- Miradi ya taka sifuri shuleni si tu suluhisho la usafi wa mazingira, bali ni mkakati wa kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.
- Mfumo huu hauhusishi matumizi ya kemikali hatarishi, unategemea michakato ya asili na mbinu rahisi zinazoweza kudhibitiwa na washiriki.
- Taka zinapotupwa ovyo mitaani huingia katika vyanzo vya maji kama vile mifereji na hupelekwa baharini na kuathiri viumbebahari.
- Kutenganisha taka za kikaboni na kuzigeuza mboji badala ya kuzipeleka dampo, hupunguza uzalishaji wa gesi chafu.
Nchini Tanzania, kaya nyingi huona taka kama uchafu usio na thamani. Mabaki ya chakula yanapooza na kutoa harufu kali na plastiki zinazotapakaa karibu na makazi, familia nyingi mijini huwa na wasiwasi wa kupata athari za kiafya, hivyo hukimbilia kuzichoma, kuzitupa ovyo au kuzikusanya kwenye magari ili zipelekwe dampo.
Vitendo hivyo huchafua mazingira, na kuchochea uzalishaji wa gesi aina ya Methane, ambayo hutokana na vitu vya kikaboni kama mabaki ya vyakula na taka vinapooza. Gesi hii huchangia kwa kiasi kikubwa athari za mabadiliko ya tabianchi ambayo yanaathiri maisha ya kiuchumi na kijamii ya wanadamu.
Taarifa ya Ofisi ya Makamu wa Rais iliyowekwa kwenye Mkakati wa Kitaifa wa Usimamizi wa Taka (2025), inasema Tanzania huzalisha kati ya tani milioni 14.4 hadi 20.7 za taka ngumu kwa mwaka. Kati ya hizo, zaidi ya asilimia 60 ni taka za kikaboni, ikiwemo mabaki ya chakula, majani
Ripoti ya Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) ya mwaka 2020, inaonyesha kuwa Jiji la Dar es Salaam linaongoza kwa uzalishaji wa taka ambapo kwa mwezi linazalisha taka tani 400,000, kati ya hizo, asilimia 75 huzalishwa majumbani na ni asilimia 30 tu hutupwa kwenye dampo lililopo Pugu Kinyamwezi, Wilaya ya Ilala. Zile zilizosalia huishia kwenye vyanzo vya maji kama vile mifereji, mito, mabwawa na baharini.
Boniface Kyaruzi, Mtaalam wa taka na Ofisa Mkuu wa Mazingira NEMC, anasema taka zinapotupwa ovyo mitaani bila kuwa na usimamizi thabiti, huchafua mazingira na kuyasababisha yakose mvuto.
Anasema taka hizo zinapokuwa zimezagaa barabarani, maji ya mvua huzipekeka kwenye mito na mifereji na husababisha kuziba kwa njia za maji na kuongeza hatari ya mafuriko. Taka nyingine, hasa za plastiki, hupelekwa baharini na kuathiri viumbe wa bahari kwa kuharibu makazi yao na kuingia katika minyororo yao ya chakula.
“Kwa ujumla, hali hii inadhoofisha mifumo ya ikolojia ya mijini na kusababisha gharama kubwa za kijamii na kiuchumi kwa wakazi. Kwa mfano, hapa Dar es Salaam unaona ikinyesha mvua siku moja tu, mitaro inajaa maji na kusababisha mafuriko barabarani, na usafiri unakuwa na shida,” anasema.
Taarifa ya Benki ya Dunia ya mwaka 2023 ya Benki ya Dunia ya mwaka 2023 kuhusu Awamu ya Pili ya Dar es Salaam Metropolitan Development Project (DMDP II) inaonyesha kuwa asilimia 40 ya taka zinazokusanywa katika Jiji la Dar es Salaam humwagwa kwenye dampo la wazi la Pugu, ambalo limejaa na kuendelea kuwa tishio kwa mazingira na afya ya jamii.

