- Asilimia 90 ya kaya za Tanzania hutegemea zaidi mkaa au kuni.
- Kupikia nishati ya umeme kunaweza kupunguza ukatwaji wa misitu, lakini hilo litawezekana tu ikiwa nishati hiyo itapatikana kwa kaya zenye kipato cha chini.
- Muundo wa sasa wa ruzuku kwa majiko ya umeme sio rafiki kwa sababu haujawafikia walengwa wengi ambao ni masikini.
- Mifumo zaidi ya nishati jadidifu kama vile umeme jua, umeme wa upepo na ule unaotokana na kinyesi vitaimarisha upatikanaji wa umeme kwa bei nafuu.
Hii ni sehemu ya kwanza ya habari kuhusu Mkakati wa Taifa wa Nishati Safi ya Kupikia, mpango uliozinduliwa kwa lengo la kuokoa misitu. Soma sehemu ya pili hapa.
Katika kipindi ambacho misitu ya Tanzania inaendelea kupotea kwa kasi kutokana ukataji miti unaochochewa na matumizi makubwa ya kuni na mkaa, serikali imezindua Mkakati wa Taifa wa Nishati Safi ya Kupikia (NSCCE 2024–2034). Lengo la mkakati huo ni kuhakikisha kuwa asilimia 80 ya kaya za Watanzania zinatumia nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034.
Uamuzi huu ulitangazwa Mei 2024 na Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan kama sehemu ya jitihada za kupunguza ukataji misitu, kulinda afya za wananchi wanaotumia mkaa na kuni, na kufikia malengo ya kimataifa ya kupunguza athari za mabadiliko ya tabianchi.
Ripoti ya utafiti wa mwaka 2021 uliofanywa na Taasisi ya Tanzania Traditional Energy Development Organization (TaTEDO) ilionyesha kuwa asilimia 90 ya kaya za Tanzania hutegemea zaidi mkaa au kuni, huku asilimia 97 ya familia za vijijini zikiathiriwa na moshi hatari wa kuni wanapopika majumbani.
Ripoti hiyo inaonyesha ongezeko la matumizi ya mkaa katika kipindi cha miaka kumi — 2007 hadi 2017 — kutokana na miji kuongezeka, hali inayoongeza hatari ya uharibifu wa misitu. Ripoti hiyo ilionya kuwa iwapo hatua za haraka hazitachukuliwa kudhibiti hali hiyo, matumizi ya nishati hiyo yanakadiriwa kuongezeka maradufu ifikapo mwaka 2030.
Wakati huo huo, Ripoti ya Pamoja ya Utendaji wa Kiuchumi wa Kanda ya Mwaka 2025 (Consolidated Zonal Economic Performance Report 2025) inaonyesha kuwa mauzo ya mkaa nchini Tanzania yaliongezeka kutoka $1,377,953 (TSh bilioni 3.5) kwa mwaka ulioishia Machi, 2023 hadi $2,992,126 (TSh bilioni 7.6) Machi, 2025, hali inayoashiria ongezeko kubwa la mahitaji ya mkaa.
Kwa mujibu wa tathmini za setilaiti za Global Forest Watch, Tanzania ilipoteza hekta milioni 3.48 za misitu kati ya mwaka 2001 na 2024. Kwa mwaka 2024 pekee, misitu iliyopotea ni hekta 271,000.
Mkakati wa Taifa wa Nishati Safi ya Kupikia (NSCCE 2024–2034), unasisitiza matumizi ya majiko ya umeme kama mbadala wa kuni na mkaa. Pia unalenga kubadilisha mamilioni ya kaya kutoka matumizi ya mfumo hatari wa kuni na mkaa kwenda kwenye matumizi ya nishati safi. Ikiwa ni zaidi ya mwaka mmoja tangu kuzinduliwa kwa mkakati huo, swali la msingi linalowaumiza watu vichwa ni: Je, malengo ya kuhakikisha asilimia 80 ya kaya za Watanzania zinatumia nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034 yanatekelezeka?
