- Ujenzi wa kuta hai umeleta suluhisho linalonufaisha binadamu na mazingira.
- Wananchi sasa wanaelewa umuhimu wa kuwalinda wanyamapori badala ya kuwaua, jambo ambalo lina manufaa kwao wenyewe na kwa jamii.
- Kuna maeneo mengine wanyama kama simba walikuwa karibu kutoweka. Sasa wamerejea kwenye mazingira yao.
- Mafanikio ya mradi yamechangiwa na ushirikishwaji mpana wa wanajamii wenyewe katika utekelezaji wake.
Kwa miongo kadhaa, migogoro kati ya binadamu na wanyamapori imekuwa chanzo cha vifo vya simba, mauaji ya mifugo, kukatwa kwa miti na kuharibu mifumo ya ikolojia Kaskazini mwa Tanzania.
Hata hivyo, suluhisho kupitia ujenzi wa ukuta hai umewezesha, kwa kiasi kikubwa, kupunguzwa kwa matukio hayo, na kuibuka kuwa kielelezo bora cha namna binadamu na wanyamapori wanavyoweza kuishi kwa amani.
Elvis Kisimir, Meneja wa Miradi wa African People na Wildlife (APW), taasisi iliyobuni mpango huo, anasema mradi unatekelezwa katika wilaya mbalimbali za Kaskazini mwa Tanzania, zikiwemo Simanjiro, Monduli, Babati, Ngorongoro, Longido, Same na Mwanga. Lakini pia utekelezaji wake umeanza katika mkoa wa Morogoro katika wilaya ya Kilosa.
Kwa mujibu wa takwimu za APW, hadi sasa mradi huo umenufaisha vijiji 73, vikiwemo vinne kutoka Wilaya ya Kilosa, Mkoa wa Morogoro. Jumla ya kuta hai zilizojejngwa hadi sasa ni 2,117 wakati idadi ya wananchi wanaonufaika ni 24,634.
Migogoro ya watu na wanyamapori
Ukuta hai ni mradi ulioanzishwa kwa lengo la kutafuta ufumbuzi wa kudumu dhidi ya matukio ya wanyamapori kudhuriwa au kuuawa kutokana na vitendo vya ulipizaji kisasi kutoka kwa wananchi, kufuatia uvamizi wa mazizi na wanyamapori pamoja na kuliwa kwa mifugo yao, anasimulia Elvis.
Raphael Leemai Siria, mkazi wa kijiji cha Narakauwo, wilaya ya Simanjiro mkoani Manyara, alikuwa akipoteza mifugo yake mara kwa mara kutokana na uvamizi wa wanyamapori kama simba, mbwa mwitu na fisi waliokuwa wakivamia maeneo ya makazi. “Miaka iliyopita, zaidi ya asilimia 25 ya mifugo yangu ilikuwa ikiliwa kila mwaka na wanyamapori. Kuna wakati nilipoteza mbuzi na kondoo 30 katika tukio moja la uvamizi,” anasema.
“Kifo cha ng’ombe, mbuzi au kondoo ni hasara kubwa kwetu. Kulipiza kisasi kwa kuua wanyama walioua mifugo yetu ndiyo lilikuwa suluhisho,” anasema.

Wananchi katika wilaya hizo, kila mmoja alikuwa na simulizi yake ya maumivu, huku wote wakijaribu mbinu mbalimbali kumaliza kadhia hiyo, lakini bila mafanikio.
“Nikiwa katika hali ya kuchanganyikiwa kufuatia matukio ya uvamizi wa mifugo yangu yaliyokuwa yakijirudia, nilisikia taarifa kuhusu ukuta hai. Baadaye nilipata fursa ya kuona moja ya mazizi yaliyojengwa kwa jirani yangu. Nilipoulizia, nilipewa mawasiliano ya APW na nilipowasiliana nao, wakakubali kunisadia kujenga zizi imara,” anasema Raphael.
Anaongeza kuwa, kwa mujibu wa taratibu za mradi huo, alichangia asilimia 25 ya gharama na ujenzi, kisha ujenzi ukatekelezwa. “Uanzishwaji wa mradi huu wa ukuta hai umeleta suluhisho linalonufaisha pande zote mbili, yaani binadamu na mazingira,” anasema.
Leo, Raphael hana tena wasiwasi wa kuvamiwa kwa mifugo yake.
Dhana ya ukuta hai
Mazizi hayo huitwa ukuta hai kwa sababu matawi ya miti yanayotumika katika ujenzi wake, japokuwa hukatwa, hupandwa na kuota upya kisha kuendelea kukua kuelekea juu hadi kuunda uzio. Miti inayotumika ni ya asili ya eneo husika, haichukuliwi kutoka maeneo mengine. Kwa mfano, katika Wilaya ya Simanjiro, Mkoa wa Manyara, miti ya asili inayotumika kwa wingi ni ubani [Commiphora], ambayo Wamaasai pia huita Olosokonoi.