Taarifa hiyo inaeleza kuwa kujaa kwa dampo hilo kunasababisha ajali za mara kwa mara za magari yanayokwenda kumwaga taka, hivyo kusababisha msongamano wa magari hasa kipindi cha mvua. Hali hii imechochea ongezeko la utupaji taka ovyo katika maeneo yasiyo rasmi kwa sababu taka zinakaa majumbani kwa muda mrefu bila ya kukusanywa na magari. Matokeo ya hali hiyo ni uchafuzi zaidi wa mazingira.
Boaz Ackim, Mkurugenzi wa Kampuni ya Taka ya Busae ya jijini Dar es Salaam, anasema kuwa kwa sasa wanatumia mwezi mzima kukaa kwenye foleni ya kumwaga taka katika dampo la Kinyamwezi kwa sababu ya miundombinu mibovu inayochangiwa na eneo hilo kuzidiwa na wingi wa taka.
Katikati ya changamoto hizo, mabadiliko chanya yanaanza kuonekana katika jiji la Dar es Salaam. Baadhi ya shule za msingi na sekondari zimeanza kutekeleza mfumo wa taka sifuri unaobadili taka za kikaboni kama vile mabaki ya chakula, matunda na mboga kuwa mboji na vyakula vya mifugo kama samaki na kuku, huku taka za karatasi zikibadilishwa kuwa mapambo ya nyumba.
Mradi wa Taka Sifuri unaotekelezwa na Taasisi za Mazingira Plus, Tanzania Cleanup and Conservation Initiative (TCCI), pamoja na Partners for Klima and Nature (PKN), umejikita katika kutoa mafunzo ya namna ya kugeuza taka hizo kuwa malighafi, kuzitenganisha taka na kuzichakata kuwa mbolea, mapambo na vyakula vya mifugo. Unashirikisha shule za msingi na sekondari katika mkoa wa Dar es Salaam.
Kupitia mradi huo, ulioanzishwa mwaka 2023, taasisi hizo pia huzijengea shule majengo ya kuhifadhi na kutenganisha taka na pia huwapatia vifaa vya kutenganishia na kuchakata taka. Pia huwapa elimu ya biashara ili iwasaidie kuuza bidhaa zitokanazo na taka hizo, pamoja na kuwatafutia masoko.
Lengo la mradi huo ni kupunguza uchafuzi wa mazingira na uzalishaji wa gesi chafu kama methane.
Taka za plastiki kama vile chupa za vinywaji, mafuta na vifungashio nazo hazijaachwa nyuma, hukusanywa na kuhifadhiwa sehemu nzuri na kuuzwa kwa kampuni ambazo hutengeneza viti, meza na mapambo ya nje na ndani ya nyumba.
Suleiman Mang’oro, Mratibu wa mradi wa taka sifuri kutoka Taasisi ya Mazingira Plus, anasema wanatekeleza mradi huo katika shule 10 jijini Dar es Salaam kwa kushirikiana na taasisi ya Tanzania Cleanup and Conservation Initiative (TCCI Mazingira). Anasema walifadhiliwa $51822 (TSh138,200,000) na PKN.
“Tuliamua kutekeleza mradi huo katika shule za msingi na sekondari za jijini Dar es Salaam kwa sababu jiji hili ndilo linaongoza kuzalisha taka nyingi,” anasema.
Aidha, anasema wanakusudia kujenga uelewa kwa wanafunzi na jamii kuhusu biashara ya urejeshaji wa taka (circular economy), kukuza afya bora ya mazingira ya shule, na kuchochea kizazi chenye maarifa na uwajibikaji katika kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi.
Kupitia mpango huo, mradi unatarajia kupunguza asilimia 80 ya taka za kikaboni zinazotupwa kwenye dampo. Taka hizo ni zile zinazotokana na mabaki ya vyakula na matunda, taka za plastiki kama vile chupa za maji, juisi na vifungashio na taka za zitokanazo na karatasi na maboksi.
Taka na mabadiliko ya tabianchi
Taka zinazotupwa dampo bila kutenganishwa, hasa za kikaboni kama mabaki ya chakula, majani na karatasi, huwa chanzo kikubwa cha uzalishaji wa gesi ya methane ambayo ni chafu na hatari kwa tabianchi.