Kupikia umeme bado ni kitendawili
Matumizi ya umeme bado ni changamoto kubwa kwa kaya nyingi, hususan zile za vijijini. Utafiti wa mwaka 2025 kuhusu mabadiliko ya nishati ya kupikia katika kaya za Tanzania uliofanywa na Jires Tunguhole na wenzake, ulionyesha kuwa licha ya upatikanaji wa umeme kuongezeka kitaifa, bado hautumiwi na kaya nyingi kama nishati ya kupikia kutokana na sababu mbalimbali, zikiwemo za uwezo mdogo wa kiuchumi.
Kwa mujibu wa Irene Goele, Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano na Huduma kwa Wateja wa TANESCO, kufikia mwaka 2025, shirika hilo limefikisha wateja milioni 5.6, hii ikiwa ni idadi ya watumiaji umeme nchini Tanzania. Kwa mujibu wa Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2022, nchi nzima ina kaya milioni 14.2.
Kwa upande wa vijijini, idadi ya watumiaji wa umeme bado ni ndogo. Ripoti ya Mabadiliko ya matumizi ya nishati ya kupikia katika kaya nchini Tanzania inaonyesha ni asilimia 16.47 pekee ya kaya zenye ajira za mishahara zinazotumia umeme kama nishati yao kuu ya kupikia, wakati kaya za wakulima zikiwa ni asilimia 11.01 na kaya zisizokuwa za wakulima idadi yao ikiwa ni asilimia 2.44.
Ripoti hiyo inaonya kuwa upatikanaji wa umeme pekee hautoshi kutegemea kama nishati kuu ya kupikia kutokana na vikwazo vingi vya kimuundo na kijamii ikiwemo gharama kubwa za vifaa vya umeme vya kupikia, upatikanaji mdogo wa vifaa vyenye ufanisi wa nishati hiyo kama vile majiko, masufuria pamoja na hitaji la kuboresha mifumo ya nyaya za majumbani ili kuhimili mzigo wa kupikia.
Kwa sasa majiko ya kupikia ya umeme yanauzwa kwa kati ya $59 na $138 (TSh150,000 na TSh350,000), huku masufuria yakigharimu $24 hadi $30 (TSh60,000 – TSh75,000) kwa seti, gharama ambazo kaya zenye kipato cha chini haziwezi kumudu.
Utafiti pia unaonyesha kuwa kukosekana kwa umeme wa uhakika, changamoto inayotokana na kukatika mara kwa mara kwa umeme na mabadiliko ya viwango vya umeme, hupunguza imani ya watu kutumia majiko ya umeme kupikia.
Changamoto nyingine ni gharama ya kuunganisha umeme majumbani. Kaya nyingi haziwezi kumudu gharama za waya na vifaa vya usalama na ufungaji wa mita. Pia, uelewa mdogo kuhusu faida na matumizi sahihi ya majiko ya umeme, pamoja na imani potofu kwamba umeme ni ghali kupikia, umechangia kaya nyingi kuendelea kutegemea kuni na mkaa.
Kwa baadhi ya maeneo ya vijijini, upatikanaji hafifu wa umeme na miundombinu dhaifu ya usambazaji bado ni kikwazo kikubwa.
Kwa mujibu wa utafiti huo, matumizi ya kuni kupikia yanaongoza vijijini kwa asilimia 75.15, huku mkaa ukiendelea kuwa nishati inayoongoza mijini kwa asilimia 43.99, hali inayoonyesha kuwa hata kaya zenye kipato cha uhakika zinaendelea kutumia mkaa na umeme.
Utafiti unapendekeza kuwa serikali, kwa kushirikiana na sekta binafsi na washirika wa maendeleo, zichukue hatua mahsusi za kuboresha huduma za umeme ili wananchi wamudu gharama. Hatua hizo ni pamoja na kutoa ruzuku kwa vifaa bora vya umeme vya kupikia.

Hatua nyingine ni kuweka viwango maalum vya umeme kwa ajili ya matumizi ya kupikia, na kuanzisha mifumo rahisi ya ufadhili kwa kaya zenye kipato cha chini ili kuongeza matumizi ya nishati safi ya kupikia.
Nishati safi: Nini kimefanyika?