Kwa mujibu wa Elvis, ujenzi wa ukuta hai ni rahisi, unatumia gharama nafuu, unastahimili mabadiliko ya tabianchi na pia unadumu kwa zaidi ya miaka 25.
“Hatua ya kwanza ni kukata matawi ya miti ya asili ya eneo husika na kuyapanda kwa umbo la duara. Baada ya hapo, huchimbwa mfereji unaozunguka eneo lote, na baadaye kuwekwa uzio wa waya wa chuma ndani ya mfereji huo kabla ya kuuzungusha kwenye miti itakayoendelea kukua na kuongeza urefu. Zizi linalojengwa kwa utaratibu huo ni imara na hakuna mnyama anayeweza kupenya,” anasema Elvis.

Katika utekelezaji wa mradi huo, mwananchi huchangia asilimia 25 ya gharama za ujenzi, huku taasisi ya APW ikigharamia asilimia iliyobaki. Aidha, wananchi hushiriki katika kuandaa miti na taasisi hiyo hutoa wataalamu wake kwa ajili ya ujenzi.
Elvis anafafanua kuwa wanyamapori wanapofika katika maeneo ya makazi na kujaribu kubomoa boma la kwanza na kukutana na ukuta hai, la pili na la tatu na kukuta hali ile ile, hukata tamaa na kuondoka kurejea katika maeneo yao ya kawaida. Kwa kuwa hawaleti madhara yoyote, hakuna anayewadhuru, na mara nyingi hawarudi tena eneo hilo. Kutokana na hali hiyo, hata maboma ambayo hayajazungushiwa kuta hai hubaki salama.
Kabla ya kuanza kwa mradi huo, katika maeneo hayo kulikuwa na matukio mengi ya wanyamapori kuvamia makazi ya watu na kula mifugo na kuharibu mali.
Frankline Masika, mtalaam wa masuala ya uhifadhi, anasema Kaskazini mwa Tanzania, matukio ya wanyamaporti kuvamia maeneo ya makazi ya wananchi yamekuwa yakijitokeza mara kwa mara, hususan katika kipindi cha ukame, ambapo wanyama hulazimika kutoka katika makazi yao ya asili kutafuta malisho na maji. Hali hiyo husababisha changamoto kubwa kati ya wananchi na wanyamapori, na wakati huohuo kuzua migogoro kati ya wananchi na wahifadhi. Baadhi ya wananchi wanapojaribu kulipiza kisasi kwa kuwadhuru wanyamapori, hujikuta wamekiuka sheria na kuchukuliwa hatua za kisheria.
Julius Hakalo, mkazi wa Kijiji cha Loibor Sirek, wilaya ya Simanjiro, mkoani Manyara, anasema licha ya kuwaua wanyama waliovamia mifugo yao, “pia tulikata miti mara kwa mara kwa ajili ya kujengea mazizi, lakini simba waliendelea kutuvamia kwa kuwa mazizi hayo hayakuwa imara. Tulilazimika kuamka usiku kulinda mifugo yetu isivamiwe na kuliwa.
“Sasa tuna amani na tunalala usingizi mzuri. Idadi ya simba imeongezeka kwa sababu hakuna anayewaua tena, hata tunapokutana nao, hupishana bila madhara,” anasema.
Kwa mujibu wa Elvis, katika utekelezaji wa mradi huo, shughuli zote hufanywa na wanaume na wanawake. Hata hivyo, anaeleza kuwa awali ilikuwa vigumu kwa wanawake kukubalika, lakini kadri muda ulivyopita, walipata ushirikiano kutoka kwa wananchi kama ilivyo kwa wanaume.
Aidha, Elvis anasema kuwa wamekuwa wakipata ushirikiano mzuri wa serikali katika ngazi zote. “Serikali katika ngazi zote, kuanzia wilaya hadi kijiji, inashirikiana nasi kwa kiwango kikubwa. Kwa mfano, maafisa wetu hupitia Serikali ya kijiji kabla ya kuanza shughuli za kuwaelimisha wananchi, kukusanya taarifa au kufuatilia mifugo iliyopotea,” Elvis aliiambia Mongabay.
“Pia, katika ngazi ya wilaya, kuna mratibu maalum anayeturahisishia mawasiliano. Vilevile, tunapotaka kufanya vikao na wananchi, Serikali hubeba jukumu la kuitisha vikao hivyo, jambo ambalo limechangia kwa kiasi kikubwa kujenga imani ya wananchi kuhusu shughuli zetu. Serikali imekuwa ikishiriki moja kwa moja, kuanzia hatua za awali za vikao,” aliongeza.
