- Mradi wa ufugaji nyuki ni kielelezo kwamba maendeleo yanaweza kwenda sambamba na uhifadhi wa rasilimali za asili.
- Wananchi wanalinda misitu kwa sababu uoto, miti na vyanzo vya maji ni rasilimali muhimu kwa uzalishaji wa asali.
- Ufugaji umewapa wanawake uhuru wa kiuchumi na fursa ya kulinda misitu na ardhi yao.
- Ukame unaotokana na mabadiliko ya tabianchi huathiri mpangalio wa maua kwenye mimea.
Naserinyi ole Saitoti, anatoka katika jamii ya Kimasai ambako wanawake hawana sauti katika maamuzi yanayofanywa nyumbani kwa sababu huwategemea waume zao kwa kila kitu.
Yeye hafurahishwi na hali hiyo. Anatamani kuwa na kipato chake mwenyewe. Anachukua uamuzi unaopingana na mazoea, kwa kuungana na wenzake na kuanzisha mradi wa ufugaji wa nyuki. Mradi huo haumpi tu kipato, bali unazua mjadala mzito kijijini kuhusu namna uhuru wa kiuchumi unavyoweza kushamiri bila kuharibu mazingira. Leo wanawake wengi wa jamii hiyo, wamefuata nyayo zake, wakitafuta uhuru wa kiuchumi huku wakilinda misitu na ardhi yao.
Mafanikio ya Naserinyi na wanawake wenzake yameandika historia inayowaonyesha wanawake kama walinzi wa makazi muhimu ya viumbe hai na washiriki wakuu katika kutafuta suluhisho za athari zinazotokana na mabadiliko ya tabianchi, badala ya simulizi zilizozoeleka zinazowaonyesha kama waathirika wakuu wa majanga hayo.
Wanawake hao kutoka vijiji kumi vya wilaya za Simanjiro na Monduli, mkoani Manyara na Babati mkoani Arusha, wamekuwa wakichangia uhifadhi wa mazingira kupitia mradi wao wa ufugaji wa nyuki pamoja na kushiriki kwenye shughuli nyingine za uhifadhi.

Afisa wa Programu hiyo ya Ufugaji wa Nyuki, Samsom Beah, anasema uendeshaji wa mradi wa nyuki umewapa fursa wanawake kuwa walinzi wa misitu kwa vitendo, kushiriki moja kwa moja kwenye shughuli za uhifadhi wa mazingira kama upandaji miti ya asili, upandaji wa maua, usafi wa mazingira kwenye maeneo ya jamii kama hospitali na sokoni au kuanzisha shughuli nyingine inayolenga kulinda, kuhifadhi au kutunza mazingira kulingana na eneo walipo.
“Kwa hawa wanawake, ufugaji wa nyuki si mradi wa kiuchumi tu bali ni kielelezo kwamba maendeleo yanaweza kwenda sambamba na uhifadhi na shughuli endelevu kwa rasilimali za asili,” anasema Beah.
Fatuma Salum, Afisa Mwezeshaji Wanawake anasema hadi sasa akinamama wanaofanya ufugaji wa nyuki ni takribani 2,000 na wamejiunga katika vikundi 105, huku kila kikundi kikiwa na watu 20. Kabla ya kuanza kufuga, lazima waeleze ni kwa namna gani watashiriki kwenye utunzaji wa mazingira.
Mradi huo unafadhiliwa na shirika lisilo la kiserikali la African People & Wildlife (APW), ambalo huwajengea uwezo wanawake hao na pia kuwapa fedha za mradi.
Nyuki na uhifadhi
Kwa mujibu wa Beah, ufugaji wa nyuki katika wilaya hizo umechangia kwa kiasi kikubwa uhifadhi wa mazingira.
“Kwanza katika maeneo ambayo ufugaji wa nyuki unafanyika, ni marufuku kukata miti. Sheria ya Tanzania ya Ufugaji Nyuki inakataza kukatwa kwa miti iliyowekwa mizinga. Lakini pia watu huogopa kusogelea miti yenye mizinga kwa kuhofia kushambuliwa. Shughuli za kulima kwenye maeneo hayo pia haziruhusiwi,” anasema.
