja kuwezesha spishi hii kuanza kuongezeka tena, huku idadi yao ikiongezeka kwa takribani asilimia 28 ikilinganishwa na viwango vya miaka ya 1970 na 1980.
Umuhimu wa kasa kwa ikolojia ya bahari
Watafiti wa viumbe hao majini wanasema kasa wa baharini wana jukumu muhimu katika ikolojia na kudumisha usawa wa mifumo ya baharini.
Morch anasema: “Wanahamisha virutubisho, kudhibiti ukuaji wa nyasi za baharini, na kuchangia katika mfumo wa miamba ya matumbawe yenye afya.”

Miamba ya matumbawe na nyasi za baharini hutajwa kuwa ni sehemu muhimu za kuzalia samaki wa aina mbalimbali.
Ni nini kinasumbua kasa wa Zanzibar
Kwa mujibu wa mamlaka za Zanzibar, na wahifadhi wengineo, vitisho vikubwa kwa kasa ni pamoja na uendelezaji wa ukanda wa pwani, uvuvi na nyavu hatarishi, uwindaji, shinikizo la utalii pamoja na mabadiliko ya tabianchi ambayo huathiri jinsia ya vifaranga kwa kuwa joto la juu huzalisha zaidi majike.
Mkurugenzi Idara ya Uhifadhi wa Bahari Zanzibar, Dkt. Makame Omar Makame, anasema kuwa serikali inashirikiana na wadau kuhakikisha wanaongeza nguvu katika uhifadhi.
“Tunaweka njia bora za kudhibiti, lakini pia kuhakikisha wananchi wananufaika na rasilimali, tumefanya hivyo ili kulinda viumbe hai na kuhakikisha kuwa hifadhi inakuwa salama. Tutadhibiti shughuli za uvuvi na utalii sehemu zingine kwa ajili tu ya kurudisha hali kawaida kisha tunaweka utaratibu bora usioleta athari kwa ikolojia,” Makame aliiambia Mongabay.
Hata hivyo, wahifadhi wanasema uhamasishaji, ushirikishwaji wa jamii na tafiti za muda mrefu ni muhimu ili kuokoa na kurejesha usawa wa mfumo wa ikolojia wa bahari ya Zanzibar.
Akizungumzia athari za uvuvi, Morch anasema vifaa vya uvuvi vinaweza kuwa hatari zaidi kwa kasa, kwani vinaweza kuzuia wasipate hewa na hivyo kufa. “Kama kasa atashikiliwa chini ya maji na vifaa vya uvuvi, atazama na kufa kwani hutegemea kuvuta pumzi ya hewa ili kuishi,” anaeleza.

Hata hivyo, watafiti mbalimbali wanasema ili kuweza kuchukua hatua madhubuti ni lazima kuwepo kwa takwimu au data za idadi halisi ya kasa katika eneo la bahari.
“Hatujui idadi halisi ya kasa waliopo au sehemu zote walipotaga mayai yao…ili kuunda mkakati wenye ufanisi, kwanza lazima tujenge hifadhidata itakayosaidia juhudi tunazoendelea nazo na zinginezo,” lilisema shirika hilo.
Mabadiliko ya tabianchi yanavyoathiri uzazi kwa kasa
Joto la maji ya bahari, kutokana na mabadiliko ya tabianchi, linaongeza hatari nyingine kwa kasa.
Morch anasema, katika suala la kuzaliana iwapo joto litaongezeka sana, watazaliwa kasa jike ambapo wakiwa wengi huenda wasiweze kuongezeka kwa kasi siku za mbeleni.
Mtafiti huyo anasema: “Kiwango cha takriban nyuzi 28 za Celsius kinazalisha kasa wa kiume kwa wingi. Kati ya nyuzi 28 hadi 30, inaweza kuzalisha wa jinsia tofauti lakini ikiwa ni zaidi ya nyuzi 30, wengi watazaliwa majike.”
Under the Wave wanasema kadri joto la dunia linavyoongezeka, uwiano usio sawa wa jinsia unaweza kuathiri uwezo wa muda mrefu wa idadi ya kasa kuendelea kuishi.
Walaji, wavuvi wadhibitiwa
Wakazi wa visiwa hivyo wanadai kuwa kasa wameadimika sokoni na hiyo inatokana na upatikanaji wake, lakini pia udhibiti unaofanywa na serikali ya Zanzibar.
Abdul Sakaza ni mkazi wa mkoa wa Kaskazini Unguja, na anasema hapo awali kasa walipatikana kwenye masoko ya samaki ya Matemwe na Tumbatu yaliyopo kwenye mkoani humo.
“Mara ya mwisho nilikula miaka saba iliyopita, kwa sasa hawapatikani kabisa kwenye masoko rasmi ya samaki, na hata wakipatikana ni kinyemela na wavuvi wanawauza kwa kujificha na kwa bei ya juu,” anasema Sakaza, huku akisisitiza kuwa Serikali inadhibiti biashara ya kasa.
Pia, anabainisha kuwa walaji kwa miaka ya hapo nyuma walipungua kwasababu ya matukio ya watu kufa kwa sumu inayodaiwa kuwa kwenye baadhi ya kasa hao.

Machi 05, mwaka 2024, mamlaka za Zanzibar zilithibitisha vifo vinane na watu wengine 78 kulazwa kwa madai ya kula kasa katika mkoa wa Kusini Pemba. Wataalamu wa afya hawakuweka hadharani aina ya sumu iliyodaiwa kuwa kwenye kasa hao.
Sheria ya Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi na Maliasili za Baharini ya mwaka 2023, imeainisha kuwa italinda kasa kama rasilimali muhimu ya bahari visiwani Zanzibar.
Sheria hiyo inazuia uvuvi, uuzaji, au uharibifu wa kasa na mayai yao ni marufuku, lengo likiwa kuhifadhi bioanuwai na kukuza utalii endelevu, huku taratibu za kisheria zikiendelea kuimarishwa.
Picha ya bango: Wataalamu Zanzibar, nchini Tanzania, katika shuguli za kuhifadhi kasa. Pich kwa hisani ya Under the Wave.