Matokeo chanya
Ukuta hai unaelezwa kuwa miongoni mwa miradi ambayo imekuwa na mafanikio makubwa, si kwa wanajamii pekee bali pia katika kuimarisha bayoanuai na mifumo ya ikolojia katika maeneo unakotekelezwa.
Frankline Masika, mtalaam wa masuala ya uhifadhi, anasema faida za ujenzi wa kuta hizo ni kubwa zaidi ikilinganishwa na hasara zinazotokea pale wanyamapori wanapovamia maeneo ya makazi ya wananchi.
“Kuta hizi zina faida kubwa, si tu katika kuzuia wanyamapori kuvamia mifugo na makazi ya watu, bali pia katika uhifadhi wa mfumo wa ikolojia. Mfumo wa ikolojia ni mwingiliano kati ya viumbe hai na visivyo hai. Wananchi wanapoacha kukata miti hovyo, huchangia kuboresha makazi ya wanyamapori na kulinda mazingira yao ya asili,” anasema.
Akizungumza kuhusu mafanikio hayo, Elvis anasema kuwa uwezo wa wananchi kutambua kwamba wanyamapori ni rasilimali muhimu inayowanufaisha umeongezeka kwa kiasi kikubwa, jambo ambalo lina manufaa makubwa kwao wenyewe na kwa jamii kwa ujumla.
Anafafanua zaidi kuwa ongezeko hilo la uelewa linajidhihirisha kupitia ushirikiano wanaoutoa wananchi kwa maafisa wa maliasili, michango yao wakati wa vikao mbalimbali, pamoja na mabadiliko ya mitazamo yao kuhusu wanyamapori kutoka ile ya awali ya kuwachukulia kama maadui na waharibifu wanaostahili kuuawa, hadi kama viumbe wenye manufaa kwao na vizazi vijavyo.

Yamat Lengai, Ofisa wa APW anayesimamia masuala ya ukusanyaji na ufuatiliaji wa taarifa za utekelezaji wa mradi, upimaji wa matokeo na uboreshaji wa mradi, anaeleza kuhusu matokeo mengine chanya ya mradi huo.
“Ukifuatilia katika maeneo mengi yenye kuta hai, matukio ya wanyamapori kuvamia makazi ya watu na kuua mifugo yamepungua au kutokomea kabisa, na wanyamapori hawauawi tena kama ilivyokuwa awali,” anasema.
Kwa mujibu wa Raphael, kingine ni kwamba wananchi sasa wanaokoa gharama kwa kutotumia fedha zao katika matengenezo ya mara kwa mara ya mazizi yaliyochakaa au kujenga mapya baada ya yaliyopo kuharibika.
Pia mifugo yao inaendelea kuzaliana na kuwapatia faida kwa kuwa haiuliwi tena na wanyamapori. Raphael anasema: “Mazizi haya mapya yameleta mabadiliko makubwa katika maisha yangu.”
Maria Samwel, mkazi wa Kijiji cha Loibor Siret, anayefanya kazi kama mhamasishaji wa masuala ya mazingira katika Wilaya ya Simanjiro, anasema kuwa ukuta hai umeleta manufaa pia kwa wahifadhi, kwani matukio ya kuwadhuru wanyamapori yamepungua. “Ninashauri maeneo mengine ambako jamii zinaishi jirani na wanyamapori kuiga mfano huu,” anasema.
“Kabla ya kuanza kutumia ukuta hai, maboma yalikuwa yakiharibika mara kwa mara, hivyo wananchi walilazimika kukata miti mingine ili kuyakarabati. Ukataji huo wa mara kwa mara ulikuwa unachangia kupungua kwa bayoanuai, mabadiliko ya tabianchi na uharibifu wa mifumo ya ikolojia kwa njia mbalimbali, kwa kuwa miti ni mhimili muhimu wa uhai wa viumbe na mazingira,” anasema Yamat, na kuongezea: “Kwa sasa wakishajenga boma wanafanya marekebisho madogo ya kuongeza kupanda miti michache iliyokauka na kuanguka.”
Kwa upande wa mazingira, mradi huo umechangia kwa kiasi kikubwa katika uhifadhi na ustawi wa mazingira, kwani vitendo vya ukataji wa miti wa mara kwa mara vimepungua sana, huku uoto wa asili unaozunguka mazizi hayo ukianza kurejea upya, anasema Yamat.