Kyaruzi anasema taka zinapomwagwa dampo zinakuwa na hewa ya oksijeni na bakteria huanza kuoza kwa kutumia hewa hiyo. Lakini kadri muda unavyopita, oksijeni huisha na mazingira ya ndani ya dampo hubadilika na kuwa yasiyo na hewa.
Katika hatua hiyo, bakteria maalum wanaoitwa methanogens huvunja mabaki ya kikaboni na kuzalisha methane (CH₄) pamoja na hewa ya ukaa (CO₂). Kwa mujibu wa maelezo yake, gesi inayotoka dampo huwa na takribani asilimia 40 hadi 60 ya methane na hewa ukaa, na uzalishaji huo unaweza kuendelea kwa miaka mingi hata baada ya dampo kufungwa rasmi.
Kwa mujibu wa Kyaruzi, Methane ni gesi chafu yenye nguvu kubwa zaidi kuliko hewa ukaa katika kunasa joto angani. Kwa kipimo cha miaka 100 kinachotumika kisayansi (GWP100), methane ina uwezo wa kunasa joto mara 28 hadi 34 zaidi ya hewa ukaa, na katika kipimo cha miaka 20, athari zake huwa kubwa mara 84 hadi 86 zaidi ya hewa ukaa. Hii inaifanya Methane kuwa hatari sana katika kuongeza kasi ya mabadiliko ya tabianchi kwa muda mfupi.
“Methane inachangia takribani asilimia 30 ya ongezeko la joto duniani tangu mapinduzi ya viwanda, hivyo usimamizi duni wa taka kwenye dampo si tu tatizo la uchafuzi wa mazingira, bali pia ni kichocheo kikubwa cha athari za mabadiliko ya tabia nchi,” Kyaruzi anasema.
Taka sifuri ina manufaa gani?
Kyaruzi anaeleza kuwa endapo shule zitatenganisha taka za kikaboni na kuzigeuza mboji badala ya kuzipeleka dampo, zitasaidia katika utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs) ya kuzuia asilimia 80 ya taka za kikaboni kutupwa dampo na kupunguza kwa kiasi kikubwa uzalishaji wa Methane na gesi chafu kwa ujumla. Mpango huu unagusa namba 12 (Matumizi ya uazalishaji endelevu), na namba 13 (Hatua dhidi ya Mabadiliko ya Tabianchi) ya maendeleo endelevu.
Anasema taka za kikaboni zinapotengenezwa mboji kwa kutumia hewa (aerobic composting), uzalishaji wa Methane huwa mdogo sana au karibu haupo. Utafiti wa Shirika la Ulinzi wa Mazingira la Marekani (EPA), zinaonyesha Methane inaweza kupungua kwa kiasi cha kati ya asilimia 90 hadi 99 iwapo taka hizo zitachakatwa kwa kutengenezwa mboji.
Faida hizo haziishii kwenye Methane pekee, bali pia hupunguza gesi chafu kwa ujumla kwa wastani wa asilimia 30 hadi 70 ukilinganishwa na mfumo wa kutupa taka dampo. Kiwango hicho kinaweza kuwa kikubwa zaidi ikiwa mboji inayozalishwa itatumika kuchukua nafasi ya mbolea za kemikali, anafafanua.
Aidha Kyaruzi anataja faida nyingine ya kutengeneza mboji kwa kutumia taka kuwa ni kuzuia uzalishaji wa gesi ya Methane dampo, kupunguza utegemezi wa mbolea za viwandani, kuongeza uhifadhi wa kaboni kwenye udongo (soil carbon sequestration) na kupunguza gharama pamoja na nishati inayotumika kusafirisha taka kwenda dampo.
Nini kifanyike kudhibiti taka
Kyaruzi anasisitiza kuwa dampo lililowekwa taka zaidi ya uwezo wake linaweza kudhibitiwa kwa hatua madhubuti za kitaalamu, ikiwemo kupunguza taka zinazoingia dampo (waste diversion).
