- Ukuta wa mzunguko wenye urefu wa mita 4 ulijengwa kando ya kijiji kinachopakana na Hifadhi ya Msitu wa Ngezi wakati ujenzi wa eneo la kifahari la mapumziko ulipoanza katika kisiwa cha Pemba, Zanzibar.
- Barabara ya changarawe inayopita katikati ya hifadhi ya msitu imepanuliwa ili kurahisisha usafirishaji wa bidhaa.
- Watafiti wanaonya kwamba hakuna mipango ya mazingira iliyofanywa na kwamba spishi za wanyama na mimea zaweza kutoweka iwapo mradi huo wa maendeleo utaendelea.
Mapema mwaka huu, wafanyakazi walijenga ukuta wa mzunguko kwa ajili ya hoteli ya kifahari katika kisiwa cha Pemba kando ya pwani ya Tanzania. Kuna taarifa chache za umma kuhusu maendeleo ya Mantuli, lakini ukuta huo upo mita mia chache tu magharibi mwa ardhi ya hekta 1,440 (sawa na ekari 3,558) ya Hifadhi ya Asili ya Msitu wa Ngezi-Vumawimbi, ambako wanasayansi wamegundua zaidi ya aina 80 za mimea katika miaka ya hivi karibuni, ambazo baadhi wanahofia zitatoweka kutokana na maendeleo hayo.
Kulingana na bao la matangazo karibu na msitu na mipango iliyochapishwa awali kwenye tovuti ya kampuni ya Acoarch Architects iliyo na makao yake makuu Afrika Kusini, vyumba vya mapumziko, madimbwi ya kuogelea, kituo cha mazoezi ya mwili na sehemu za kahawa vitaenea kando ya umbali wa kilomita 3 (karibu maili 2) ya fukwe za Vumawimbi, kuwanyima wakazi wa kijiji cha Makangale kilicho karibu na bahari ufikiaji wa bahari hiyo. Baadhi ya maudhui ya mtandaoni yametolewa, na kampuni ya usanifu majengo haikujibu maswali ya Mongabay.
Tim Caro ni mwanaikolojia wa mageuzi ambaye amefanya utafiti katika eneo hilo na ni mwanachama wa shirika la hisani lililosajiliwa nchini Uingereza, kwa jina la Friends of Ngezi, ambalo hufanya kazi na jamii na kukuza uhifadhi wa msitu. Alisema karibu theluthi moja ya wakazi wa Makangale hujihusisha na shughuli za uvuvi, wakifanya safari za kuvua na boti zao kutoka fukwe za Vumawimbi, ambazo pia ni sehemu maarufu ya kubarizi na burudani kwa wakazi wa kisiwani humo.
“Kulingana na ripoti za kila wiki tunazozipokea kutoka kwa jamii, ukuta wa mzunguko unazuia wanakijiji wa Makangale kufikia maeneo yao ya uvuvi, makaburi ya mababu zao, uwanja wao wa mpira, na njia za kuelekea vijiji vingine,” mwakilishi wa Friends of Ngezi aliiambia Mongabay kupitia barua pepe.

Hifadhi ya Msitu wa Ngezi ni makazi ya spishi nyingi za mimea na wanyama, ikiwa ni pamoja na mitende ya Pemba (Dypsis pembana), spishi ya Pemba flying fox (Pteropus voeltzkowi), na Watson’s reed frog (Hyperolius watsonae) pamoja na spishi ya Pemba featherleg damselfly (Platycnemis pembinges), zote zikiwa katika hatari ya kutoweka na zinazopatikana zaidi kisiwani Pemba.
Viola Clausnitzer ni mtaalamu wa wadudu na mwanachama wa Kikundi Maalum cha Wataalamu wa Dragonfly katika shirika la IUCN, mamlaka ya kimataifa ya uhifadhi wa wanyamapori, aliiambia Mongabay kwamba mimea na wanyama wengi waliopo katika hifadhi hiyo bado hawajafanyiwa utafiti.
“Hususan kwa wanyama wasio na uti wa mgongo bado hatuna ujuzi wowote. Kutokana na utafiti wa wanyama wenye uti wa mgongo na Odonata, tunaweza kudhania kuwa asilimia ya viumbe hai inaweza kuwa kubwa zaidi miongoni mwa wanyama wasio na uti wa mgongo,” aliiambia Mongabay kupitia barua pepe.
Alisema anatarajia kazi ya ujenzi wa barabara pamoja na ujenzi wa hoteli ya kifahari ya mapumziko katika msitu utamaanisha kuwa idadi isiyojulikana ya viumbe itakabiliwa na hatari ya kutoweka kabla hata ya kuelezewa kwa sayansi.

