- Elgeyo-Marakwet na mifumo mingine muhimu ya ikolojia kama Rimoi National Reserve ni makazi ya spishi kadhaa mashuhuri, adimu na zilizo hatarini.
- Zimetajwa kama African elephant (Loxodonta africana), ambaye ingawa si adimu duniani kote, yuko hatarini na ana umuhimu mkubwa.
- Wakazi wa Chesongoch walisema wakati wa maporomoko, waliona nyani ambao huwa ni nadra sana kuonekana katika eneo hilo.
Hii ni sehemu ya pili ya nakala hii kuhusu maporomoko ya ardhi yaliyotokea nchini Kenya baada ya musimu wa mvua. Soma sehemu ya kwanza hapa.
KERIO VALLEY – Kenya. Siku chache baada ya mvua kubwa ya mfululizo kunyesha kwenye vilima vilivyokatwa miti, juu ya kijiji cha Chesongoch, Marakwet Mashariki, katika Bonde la Ufa nchini Kenya, udongo mwepesi wa volkeno uliteleza na kuporomoka. Kilichoanza kama mtikisiko mdogo wa ardhi mara kiligeuka kuwa jinamizi la vifusi vilivyoanguka na makazi ya watu kusombwa.
Takwimu zinazotolewa kuhusu idadi ya vifo vilivyotokana na kadhia hiyo, zinatofautiana huku baadhi ya watu wakisema waliofariki ni 26, wengine wakitaja 31 na 39. Zaidi ya familia 600 ziliripotiwa kukosa makazi katika janga hilo lililotokea Novemba mwaka 2025, ambalo wanasayansi wamelihusisha na mabadiliko ya tabianchi, jiolojia pamoja na shughuli za binadamu, ikiwemo uharibifu wa kasi wa mifumo ya ikolojia katika maendeo ya nyanda za juu.
Wahifadhi wa mazingira wanaeleza kuwa majanga kama maporomoko ya ardhi ya Chesongoch yana athari mengi zaidi ya vifo na uharibifu wa mali unaoripotiwa mara kwa mara. Philip Muruthi, Makamu wa Rais wa Uhifadhi wa Spishi na Sayansi katika African Wildlife Foundation, yenye makao yake jijini Nairobi, anasema mara nyingi msisitizo mkubwa huwekwa kwenye athari za kijamii na kiuchumi kwa binadamu, huku madhara kwa bioanuwai yakipuuzwa.

Madhara ya kiikolojia ya maporomopo
Moja ya athari hizo, anasema, ni kuvurugika kwa njia za uhamaji wa wanyamapori, tatizo ambalo huenda chanzo chake ni janga la Chesongoch. Matokeo yake ni athari kubwa kwa idadi ya wanyama katika Bonde lote la Ufa nchini Kenya.
“Huenda hatutajua kamwe ni kiasi gani cha mimea na wanyama tulipoteza katika tukio hili moja tu. Baadhi ya spishi za wanyama na miti zimekuwepo kwa mamilioni ya miaka, na huenda tusizipate tena hata baada ya mamilioni mengine ya miaka,” Muruthi aliiambia Mongabay.
Wakazi wa Chesongoch walisema wakati wa maporomoko, waliona nyani ambao huwa ni nadra sana kuonekana katika eneo hilo. “Baadhi yao walikuwa wameshikilia miti iliyokuwa ikisukumwa na maporomoko kuelekea chini ya mto. Pia nyoka wa ajabu wameonekana kijijini,” alisema Gregory Kimutai, mkazi wa Chesongoch.
Kwa mujibu wa wakazi waliohojiwa na Mongabay, maporomoko hayo pia yalisomba baadhi ya “spishi kubwa za miti ya asili.”
Kwa mujibu wa Muruthi, eneo la Elgeyo-Marakwet ni makazi ya nyani adimu na walio hatarini wanaojulikana kama De Brazza’s monkey (Cercopithecus neglectus), ambao pia hupatikana katika Wilaya ya Tororo mashariki mwa Uganda, pamoja na maeneo ya Trans-Nzoia na West Pokot, magharibi mwa Kenya. Spishi hii ya nyani imeorodheshwa katika Orodha Nyekundu ya viumbe walio hatarini ya IUCN.
Vitisho vikubwa dhidi ya nyani hawa ni ukataji miti unaofanywa na watu kwa ajili ya mbao na kilimo, pamoja na uwindaji kwa ajili ya kitoweo cha porini. “Huenda huyu ndiye nyani ambaye wakazi walisema walimuona kipindi cha maporomoko. Spishi hii ni adimu sana na ni vigumu kumuona. Huhamahama kati ya Bonde la Kerio na Milima ya Cherangani, na maporomoko ya ardhi yanaweza kuathiri njia zao za uhamaji,” anasema Muruthi.
Elgeyo-Marakwet na mifumo mingine muhimu ya ikolojia kama Rimoi National Reserve ni makazi ya spishi kadhaa mashuhuri, adimu na zilizo hatarini, ikiwemo African elephant (Loxodonta africana), ambaye ingawa si adimu duniani kote, yuko hatarini na ana umuhimu mkubwa.

Spishi nyingine zilizoorodheshwa katika Orodha ya IUCN ni pamoja na Pangolin (Manis phataginus), mamalia anayeuzwa zaidi kinyume cha sheria duniani, na ambaye pia ameainishwa kuwa yuko hatarini kutoweka.
Wengine ni wanyama adimu na wenye kujificha kama Black duiker (Cephalophus niger), Bushpig (Potamochoerus larvatus), na wanyama wala nyama wadogo wa usiku kama African civet (Civetticus civetta), Common genet (Genetta genetta), African wild dog (Lycaon pictus), pamoja na baadhi ya spishi adimu za ndege.
“Ingawa hatuna takwimu kamili zinazoonyesha ni kwa kiasi gani maporomoko ya ardhi ya mara kwa mara katika eneo hili yameathiri spishi za wanyama na mimea kwa miaka mingi, hili ni onyo kwamba tunapaswa kuchukua hatua zinazohitajika kupunguza matukio kama haya ili kuzuia madhara zaidi,” anasema Muruthi.
Picha ya bango: Uharibifu uliosababishwa na maporomoko ya ardhi katika kijiji cha Chesongoch, Marakwet Mashariki, katika Bonde la Kerio. Picha na Dann Okoth.