Hii inahusisha kutenganisha taka tangu zinapozalishwa kulingana na aina zake, kwa mfano, taka za kikaboni zinazoweza kurejeshwa zinawekwa sehemu yake, taka za plastiki zinakusanywa na kuuzwa na zile hatarishi pia zinawekwa sehemu yake.
Anashauri pia kuanzishwa kwa programu za kuchakata taka za kikaboni pamoja na kuimarisha urejelezaji wa taka za plastiki, karatasi, metali na glasi ambazo kwa sasa utekelezwaji wake ni mdogo kwa kuwa hakuna teknolojia ya kutosha. Kwa kufanya hivyo, kiasi cha taka kinachofika dampo kitapungua kwa kiasi kikubwa, na hivyo kupunguza uzalishaji wa methane na msongamano wa taka.
Aidha, anashauri pia kuzuia maji ya mvua kuingia moja kwa moja kwenye taka, na kufunika taka mara kwa mara. Kuhusu udhibiti wa gesi inayozalishwa kwenye dampo, anasema ni lazima kufunga visima vya kukusanya gesi (gas wells), kuteketeza gesi kwa njia ya kufunga mitambo ya kuzalisha nishati pamoja na kufanya ufuatiliaji wa viwango vya gesi kwenye maeneo ya karibu ili kuzuia milipuko na kupunguza mchango wa Methane katika mabadiliko ya tabianchi.
Mradi wa Taka Sifuri shuleni
Awamu ya kwanza ya mradi huo ulioanza mwaka 2023 hadi 2025 ulitekelezwa katika shule nne za sekondari na moja ya msingi katika jiji la Dar es salaam, ikiwemo Shule ya sekondari Jangwani iliyopo wilaya Ilala, kutoka wilaya ya Ubungo na Kibasila iliyoko Wilaya ya Temeke. Shule ya Msingi ni Taifa, iliyopo wilaya ya Temeke.
Katika awamu hiyo ya kwanza, wanafunzi 200 na walimu watano walinufaika katika kila shule kupitia klabu za mazingira na hivyo kufanya jumla ya wanufaika kuwa 1,000 kwa upande wa wanafunzi na 20 kwa upande wa walimu.

Awamu ya pili ya mradi huo ilianza Januari 2026 na unatekelezwa katika shule tano katika jiji hilo, ikiwemo sekondari za Pugu, Buza na Temeke zilizopo Wilaya ya Temeke, Mbweni iliyoko Wilaya ya Kinondoni na Nguva iliyo katika Wilaya ya Kigamboni. Unatekelezwa pia katika shule ya msingi ya Buguruni Viziwi iliyoko katika Wilaya ya Ilala. Jumla ya walimu 10 na wanafunzi 1,000 wanapatiwa mafunzo ya kubadili taka kuwa rasilimali.
Utekelezaji wa mradi
Kupitia mradi huo walimu na wanafunzi wanapewa mafunzo maalum ya kutenganisha taka za chakula, za karatasi na hatarishi na namna ya kuzitumia kutengeneza chakula cha mifugo na mapambo ya ndani. Pia shule zinajengewa vibanda maalum vya kutenganisha taka na vizimba vya kuchakata taka.
Kwa mujibu wa Mango’ro, wanafundisha jinsi ya kutenganisha taka mwanzoni kwa sababu zoezi hilo hurahisisha urejeshaji wa taka, hivyo hupunguza kiasi kinachopelekwa dampo. Hii pia husaidia kuhifadhi mazingira dhidi ya uchafuzi na hupunguza utoaji wa gesi chafu kutoka kwa taka za chakula.
“Taka zinapokuwa zimetenganishwa baada ya kuzalishwa na kila kundi likiwekwa kwenye sehemu yake, inarahisisha urejeshaji, kwa sababu kila kundi la taka lina matumizi yake binafsi, mfano taka za chakula zinatengeneza mbolea wakati taka za karatasi zinatengeneza mapambo. Kwa hiyo cha kwanza tunataka mwanafunzi ajifunze kutenganisha taka” anasema Mangoro.