Kwa mujibu wa Jiolojia Mkuu katika Wizara ya Nishati, Ngereja Mgejwa, tangu kuzinduliwa kwa Mkakati wa Taifa wa Nishati Safi ya Kupikia, serikali imechukua hatua kadhaa za awali, ikiwemo usambazaji wa majaribio wa majiko ya umeme 5,000 kupitia mpango wa mikopo isiyo na riba unaolipwa kupitia bili za umeme.
Katika mfumo huo, kaya zinazounganishwa na umeme kwa mara ya kwanza hukopeshwa majiko ya umeme kwa $59 (TSh150,000) na gharama ya jiko hulipwa kidogo kidogo kwa kukatwa asilimia 25 ya malipo ya bili za umeme kwa kipindi cha mwaka mmoja.
Mgejwa anasema kuwa hadi sasa, majiko hayo ya umeme yamesambazwa katika wilaya 13 tu zilizopo katika mikoa ya Dar es Salaam, Dodoma, Mwanza, Morogoro, Pwani na Kagera, kupitia mradi wa Connect Umeme unaotekelezwa na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO).
Sambamba na hilo, Wizara ya Nishati imetoa kibali kwa kampuni za wazawa 28 kuuza na kukopesha majiko hayo. Kampuni hizo tayari zimesambaza zaidi ya majiko ya umeme 10,000.
Mgejwa anasema kuwa chini ya mkakati huo, sekta binafsi inatarajiwa kuwa na jukumu la msingi ambalo ni kuongeza usambazaji wa majiko, ili kuwafikia wananchi wengi ndani ya muda mfupi, kwa kuwa serikali peke yake haiwezi kufikia malengo hayo.
Licha ya juhudi hizo, kiwango cha utekelezaji bado ni kidogo. Wakati mkakati wa taifa unalenga kuhakikisha asilimia 80 ya kaya zote Tanzania zinafanya upishi safi ifikapo mwaka 2034, ni takribani majiko ya umeme 15,000 pekee ambayo yamesambazwa hadi sasa kati ya kaya milioni 5.6 zinazotumia umeme, hali inayoonyesha usambazaji huo unakwenda kwa kasi ndogo ikilinganishwa na mahitaji halisi ya kufikia malengo hayo.
Mhandisi Matthew Josephat Matimbwi, Katibu Mtendaji wa Chama cha Nishati Jadidifu Tanzania (TAREA), anasema kupikia nishati ya umeme kunaweza kupunguza ukatwaji wa misitu, lakini hilo litawezekana tu ikiwa nishati hiyo itapatikana kwa kaya zenye kipato cha chini, ambazo ndizo nyingi nchini na pia asilimia kubwa zinatumia kuni.
Anasema ili kufikia malengo ya asilimia 80 ya kaya zote nchini kutumia majiko ya umeme kupikia ifikapo mwaka 2034, Tanzania itahitaji kuwa na viwango maalum vya umeme kwa ajili ya kupikia, ruzuku endelevu zisizoharibu soko, uboreshaji wa gridi ya usambazaji umeme, pamoja na teknolojia ya kuzalisha majiko hayo ndani ya nchi ili kupunguza gharama ya kuyanunua kutoka nje.
Hivi sasa, majiko hayo kwa mkopo yanauzwa kwa bei ya takriban $49 – $126 (TSh125,000 – TSh320,000) kila moja, kiasi ambacho kwa Watanzania wa kawaida bado ni kikubwa.
Bila hatua za kupunguza gharama hizo, Matimbwi anaonya kuwa kasi ya kuhamia kwenye matumizi ya nishati hiyo kupikia itaendelea kuwa ndogo na kufanya malengo hayo kutofikiwa, hususan kwa kaya zenye kipato cha chini na zile za vijijini zinazotegemea zaidi mkaa na kuni.
“Iwapo umeme hautakuwa wa uhakika au utakuwa ghali sana, watu wataendelea kutumia mkaa na kuni. Kwa hiyo utegemezi wa umeme wa gridi ya taifa pekee kama nishati ya kupikia hauwezi kuokoa misitu,” anafafanua.
Matimbwi anashauri serikali kushirikiana na kampuni binafsi kufunga mifumo zaidi ya nishati jadidifu (off-grid) kama vile umeme jua, umeme wa upepo na ule unaotokana na kinyesi cha wanyama na binadamu ili kuimarisha upatikanaji wa umeme kwa bei nafuu.