Anafafanua kuwa kitendo cha kutokatwa miti kinasaidia kwa namna mbalimbali kwenye uhifadhi. Anasema: “Misitu ni makazi ya wanyama, ndege na wadugu kwa hiyo kutunza makazi ya viumbe hivi, moja kwa moja kunasaidia kulinda bioanuwai. Miti pia hutoa oksijeni ambayo husafisha hewa kwa kunyonya gesi hatari kama kaboni dioksidi na kuzipunguza hewani, hivyo kufanya hewa kuwa safi zaidi. Mizizi nayo ina faida yake ya kuzuia mmomonyoko wa udongo huku majani yanayoanguka na kuoza, yakisaida kuleta virutubisho kwenye ardhi”.
Kwa mujibu wa Beah, nyuki pia wana mchango mkubwa katika kustawisha mazingira ya asili kupitia kuchavusha maua pamoja na kusaidia mimea kuzaliana kupitia kitendo cha kusambaza mbegu ambazo baadaye huota maeneo mengine.
Ingawa Beah hakutoa takwimu zinazothibtisha kiwango cha uchavushaji maua katika maeneo yote ya mradi, APW katika taarifa yake inayoonyesha kwa makadirio mizinga ya nyuki iliyotundikwa huchochea uchavushaji wa mimea ya asili katika eneo la zaidi ya kilomita za mraba 2100 (maili za mraba 810) za nyasi.

Taarifa kutoka kwenye tovuti ya Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania inaonyesha sekta ya ufugaji nyuki nchini Tanzania, huchangia usimamizi wa mazingira kwa kuhakikisha uhifadhi wa misitu na maeneo ya vichaka. Uhifadhi wa uoto wa miti husaidia kupunguza ukataji miti na uharibifu wa misitu, pamoja na kuimariha uwezo wa kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.
Kwa mujibu wa Fatuma, mkakati mwingine unaotumiwa na akinamama hao kuhifadhi mazingira ni kutengeneza bidhaa rafiki kwa mazingira. “Kutokana na nyuki wanatengeneza vitu mbalimbali vikiwemo vipodozi vya asili kama losheni, sabuni, mafuta ya ngozi na mafuta ya kulainisha midomo. Pia wanatengeneza shampoo, jeli ya kuogea na mishumaa ambayo haina kemikali hatarishi na isiyotoa moshi wenye sumu,” anasema.
Huuza bidhaa zao kwenye masoko ya kawaida, hoteli za kitalii, masoko maalum na kwenye maonyesho ya biashara ya kitaifa na kimataifa.
Mwaka jana pekee, jumla ya mizinga 263 ilivunwa na vikundi 31 vya wanawake na kuzalisha zaidi ya kilo 3000 za asali ghafi. Katika kipindi kinachoanzia mwaka 2022 hadi 2026, mapato yaliyotokana na mauzo ya asali na bidhaa nyingine zitokanazo na nyuki, yalikuwa Shilingi za Tanzania 27,357,000 (Dola za Marekani 10,395.7).
Licha ya asali, bidhaa nyingine zinazozalishwa ni mafuta ya kupaka mikono, losheni, sabuni, mishumaa pamoja na bidhaa za utunzaji wa ngozi zilizotengenezwa kutokana na nta na bidhaa za asali, anasema Fatuma.

Fatuma anasema kabla ya kuanza mradi, wanawake lazima waeleze ni kwa namna gani watashiriki kwenye uhifadhi wa mazingira ambapo wengi wamekuwa wakichagua kushiriki kwenye shughuli za uoteshaji miti, kusafirisha mazingira, kupanda maua, kazi za urejeshaji wa vyanzo vya maji, kuokota takataka za plastic kwenye maeneo ya jamii kama hospitali na sokoni na shughuli nyingine kulingana na asili ya eneo kila mmoja analoishi.
Licha ya shughuli hizi kuboresha uhifadhi lakini zinasaidia kubadilisha mitazamo ya jamii kuhusu uhifadhi, kwani watu wanapoona manufaa ya shughuli hizo, huvutiwa.
Kwa mujibu wa Fatuma, kabla ya mradi, ukataji miti kwa ajili ya kuni na kuchoma mkaa vilikuwa vimekithiri. “Maeneo mengine yalikuwa yameharibika kabisa. Eneo kama Loibosereti lililoko katika wilaya ya Simanjiro mkoa wa Manyara asili yake ni ukame na miti ilikuwa haioti lakini kwa sasa hali imebadilika, uoto umeanza kurejea na mapori yameanza kustawi tena na kuna miti mingi,” anasema Fatuma.