Shule pia zinapewa mafunzo ya ujasiriamali wa taka ikiwemo namna ya kujua maeneo ya kupata taka zaidi, kupata masoko na kuandika miradi ya kuomba fedha kwa ajili ya utunzaji wa mazingira ili shule zijiendeshe zenyewe pale mradi unapokwisha.
Kwa mujibu wa Mang’oro, walimu wanaopata mafunzo ni wale wanaosimamia miradi hiyo mashuleni, ambao wakishahitimu huwafundisha wanafunzi wao wakati wa vipindi vya klabu za mazingira.
Suluhisho la mazingira
Suleiman Mang’oro anasema kuwa kabla ya kuanza mradi huo walifanya uchunguzi mwaka 2021 na kugundua kuwa taka nyingi zinazozalishwa kwenye taasisi zikiwemo shule, zinaweza kugeuzwa kuwa malighafi nyingine, hivyo kupunguza kiasi cha taka zinazopelekwa dampo.
Katika uchunguzi wao wa awali katika shule nne za msingi na sekondari walizotekeleza awamu ya kwanza ya mradi, Mazingira Plus iligundua kuwa kila shule inazalisha zaidi ya kilo 200 za taka za vyakula, na kilo 200 za taka za plastiki kila mwezi.
Mang’oro anasema tathmini ya mwisho katika shule hizo waliyofanya Desemba mwaka 2025, ilionyesha kuwa shule zote kwa ujumla zinabadili kilo 1,000 za taka za vyakula kuwa mbolea na zinakusanya kilo 200 za taka za plastiki kila mwezi.
“Pia tumefanikiwa kupunguza matumizi kwa asilimia 70 ya vifungashio vya plastiki kama vile matumizi ya vifuko laini vinavyowekewa karanga, ubuyu na vyakula. Mafanikio hayo yametokana na mafunzo kuhusu madhara ya vifungashio kwa afya na mazingira ya shule tuliyowapa wakati wa utekelezaji wa mradi. Sasa hivi kwa kiasi kikubwa wanatumia vifungashio vya karatasi,” anasema Mang’oro.
Anasema hali hiyo imepunguza uchafuzi wa taka zinazodumu kwa muda mrefu ardhini na majini bila kuoza kwa sababu plastiki laini kama vifuko vya karanga na ubuyu mara nyingi hazirejelezeki kwa urahisi na huishia kutupwa ovyo, kuziba mifereji ya maji na kusababisha mafuriko wakati wa mvua.
“Kwa hali hiyo shule hizi zinachangia kupunguza mzigo wa taka kwenye madampo, kupunguza hatari ya plastiki kuingia kwenye mito na bahari, na kulinda viumbe wa majini dhidi ya kumeza au kunaswa na plastiki. Aidha, hatua hii inapunguza uzalishaji wa gesi chafu zinazotokana na uzalishaji na uchomaji wa plastiki, hivyo kusaidia juhudi za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi,” anafafanua.
Antigone Mrema, Mwalimu wa Mazingira wa Shule ya Sekondari ya Jangwani, anasema kabla ya mradi huo shule ilikuwa na mashimo 10 ya taka mchangayiko ambazo zilikuwa zikizotoa harufu kali, hali iliyokuwa inaharibu taswira ya mazingira ya shule na kuhatarisha afya za wanafunzi.
Anasema harufu kali kutoka katika taka hizo zilikuwa kero kwa wanafunzi na kuwafanya wasifurahie kuwepo katika mazingira ya shule. “Walikuwa wakipita maeneo ya karibu na mashimo ya taka unawaona wakiziba pua, hali inayoonyesha hawafurahii harufu hiyo,” anasema.

Anafafanua kuwa wakati wa mvua, taka za vyakula zilikuwa zinaoza haraka na kutoa wadudu aina ya funza ambao walikuwa wakisambaa maeneo ya shule na kuwa kero kwa walimu na wanafunzi. Pia mabaki ya chakula na maji yanayotuama yalikuwa yakivutia wadudu kama nzi, mbu pamoja na panya, hali iliyowaweka kwenye hatari ya kukumbwa na maradhi kama kuhara, kipindupindu na malaria.