Anasema mifumo hiyo tayari imeanza kufanya kazi nchini japo kwa kiwango kidogo, lakini imetoa matokeo makubwa. Baadhi ya kampuni chini ya mwamvuli wa TAREA zinatoa huduma ya umemejua kwenye shule na hospitali unaotumika kupikia idadi kubwa ya watu.
Kwa mujibu wa Matimbwi, kwa kubadili matumizi ya kuni na mkaa kwenda mpaka kupikia umeme unaotokana na nishati ya jua, taasisi hizo zinapunguza kwa kiasi kikubwa matumizi ya kuni na mkaa.
“Kwa kuwa shule hupika chakula kingi kila siku, zinatumia kuni au mkaa mwingi kwa siku, kwa kuhamia kwenye majiko ya umeme zinapunguza uharibifu wa misitu kwa kiasi kikubwa,” anasema.
Matimbwi pia anataja mifumo ya gridi ndogo ya umeme kama njia nyingine itakayosaidia kupunguza matumizi ya kuni na mkaa kama serikali itatoa ruzuku katika uendeshaji wa mitambo. Anatoa mfano katika Wilaya ya Mufindi mkoani Iringa, ambapo taasisi zilizo chini ya TATEDO zimeunganisha vijiji 30 na mfumo mdogo wa umeme unaochanganya umeme wa maji.
Anasema wanakijiji wananufaika na umeme huo japokuwa gharama zake ni kubwa ukilinganisha na umeme wa REA kwa sababu kampuni zilizowekeza zinatumia gharama kubwa kuendesha mitambo yao kwa kuwa hawapati ruzuku kutoka serikalini.
“Wananchi wanapopika kwa kutumia umeme, matumizi ya umeme huongezeka. Kwa hiyo hata biashara za mini-grid zinaimarika na wakati huohuo kupunguza utegemezi wa kuni na mkaa,” anaeleza Matimbwi.
Msaada wa kumudu gharama
Ili kusaidia kaya zisizo na uwezo wa kumudu gharama za matumizi zinazoambatana na matumizi ya nishati safi, Serikali ilianzisha mradi wa Connect Umeme. Kwa mujibu wa Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano na Huduma kwa Wateja wa TANESCO Irene Goele, mpango wa Connect Umeme ulianzishwa mahsusi baada ya kuzinduliwa mkakati ili kuziwezesha kaya zisizo na uwezo pia kunufaika na mipango ya upishi wa kutumia nishati safi.

Mpango huo unalenga kuwafikia wateja wasiokuwa na uwezo wa kumudu gharama za majiko ya umeme ya kisasa, ambazo zilikuwa zikikwamisha kufikiwa kwa malengo ya serikali.
Chini ya mpango huo, kaya hupokea majiko ya umeme yenye thamani ya $59 (TSh150,000). Badala ya kulipa fedha taslimu mara moja, wateja hulipa taratibu: asilimia 25 ya thamani ya kila ununuzi wa umeme hukatwa moja kwa moja, huku malipo ya kila mwezi yakiwa yamewekewa kikomo cha $5 (TSh12,500).
Anasema katika awamu ya kwanza ya majaribio ya mpango wa Connect Umeme, ulioungwa mkono na mradi wa Modern Energy Cooking Services (MECS), zilifikiwa jumla ya kaya 1,000 katika maeneo teule ya mijini na pembezoni mwa miji, ikiwemo baadhi ya maeneo ya Dar es Salaam na Dodoma.
Goele anasema serikali inaitumia awamu hii kuchunguza mahitaji, kuelewa sifa za majiko zinazothaminiwa zaidi na kaya, na kubaini vikwazo, ili awamu ya pili iweze kufikia vyema kaya zenye kipato cha chini.
“Kwa nusu uniti ya umeme, inayogharimu takribani $0.07 (TSh175), kaya inaweza kupika mlo wa siku nzima, ikiwemo maharage. Kwa kaya nyingi za Tanzania, gharama hii ni ndogo ikilinganishwa na matumizi ya kila siku ya mkaa au kuni, hususan katika maeneo ya mijini ambako bei ya mkaa ni kubwa,” anasema.