Matokeo mengine chanya ya mradi huo ni kuongezeka kwa uelewa kwenye jamii kuhusu faida za uhifadhi. “Kwa sasa wananchi wanaelewa masuala ya uhifadhi na faida zake. Zamani ulikuwa ukitundika mzinga, inaibiwa, lakini sasa hivi hawafanyi hivyo kwa kuwa wameona faida zake,” anasema Fatuma.

Helena Mbarnot, mmoja wa wajumbe wa vikundi vya wanawake wanaoshiriki katika mradi, anasema mradi huo licha ya kuwapa nguvu ya kiuchumi pia umewaongezea mwamko kwenye ushiriki katika shughuli za uhifadhi.
Akizungumzia namna mradi huo ulivyowapa sauti wanawake, Helena anasema; “Wanawake wengi katika jamii zetu hawana sauti katika maamuzi yanayofanyika nyumbani kwa sababu wanawategemea waume zao kifedha. Lakini kama mwanamke ana chanzo chake mwenyewe cha kipato, anaweza kushughulikia mambo ya familia ambayo ni muhimu kwake.
“Kwa mfano, wanaume wengi katika jamii zetu, hawaoni umuhimu wa kuwapeleka mabinti shule, lakini wanawake wanaelewa umuhimu wa elimu. Hivyo kuwa na chanzo chetu cha kipato, inatuwezesha kuhakikisha kwamba mabinti zetu wanapata elimu.’’
Kwa mujibu wa Fatuma, mradi huo umebadilisha mitazamo ya wanaume kuhusu umuhimu wa wanawake kushiriki kwenye shughuli za kiuchumi.
“Wakati mradi unaanza, wanaume walikuwa wakilalamika wanawake wanapokwenda kwenye shughuli za mradi lakini walipoanza kupata mavuno na pesa, walihamasika na kuwaunga mkono wake zao kiasi kwamba hivi sasa wengine wanakwenda na wake zao kurina asali. Hilo linaonyesha jinsi wanavyothamini mchango wao.’’

Brown Piano, Afisa Ufugaji Nyuki wa Wilaya, anasema maeneo mengi yaliyowekwa mizinga ya nyuki ni vigumu kuharibiwa. Maeneo mengine ulinzi umeimarishwa na watu waliokuwa wakikata miti na kuchoma mkaa, sasa hawawezi kuingia kwenye maeneo yenye mizinga.
“Maeneo yaliyokuwa yameharibiwa, sasa uoto umerudi. Kuna mabadiliko makubwa sana. Pia kuna hamasa kubwa ya watu kutunza mazingira na hili limeonekana kupitia namna wanavyoshindana yanapotangazwa mashindano katika kutunza mazingira.’’ Alisema Brown bila kutoa takwimu zinazoonyesha ni eneo lenye ukubwa wa ekari ngapi limerejea kwenye hali yake ya asili.
Ufugaji wa nyuki kama nyenzo ya kulinda misitu
Ufugaji nyuki ni mradi rafiki kwa mazingira ambao umeonyesha mafanikio makubwa nchini Tanzania. Frankline Masika, Mtalaam wa Masuala ya Uhifadhi, anaeleza uzoefu wake katika utekelezaji wa miradi miwili iliyompa fursa ya kufanya kazi moja kwa moja na wanajamii kufuga nyuki kama nyenzo ya kulinda misitu.
Mradi wa kwanza ulifanyika Mufindi na Iringa kati ya mwaka 2014 na 2017 na kushirikisha vikundi 32 vilivyojumuisha wananchi wanaoishi maeneo mbalimbali yakiwemo ya pembezoni mwa hifadhi ya Ruaha (hasa vikundi vinavyounda hifadhi ya jumuiya ya MBOMIPA), pembezoni mwa bwawa la Mtera na pembezoni mwa misitu ya kupanda ya Sao Hill, na vijiji vyenye utajiri wa misitu ya asili.