Anasema baada ya kupata mafunzo, shule hiyo yenye wanafunzi takribani 1,000 sasa inakusanya kilo 500 za taka za vyakula kwa mwezi na huzitumia kutengeneza kilo 300 za mbolea. Kati ya kilo 300 za mbolea, kilo 100 huziuza na kukusanya $65.6 (TSh170,000). Kilo 200 zilizosalia huzitumia kuboresha bustani zao za mboga.
Dominick Salamba, Ofisa wa Mazingira Mkoa wa Dar es Salaam, anapongeza uanzishwaji wa mradi wa Taka Sifuri akisema umepunguza adha ya mlundikano wa taka zinazokwenda dampo hivyo kuhifadhi mazingira ya jiji.
Anasema kwa vile shule moja inazalisha kilo 300 za taka kwa mwezi, kwa shule 10 zilizofikiwa na mradi mpaka sasa zinafanya kilo 3,000 za taka zisiende dampo au kuzagaa mitaani.
Kwa matokeo mazuri yanayoletwa na mradi huo, Ofisi ya Mazingira Mkoa wa Dar es Salaam imeweka mikakati ya kusaidia mradi wa Taka Sifuri ili uwe wa kitaifa na kuzifikia shule nyingi zaidi.
Katika kuunga mkono juhudi hizo, ofisi ya mkoa huo inatoa vibali vya kuendesha miradi hiyo haraka na kuwapatia maofisa kutoka ngazi za wilaya na kata wanaofanya nao kazi kwa ukaribu.
Kwa mujimu wa Salamba, mwamko wa shule kuupokea mradi huo ni mzuri, kwa sababu katika awamu ya pili walipokea maombi kutoka shule 15 za sekondari na msingi zikiomba kufikiwa na mradi huo, jambo ambalo katika awamu ya kwanza halikufanyika licha ya shule kuwa na taarifa. Anasema walilazimika kuzichagua shule zinazozalisha taka nyingi.
“Matokeo ni mazuri lakini tuna wajibu wa kuongeza elimu ya teknolojia hii kwa shule nyingi zaidi na kusaidia kutafuta wafadhili ili tuzifikie taasisi nyingi zaidi,” anasema.
Mifumo duni ya usimamizi wa taka inatajwa na wataalam kuwa huongeza uzalishaji wa gesi joto, kuchochea mabadiliko ya tabia nchi na kuongeza athari zake kwa jamii na mazingira.
Profesa Philip Bwathondi, Mhadhiri Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, UDSM, Shule ya Sayansi na Teknolojia ya Uvuvi (Soaf), anasema taka hatarishi kama vile sindano zilizotumika kwa wagonjwa, pamba na madripu ya dawa, yanapoingia baharini huambukiza samaki maradhi ya binadamu. Mtu anapomla samaki huyo au kuchomwa na sindano, hupata maambukizi.
“Wakati mwingine samaki wanavibeba vimelea vya magonjwa kama kansa kutoka katika taka za plastiki na mlaji wa mwisho ni binadamu. Katika kila hatua vimelea vinapenya mpaka vinafika katika mwili wa binadamu na hatimaye kusababisha magonjwa kama kansa,” anafafanua Bwathondi.
Manufaa ya mradi
Mradi wa taka sifuri umeleta faida za kiuchumi na kiafya kwa wanafunzi na walimu wa shule kupitia biashara ya maligafi zilizotengenezwa kutokana na taka zinazokusanywa.
Mang’oro anasema kuwa moja ya malengo ya kuutekeleza mradi huo shuleni ni kuonyesha kuwa taka zinaweza kuwa fursa za kiuchumi, na kutengeneza jamii ya wajasiriamali watakaowekeza kwenye taka siku zijazo. Anasema anafarijika kuona ndoto hiyo ikitimia.