Masika anaongeza: “Uoto wa asili ni chakula cha wanyamapori. Eneo linapokosa uoto wa kutosha, linakuwa si salama kwa wanyama wala kwa binadamu”.
Aidha, amefafanua kuwa katika kipindi cha zaidi ya miaka kumi aliyofanya kazi katika maeneo ya uhifadhi, ameshuhudia kwa dhahiri faida kubwa zinazotokana na matumizi ya kuta za aina hiyo pamoja na hasara nyingi zinazosababishwa na migongano ya mara kwa mara kati ya wanyamapori na jamii zinazozunguka maeneo ya hifadhi.
Mradi huo pia umechangia kutoa ajira kwa wananchi. Kwa mfano, maofisa wanaofuatilia migogoro kati ya binadamu na wanyamapori, wanaokusanya na kuhifadhi takwimu, pamoja na wale wanaotoa utaalam wa ujenzi wa ukuta hai, ni wanajamii wenyewe, anasema Yamat.
“Kuna maeneo mengine wanyama kama simba walikuwa karibu kutoweka. Sasa wamerejea kwenye mazingira yao. Tunajisikia fahari kuwarejesha wanyama hao maarufu,” anasema Elvis.
Takwimu za utekelezaji wa mradi huo zinaonyesha kuwa idadi ya mifugo iliyookolewa imekuwa ikipanda kulingana na ongezeko la kuta hai. Kwa mfano, katika kipindi cha kuanzia mwaka 2008 hadi 2009, mradi ulipoanza, kulikuwa na kuta hai nne, na jumla ya mifugo 141 iliokolewa. Hata hivyo, kufikia kipindi cha mwaka 2025 hadi 2026, idadi ya kuta hai ikiwa 2,117, mifugo iliyookolewa ni 318,895.
Changamoto
Licha ya mafanikio ya mradi huo, bado zipo changamoto mbalimbali zinazoukabili utekelezaji wake. Elvis anasema kuwa wakati mwingine mahitaji ya ujenzi wa kuta hai huwa makubwa ikilinganishwa na raslimali zinazopatikana. Kutokana na hali hiyo, wakati mwingine hukosekana raslimali za kutosha zinazowezesha utoaji wa huduma kwa wakati unaohitajika.
Mfano wa kuigwa
Mafanikio ya mradi huo yanatoa funzo kwa taasisi nyingine kuhusu nguvu ya ushirikishwaji wa jamii katika kufaninikisha miradi ya unifadhi.
“Kitu kikubwa kilichochangia mafanikio ya mradi huu ni ushirikishwaji mpana wa wanajamii wenyewe katika utekelezaji wake. Ushirikishwaji huo umejenga imani miongoni mwa wanajamii, umewafanya waone fahari kuwa sehemu ya mradi, na zaidi ya yote, umewapa fursa ya kufanya kazi kwa pamoja na kubadilishana maarifa wao kwa wao, anasema Yamat.

Elvis anasema kuongezeka kwa uelewa miongoni mwa wanajamiii kuhusu umuhimu wa wanyamapori kwa jamii na mazingira kwa ujumla, pamoja na kuwepo kwa utaratibu unaowawezesha maafisa wa utatuzi wa migogoro kuendelea kuwaelimisha watu kuhusu namna ya kuepuka migogoro kati ya binadamu na wanyamapori, vinabaki kuwa kielekezo muhimu kwa maeneo mengine yanayokabiliwa na changamoto za migogoro hiyo.
Pamoja na kutoa elimu kwa wanajamii, maafisa hao, ambao kila kijiji huwa idadi yao ni kati ya watatu hadi wanne, pia hukusanya taarifa kuhusu migogoro inayojitokeza katika maeneo yao. Hatua hiyo husaidia upatikanaji wa takwimu sahihi zinazowezesha kufanya maamuzi bora kuhusu hatua stahiki za kuchukua.
Akizungumzia kuendelezwa kwa mradi huo, Elvis anabainisha kuwa kiwango cha uelewa walichonacho wananchi kuhusu umuhimu wa kulinda wanyamapori, matumizi ya mbinu salama za kuwafukuza wanyama katika maeneo yao, pamoja na hamasa waliyonayo ya kujenga kuta hai wao wenyewe, vinadhihirisha wazi kuwa mradi huo ni endelevu na una matarajio makubwa ya kuendelea kufanya vizuri siku zijazo.
Aidha, Elvis anaeleza kuwa wamekuwa wakipokea wageni kutoka nchi mbalimbali barani Afrika wanaokuja kujifunza kutokana na uzoefu wao. Anasema hali hiyo ni ushahidi wa wazi kuwa kazi wanayoifanya ni nzuri na ni mfano wa kuigwa na wengine.