“Vikundi hivyo vilihamasika kulinda misitu kwa sababu uoto, miti na vyanzo vya maji ni rasilimali muhimu kwa uzalishaji wa asali. Hii iliwafanya washiriki kuwa mstari wa mbele katika kuzuia uchomaji moto na kulinda misitu, kwani wengi walitundika mizinga yao humo,” anasema.
Anafafanua kuwa uzalishaji wa asali ulikwenda sambamba na ubora wa mazingira. “Kwa mfano, Mufindi hususani pembezoni mwa Sao Hill, vikundi vilivuna asali nyingi na zaidi ya mara moja kwa mwaka kutokana na unyevunyevu, miti yenye maua na vyanzo vya maji. Hata hivyo, hali haikuwa hivyo kwenye maeneo ya ukame,” anasema.
Mradi wa pili ulifanyika Nkasi na Sumbawanga kati ya mwaka 2020 na 2025. Huu ulitumia tope, kinyesi cha ng’ombe na mabaki ya mabua ya zao la alizeti kutengeneza mizinga ya kienyeji. Lengo lilikuwa kutumia rasilimali zinazopatikana kwa urahisi ili kupunguza ukataji wa magogo makubwa.
Anasema mafanikio makubwa yalipatikana kwani wananchi, hasa wasio na mitaji, waliweza kutengeneza mizinga na kutundika kwenye misitu ya kijiji. Faida kubwa ilikuwa kuzuia moto kichaa kwenye misitu ya kijiji, kutumia mabaki ya mazao ambayo mara nyingi huchomwa wakati wa maandalizi ya mashamba, na kudhibiti uingiaji holela misituni.
“Kwa ujumla, nyuki wamekuwa chachu ya uhifadhi wa mazingira na bidhaa zao kama asali na nta zimekuwa rafiki kwa mazingira kwa kutoa kipato endelevu bila kuharibu misitu,’’ anasema.
Changamoto ya ukame
Brown alitaja mabadiliko ya tabianchi kama changamoto kubwa wanayokabiliana nayo. Alisema mpangalio wa maua kwenye mimea unaathirika kutokana na baadhi ya maeneo kuwa makame. Kadhalika alitaja ongezeko la watu kama changamoto inayoweza kulazimisha watu kuingia kwenye maeneo yaliyotunzwa.
Kuhusu ushiriki wa Serikali, Fatuma alisema wanawake wamekuwa wakipewa ushirikiano wa kutosha katika ngazi mbalimbali. Alifafanaua kuwa ardhi waliyojenga viwanda vya kuchakata asali na vituo vya biashara wamepewa na halmashauri za wilaya na tayari wamepewa umiliki. Alisema maafisa wa Serikali hushiriki pia katika kutoa utaalam na kuwatafutia masoko kwa ajili ya biadhaa zao.
Kuhusu mradi huo kuwa endelevu, Fatuma anasema kwa kuwa usimamizi uko mikononi mwa wanawake wenyewe, wamejengewa uwezo, wanakopesheka na vikundi vyao sasa vinaaminika, mradi huo utaendelea kufanya vizuri.
Sera na Sheria ya Ufugaji Nyuki
Ufugaji nyuki nchini Tanzania unaongozwa na sera na sheria mbalimbali zikijumuisha Sera ya Taifa ya Ufugaji Nyuki (1998), Sheria ya Ufugaji Nyuki (2002), Kanuni za 2005, pamoja na sera za misitu, wanyamapori na ardhi za vijijini. Vyote hivi vinalenga kuendeleza sekta hiyo kwa maendeleo ya kiuchumi, kijamii na uhifadhi wa mazingira.

Taarifa kutoka kwenye tovuti ya Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania inaonyesha sekta ya ufugaji wa nyuki nchini Tanzania, inakadiriwa kuzalisha kiasi cha dola za Marekani milioni 77.5 kila mwaka kutokana na mauzo ya asali na nta. Kufuatia uzalishaji huo, sekta hiyo huchangia karibu asilimia 1 ya pato la Taida (GDP).
Sekta hiyo imeajiri watu takribani milioni 2 nchini kote ambao wanachangia hadi asilimia 33 ya mapato ya kaya hasa zile za jamii zinazoishi karibu na misitu na milima. Ufugaji wa nyuki kusaidia uhifadhi wa viumbe hai na kuongeza uzalishaji wa kilimo kupitia uchavushaji wa mimea.