Emmanuel Sedekia, Mwalimu wa Mazingira Shule ya Sekondari Kibasila, anasema kwa mwezi wanakusanya $33 (TSh85,000) kutokana na mauzo ya kilo 50 za mbolea na kilo 50 za taka za plastiki, fedha ambazo huzitumia kuendeleza mradi huo na sehemu ya mbolea hustawisha bustani za shule.
“Tangu tujue kutengeneza mbolea, watoto wetu wanakula mboga za majani za kutosha kwa sababu tunalima wenyewe hapa shuleni, hatununui mitaani, kwa hiyo tunaokoa pesa,” anasema.
Mradi huo pia umetoa fursa za kiuchumi kwa wanafunzi. Mwalimu Sedekia anasema kuwa kupitia mradi huo licha ya kutengeneza mabalozi wazuri wa Taka Sifuri majumbani, wanajivunia kuwa na vijana 10 waliojiajiri baada ya kupata mafunzo ya kutengeneza malighafi kupitia taka.
Mmoja wa wanufaika hao ni Vedasto Emanuel, ambaye alipata ujuzi wa kutengeneza picha za ukutani kwa kutumia taka za karatasi mwaka 2023 alipokuwa mwanafunzi wa kidato cha sita katika Shule ya Sekondari Kibasila.
Anasema alianza kupata kipato kutokana na ujuzi huo akiwa bado shuleni, na hata sasa akiwa mwanafunzi wa Chuo cha Usimamizi wa Fedha (IFM) anaendelea na shughuli hiyo.

“Picha moja nauza kwa $150 (TSh381,887). Wateja wangu wakubwa ni watu kutoka mataifa ya nje na kwa mwezi naweza kuuza picha zaidi ya moja, pesa ambayo inanisaidia katika matumizi yangu ya kawaida chuoni na wakati mwingine nasaidia wazazi kulipa ada,” anasema.
Afisa Afya wa Kata ya Buguruni, Rahma Nassoro, anasema kupelekwa kwa mradi huo shuleni kunaongeza nguvu ya elimu ya usafi wa mazingira na afya njema. Anasema hiyo inawasaidia kuwa na mazingira safi muda wote na pia watoto kula mlo kamili kutokana na uwepo wa bustani ya mboga za majani inayotumia mbolea ya asili.
“Watoto wakielimishwa, wanapeleka maarifa hayo kwa wazazi wao na jamii pana, na hivyo kuifanya shule kuwa kioo cha jamii katika afya,” anasema.
Uimara wa mradi
Miradi hii mara nyingi huisha baada ya miaka miwili na baada ya hapo shule huachwa zijiendeshe zenyewe chini ya uangalizi maalum wa taasisi husika, zikifanyiwa tathmini kila baada ya miezi sita. Taasisi pia zinaendelea kuwapa misaada midogo midogo kama vile kuwaunganisha na masoko pamoja kuwatafutia wafadhili ili wapate pesa za kuendesha miradi hiyo.
Mang’oro anaeleza kuwa mfumo wa Taka Sifuri waliojifunza katika nchi za Afrika Kusini, India na Kenya umeundwa kwa kuzingatia usalama wa afya na mazingira, na hauleti hatari kwa wanafunzi wala jamii inayozunguka. Anasema kuwa taka za kikaboni hutenganishwa mapema na kusimamiwa kwa njia inayodhibiti harufu, wadudu na uchafuzi, hivyo kupunguza uwezekano wa kuibuka kwa magonjwa.
“Mboji inayozalishwa hutengenezwa kwa kufuata taratibu sahihi, na inapokamilika huwa salama kutumika kwenye bustani za shule,” anasema Mang’oro. Anaongeza kuwa mfumo huu hauhusishi matumizi ya kemikali hatarishi, bali unategemea michakato ya asili na mbinu rahisi zinazoweza kudhibitiwa na walimu na wanafunzi, jambo linaloufanya kuwa salama na rafiki kwa mazingira katika maeneo ya shule.