Ruzuku endelevu
Swali lingine la msingi juu ya utekelezaji wa mpango huu ni kama ruzuku zinazotolewa ni endelevu, na je, ni kwa kiasi gani zitaweza kuchangia kufikiwa kwa malengo ya Mkakati wa Taifa wa Nishati Safi ya Kupikia?
Kwa mujibu wa Mhandisi Matthew Josephat Matimbwi, Katibu Mtendaji wa TAREA, muundo wa sasa wa ruzuku kwa majiko ya umeme sio rafiki kwani haujawafikia walengwa wengi ambao ni masikini. Badala yake, umejikita zaidi kwenye miradi ya majaribio na usambazaji wa idadi ndogo ya vifaa kupitia programu maalum.
Aidha, ruzuku nyingi hazipungui moja kwa moja kwenye bei ya sokoni, hivyo gharama ya majiko bado inabaki kuwa kubwa kwa kaya nyingi, hasa zenye kipato cha chini.
Kwa mtazamo wa wataalamu wa nishati kama TAREA, muundo unaokidhi mahitaji ni ule unaoweka ruzuku moja kwa moja kwenye bidhaa, ili bei ya jiko ishuke kwa kila mnunuzi sokoni, badala ya kutegemea miradi maalum. Anashauri pia kuwepo kwa mfumo rasmi wa mikopo nafuu kwa watumiaji, pamoja na sera ya kitaifa ya bei maalum ya umeme kwa matumizi ya kupikia.
Anaeleza kuwa majiko mengi ya umeme yanayouzwa Tanzania kwa takribani $59 (TSh150,000) tayari yamewekewa ruzuku, hata kama walengwa hawatambui hilo.
“Hizi si bei halisi za soko,” anasema. “Tayari zina ruzuku.”
Kwa lugha rahisi, baadhi ya kampuni hupunguza bei za majiko kwa kupata ruzuku kutoka serikalini na wafadhili kama vile CookFund inayoungwa mkono na Umoja wa Ulaya, ambayo husaidia wasambazaji kubeba sehemu ya gharama ili kaya zilipie kiasi kidogo mwanzoni.
“Bila ruzuku ndio unaona majiko yakiuzwa kwa takribani $137 (TSh350,000) katika maduka makubwa, bei ambazo ziko nje ya uwezo wa kaya nyingi za Tanzania,” anasema Matimbwi.

Anaonya kuwa ruzuku zisizobuniwa vizuri zinaweza kuleta madhara, akitolea mfano uzoefu wa awali wa Tanzania katika majiko banifu ya mkaa unaotokana na taka, ambayo bei yake halisi ni $19 (TSh50000) lakini yalipata mfadhili akayalipia ruzuku baadhi yakauzwa $3.9 (TSh9,000). Yalipoisha, gharama ikarudi kuwa ile ya mwanzoni.
Matokeo yake? Watu hawakununua tena majiko hayo, hivyo mauzo yalidorora, wasambazaji walifunga biashara, na vijana waliokuwa wameajiriwa katika minyororo ya ugavi wa majiko walipoteza ajira zao.
“Huwezi kamwe kumshawishi mtu aliyenunua jiko kwa TSh8,000 (aje kulinunua tena kwa TSh50,000, matokeo yake soko linakufa na wazalishaji wanabaki na hasara,” anasema Matimbwi.
Anasema pia gharama kubwa za kuunganisha umeme majumbani ni kikwazo kwani kaya nyingi hazina uwezo wa kulipia $1,170 (TSh milioni 3) na matokeo yake, familia nyingi zinaendelea kutegemea mkaa na kuni hata pale miundombinu ya umeme inapokuwa karibu.
Picha ya bango: Mashamba ya miti ni uwekezaji wa muda mrefu unaolinda mazingira, kuimarisha upatikanaji wa maji na kupunguza athari za mabadiliko ya tabianchi. Shamba la miti la Wino lililo katika wilaya ya Madaba, Mkoa wa Ruvuma, ni miongoni mwa mashamba yanayotunzwa vizuri nchini Tanzania. Picha na TFS.