Mnamo Septemba 2025, Clausnitzer alikuwa miongoni mwa wanasayansi 14 wa kimataifa waliochapisha barua inayoitaka serikali ya Zanzibar, iliyoko katika visiwa vinavyojitawala vya Tanzania vinavyojumuisha Pemba, kufikiria kuhamishia eneo la hoteli ya mapumziko mahali pengine ili kulinda hifadhi hiyo.
Sehemu ya Ngezi huenda ndilo eneo kubwa la mwisho lililosalia la msitu wa mvua la kijani kibichi kwenye pwani ya Afrika Mashariki, mtaalamu wa mimea Michael Burkart aliiambia Mongabay kupitia simu. “Kwa kweli ni kitu cha kipekee sana, na pia hakijachunguzwa kikamilifu.”
Burkart anauchunguza Sansevieria, jenasi ya mimea inayopatikana zaidi katika sehemu ya kusini mwa jangwa la Sahara, hasa Afrika Mashariki, huku spishi chache zikitokea Madagaska, Saudi Arabia, India, Sri Lanka na Myanmar. Alisema Tanzania inaaminika kuwa na aina nyingi zaidi za mimea hiyo.
“Tuligundua spishi kadhaa za mmea wa Sansevieria ambazo hazijaelezewa kisayansi kisiwani Pemba, jambo ambalo ni la kushangaza kwa sababu kisiwa ni tambarare na si kikubwa,” Burkart alisema, akiongezea kuwa spishi hizi huenda zisipatikane popote pengine.
Hakuna ujenzi ambao umeanza ndani ya ukuta mpya wa mzunguko. Lakini mara tu utakapoanza, Burkart aliiambia Mongabay, yeye na wenzake wako tayari kuzindua zoezi la uokoaji, kuhamisha mimea inayopatikana msituni hadi kwenye bustani ya mimea ili kuihifadhi, hasa katika kisiwa kikuu, kwenye Bustani ya Mimea ya Zanzibar.
Caro aliiambia Mongabay kwamba eneo lililotengwa kwa ajili ya maendeleo ni nyumbani kwa msitu mdogo wa miti ya intsia (Intsia bijuga) iliyogunduliwa hivi karibuni: “Miti hii ni ya zamani, ina umri wa miaka 100, na haipatikani popote kwingine katika bara la Afrika.”

Wakati ubao ulio karibu na msitu unaonyesha ramani ya msitu wa juu, sehemu ya ndani zaidi ya msitu, katikati ya hifadhi haitaathiriwa moja kwa moja na eneo la mapumziko. Hata hivyo, barabara nyembamba ya changarawe inayounganisha mashariki na magharibi mwa Pemba, kaskazini mwa kisiwa, ilipanuliwa na kutiwa lami mwishoni mwa mwaka wa 2025. Clausnitzer alisema barabara hii mpya ya lami itasumbua wanyamapori katika msitu. “Barabara, ambayo zamani ilikuwa njia kupitia Ngezi, sasa ni kizuizi kwa viumbe vingi.”

Kulingana na Caro, barabara hiyo inakusudiwa kusaidia usafirishaji wa bidhaa na kuwezesha ufikiaji wa hoteli zinazoibuka katika pwani ya magharibi ya kisiwa hicho. Burkart alisema hakuna shaka kuwa barabara hiyo inahudumia mradi wa Mantuli, ambao una kituo chake kikuu cha ujenzi kusini mwa kijiji cha Makangale.
Mongabay iliwasiliana na Idara ya Misitu ya Tanzania na Idara ya Kilimo kwa maoni. Hakuna hata mmoja wao aliyejibu taarifa hii ilipochapishwa.
Clausnitzer alisema haoni jinsi ujenzi katika eneo lililochaguliwa unavyoendana na kuhifadhi thamani ya kuvutia ya uhifadhi wa Ngezi: “Hauwezi kupunguza uharibifu, kwa sababu ujenzi huo utaharibu makazi ya mwisho yaliosalia ya viumbe tayari kwenye ukingo wa kutoweka.”
Picha ya bango: Iliyokuwa barabara ya changarawe katikati ya Hifadhi Asili ya Msitu wa Ngezi imepanuliwa hivi karibuni ili kuwezesha maendeleo. Picha kwa hisani ya Viola Clausnitzer.
Nukuu
Burkart, M., Kavula, K. A., Constantine, I. K., Mollel, N. P., Piniely, L. N., Sikawa, R. A., & Yinger, B. R. (2025). Sansevieria bangalalana sp. nov. (Asparagales, Asparagaceae), close to extinction in the wild, and five other narrowly endemic and threatened species of Sansevieria from Tanzania previously unknown to science. European Journal of Taxonomy, 1026(1), 65-106. doi:10.5852/ejt.2025.1026.3113
Habari hii ilichapishwa kwa mara ya kwanza hapa kwa lugha ya Kiingereza mnamo tarehe 10/03/2026.