Mipango kupanua mradi
Akizungumzia kuhusu mustakabali wa mradi wa Taka Sifuri, Mango’ro alisema taasisi hiyo ina mpango wa kuupanua zaidi ya eneo la sasa na kuufikisha katika mikoa mingine nchini. Hata hivyo, alibainisha kuwa upanuzi huo utategemea kwa kiasi kikubwa upatikanaji wa rasilimali fedha kutoka kwa wafadhili na wadau wa maendeleo.
“Tuko katika mazungumzo na washirika mbalimbali ili kupata ufadhili utakaotuwezesha kupeleka mradi huu katika mikoa mingine. Kadri tutakavyopata msaada wa kifedha ndivyo tutakavyoongeza idadi ya shule na maeneo yatakayonufaika,” aliongeza, akisisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya sekta binafsi, serikali na wadau wa mazingira katika kuhakikisha mradi huo unakuwa endelevu.
“Dhamira yetu ni kuona shule nyingi zaidi nchini zinanufaika na mpango huu, hasa katika mikoa ambayo changamoto ya usimamizi wa taka bado ni kubwa,” alisema Mango’ro.
Changamoto
Mary Edward, Mwalimu Mkuu Shule ya Msingi Taifa, anasema wanafunzi wanapata changamoto kuelewa namna ya kutenganisha taka.
Upatikanaji wa mbolea pia unatajwa kama changamoto hasa kwa shule zenye wanafunzi wachache kama Shule ya Msingi Taifa. Shule hiyo inakusanya kilo 200 za taka kwa mwezi ambazo hutoa mbolea kilo 120 ambayo huitumia kwenye bustani ya shule pekee.
Hata hivyo anasema kuwa wanatafuta wafadhili ili wawasaidie kununua vitendea kazi ikiwemo usafiri ili waweze kukusanya taka kutoka shule za jirani, hatua itakayowawezesha kuzalisha taka nyingi za kuuza na kuanza kuona matunda ya kiuchumi ya mradi huo.
Yona anashauri watunga sera kuboresha sera za mazingira na kutilia mkazo serikali kuweka mazingira mazuri kwa taasisi za kimazingira kutekeleza miradi yake kwa urahisi, ikiwemo kutoa vibali mapema na kutoa masaada wa kifedha ili kuwapa moyo.
Anashauri kuboresha miundombinu ya urejeshaji taka, na kuweka sehemu maalum za kutenganisha taka mitaani ili kuweka mazingira safi kwa watoto ili waliojifunza mbinu za kutengenisha taka shuleni wafundishe kwa vitendo mitaani.
Utekelezwaji wake duniani
Taka sifuri haifanyiki Tanzania pekee, bali hata katika nchi nyingine duniani. Katika nchi ya Kenya, miradi ya usimamizi wa taka na bustani za shule hufanyika kupitia programu za elimu ya mazingira maarufu kama ‘Eco-Schools Programme’. Kupitia miradi hii, wanafunzi hushiriki katika kutenganisha taka, kuchakata plastiki na karatasi, pamoja na kutengeneza mboji kutoka taka za chakula ili kutumika katika bustani za shule.
Nchini Ufilipino, shule za msingi na sekondari kwa kushirikiana na Serikali za mitaa na mashirika ya mazingira, zimegeuka kuwa vituo vya elimu ya mazingira vinavyosaidia kupunguza uchafuzi na kuongeza uelewa wa jamii kuhusu kupunguza na kurejelezwa kwa taka.
Kwa nchi ya Marekani wanafunzi hufundishwa kutenganisha taka, kuchakata tena plastiki na karatasi, na kutengeneza mboji kutoka mabaki ya chakula. Programu hizo zimesaidia kupunguza uchafuzi wa mazingira, kuongeza kiwango cha urejelezaji taka na kuwafundisha wanafunzi mbinu endelevu za kulinda mazingira.
Picha ya bango: Ukusanyaji taka bila kutenganishwa majumbani unapingwa na wadau wa mazingira, ukielezwa kuwa husababisha taka nyingi kutupwa dampo. Picha, Jenifer Gilla, Mongabay.